Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akisalimiana na mgeni wake Balozi wa Visiwa vya Comoro katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Mohammed Fakih Al Baadawy alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo,[Picha na Ikulu.] 06/Machi/2018.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza na mgeni wake Balozi wa Visiwa vya Comoro katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Mohammed Fakih Al Baadawy alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo,[Picha na Ikulu.] 06/Machi/2018.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kushoto) akiagana na mgeni wake Balozi wa Visiwa vya Comoro katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Mohammed Fakih Al Baadawy baada ya mazungumzo yao alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo,[Picha na Ikulu.] 06/Machi/2018.
STATE
HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF
THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 06.03.2018
RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa Zanzibar
itaendeleza uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati yake na visiwa
vya Comoro hasa katika kukuza mila na utamaduni ikiwa ni miongoni mwa
utekelezaji wa Mkataba wa Makubaliano kati ya pande mbili hizo.
Akizungumza na Balozi
wa Visiwa vya Comoro nchini Tanzania Mohammed Fakih Al Baadawy aliyefika Ikulu
mjini Zanzibar, Rais Dk. Shein alimuahidi Balozi huyo kuwa Zanzibar inathamini
sana uhusiano na ushirikiano uliopo ambao ulitiwa nguvu zaidi baada ya
kusainiwa Mkataba wa Makubaliano mnamo mwaka 2014, wakati alipofanya ziara
nchini humo.
Mbali
ya uhusiano wa kimaendeleo kati ya Zanzibar na Comoro, Dk. Shein alisema kuwa
nchi mbili hizo zimekuwa na uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu katika kukuza
mila na tamaduni sambamba na mafunzo hasa katika elimu ya dini ya Kiislamu
Katika maelezo yake,
Rais Dk. Shein alimuhakikishia Balozi huyo kuwa Zanzibar itashiriki kikamilifu
katika Kongamano la kimataifa juu ya maisha ya Marehemu Sheikh Sayyid Omar
Abdallah, maarufu Sheikh Mwinyi Baraka litakalofanyika mjini Moroni, Comoro
kuanzia April 03 hadi 06, 2018.
Rais Dk. Shein aliyapongeza
malengo ya Kongamano hilo ikiwa ni pamoja na kuwaelimisha vijana juu ya masuala
muhimu aliyoyahubiri Sheikh Mwinyi Baraka na kusisitiza kuwa kwa upande wa
Zanzibar wapo wanaomfahamu wakiwemo walimu na wanazuoni wa zamani ambapo wapo
baadhi yao ambao wako hai hivyo, ushiriki wa Zanzibar ni muhimu katika
Kongamano hilo.
Aidha, Rais Dk. Shein
alimueleza Balozi huyo kuwa Zanzibar inathamni sana ushirikiano na uhusiano
uliopo kati yake na Comoro katika sekta ya elimu, hasa elimu ya Dini ya
Kiislamu ambapo wananchi waliowengi wa Visiwa vya Comoro waliipata elimu hiyo hapa
Zanzibar na kwenda kuifanyia kazi katika nchi hiyo.
Aliongeza kuwa
Masheikh, Wanazuoni, na Maulamaa kama vile kina Sheikh Mwinyi Baraka waliweza
kufanya vyema katika kuhakikisha wanakuwa Mabalozi wazuri na kuitangaza vyema
Zanzibar katika sekta ya elimu ya dini ya Kiislamu hivyo, ni vyema wakakumbukwa
kwa juhudi zao hizo.
Hivyo, Rais Dk. Shein
alikubaliana na kupongeza wazo la Balozi huyo wa Comoro katika Ushirikiano wa
Vyuo Vikuu vya nchi hizo kikiwemo chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA ) na
Chuo Kikuu cha Comoro katika maandalizi ya Kongamano hilo la Kimataifa ambalo
litazidi kutoa mwanga wa ushirikiano katika sekta ya elimu.
Aidha, Rais Dk. Shein
alisisitiza ushiriki wa Zanzibar katika Kongamano hilo pamoja na kuunga mkono
wazo la kuwepo kwa Makumbusho maalum ya Sheikh Mwinyi Baraka nchini Comoro
ambapo akiwa katika ziara yake nchini humo mwaka 2014 alizuru kaburi la Sheikh
huyo.
Nae Balozi wa Visiwa vya Comoro nchini Tanzania Mohammed
Fakih Al Baadawy alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Comoro na Zanzibar zina
uhusiano na ushirikiano mkubwa kati ya nchi mbili hizo pamoja na watu wake
ambao wana udugu wa kihistoria.
Balozi Al Baadawy alimueleza Dk. Shein kuwa Comoro itaendeleza
na kudumisha uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya pande mbili hizo hasa
katika sekta mbali mbali za maendeleo na zile za kijamii kwa kutambua udugu wa
damu uliopo kwa watu wa nchi mbili hizo.
Aidha, Balozi huyo
alimpongeza Rais Dk. Shein kwa kuendeleza vyema uhusiano na ushirikiano uliopo
kati ya pande mbili hizo ikiwa ni pamoja na kuendelea kutekeleza Mkataba wa
Makubaliano ambapo suala la Mila na Utamaduni lilihusishwa na limekuwa
likifanyiwa kazi vyema na kuanza kuzaa matunda.
Hivyo, Balozi huyo wa
Comoro alitumia fursa hiyo kumueleza Rais Dk. Shein azma ya nchi yake kufanya
Kongamano la Kimataifa kwa ajili ya kumuenzi Sheikh Mwinyi Baraka, ikiwa ni
miaka 100 ya kifo chake sambamba na kumuelezea Sheikh huyo ili azidi kufahamika
na vizazi vilivyopo na vijavyo wakiwemo vijana, ili waweze kuutambua mchango
wake.
Alieleza kuwa ushiriki
wa Chuo Kikuu cha SUZA katika kongamano hilo ni muhimu sana na utasaidia kupata
mambo mengi muhimu kutoka kwa wasomi wa chuoni hapo pamoja na wadau wengine ikiwemo
Taasisi ya Mwinyi Baraka ya Zanzibar huku akieleza ushiriki wa wadau wengine
kutoka Marekani, Uengereza, Ufaransa, Ujerumani na sehemu nyengine duniani.
Alisisitiza kuwa Sheikh Mwinyi Baraka alikuwa na mchango
mkubwa katika kuendeleza elimu hasa elimu ya dini ya Kiislamu ambapo mbali ya
elimu ya dini ya Kiislamu pia, alibobea katika elimu ya dunia ambapo alisoma
vyuo mbali mbali duniani na kupata Shahada ikiwemo Chuo Kikuu cha Makerere Uganda,
Oxford cha Uingereza na Vyuo vyengine vya
nchi za Kiarabu.
Sheikh Mwinyi Baraka
alizaliwa Zanzibar mnamo mwaka 1918 na kufariki Comoro mwaka 1988 ambaye
alikuwa msomi na mwanachuoni mashuhuri ambapo Kongamano hilo la kwanza la
Kimataifa litaweza kuhamasisha na kuelimisha watu juu ya safari na sifa za
Sheikh huyo ambaye alikuwa mwalimu, mbunge, mwanadiplomasia, mhadhiri, mwanasayansi,
mwanasheria na msomi wa dini.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment