Habari za Punde

Haji Mwinyi kuukosa mchezo wa kesho dhidi ya Uganda

Beki wa kushoto wa Zanzibar Heroes Mwinyi Haji Ngwali ambae ataukosa mchezo wa kesho kwa kuwa na kadi mbili za njano

Na Abubakar Khatib Kisandu, Kisumu Kenya.

Mlinzi wa kushoto Haji Mwinyi Ngwali ataukosa mchezo wa kesho wa Zanzibar wakiwavaa mabingwa watetezi Uganda.

Zanzibar Heroes watakipiga na Uganda katika mchezo wa nusu fainali ya pili kwenye mashindano ya Cecafa Senior Challenge Cup, mchezo utakaopigwa saa 9:00 za Alaasiri kwenye uwanja wa Moi uliopo Kisumu.

Mwinyi ataukosa mchezo huo mara baada ya kupigwa kadi mbili za njano katika michezo miwili mfululizo iliyopita ukiwepo waliotoka sare ya 0-0 na Kenya na ule waliofungwa 1-0 na Libya ambapo kanuni ya mashindano hayo mchezaji akipewa kadi mbili mfululizo za njano katika michezo miwili mfululizo atalazimika kuukosa mchezo unaofuata.

Nafasi ya Mwinyi kesho itazibwa na Adeyum Ahmed Seif ambae pia ni mzoefu katika Mashindano hayo ya Cecafa.

Mbali ya Mwinyi pia Zanzibar Heroes itawakosa huduma za nyota wake wengine akiwepo mfungaji wao Kassim Suleiman Khamis pamoja na kiungo Amour Suleiman “Pwina” ambao wote ni majeruhi.

“Mwinyi hatocheza ana kadi 2 za njano, lakini pia Kassim na Amour nao tutawakosa kutokana na majeruhi”. Alisema Kocha wa Zanzibar Heroes Hemed Suleiman (Morocco).

Lakini kwa upande wa timu ya Uganda kesho itawakosa nyota wake wawili muhimu akiwemo Mulema Isaack na Awany Tinoethy ambao wote walipewa kadi mbili za manjano katika michezo miwili mfululizo iliyopita.

 "Ni mechi ngumu nawajua sana Zanzibar lakini na sisi tutawaonyesha kama tunataka kulitetea kombe letu". Alisema Moses Basena kocha mkuu wa Uganda.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.