Habari za Punde

Sheria ya Karafuu No 2 ina vipengele vinavyomuumiza mkulima wa karafuu


NA ZUHURA JUMA, PEMBA

WAKULIMA wa zao la karafuu Wilaya ya Wete wamesema wana mashaka na sheria ya karafuu namba 2 ya mwaka 2014 pamoja na kanuni zake, kutokana na baadhi ya vipengele vya sheria hiyo kumkandamiza mkulima.

Wakizungumza katika mkutano wa kutathmini zao la karafuu katika Ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Wete, baadhi ya Wakilima  walisema kutokana na Serikali kutegemea zao hilo kwa kiasi kikubwa, ni vyema kuangalia upya sheria hiyo, ili kuweza kumsaidia mkulima.

Walisema kuwa, kumekuwa na baadhi vipengele ndani ya sheria hiyo ambavyo vinamkandamiza mkulima katika kuendesha shughuli zake za kilimo cha zao la karafuu, jambo ambalo linawasababishia vikwazo vikubwa mbali mbali, ikiwemo kupata hasara.

“Kwa kweli sheria sio rafiki kwetu hasa hii ya kuhamisha karafuu kutoka sehemu moja kwenda nyengine inatukwaza wakulima, maana wengine mashamba yetu yako kwenye Wilaya nyengine na sisi tupo kwengine”,  walisema wakulima hao.

Mkulima Mussa Ali Mussa mkaazi wa Kiuyu Minungwini alisema bado sheria ya zao la karafuu zinawakwaza wakulima, hivyo ni vyema kwa serikali kupitia shirika hilo kuzirekebisha ili kuweza kwenda sambamba na wakulima.

“Mimi nakaa Wilaya ya Wete, lakini shamba langu lipo Wilaya ya Mkoani na huko hakuna eneo la kuanikia, hivyo ilinisababishia kupata hasara kubwa kutokana na karafuu zangu kukosa hua”

Nae mkulima, Bimkubwa OmarAmour mkaazi wa shehia ya Bopwe Wete, aliiomba Serikali kuwatafutia maeneo rasmi ya kuanikia karafuu zao, ili kuweza kuepusha zao hilo kuharibika.

“Karafuu zangu naanika pembeni mwa barabara na wakija Wizara husika wananiambia niziondoshe na kama sikuziondosha watanitolesha faini, hivi tunaelekea wapi maana tumekuwa tukihangaika ili tupate karafuu zinazotakiwa lakini kwa hali hii kila siku karafuu zetu zitaharibika”, alisema mama huyo.

Aliiomba Serikali kuzitazama upya sheria zinazomkwaza mkulima wa karafuu, ili kuepusha changamoto wanazozipata wakati wa kuchuma zao hilo.

Mwanasheria kutoka shirika la ZSTC, Ali Hilal Vuai, alisema kuwa, watachukua juhudi za kuziangalia upya sheria hizo, ili kuepuka changamoto zilizopo kwenye vifungu hivyo, ikiwemo ile ya uhamishaji wa karafuu kutoka sehemu moja kwenda nyengine.

Akichangia mada ya uadilifu katika zao hilo, Jabu Mbwana Said kutoka shehia ya Kinyasini, alisema kuwa  kuna baadhi ya wapimaji wa zao hilo wamekosa uadilifu wakatika wa kupima karafuu zinazokwenda kuuzwa, jambo mbalo linawatia huzuni wakulima hao kila wanapofikiria.

“Mimi binafsi yangu nishakwenda nikaambiwa na sisi tunakata chetu, hivyo inauma sana kwani mimi ndie niliepata shida ya kulishughulikia zao hili, hivyo shirika liwape mafunzo ya uadilifu watendaji wao, ili kuepusha kumnyonya mkulima”,  alisema mkulima huyo.

Nae Mkuu wa Wilaya ya Wete, Abeid Juma Ali, alilipongeza Shirika la Biashara la ZSTC pamoja na wakulima kwa juhudi yao ya kuuzia karafuu zao katika vituo vya kununulia zao hilo, ambapo kwa msimu huu wamefanikiwa kwa kiasi kikubwa.

“Juhudi zenu ndio mafanikio ya zao letu na nchi kwa ujumla, hivyo muendelee, ili kukuza uchumi wetu”, alisema Mkuu huyo.

Mkutano huo wa tahmini kwa zao la karafuu kwa msimu wa mwaka 2017/2018 ,kwa wakulima wa karafuu ulifanyika katika Ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Wete Pemba.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.