Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Waziri wa Nchi ya Saudi Arabia Ikulu Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) alipokuwa akizungumza na Waziri wa Mamlaka ya Saudi Arabia anayeshuhulikia Mambo ya Kiislamu,Daawa,Misaada na MiongozoMhe,Dk.Sheikh Saleh bin Abdul Aziz bin Muhammad bin Ibrahim Al Sheikh,(kushoto)alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo akifuatana na Ujumbe wake,(katikati) Mkalimani wa lugha) Sheikh Khalid Mohammed Mrisho
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                                                                30.05.2018
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa ziara ya Waziri wa Mamlaka ya Saudi Arabia anayeshughulikia Mambo ya Kiislamu, Daawa, Misaada na Miongozo, hapa Zanzibar  ni muhimu kwa maendeleo ya Zanzibar na Saud Arabia.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika mazungumzo kati yake na Waziri huyo wa Mamlaka ya Saudi Arabia anayeshughulikia Mambo ya Kiislamu, Daawa, Misaada na Miongozo aliyefika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya mazungumzo na Rais.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alieleza kuwa Saud Arabia na Zanzibar zina historia kubwa ya mashirikiano na mahusiano kati ya pande mbili hizo huku akisisitiza kuwa historia ya Uislamu inaonesha jinsi Uislamu ulivyoingia Zanzibar ambapo jamii nzima ya Kiislamu duniani inaelewa suala hilo.

Dk. Shein alieleza kuwa ziara hiyo ya kiongozi huyo pia, itaimarisha umoja na udugu wa muda mrefu uliopo kati ya Zanzibar na Saudi Arabia na kueleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na wananchi wake watauendeleza umoja huo.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa historia ya elimu hasa elimu ya dini ya Kiislamu hapa Zanzibar haiwezi kutolewa bila ya kuhusishwa Saudi Arabia kwani ni nchi ambayo Mashekhe na Maulamaa wa Zanzibar walipata elimu hiyo nchini humo hasa katika mji wa Madina.

Dk. Shein alieleza kuwa mnamo miaka ya sabini Mashekhe na Maulamaa wengi wa Zanzibar walipata fursa hiyo ya kupata elimu ya dini ya Kiislamu nchini humo na kuifanya Zanzibar kuwa na hazina kubwa ya viongozi hao wa dini ya Kiislamu.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa mbali ya sekta ya elimu Saudi Arabia imesaidia kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi ya maendeleo ukiwemo ujenzi wa miundombinu mbali mbali kama vile jengo la Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, Msikiti wa Mwembeshauri pamoja na mradi wa ujenzi wa barabara huko kisiwani Pemba kwa kushirikiana na Benki ya Maendeleo ya Afrika (BADEA).

Pia, Rais Dk. Shein alieleza kuwa hivi karibuni kuna msaada mkubwa wa ujenzi wa Hospitali ya MnaziMmoja kutoka nchini humo kwa mashirikiano ya BADEA na Kuwait.

Rais Dk. Shein pia, aliipongeza azma ya Saudi Arabia kutaka kujenga Chuo Kikuu cha Kiislamu hapa Zanzibar ambapo pia, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuiomba Saudi Arabia kufungua Ubalozi wake mdogo hapa Zanzibar kama ilivyo kwa baadhi ya nchi kama vile China, India, Misri, Msumbuji ambazo zina ubalozi mdogo hapa Zanzibar.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alipokea salamu za pongezi kutoka kwa Mfalme wa Saudi Arabia, Salmani bin Abdulzaziz al Saud pamoja na pongezi kutoka nchi hiyo kutokana mwenendo mzuri wa Mahujaji wa Zanzibar wanaokwenda kufanya Ibada ya Hijja nchini Saudi Arabia.

Nae Dk. Sheikh Saleh bin Abdul Aziz bin Muhammad bin Ibrahim Al Sheikh, Waziri wa Mamlaka ya Saudi Arabia anayeshughulikia Mambo ya Kiislamu, Daawa na Miongozo alimueleza Dk. Shein kuwa ziara hiyo imefungua mahusiano mazuri kati ya nchi hiyo na Zanzibar kupitia Wizara yake ya Nchi Ofisi ya Rais Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala Bora pamoja na Ofisi ya Mufti Mkuu ya Zanzibar.

Waziri Dk. Sheikh Saleh alitumia fursa hiyo kutoa salamu za Mfalme Salman kwa Dk. Shein pamoja na kuipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutokana na miongozo mizuri inayotoa kwa Mahujaji wake wanaokwenda kuhiji nchini humo.

Alieleza kuwa Mahujaji wa Zanzibar wamekuwa wakifanya Hijja zao vyema na kufuata taratibu na miongozo yote muhimu pamoja na kuonesha tabia njema wakati wakifanya ibada yao hiyo nchini humo.

Aidha, Waziri huyo alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa vipaumbele vyote vilivyoelezwa na Zanzibar kwa Saud Arabia atavifanyia kazi kwa kufikisha kwa Mfalme Salman pamoja na Msaidizi wake ili kufanyiwa kazi.

Kiongozi huyo alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa ziara yake hiyo haitokuwa ya mwanzo wala ya mwisho kwani amependezewa na mazingira mazuri ya Zanzibar kutokana na vivutio kadhaa vilivyopo huku akiahidi kuwa Saudi Arabia itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha na kuendeleza miradi ya maendeleo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.