Habari za Punde

Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli Azindua Pasipoti Mpya za Tanzania leo.

Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, wakimsikiliza Kamishna Mkuu wa Idara ya Uhamiaji Tanzania Dk. Anna Peter Makakala, akitowa maelezo ya Ubora wa Pasipoti hizi mpya zilizotengenezwa kwa utaalamu wa Kieletronikia, Uzinduzi huo umefanyika katika viwanja vya Makao Makuu ya Uhamiaji Kurasini Jijini Dar es Salaam leo, jumatano 31-1-2018.

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Joseph Magufuli leo amezindua Pasipoti mpya ya Tanzania ya Kielektroniki inayoenda sambamba na Mfumo wa Uhamiaji Mtandao na kuipongeza Idara ya Uhamiaji kwa kwenda na wakati pamoja na kuonesha uzalendo katika utendaji kazi wao.

Rais Magufuli aliyasema hayo katika uzinduzi huo uliofanyika katika Makao Makuu ya Ofisi za Uhamiaji Tanzania yaliopo Kurasini, jijini Dar-es-Salaam ambapo viongozi mbali mbali walihudhuria akiwemo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan na viongozi wengine wa Serikali zote mbili.

Katika maelezo yake, Rais Magufuli alieleza kuwa Pasipoti mpya ni haki ya kila Mtanzania hivyo ni vyema kuitumia fursa hiyo waliyoipata Watanzania na kuipongeza Idara ya Uhamiaji Tanzania kwa kuonesha mabadiliko makubwa.

Kuendelea kuchapa kazi, kubadilisha jina, kuwashughulikia wahamiaji wanaoingia Tanzania na kuwasaka wahamiaji na kueleza jinsi anavyofarajika kuwaona Maafisa wa Uhamiaji wanavyowashika Wahamiaji.

Alieleza haja kwa kuchukua hatua kwa wakuu wa Uhamiaji ambao wahamiaji wamekuwa wakipita kirahisi bila ya kuwakamata na kumtaka wahusika wasiotimiza wajibu wao awashughulikie ikiwa ni pamoja na kuwapunguza hata vyeo.

Alisema kuwa Idara yao ni nyeti na muhimu kwa usalama wa Tanzania huku akiwapongeza sambamba na kuwataka kuzifanyia kazi changamoto zilizopo.

Aliwapongeza kwa kazi nzuri wanazozifanya ikiwa ni pamoja na kutumia mfumo wa kiielektroniki katika kukusanya mapato, wito wa serikali kuhamia Dodoma pamoja na mambo mengine muhimu.

Alisema kuwa Idara hiyo ni muhimu hasa katika ulinzi na usalama na maendeleo ya kuiuchumi ya nchi ambayo Idara hiyo inaifanya kuwa ni nyeti na muhimu sana.
Alieleza kuwa katika miaka ya karibuni Pasipoti ziligawiwa kiholela na kuwapa mianya wahalifu na kuharibu taswira ya nchi na kufanya baadhi ya Watanzania kupata tabu katika baadhi ya nchi.

Alieleza kuwa kuna raia wengi wa kigeni walipata vibali vya ukaazi ambao si raia, wengine hawana sifa, ukusanyaji wa mapato ya viza haukuridhisha na mengineyo hatua ambayo iliifaya Idara hiyo ionekane haikuwa sawa na ndio alipoamua kufanya mabadiliko na kumteua Dk. Makakala ambaye ameanza vizuri na kumtaka kuyaondoa mapungufu.

Alimpongeza Balozi wa Ireland Paul Shercockm kwa kusaidia kupatikana Kampuni ya kutengeneza Pasipoti kwa kiwango kidogo cha fedha mbali na Kampuni za awali ambazo zilitaka fedha nyingi.

Alieleza kuwa fedha zote za mradi huo zimetolewa na Tanzania, na kusema kuwa bei ya sasa imezingatia ukubwa na ubora wake ambayo itakuwa na kurasa nyingi na kueleza haja ya kuikubali kutokana na kuimarishwa kwa usalama wa Pasipoti hiyo.

Aliwataka Watanzania kuzilinda na kuzitunza Pasipoti mpya na kueleza kuwa anaimani kuwa hakuna ujanja utakaofanyika katika Pasipoti hizo kama ilivyokuwa ikifanywa na baadhi ya watu.

Pamoja na hayo alieleza kuwa lengo nikutaka wananchi na wageni wanapewa huduma bora na wasicheleweshwe na kueleza kuwa kutokana na kushirikishwa kwa kuwataka wadau wengi katika mfumo huo kutasaidia kupata Pasipoti na huduma nyengine.

Rais Magufuli aliahidi kutoa Bilioni 10 nyengine baada ya kuwapa nyumba 103 Idara hiyo kwa ajili ya kujenga jengo zuri la Makao Makuu ya Idara hiyo mjini mjini Dodoma na kumtaka Mkuu wa Idara hiyo kutafuta eneo kwa ajili ya ujenzin huo ikiwa ni shukurani zake kwa Idara hiyo.

Alisisitiza haja ya kuwepo kwa uadilifu na uaminifu kwa watumishi wa Idara hiyo na kueleza kuwa kwa wale watumishi wachache wanaoendeleza rushwa katika Idara hiyo kufanyiwa kazi na vyenginevyo wakigunduliwa wafukuzwe.

