STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Dodoma 16.12.2017
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amepokea kwa furaha kubwa matokeo ya ushindi wa Timu ya Taifa
ya Mpira wa Miguu ya Zanzibar “Zanzibar Heroes” katika mashindano ya Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati ‘CECAFA’
2017 yanayoendelea nchini Kenya.
Kutokana na matokeo
hayo Rais Dk. Shein ametoa pongezi zake za dhati kwa wachezaji wote wa timu ya
Zanzibar Heroes pamoja na viongozi wao kwa mafanikio makubwa waliyoiletea
Zanzibar hadi kufika fainali.
Dk. Shein alieleza
kuwa, kwa hakika ushindi wa Timu ya Zanzibar ni ushindi wa Wazanzibari na
Watanzania wote kwa jumla na umeiweka Zanzibar kwenye kiwango kizuri katika
ramani ya michezo katika ukanda wa Afrika ya Mashariki na Kati na nje ya mipaka
ya Tanzania.
“Natoa pongezi za dhati kwa wachezaji wote wa “Zanzibar
Heroes” pamoja na viongozi wao kwa mafanikio makubwa waliyotuletea hadi kufikia
hatua ya fainali ya mashindano hayo”,alisema Dk. Shein.
Aidha,
Dk. Shein alieleza matumaini yake makubwa
ya timu ya Zanzibar Heroes kushinda katika mchezo wa fainali kutokana na uwezo
mkubwa walioonesha vijana wetu kwenye mashindano hayo.
Dk.
Shein alieleza kuwa Serikali na wananchi wote, wako pamoja na timu hiyo pamoja
na viongozi wao kwa hali na mali katika kuhakikisha wanarudi na ushindi.
Sambamba
na hayo, salamu hizo za pongezi alizozitoa Dk. Shein zilieleza kuwa maandalizi
ya kuwapokea na kuwarudisha nyumbani yameshaanza kupitia uongozi wa Wizara ya
Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo.
Dk.
Shein aliwataka wananchi wote wa Tanzania kuungana kwa pamoja kuwaombea dua na kuwatakia kila la
kheri katika mchezo wa kesho wa fainali watakapocheza na timu ya Harambee Stars
ya Kenya.
Timu ya Zanzibar
Heroes imetinga fainali za michuono hiyo ya Chalenji baada ya kuifunga Uganda
mabao 2-1 na kuivua ubingwa katika mchezo wa nusu fainali uliofanyika jana
uwanja wa Moi uliopo Kisumu, Kenya.
Kutokana na matokeo
hayo Zanzibar Heroes sasa itacheza fainali za mashindano hayo kwa kuwavaa
wenyeji Kenya katika mchezo utakaofanyika kesho Jumaapili.
Kenya ilitinga fainali
hizo baada ya kushinda bao 1-0, dhidi ya
Burundi katika mchezo wa nusu fainali ya kwanza iliyofanyika juzi.
Timu ya Zanzibar
ilikuwa katika kundi A, na kundi la Tanzania Bara, Kenya, Libya na Rwanda
ambapo ilianza mashindano kwa kuifunga Rwanda mabao 3-1, kabla ya kushinda
mabao 2-1 dhidi ya Tanzania Bara kisha ilitoka suluhu na Kenya na kufungwa bao
1-0 na Libya katika mchezo wa mwisho kuelekea nusu fainali.
Zanzibar Heroes
imeandika historia kwa kucheza fainali tangu ilipofanya hivyo mwaka 1995,
kuivua Uganda ubingwa lakini pia, imerudia kuifunga tena Uganda kama
ilivyofanya mwaka huo 1995 katika fainali ilipotwaa ubingwa kwa kuifunga Uganda
bao 1-0 lakini jana iliifunga mabao 2-1.
Mashindano ya Kombe la
Chalenji yanayoandaliwa na Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati
‘CECAFA’ yalianza Disemba 2 na yanatarajiwa kumalizika kesho Jumaapili.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment