Habari za Punde

Tamko la kulaani tukio la Bw Nassor Msingili kukatwa mkono

TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA
Kitalu Na. 8, Mtaa wa Luthuli
S.L.P 2643, DAR ES SALAAM
Simu: +255 22 2135747/8; 2137125; 2135222
Faksi: +255 22 2111281
Barua Pepe: chragg@chragg.go.tz
Tovuti: www.chragg.go.tz
Oktoba 06, 2017

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Tamko la THBUB kulaani tukio la Bwana Nassoro Msingili kukatwa mkono    

Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) imepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kukatwa mkono kwa mtu mwenye ualbino, Bwana Nassoro Msingili (75) wa Kijiji cha Nyarutanga Kata ya Kisaki, Morogoro Vijijini, tukio lililotokea usiku wa kuamkia Jumanne Oktoba 3, 2017.

Tume inalaani vikali kitendo hicho cha kikatili. Aidha, Tume inaungana na Watanzania wengine nchini kote kumpa pole Bwana Msingili na kumtakia apone haraka.

Tume, kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imekuwa ikitoa elimu kwa Watanzania kwa ujumla kuhusu umuhimu wa kuheshimu utu, haki na stahiki mbalimbali za watu wenye ualbino kwa kuwa ni binadamu sawa na binadamu wengine.

Aidha, Tume inavitaka vyombo vyote vya dola pamoja na wananchi kwa ujumla kutoa ulinzi kwa watu wenye ualbino, ambao wako kwenye hatari ya kushambuliwa. Kinachojidhihirisha kutokana na yaliyomkuta Bwana Msingili ni dhahiri kuwa jukumu hili halijafanyika kikamilifu.

Tume inapenda kuwakumbusha Watanzania wote kuhusu kuheshimu na kulinda haki za watu wenye ualbino. Kwa hiyo Tume:

1.   Inaikumbusha Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kudhibiti vitendo vya kikatili kwa watu wenye ualbino nchini na kulitafutia ufumbuzi wa kudumu tatizo hili.

2.   Inawakumbusha wananchi kuwa vitendo vya ukatili, mauaji, na matendo yote yanayokiuka Sheria yanayofanywa na raia wasio wema ni ukiukwaji wa Sheria, haki za binadamu na misingi ya utawala wa sheira; Hivyo Tume inakemea matendo haya na kutaka yapigwe vita.

3.   Inapendekeza Kamati za Ulinzi na Usalama katika ngazi za Wilaya, Kata, Vijiji na Vitongoji wakiwemo watendaji watimize wajibu wao ili kuhakikisha usalama wa watu wenye ualbino katika maeneo yao.

4.   Inalipongeza Jeshi la Polisi kwa hatua za kuwakamata watuhumiwa haraka. Aidha, inaliomba Jeshi hilo lifanye uchunguzi wa kina na kuwafikisha mbele ya vyombo vya sheria wote watakaobainika kuwa walihusika na ukatili huo.

5.   Tume na wadau wengine wataendelea kutoa elimu zaidi kwa umma kuhusu haki za watu wenye ualbino na masuala ya haki za binadamu na wajibu, sheria, utawala bora na uraia.

Mwisho, Tume inatoa wito kwa wananchi wa Kijiji cha Nyarutanga na maeneo mengine kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi katika kuhakikisha wote waliohusika na unyama huu wanakamatwa na kufikishwa katika vyombo husika ili sheria ichukue mkondo wake.

Imetolewa na:

(SIGNED)
Mhe. Bahame Tom Nyanduga
MWENYEKITI

TUME YA HAKI ZA BINADAMU NA UTAWALA BORA


Oktoba 6, 2017

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.