Habari za Punde

Mapitio ya Uchumi na Utekelezaji wa Bajeti (2017/18)na Mwelekeo wa Uchumi na Bajeti Kwa Mwaka 2018/2019.


Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar Mhe. Dkt Khalid Salum Mohammed akizingumza na Waandishi wa Habari wa Vyombo Mbalimbali Zanzibar Muelekeo 
wa Bajeti ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019
..Ndugu Waandishi wa Habari,
Ndugu wananchi mnaotusikiliza
1.                 Kwanza kabisa, napenda nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu mwenye ukarimu alietuwezesha kukutana tena tukiwa wenye afya njema ili tuweze kuelezana kwa muhtasari kuhusu Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo na Mwelekeo wa Bajeti kwa mwaka wa fedha 2018/2019.
HALI YA UCHUMI, 2017
2.                 Pato la Taifa limeongezeka kutoka thamani ya shilingi za kitanzania 2,628 bilioni mwaka 2016 hadi kufikia 3,099 bilioni mwaka 2017 kwa kutumia vigezo vya bei ya mwaka husika. Ukuaji halisi wa uchumi  umefikia asilimia 7.5  kwa mwaka 2017  Aidha, kwa ukuaji huo wa uchumi kumejitokeza ongezeko la wastani wa Pato la Mtu binafsi kwa mwaka 2017 na kufikia Pato la Kila Mtu la TZS 2,020,000 (USD 907) ikilinganishwa nawastani wa TZS 1,806,000 (USD 830) kwa mwaka 2016.
3.                 Sekta ya kilimo imeongoza kwa ukuaji katika Pato la Taifa na kufikia wastani wa asilimia 8.8 mwaka 2017 kutoka ukuaji wa wastani wa asilimia 6.3 mwaka 2016. Sekta ya Huduma nayo imekua kwa wastani wa asilimia 8.2 mwaka 2017 kutoka wastani wa asilimia 7.2 mwaka 2016 na Sekta ya Viwanda imekua kwa asilimia 7.9 ikilinganishwa na asilimia 9.7 mwaka 2016.
MFUMKO WA BEI
4.                 Kasi ya mfumko wa bei za bidhaa na huduma nchini imeshuka hadi kufikia wastani wa asilimia 5.6 ikilinganishwa na wastani wa asilimia 6.7 mwaka 2016. Kushuka huko kumesababishwa na kushuka kwa mfumko wa bei za bidhaa za chakula, kuongezeka kwa uzalishaji wa ndani kulikotokana na hali nzuri ya hewa pamoja na utulivu wa thamani ya Shilingi ya Tanzania dhidi ya Dola ya Kimarekani.
MAPATO NA MATUMIZI YA SERIKALI
6.                 Kwa upande wa misaada kutoka nje, jumla ya TZS 380.5 bilioni zilitarajiwa kukusanywa katika mwaka 2017/18. Kati ya Fedha hizo, Ruzuku ilikuwa ni TZS 82.2 bilioni na Mikopo ni TZS 298.3 bilioni. Ili kuziba nakisi iliyojitokeza ya Bajeti Jumla ya TZS 30.0 bilioni zilitarajiwa kukopwa katika soko la ndani.
UTEKELEZAJI HALISI KWA MIEZI TISA (JULAI – MACHI,2018)
8.                 Katika kipindi cha mapitio (Julai – Machi 2018), Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imepokea Ruzuku na Mikopo kwa ajili ya Miradi na Programu za Maendeleo iliyofikia TZS 151.0 bilioni.
9.                 Kwa upande wa Matumizi, Serikali ilikadiria kutumia jumla ya TZS 1,087.4 bilioni ikijumuisha, TZS 590.7 bilioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na TZS 496.6 bilioni kwa matumizi ya kazi za maendeleo.  Kati ya fedha hizo za maendeleo, TZS 116.1 bilioni ni mchango wa Serikali na TZS 380.5 bilioni kutoka kwa washirika wa maendeleo.
10.             Hadi kufikia Machi 2018, matumizi halisi yalifikia TZS 681.6 bilioni sawa na asilimia 98 ya makadirio ya kipindi hicho. Kati ya matumizi hayo TZS 457.1 bilioni zilitumika kwa kazi za kawaida na TZS 224.5 bilioni kwa kazi za maendeleo.
DENI LA TAIFA
11.             Hadi kufikia Machi 2018, Deni la Taifa limefikia TZS 519.7 bilioni, likimaanisha ukuaji wa asilimia 37.8 kutoka TZS 377.1 bilioni lililokuwepo mwezi Machi 2017. Katika kiasi hicho, deni la ndani limefikia TZS 158.3 bilioni na deni la nje limefikia TZS 361.4 bilioni. Deni hilo ni sawa na asilimia 16.8 kwa Pato la Taifa, hivyo, bado tuna kiwango kidogo cha kudaiwa, deni letu linahimilika na tuna fursa zaidi ya kukopa tukihitaji, kwa ajili ya kuharakisha maendeleo yetu
MWELEKEO WA UCHUMI NA BAJETI KWA MWAKA 2018/2019
12.             Kwa mwaka 2018, Pato la Taifa linatarajiwa kukua kwa kasi ya wastani wa asilimia 7.7. Matarajio ya ukuaji wa uchumi yatatokana na mambo yafuatayo:
                                i.            Kuendelea na juhudi za kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula kwa ununuzi wa matrekta 20 mapya ambayo yatasaidia kuongeza kasi ya uzalishaji wa ndani.
                              ii.            Kuongezeka kwa uhamasishaji wa uwekezaji wa ndani na nje kwa kutekelezwa miradi mipya ikiwemo miradi ya ujenzi wa miundombinu ya barabara, uwanja wa ndege na makaazi (Kwahani, Chumbuni) pamoja na miradi binafsi ya uwekezaji katika maeneo ya Nyamanzi, Fumba, Mtoni na Matemwe.
                            iii.            Kuongezeka kwa kiwango cha idadi ya watalii wanaoingia nchini kutokana na kuendelea kuutangaza utalii na kupatikana kwa masoko mapya.
                           iv.            Kuendelea kuwepo kwa amani na utulivu.
MAENEO YA VIPAUMBELE KWA MWAKA 2018/19
13.             Kwa mwaka 2018/19, maeneo yatakayopewa kipaumbele katika utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo ni kama yafuatayo:-
        i.            Kuimarisha Miundombinu ya Maeneo ya Uingiaji Nchini, Barabara na Nishati;
      ii.            Kuendeleza sekta ya Utalii;
    iii.            Kuimarisha Viwanda Vidogo Vidogo kwa Kuongeza Thamani Bidhaa na Ubora wa Vifungashio;
   iv.            Kuimarisha Kilimo kwa Kujenga Miundombinu ya Umwagiliaji Maji, Uvuvi na Mifugo;
     v.            Kuimarisha Ubora wa Huduma za Kijamii zikiwemo Elimu, Afya, Michezo na Upatikanaji wa Maji safi na Salama;
   vi.            Kukuza Uwezo wa Watu;
 vii.            Utawala Bora,Uimarishaji wa Taasisi na Uwekaji Mji katika Hali ya Usalama;
viii.            Ajira kwa Vijana;
   ix.            Kuendeleza Tafiti.

