Habari za Punde

Waziri Mhe. Kigwangalla Afungua Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Karibu Kili Fair 2018



Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Bodi ya Utalii Tanzania, Jaji Mst. Thomas Mihayo (kulia) akitoa maelezo kwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla kuhusu Maonesho ya Utalii ya Kimataifa ya Karibu/Kili Fair 2018 kabla ya kuzindua maonesho hayo katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika mjini Moshi. Wengine pichani ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi, Maliasili na Utalii na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Nape Nnauye (wa tatu kulia), Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Kippi Warioba (wa pili kulia) na Mwenyekiti wa Kampuni ya Kilifair Promotion, Tom Kunkler (kushoto).

Na Hamza Temba-WMU-Moshi
....................................................................... 
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla ametoa wito kwa taasisi za Serikali, jamii, sekta binafsi na wadau kwa pamoja kushirikiana kuendeleza utalii katika maeneo yao ili sekta hiyo iweze kunufaisha zaidi taifa kwa kiwango kinachostahiki kuliko ilivyo hivi sasa.


Ametoa wito huo juzi katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika mjini Moshi wakati akifungua maonesho ya kimataifa ya utalii ya Karibu/Kili Fair 2018 ambayo yameshirikisha makampuni na wadau wa utalii zaidi ya 350 kutoka nchi zaidi ya 12 duniani huku na kuvutia watu zaidi ya 4,000 kuyatembelea.



Amesema ushirikiano huo utaiwezesha sekta hiyo kuongeza mchango wake katika uchumi wa Taifa ambao kwa sasa ni takriban asilimia 17.2 ya pato la Taifa, zaidi ya asilimia 24 ya mapato yote ya fedha za kigeni sambamba na zaidi ya asilimia 10 ya ajira zote nchini.

Amesema mchango huo bado ni mdogo ukilinganisha na aina na idadi ya vivutio vilivyopo hapa nchini.

Dkt. Kigwangalla amesema Serikali ya awamu ya tano imeshaanza kuchukua hatua mbalimbali zitakazosaidia kuboresha sekta hiyo ikiwemo ujenzi unaoendelea wa reli ya kisasa ya Standard Gauge, ujenzi wa Terminal 3 katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Dar es Saalam na uboreshaji wa Shirika la Ndege la ATCL.

Pamoja na hayo amesema Serikali kupitia wizara yake inaendelea na mpango wa kupanua wigo wa vivutio vya utalii nchini ili kuongeza idadi ya watalii na mapato ambapo Mapori matano ya Akiba mkoani Kagera na Geita yatapandishwa hadhi kuwa Hifadhi za Taifa (Burigi, Biharamulo, Kimisi, Ibanda na Rumanyika).

"Napenda kumshukuru sana Mhe. Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuridhia mapendekezo yetu ya kupandisha hadhi Mapori matano ya Akiba kuwa Hifadhi ya Taifa ambayo itaitwa Chato National Park, 'Tunatake pia advantage' ya uwepo wa uwanja wa ndege wa Chato ambao unajengwa katika kiwango cha kutua ndege kubwa zitakazowawezesha watalii kufika katika hifadhi hiyo" amesema Dkt. Kigwangalla. 

Amesema hatua hiyo itafungua utalii wa kanda ya Kaskazini Magharibi tofauti na ilivyo hivi sasa ambapo ni kanda ya kaskazini pekee inayofanya vizuri zaidi kwenye sekta hiyo. Amesema mpango huo unakwenda sambamba na kufungua utalii wa kanda ya kusini ambapo mradi wa Kusimamia Maliasili na Kuendeleza Utalii Kanda ya Kusini (REGROW) upo katika hatua ya utekelezaji.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Bodi ya Utalii Tanzania, Devotha Mdachi amesema Serikali kupitia bodi hiyo itaendelea kushirikiana na wadau kutangaza utalii wa Tanzania katika maonesho mbalimbali ya ndani na nje ya nchi sambamba na kuwashirikisha kunadi kauli mbiu mpya ya utalii wa Tanzania, "Unforgettable, Tanzania".

