Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Akifungua Warsha ya Uelewa Itakayosimamia Viwanda Vidogo Vidogo Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, akifungua Mkutano wa Warsha ya Kutoa Uelewa Juu ya Mamlaka Itakayosimamia Viwanda Vidogo vidogo na Vya Kati,(SMIDA) iliofanyika katika kumbi wa Zamani wa Baraza la Wawakilishi Kikwajuni Zanzibar,ilioandaliwa na Wizara ya Biashara Viwanda na Masoko Zanzibar.

SERIAKLI ya Mapinduzi ya Zanzibar imeamua kuanzisha Taasisi ya Wakala wa Serikali wa Kusimamia Maendeleo ya Viwanda vidogo vidogo na vya kati, Zanzibar (SMIDA) ili sekta ya viwanda iweze kuimarika, kusimamiwa kwa karibu pamoja na kusaidiwa kwa lengo la kuvilea viwanda hivyo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema hayo leo katika uzinduzi wa Warsha ya Utambulisho wa Wakala wa Serikali wa Kusimamia Maendeleo ya Viwanda vidogo vidogo na vya kati (SMIDA), hafla iliyofanyika katika ukumbi wa zamani wa Baraza la Wawakilishi, Kikwajuni Mjini Unguja.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alisema kuwa mifano ya Taasisi kama hiyo ipo mingi katika nchi mbali mbali ambapo kwa upande wa Tanzania Bara lipo Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo Vidogo (SIDO), India kuna Shirika la Taifa la Viwanda Vidogo Vidogo la India, na Mauritius lipo (SMIDA), kama iliyo kwa Zanzibar.

Alieleza kuwa katika nchi nyengine zipo taasisi mahsusi zilizoanzishwa kwa lengo lamkusaidia na kusimamia uanzishwaji na maendeleo ya miradi midogo midogo ya Wajasiriamali kama vile nchini Kenya, Pakistani, Malaysia na Bangladesh.

Hivyo, Dk. Sheijn alieleza kuwa itakuwa ni fursa muhimu ya kujifunza mikakati ya mafanikio yao na kutambua changamoto zilizowakabili kuweza kubuni mbinu nzuri za kukabiliana na changamotio za aina hiyo.

Dk. Shein alitoa wito kuitumia vyema fursa hiyo na nyenginezo kwa kujifunza kutoka nchi mbali mbali kama hizo ili malengo ya Serikali ya kuanzisha Mamlaka hiyo yaweze kufikiwa na kuleta manufaa yaliyokusudiwa.

Aliongeza kuwa katika awamu mbalimbali za uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Zanzibar imekuwa ikiandaa mipango na kutekeleza mikakati ya kuimarisha sekta ya viwanda kwa kutambua umuhimu wake na kusisitiza kuwa Sekta ya viwanda ina umuhimu wake katika kuchangia uchumi, kuimarisha sekta nyengine za uzalishaji na biashara, kuimarisha upatikanaji wa bidhaa mbali mbali na kutoa fursa kubwa ya ajira kwa wananchi.

Alieleza kuwa mchango wa sekta ya viwanda umeendelea kuimarika nchini na kuchangia pato la Taifa kutoka TZS bilioni 417.0 mwaka 2015 na kufikia TZS bilioni 487.9 mwaka 2016 ambapo mchango huo umefikia asilimia 18.6 mwaka 2016 kutoka asilimia 18.1 mwaka 2015 katikajumlaya pato la Taifa.

Dk. Shein alieleza kuwa mchango huo umeimarika zaidi kufuatia kufanya kazi kwa viwanda vya maji ya chupa, kiwanda cha Azam na kiwanda cha Sukari cha Mahonda ambapo kwa mujibu wa Dk. Shein Serikali kupitia Mamlaka ya Uwekezaji Vitega Uchumi (ZIPA) imeshaidhinisha ujenzi wa viwanda vipya vitano katika eneo la Viwanda Vidogo Vidogo Amani na maeneo ya Maruhubi.

Aidha, Dk. Shein alieleza kuwa kuanzishwa na kufanya kazi ipasavyo kwa Wakala wa Serikali wa Kusimamia Maendeleo ya Viwanda uliozinduliwa leo kutapunguza kwa kiasi kikubwa changamoto zinazoikabili sekta ya biashara kwani miongoni mwa majukumu yake ni kutoa mafunzo kwa wenye nia ya kuanzisha miradi ya uzalishaji mali na wale ambao tayari wanayo miradi ya aina hiyo.

Kutokana na hilo, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwataka Wakuu wote wa Wilaya Zanzibar kuhakikisha kila Wilaya inakuwa na kiwanda na kutokana na uzoefu wao wa kazi alisisitiza kuwa ana uhakika hilo linawezekana.

Dk. Shein alieleza kuwa Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya mwaka 2015-2020 imezielekeza Serikali zake mbili kuelekea katika uchumi wa Viwanda, ili iwe ni ukombozi halisi wa kuwapatia fursa zaidi za ajira vijana.

Pia, Dk. Shein alieleza jinsi alivyolizungumizia suala zima la ajira katika ziara yake aliyoifanya wiki iliyopita, kuanzia tarehe 20 hai 27 katika Umoja wa nchi za Falme ya Kiarabu (UAE) wakati alipokutana na viongozi wa Umoja huo akiwemo Mtawala wa Abu Dhabi, Sheikh Muhammed bin Zayed Al Nahyan.

Nae Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko Balozi Amina Salum Ali alieleza kuwa Wizara yake katika kumaliza Mpango wa Zanzibar kukuza Uchumi (MKUZA) na katika kujipanga na mpango mpya wa uchumi wa mwaka 2010 imejipanga kutekeleza mkakati wa kuendeleza viwanda kwa kupitia upya sera ya Viwanda na kuja na Sera mpya na Sheria itakayowezesha kwenda kwa kasi mpya katika kujenga viwanda vitakavyoongeza ajira.

Aliongeza kuwa Sekta zote zinaendelea kufanyiwa tathmini ili kuona zitawezaje kuwezesha viwanda vihamie Zanzibar na kutoa mchango mkubwa  na kusisitiza kuwa Zanzibar ya viwanda inawezekana.

Balozi Amina alieleza kuwa Awamu hii ya Saba, Serikali imefanya mapitio ya Sera ya Ujasiriamali na kupendekeza uanzishaji wa wakala wa Serikali wa kusimamia viwanda, ambao madhumuni yake makubwa ni kujenga viwanda vya msingi vitakavyoweza kuchangia viwanda vikubwa ambavyo vitaendeshwa ili kuongeza ukuaji wa sekta zote za uchumi ikiwemo utalii, kilimo, uvuvi, bahari, madawa, teknoloji, mafuta na gesi asilia.

Sambamba na hayo, Waziri huyo alichukua nafasi hiyo kutoa taarifa rasmi kuwa Sheria ya Wakala imeshakuwa inafanya kazi baada ya Rais kuitia saini na bajeti ya uanzishwaji kwa fedha za SMZ zimetengwa huku akieleza kuwa tayari Wizara imeshaona eneo la kuanzia makao makuu na kuiomba Serikali kuwapatia.

Mapema, Kaibu Mkuu wa Wizara hiyo Juma Ali Juma alieleza kuwa Wakala hiyo inatarajiwa kutoa fursa kubwa sana kwa wajasiriamali wa hapa nchini katika kuimarisha uzalishaji wa bidhaa zao kwa kutumia viwanda.

Alieleza kuwa kutokana na wingi wa vijana wanaomaliza masomo kila mwaka katika ngazi mbali mbali, suala la kuajiriwa wote Serikalini limekuwa changamoto kubwa na ndio maana Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikatilia mkazo suala la uanzishwaji wa Mifuko ya Uanzishaji wananchi kiuchumi na sasa suala la uanzishaji wa viwanda vidogo, vidogo na vya kati ili kutoa fursa ya ajira.

Alisema kuwa suala hilo na uazishaji wa viwanda bado halijafahamika vizuri  wananchi wengi na hasa vijana hawana uwelewa wataanza vipi uzalishaji wa viwanda, bidhaa gani zinaweza kuzalishwa nchini kutokana na rasiliamali zilizopo, ubora sambamba na uwelewa wa soko.

Hivyo, Katibu Mkuu huyo, alisisitiza kuwa Warsha hiyo aliyoifungua Rais madhumini yake ni kutoa uelewa kwa wananchi pamoja na lengo la kuwataka kuelewa kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeshatenga Sheria na tayari imeshaanza kufanya kazi hivyo wakae mkao wa kula kwa kunufaika na malengo yaliokusudiwa.

Alieleza kuwa wanakusudia kutoa uelewa katika ngazi ya Taifa ambapo leo hii wamezindua rasmi hadi ngazi za Serikali za Mitaa ambako ndiko waliko wananchi wengi na ndiko ambako kutaanzishwa maeneo ya uzalishaji wa viwanda.

Sambamba na hayo, Katibu Mkuu huyo alieleza matumaini makubwa ya kushirikiana na Shirika la Maendeleo ya Viwanda, Tanzania (SIDO) ambao wana uzoefu mkubwa katika kuendeleza viwanda vidogo vidogo Tanzania.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Viwanda Tanzania (SIDO), Inginia Profesa Sylvester Mpanduji alitoa pongezi kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuanzisha Wakala wa Serrikali wa Kusimamia Maendeleo ya Viwanda Vidogo Vidogo na vya kati (SMIDA) huku akiwataka Watanzania kuzitumia bidhaa za hapa nchini.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.