MWELEKEO WA MAPATO

14.             Kwa mwaka wa fedha 2018/19, Serikali inatarajia kukusanya jumla ya TZS 1.315.1 trilioni zikiwemo TZS 807.5 bilioni zitokanazo na vyanzo vya ndani, TZS 464.2 bilioni kutoka kwa washirika wa maendeleo, TZS 3.4 bilioni Mfuko wa wafadhili na TZS 40 bilioni mikopo ya ndani.

Mapato ya Nje

15.             Kwa mwaka wa fedha 2018/19, Serikali inatarajia kupokea jumla ya TZS 463.9 bilioni kutoka kwa washirika wa maendeleo, zinazojumuisha Ruzuku ya TZS 77.6 bilioni na Mikopo ya TZS 386.3 bilioni.

MWELEKEO WA MATUMIZI

16.             Serikali inakadiria kutumia jumla ya TZS 1,315.1 bilioni katika mwaka wa fedha 2018/19 ikiwemo matumizi ya kazi za kawaida ya TZS 702.2 bilioni na matumizi ya kazi za maendeleo ya TZS 612.9 bilioni.

HITIMISHO

17.             Nachukua fursa hii kuwashukuru kwa dhati kabisa na kuwapongeza mmoja mmoja Washiriki wote wa Maendeleo kwa kutimiza wajibu wao wa kutaka kusaidia katika Bajeti yetu. Nasi kwa upande wetu tutaendelea kutimiza wajibu wetu wa kutekeleza bajeti hiyo ili kufikia malengo tuliyokubaliana.
18.             Bajeti ya mwaka 2018/19 itaendana na mambo muhimu matano ambayo yatatoa fursa kubwa ya kukuza uchumi na maendeleo ya jamii ya Mzanzibari.  Matumaini yangu kuwa wananchi wa Zanzibar wataitumia fursa hiyo muhimu kwa nia ya kuimarisha amani na kujenga Zanzibar yenye maendeleo makubwa ya kiuchumi na kijamii.
19.             Maeneo hayo ya fursa za kiuchumi ni pamoja:
a)     Maendeleo ya viwanda (Industrial Parks), kuendeleza wazalishaji wadogo wadogo pamoja na usarifu wa mazao ya kilimo
b)     Upatikanaji wa ajira kwa vijana wetu pamoja na jitihada mbali mbali ambazo Serikali itazichukua kukabiliana na uchache wa fursa za ajira kwa vijana wetu.
c)     Utafutaji wa mafuta na gesi ambapo Serikali itaendelea kuchukua hatua kadhaa ili kuendeleza zoaezi hilo pamoja na kujitayarisha kitaalamu na kiuchumi kukabiliana na matokeo chanya ya zoezi hilo.
d)     Kuendeleza miundombinu na Huduma za Jamii ambapo Serikali imetenga kiasi kikubwa cha bajeti yake kuendeleza huduma za Elimu, Afya, miundombinu na mawasiliano.
e)     Ugatuzi wa madaraka mikoani ambapo huduma zitasogezwa zaidi kwa wananchi pamoja na kuwapa fursa za kujiendeleza kiuchumi katika sehemu zao.
20.             Kazi kubwa itakayotukabili ni uwajibikaji wetu pamoja na mashirikiano mazuri kati ya sekta ya umma na jamii kwa jumla ili utekelezaji wa bajeti ijayo ufikie lengo lililokusydiwa. Ni muhimu sana watendaji na wananchi wote kwa pamoja kuzidisha moyo na ari ya maendeleo ili tufikie katika kiwango kizuri cha utekelezaji wa bajeti na hivyo kufikia malengo yetu ya ukuaji wa uchumi tulioutarajia pamoja na ustawi wa jamii kwa jumla.
Inawezekana, tutimize wajibu wetu.
Ahsanteni
Dr. Khalid Salum Mohamed
Waziri wa Fedha na Mipango
Zanzibar

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.