Habari za Punde

Wazee kisiwani Pemba wataka kuthaminiwa na kuenziwa

Na Salmin Juma , Pemba

''Tupeni miradi tunayoweza kuifanya sisi kama wazee, kwani tunahitaji kujikwamua hasa ukizingatia wazee roho zetu zimeshatangalia kwa Mungu hivyo hatuwezi kufanya hiyana katika miradi hiyo na tofauti na vijana wa leo wanapopewa miradi'' 

Hii ni kauli yakutilisha imani na  kusikitisha iliyotoka kinywani mwa  Mzee Ali Omar Abdalla mwenye umri wa miaka 73 mkaazi wa vitongoji wilaya ya Chakechake mkoa wa kusini Pemba.

Kauli hii imekuja wakati alipokua akizungumza nami juu ya hali ya kuthaminiwa, kujaliwa  na kuenziwa kwa wazee wa kisiwani Pemba.

Ilikua ni katika harakati za kutafuta habari ikiwa ndio desturi yangu maishani katika ulimwengu wa tasni ya habari, nilikutana na wazee wengi katika maeneo tofauti ya kisiwa hiki cha Pemba ambao kiujumla wao niliwaona wapo katika hali isiyoyakuridhisha kimavazi na hata katika mtazamo wa kawaida wanaonekana ni wenye kuchoka kwa shida achiliambali uzee wanaoendelea kuwavaa.

Wazee hao baada ya kuwaona, moyoni nikajengeka hamu ya kutaka kuzungumza na baadhi yao  ili kutaka kujua, jee uzee wao ndio sababu ya wao kua katika hali kama niliyokwisha ieleza hupo juu.

Kwa lengo la kutaka kujua, safari ya kwanza nilielekea huko Wingwi Mapofu mkoa wa kaskazini Pemba,  ambapo nilikutana na wazee wengi wasiopungua 10 kike kwa kiume, nami nikaketi chini baada ya kukaribishwa na hapo ndipo ulipokuwa mwanzo wa maongezi yetu, lengo ikiwa ni kutaka kujua ni kwa namna gani wazee wenye umri wa kuanzia miaka 60  kwenda juu wamekua wakijaliwa na kuthaminiwa nchini mwetu, hasa ukizingatia miongoni mwao wamo wastaafu ambao walishajitolea nguvu zao miaka mingi kutumikia nchi hii.

Wakati tukiendelea na mazungumzo huku nikiwadadisi kutaka kujua wao kama wazee wana eneo maalum ambalo wanaweza kufikisha kiliochao pindi wanapofikwa na shida , nikagundua kuwa kumbe kuna mpango kabambe uliyotengengezwa kwa lengo la kuwasaidia nao ni ''Mabaraza ya wazee'' katika kila shehia.

Na kati ya hao niliyokaa nao kumbe alikuwamo M/kiti wa baraza la wazee wa shehia ya Wingwi Mapofu mzee  Mzee Salum Said Ali (67), tulizungmza mengi na ya kutosha lakini makubwa kati ya hayo alisema, nia na makusudio ya baraza lao ni kujikwamua na hali ngumu za kimaisha wanazokumbana nazo wazee pamoja na kuwa na chombo cha kufikisha na kushtaki kiliochao.

Alisema lengo la baraza lao ni zuri lakini bado hawajafikia lengo kuu ambalo ni kumuona mzee anakua katika mazingira mazuri yaliyokusudiwa ingawa wameshaanza kuona mwanga na wangali wanajipa matumaini makubwa.

''Serikali ipo lakini sio kila kitu tuikumbizie serikali, sisi kama wazee tunaweza kujisaidia na ndio maana tukakaa pamoja kupanga mikakati ya kupiga hatua za kimaendeleo mbele'' alisema Mzee Ali.
Katika hatua nyengine alisema ingawa wana azma kubwa ya kujisaidia lakini pia inawawiya vigumu kufikia malengo kwasababu ya upungufu wa pesa za kujiendeshea, alitolea mfano kwakusema '' unapata semina ukashiriki mafunzo fulani mjini chakechake lakini nikijitazama sina kitu mfukoni, naamua kufunga safari hivyo hivyo hatimae nachelewa na nikifika hakuna kitu nilichowahi'' alisema Mzee Ali.

Mzee Ali aliendelea kunieleza kuwa, kutokana na hali hiyo ngumu wanayokabiliana nayo kwa makusudi wakamua kuweka utaratibu wa kuchangishana kila mwezi shilingi 1,000/= ili kujikwamua pale wanapokwama.

Hali za wazee hao kwakweli bado zinaonekana kuwa dhaifu kiuchumi, sikusita  kuwauliza ,  jee muna mradi wowote ambao mumeuanzisha au munaotaka kuuanzisha ili alau mupate ahuweni katika mambo yenu? alinijibu ''Ndio tumeanzisha nasari ya minazi na mpaka muda huu tunaminazi 85 ambayo tunatarajia kuipanda vizuri baadae tuuze nazi ili kipato kikue katika baraza letu'' alisema Mzee Ali.

Baraza hili linaonekana kukamilika , lina mratibu wa shuhuli zao zote  bw: Said Yussuf Hamad, Katibu wa baraza Bi Fatma Rashid Nassor na wajumbe wake 10 ambao ni mchanganyiko wa wanawake na wanaume.

Nilichojifunza ni kwamba, wazee wamethubutu na wameweza na ndio maana wakamua kujikusanya pamoja kuunda baraza la wazee ili kukaa  pamoja na kuzaa mbinu mbadala  ya kujondoa katika hali ngumu za kimaisha, kama waswahili wanavyosema ''UKUBWA DAWA''

Lakini juu ya kuthubutu kwao hali ya wazee hao inaonekana kuwa ngumu kiuchumi na katika maeneo mengine muhimu ya huduma za binaadamu.

