Habari za Punde

Balozi wa Kuwait Nchini Tanzania Akabidhi Msaada wa Laptop na Printer Kwa Skuli za Jimbo la Tunguu Zanzibar.

Balozi wa Kuwait nchini Tanzania Mhe. Jassem Al Najem akikabidhi kompyuta za mkononi kwa walimu wakuu wa baadhi ya shule zilizoko katika jimbo a Tunguu Wilaya ya Kati Unguja. Katikati ni Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mmanga Mjengo Mjawiri, akifuatiwa na Mwakilishi wa jimbo hilo Simai Mohammed Said.
Balozi wa Kuwait nchini Tanzania Mhe. Jassem Al Najem akikabidhi kompyuta za mkononi kwa walimu wakuu wa baadhi ya shule zilizoko katika jimbo a Tunguu Wilaya ya Kati Unguja. Katikati ni Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mmanga Mjengo Mjawiri, akifuatiwa na Mwakilishi wa jimbo hilo Simai Mohammed Said. (Picha na Salum Vuai, MAELEZO ZANZIBAR).  


Na Salum Vuai, MAELEZO
UBALOZI wa Kuwait nchini Tanzania, umezizawadia skuli mbalimbali zilizomo katika jimbo la Tunguu kompyuta 20 za mkononi (Laptops) na printa kumi ili kuwaongezea maarifa ya kielimu walimu na wanafunzi.

Makabidhiano ya kompyuta hizo yalifanyika Disemba 14, 2017 katika kituo cha walimu Dunga Wilaya ya Kati, ambapo Balozi wa Kuwait Jassem Al Najem akishirikiana na Mwakilishi wa jimbo la Tunguu Simai Mohammed Said.

Aidha Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mmanga Mjengo Mjawiri, alihudhuria hafla hiyo akiwa mgeni rasmi, pamoja na Mbunge wa jimbo hilo Khalifa Salum Suleiman, maofisa kadhaa wa elimu pamoja na masheha.

Akizungumza na washiriki wa hafla hiyo, Mjawiri alitaka vifaa hivyo vitumike katika njia sahihi ya kuendeleza elimu  badala ya matumizi yaliyo kinyume na maadili na silka za Mzanzibari.

Alisema kompyuta hizo zitakapofika katika skuli zilizokusudiwa, zitumike kutafuta mambo ya kielimu yatakayorahisisha usomeshaji kwa walimu na usomaji kwa wanafunzi.

“Hatutaki zitumike kama pambo bali zifanye kazi iliyokusudiwa ya kutafuta elimu. Ni matarajio yetu baada ya mwaka mmoja tutaona mabadiliko katika maendeleo ya elimu jimboni humu, nasi Wizara ya Elimu tutakuwa tukifuatilia kuona tafauti kati ya sasa na baadae,” alieleza Naibu Waziri huyo.

Aidha alisema Wizara yake itaendelea kutimiza wajibu wake pale hali itakaporuhusu kusambaza na kuongeza vifaa kama hivyo katika skuli mbalimbali za Unguja na Pemba.

Mjawiri alimpongeza Mwakilishi wa jimbo hilo kwa juhudi anazochukua kwa kutafuta vianzio mbalimbali vya maendeleo, akisema anaamini baada ya miaka mitano Tunguu itakuwa mfano mzuri kwa majimbo mengine kujifunza kutokana na ufanisi wake.

Naibu Waziri huyo wa Elimu hakuacha kuwakumbusha wazazi na walezi, umuhimu wa kuwa karibu na watoto wao ili kuhakikisha hawadhuriwi na vitendo vya udhalilishaji na ubakaji kwa wanawake na watoto vilivyoshamiri nchini kwa sasa.

Aidha alimshukuru Balozi wa Kuwait Jassem Al Najem kwa msaada huo  muhimu, akisema umeonesha mapenzi makubwa aliyonayo kwa wanafunzi na wananchi wa Zanzibar.

Kwa upande wake, Balozi Al Najem alisema vifaa hivyo vyenye thamani ya shilingi 25,000,000, si msaada bali ni zawadi kutoka kwa wananchi wa Kuwait kwa ndugu zao wa Zanzibar ili viwasaidie katika kuchimba hazina ya elimu.

Aidha alieleza kufurahishwa na mapokezi aliyopata kutoka kwa wananchi wa jimbo hilo, na kuahidi kuendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar pamoja na jimbo hilo kwa kupeleka aina tafauti za miradi jimboni humo ikiwemo pia sekta ya michezo.

Alieleza kuwa utoaji wa vifaa hivyo ni katika kuunga mkono mradi ulioanzishwa na ubalozi wa nchi yake uliopewa jina la ‘KUELEKEA ELIMU BORA ZAIDI’.

Alitumia fursa hiyo kuwapa pole familia, serikali, Jeshi la Wananchi wa Tanzania na wananchi wote kwa msiba mkubwa wa kuuwawa kwa wanajeshi huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Disemba 7, 2017.

Mwakilishi wa Tunguu Simai Mohammed Said akimshukuru balozi huyo, alisema anaamini vifaa hivyo vitasaidia kukuza vipawa vya elimu kwa walimu na wanafunzi, ili waendane na kasi ya mabadiliko ya teknolojia duniani.


Alisema kwa kushirikiana na viongozi wengine wa jimbo wakiwemo madiwani na taasisi za serikali, wataendelea kuzitafutia ufumbuzi hatua kwa hatua changamoto mbalimbali za jimbo hilo ili kuliletea maendeleo zaidi na kuinua ustawi wa watu wake.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.