Naye Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi, Maliasili na Utalii na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Nape Nnauye amesema kamati hiyo itaendelea kutoa ushirikiano kwa Serikali na wadau hususan katika eneo la mabadiliko na maboresho ya sheria za kusimamia sekta hiyo iweze kuondokana na changamoto zilizopo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla akijaribu kuendesha baiskeli maalum ambayo hutumika kwenye utalii wa baiskeli kwenye maeneo mbalimbali ya hifadhi nchini baada ya kuzindua Maonesho ya Utalii ya Kimataifa ya Karibu/Kili Fair 2018 katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika mjini Moshi. 
Kutoka kushoto ni Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Aloyce Nzuki, Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Bodi ya Utalii Tanzania, Jaji Mstaafu Thomas Mihayo na Mkurugenzi Mkuu wa bodi hiyo, Devotha Mdachi wakiwa katika meza kwenye hafla ya ufunguzi wa maonesho hayo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla akiteta jambo na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi, Maliasili na Utalii na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Nape Nnauye kabla ya kuzindua Maonesho ya Utalii ya Kimataifa ya Karibu/Kili Fair 2018 katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika mjini Moshi.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi, Maliasili na Utalii na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Nape Nnauye, Mkurugenzi wa Kampuni ya Kilifair Ltd,Tom Kunkler, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira, Mkurugenzi wa Karibu Fair, Dominick Shoo na viongozi wengine wa Serikali na sekta binafsi wakiwa kwenye picha ya pamoja baada ya kuzindua Maonesho ya Utalii ya Kimataifa ya Karibu/Kili Fair 2018 katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika mjini Moshi. 
Mkurugenzi wa Karibu Fair, Dominick Shoo akiratibu ratiba nzima ya ufunguzi wa maonesho hayo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla akiwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi, Maliasili na Utalii na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Nape Nnauye kwenye eneo la mfano wa kilele cha Uhuru cha mlima Kilimanjaro baada ya kuzindua Maonesho ya Utalii ya Kimataifa ya Karibu/Kili Fair 2018 katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika mjini Moshi.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi, Maliasili na Utalii na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Nape Nnauye na viongozi wengine wa Serikali na sekta binafsi wakiwa kwenye eneo la mfano wa kilele cha Uhuru cha mlima Kilimanjaro baada ya kuzindua Maonesho ya Utalii ya Kimataifa ya Karibu/Kili Fair 2018 katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika mjini Moshi. 
Waziri Kigwangalla akisalimia baadhi waoneshaji katika banda la utalii wa kiutamaduni kwenye maonesho hayo.
Waziri Kigwangalla akiangalia moja ya gari la kitalii la wazi katika maonesho hayo.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla akikagua moja ya gari maalum la kusafirisha watalii ambalo limebuniwa hapa nchini na kampuni ya Hanspaul Automechs Ltd ya Jijini Arusha baada ya kufungua Maonesho ya Utalii ya Kimataifa ya Karibu/Kili Fair 2018 katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika mjini Moshi mwishoni mwa wiki. Kulia ni Mkurugenzi mkuu wa Kampuni hiyo, Satbir Singh Hanspaul.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla akiwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi, Maliasili na Utalii na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Nape Nnauye (kulia) kwenye moja gari maalum la kifahari la kusafirisha watalii ambalo limebuniwa hapa nchini na kampuni ya Hanspaul Automechs Ltd ya Jijini Arusha baada ya kufungua Maonesho ya Utalii ya Kimataifa ya Karibu/Kili Fair 2018 katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika mjini Moshi.
Waziri Kigwangalla akipanda gari maalum la kusafirisha watalii katika maonyesho hayo.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Bodi ya Utalii Tanzania, Jaji Mstaafu Thomas, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Aloyce Nzuki na Mkurugenzi wa Idara ya Utalii wa wizara hiyo, Deogratious Mdamu wakiwa ndani ya gari hilo maalum la kusafirisha watalii kwenye maonyesho hayo.
Waziri Kigwangalla akiwa amejilaza kwenye moja ya kitanda maalum katika hema la kitalii katika maonesho hayo. 
Waziri Kigwangalla akiteta jambo na Naibu Balozi wa Ujerumani hapa nchini, Jorg Herera katika moja ya chumba maalum cha wazi cha kitalii katika maonesho hayo.
Waziri Kigwangalla, Naibu Balozi wa Ujerumani hapa nchini, Jorg Herera na viongozi wengine wakishuka kutoka kwenye chumba hicho cha wazi cha kitalii katika maonesho hayo.
Waziri Kigwangalla akiwa kwenye banda la Bodi ya Utalii na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa bodi hiyo, Jaji Mstaafu Thomas Mihayo (kushoto), Mkurugenzi wa Bodi hiyo, Devotha Mdachi (wa pili kushoto), wafanyakazi wa bodi hiyo na Mkurugenzi wa Kampuni ya Kilifair Promotion Tom Kunkler.
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla akishiriki kupekecha mti maalum uliokuwa ukitumika enzi za mababu kwa ajili ya kufua moto katika Maonesho ya Utalii ya Kimataifa ya Karibu/Kili Fair 2018 yanayoendelea katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika mjini Moshi.Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge Ardhi, Maliasili na Utalii na Mbunge wa Jimbo la Mtama, Nape Nnauye (kulia) na Mbunge wa Jimbo la Longido, Dkt. Steven Kiruswa (wa pili kulia) wakishiriki kucheza ngoma za kimasai na kikundi cha ngoma cha kabila hilo baada ya kuzindua Maonesho ya Utalii ya Kimataifa ya Karibu/Kili Fair 2018 katika uwanja wa Chuo Kikuu cha Ushirika mjini Moshi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.