Habari za Punde

Zanzibar Heroes kukutana na Uganda Cranes nusu fainali Kombe la Cecafa




Timu ya taifa ya Zanzibar, Zanzibar Heroes itakutana na Uganda katika nusu fainali ya Kombe la Cecafa.

Uganda iliyoibuka mshindi katika kundi lake inakabiliana na Zanzibar iliyoibuka mshindi wa pili baada ya kupoteza mchezo wake wa mwisho na Libya ambapo wangeweza kuiepuka Uganda na kukabiliana na Burundi ambao wameibuka waashindi wa pili.

Katika nusu fainali nyengine wenyeji Kenya watavaana na Burundi.

Michezo yote ya nusu fainali itafanyika katika Uwanja wa Kisumu siku ya Alkhamisi tarehe 14/12/17 wakati fainali itafanyika katika mji wa Machakos siku ya Jumapili tarehe 17/12/17

Uganda Cranes wamewahi kukutana na Zanzibar Heroes mara 14 ambapo Cranes wameweza kushinda mara 12 kutoka sare mara moja na kupoteza mara moja.

Timu ya Taifa ya Zanzibar iliwahi kushinda mara moja tu Kombe la Cecafa  mwaka 1995 ambapo iliwaondoa Waganda kwa kuwafunga 1-0 goli lililofungwa na Victor Bambo.

Zanzibar Heroes imeweza kuwashangaza wengi katika mashindano ya Cecafa mwaka huu huku wakionesha kandanda safi inayotegemea pasi fupi fupi na wachezaji wenye kujituma wakiwa uwanjani huku wakijua majukumu yao.

Licha ya rekodi kuonesha Uganda Cranes wana rekodi nzuri dhidi ya Zanzibar Heroes hata hivyo kikosi cha Heroes mwaka huu chini ya Kocha Hemed Morocco kina uwezo wa kuigeuza historia hii na kuwafurahisha wazanzibari kwa kuiondoa Uganda na kuingia Fainali.

Katika Soka kila kitu kinawezekana hivyo uwezo wa kuwafunga Uganda tunao na ninaamini wachezaji ari wanayo na Zanzibar kwa ujumla inaamini hivyo.

Timu ya Zanzibar Heroes imepita katika majaribu ya wachezaji wake kupimwa mkojo wakidhaniwa kutumia madawa ya kuongeza nguvu hasa ukizingatia uwezo wao walioweza kuonesha uwanjani kuwashangaza wengi mpaka Cecafa kuamua kuchagua wachezaji wane wa timu kupimwa mkojo ambapo vipimo vyao vimepelekwa Afrika Kusini kwa uchunguzi zaidi

Ninaamini Kocha Morocco pamoja na benchi lake la ufundi litawajenga vijana kisaikolojia waweze kuondokana na kasumba hii na kuwaweka tayari kwa mechi ya kesho na kufanya kile ambacho taifa la Zanzibar limewatuma kwenda kukifanya na kuiletea heshima Zanzibar na kutuma ujumbe kwa vitendo CAF na FIFA kwamba  Zanzibar soka lipo na tulipoomba kujiunga hatukubahatisha.

Wazanzibari kwa pamoja tuwaunge mkono Timu yetu kwa hali na mali kwani sehemu pekee ambapo wimbo wetu wa Taifa la Zanzibar na bendera ya Taifa la Zanzibar hutumika nje ya visiwa hivi ni pale vijana wetu wanaposimama kuimba kwa moyo wa uzalendo wakituwakilisha na kuthibitisha kwamba Zanzibar haitoweza kufutika katika medani ya Soka.

Kama kawaida blog ya ZanziNews inawatakia Heroes kila la kheri na sote tuwe pamoja kuiombea dua iibuke na ushindi kuzidi kuwafurahisha Wazanzibari na kuijengea heshima nchi yetu.

Go Zanzibar Heroes Go!


Kila la kheri Zanzibar Heroes 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.