Dk. Magufuli aliwahakikishia kuwa iwapo wataendelea na mwendo wao huo wa kubadilika na changamoto zitabadilika na kuwataka kutembea kifua mbele na kuwataka wajue kuwa wana jukumu kubwa katika nchi hii.

Pamoja na hayo, Rais Magufuli aliwahakikishia wakaazi wa Dar-es-Salaam kuzitatua changamoto walizonazo ikiwa ni kuimarisha miundombinu ya barabara, reli, huduma za kijamii kama maji, afya, elimu na kuwataka wananchi waendelee kuiunga mkono Serikali sambamba na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Dk. Mwigulu Nchemba, alimpongeza Rais Magufuli kwa kuipeleka Tanzania katika hatua moja muhimu na ya kihistoria na kuwa nchi moja ya mfano kwa nchi za Afrika Mashariki na Kusini mwa Jangwa la Sahara  pamoja na mambo mbali mbali aliyoanza kuyafanya ikiwa ni pamoja na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa kiasi kikubwa.

Dk. Nchemba alisema kuwa hatua hiyo ni muhimu sana katika mapambano ya uhalifu kwa kutumia teknlolojia hiyo sambamba na kusaidia kufuta makosa yaliojitokeza hapo siku za nyuma huku akisema kuwa gharama ya Pasipoti hiyo ni TZS 150,000 ambayo itatumika kwa miaka kumi.

Nae Kamishna Jenerali wa Uhamiaji Dk. Anna Peter  Makakala, alieleza kuwa Uhamiaji Mtandao ni muunganiko wa Mifumo mbali mbali ambayo imesanifiwa kufanya kazi kwa pamoja na kutoa taarifa kwa watumiaji na wadau wa huduma za kiuhamiaji ambao mchakato wake ulianza mwaka 2013 na kuanza tena 2017 mwezi Juni.

Alieleza kuwa lengo kuu la Uhamiaji Mtandao ni kuimarisha Ulinzi na Usalama wananchi, kudhibiti ukusanyaji wa maduhuli ya serikali na kuimarisha utoaji wa huduma za kiuhamiaji kwa raia na wageni wanaoingia na kuishi hapa nchini kwa madhumuni mbali mbali.

Aliongeza kuwa Mfumo wa Uhamiaji Mtandao utawezesha Idara ya Uhamiaji kutoa viza kielektroniki (e-Visa) ambapo mgeni ataweza kuwasilisha ombi lake na kupata majibu kwa njia ya kielektroniki, mfumo ambao utasaidia Serikali kupata taarifa sahihi za malipo ya viza na hivyo kuchangia ukuaji wa sekta ya utalii nchini.

Dk. Makakala alisema kuwa mfumo huo utasaidia udhibiti na usimamizi wa mipaka kielektroniki ambao utasaidia kudhibiti na kuwezesha uingiaji na utokaji wa raia wa Tanzania na wageni nchini sambamba na kuchuja wageni wasiotakiwa kuingia nchini, Pia utasaidia kuimarisha usimamizi wa utoaji vibali.

Pamoja na hayo alieleza kuwa mfumo huo ambao ndio wa kwanza katika utekelezaji wa Mradi wa Uhamiaji Mtandao, utawezesha waombaji wa huduma ya Pasipoti kuwasilisha maombi yao kwa njia ya kielektroniki kutoka mahali popote walipo na kuweza kufuatilia maombi yao kielektroniki ambayo pia itakuwa imara.

Alitoa pongezi kwa kupewa nyumba 103 za watumishi wa Idara hiyo na Rais Magufuli na kueleza kuwa Idara yake imeanza kutekeleza Sera ya Uhamiaji,  na kusisitiza kuwa kutokana na kuzinduliwa kwa Pasipoti hizo mpya Pasipoti za Kawaida mwisho wake itakuwa ni Januari mwaka 2020 na baada ya hapo zitaondolewa katika matumizi na Pasipoti ya Afrika Mashariki haitotolewa tena.

Sambamba na hayo, alieleza kuwa Mradi huo unatekelezwa kwa awamu nne ambazo ni mfumo wa pasipoti za kielektroniki, mfumo wa kielektroniki wa visa, mfumo wa kielektroniki wa vibali vya ukaazi na pasi pamoja na mfumo wa kielektroniki wa usimamizi na udhibiti wa mipaka.

Pia, alitoa shukurani kwa Rais kwa kutoa ajira 1510 kwa mwaka 2017 hadi 2018
Katika hafla hiyo viongozi mbali mbali walikabidhiwa Pasipoti zao akiwemo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassa, Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Rais mstaafu wa Zanzibar Amani Abeid Karume na baadhi ya viongozi wengineo huku ikielezwa kuwa kwa upande wa viongozi wa Zanzibar zitaendelea kutolewa Zanzibar.

Balozi wa Ireland Paul Shercock alitoa pongezi kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuanza Mradi huo ambao utaipelekea Tanzania kuimarika katika uchumi wake na kuwa salama.

Mwakilishi wa Kampuni ya HID Robert Haskan alieleza jinsi hatua zilizochukuliwa katika kuhakikisha mfumo huo unaimarika na kuwa wa uhakika na ina sifa za pasi yenye taarifa za kielektroniki sambamba na kupunguza muda na gharama.  

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.