Nimeyasema haya kwa sababu mmoja kati ya wajumbe hao  Mzee Hamad Faki Mwinyi (80) alinieleleza kuwa ingawa wanabaraza hilo na linawasaidia katika mambo mengine lakini bado huduma ya afya ni kikwazo '' bado kutibiwa ni tatizo, kama huna pesa ni tatizo'' alisema Mzee Mwinyi.

Baada ya mazungumzo hayo nikafunga tena safari moja kwa moja mpaka maeneo ya Vitongoji mkoa wa kusini Pemba nako nikakutana na wazee kama wale wa Wingwi, walikua na baraza baraza ya wazee shehia ya Vitongoji, na mwonekano wao pia haukupishana na wale wa kule Wingwi, walionekana kuchoka kimwili , niliomba kuzungumza na mwenyekiti wa baraza hilo ambae ni Mzee Ali Juma Khamis kwa heshima na taadhima walinikaribisha na kuanza mazungumzo yetu, narudia tena hapa, lengo langu ni lile lile kutaka kujua ni kwanamna gani wazee kisiwani Pemba wanajaliwa na kuthaminiwa?

Mzee Juma aliniambia, baada ya kuona hali zao zimekua mbaya na hakuna wa kuwafatilia moja kwa moja wakaanzisha baraza la wazee , waweze kujisemea shida zao pamoja na mahitaji yao yote.

Alisema kabla ya uwepo wa baraza hilo mambo yalikua ni mashaka matupu, huduma za afya bora kwao ilikua ni kama ndoto na hata ikitokea misaada hakuna anaowaona lakini hali hivi sasa kidogo inaonekana kuwa nzuri kupitia baraza lao la wazee.

Hakika maneno haya yanatia moyo na sasa unapata picha uwepo wa mabaraza haya ya wazee ni dira ya maendeleo kwao.

Akiendelea kunielezea faida wanazonufaika nazo mwenyekiti huyo alisema kwa mambo yanavyokwenda huko baadae wanatarajia kupata mafunzo tofauti ya kimaendeleo na yatasimamiwa na baraza hilo hilo kuonyesha kwamba wazee wanaweza na si wakubezwa.

''Wazee tulikua tunatupya, lakini sasa hivi tunatarajia kupitia baraza letu hili mambo yatakua safi sana'' alisema Mwenyekiti huyo.

Kwa upande wake mshika fedha wa baraza hilo Bi Jine Ali Abeid (67) alisema bado wanaiomba serikali na wadau wengine wajitokeze kuwapatia miradi maalum ya wazee ambayo wataweza kuiendesha wenyewe.

Alitolea mfano wa miradi hiyo kama vile miradi ya biashara ambapo alisema, wakiekewa mradi wa duka wanaweza kuuwendesha vizuri na malengo yakafanikiwa , pia wanahitaji kinu cha kusagishia nafaka na kwa upande mwengine hata kuwezeshwa kukopeshana wao  kwa wao.

Utafiti niliyoufanya umenionyesha kuwa kuna mawazo mazuri yaliyowekwa kwaajili ya kuwathamini wazee  lakini juhudi za kufanikisha malengo hayo bado zingali zinasuasua ,ingawa wazee wenyewe wanatamaa ya maisha bora lakini muda mrefu utapita.

Kabla ya kufanya hitimisho katika jambo hili, niliwatafuta jumuiya ya wazee Zanzibar (JUWAZA) ili kuona nao wanamtazamo gani juu ya mabaraza haya ya wazee na vipi wamepanga kuwasaidia.

Nilibahatika kukutana na mratibu wa mabaraza ya wazee Pemba kutoka jumuiya hiyo Bi Sifuni Ali Haji alisema,wao kama ni wadau wakubwa kwa mabaraza hayo, na wanafurahi kuwepo kwa wingi kwani ndio kutapatina maendeleo sahihi kwa wazee hao.

Alisema JUWAZA wanawatembelea mabaraza hayo ili tujue wanamipango gani ya kimaendeleo , badae wanaichukua mipango hiyo na kuwatafuta wadhamini na wahisani ili wawezeshwe kufikia malengo.

Bi Sifuni alitoa wito kwa kuwataka masheha wote katika kisiwa cha pemba kuunda mabaraza ya wazee kwani kutasaidia pakubwa katika kuwatatulia wazee shida zao ambao wanaonekana kuwa  katika hali ngumu za kimaisha hivi sasa.

Sambamba na hayo, Bi Sifuni alitoa wito kwa wahisani kujitokeza kwa wingi kuunga mkono juhudu hizo ambapo na mimi hapa ndipo ninapotaka kukazia kamba.

Wazee kisiwani Pemba wanateseka na wanaendelea kuhilikika katika kila eneo la maisha , katika upande wa sekta ya afya matibabu ni mtihani mkubwa kwao, hata misaada mengine ya kawaida kuipata ni nadra.

Tukumbuke kuwa sio wazee wote kisiwani Pemba wana uwezo wa kumudu huduma za kimaisha , wapo wasiojiweza , wanaoteseka katika kusaka huduma hizo, kwapamoja tuungane kuwakomboa wazee wanaonekana kuwa katika madhila makubwa.

Serikali na taasisi zake,  wahisani na wadau wote wa maendeleo , pamoja jitokezeni kudhamini mabaraza haya ya wazee, kwa lengo lile lile la kuwatatulia shida zinazowakabili katika maish, ili nao ifike siku wajione wanathaminika katika kisiwa hiki.




No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.