Habari za Punde

Naibu Waziri wa (O R- TAMISEMI) Mhe. Josephat Kadenge Aagiza Kituo cha Afya Lubanda Kikamilike Kwa Wakati.

Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI) Josephat Kandege akisaini kitabu cha wageni ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Songwe kabla ya kuanza ziara ya kikazi kukagua ujenzi wa Vituo vya afya.
Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI) Josephat Kandege (aliyevaa koti jeupe) akitoka kukagua ujenzi wa kituo cha Afya cha Lubanda kinachoonekana  nyuma yake na kuhimiza ujenzi wa kituo hicho ukamilike kwa wakati uliopangwa.

Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI) Josephat Kandege jana amefanya ziara ya kikazi Wilaya ya Ileje kukagua ujenzi wa kituo cha Afya cha Lubanda na kuagiza ujenzi wa kituo hicho ukamilike kwa wakati uliopangwa.
Kandege amesema uwepo wa mvua nyingi ambazo huanza mapema katika wilaya hiyo utakwamisha kituo hicho kukamilika mapema endapo hawatautumia muda huu ambao hauna mvua kumalizia ujenzi kwa haraka.
“Ninaamini kama isingekuwa mvua nyingi kunyesha pamoja na kuharibika kwa barabara nimatumaini yangu ujenzi wa kituo hiki cha Afya ungekuwa umekamilika, sasa jitahidini kumaliza haraka kabla ya mvua kuanza, ili mradi huu ukamilike na uanze kuwanufaisha wananchi wa Lubanda na maeneo ya jirani”, amesisitiza Kandege.
Aidha amemuelekeza Mganga Mkuu wa Wilaya ya Ileje Enock Mwambalaswa kubana matumizi ya fedha zilizotolewa kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho ili fedha zitakazobaki zitumike kumalizia jengo  la wazazi na wagonjwa wa nje ambalo lilianza kujengwa kwa nguvu za wananchi pamoja na kujenga nyumba nyingine za watumishi.
Kandege amemuelekeza pia Mhandisi wa Halmashauri ya Ileje kuangalia uwezekano wa kuunganisha wodi ya wazazi na chumba cha upasuaji ili kuendana na ramani mpya za vituo vya afya, aidha ameelekeza utaratibu wa kufikisha umeme kituoni hapo hasa kupita mpango wa REA uanze kufanyika haraka.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Ileje Haji Mnasi amemueleza Naibu Waziri OR TAMISEMI Josephat Kandege kuwa halmashauri ilipokea shilingi milioni mia tano kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha Afya cha Lubanda na mpaka sasa ujenzi umefikia asilimia 95 na matarajio ni kuwa kituo hicho kitakamilika ifikapo Julai 25, 2018.
Mnasi amemshukuru Naibu Waziri Kandege kwa kufanya ziara ya kukagua kituo hicho na amemuhakikishia kuwa atazingatia maelekezo ya kuwapangia watumishi wapya wa sekta ya afya watakaoajiriwa hivi sasa katika vituo vya afya vinavyojengwa ili vitoe huduma kwa wananchi mara baada ya kukamilika.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.