Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Aupongeza Uongozi na Wafanyakazi Wote wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Kwa Mashirikiano Yao.na Utendaji Mzuri wa Kazi.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameupongeza uongozi na wafanyakazi wote wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa utendaji mzuri wa kazi zao zinazopelekea kujenga taswira nzuri ya Ofisi hiyo kwa jamii.

Dk. Shein  aliyasema hayo leo, Ikulu mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi wakati ulipowasilisha Utekelezaji wa Mpango Kazi wa Mwaka 2017/2018, na Mpango Kazi wa Utekelezaji kwa mwaka 2018/2019, Ofisi ambayo imefunga dimba mikutano ya kukutana na Wizara zote za SMZ iliyoanza Juni 25 mwaka huu.

Rais Dk. Shein alitoa pongezi za dhati kutoka ndani ya nafsi yake kwa uongozi na wafanyakazi wote wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa mashirikiano yao na utendaji mzuri wa kazi zao hatua inayompelekea kuendelea kufanya kazi zake vyema za kuwatumikia wananchi kwa ufanisi.

Alieleza kuwa uwasilishwaji mzuri wa Mpango Kazi wa Ofisi hiyo umetokana na uzoefu wa muda mrefu uliopatikana tokea kuanza kwa zoezi hilo la Bango Kitita ambalo lilianza mara tu alipoingia madarakani na kuendelea hadi hivi leo na kuipongeza Ofisi hiyo kwa kutekeleza vyema Mpango Kazi wake huo.

Dk. Shein alitumia fursa  hiyo kumpongeza Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Ussi Haji Gavu kwa kumsaidia katika shughuli mbali mbali za kazi na kumpongeza Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee kwa utendaji wake mzuri wa kazi sambamba na mashirikiano mazuri anayompa.

Aidha, Dk. Shein aliwashukuru na kuwapongeza Washauri wake wote kwa kuendelea kumshauri mambo mbali mbali ya msingi na kutoa nasaha kwa uongozi wa Ofisi hiyo huku akiwataka kuwa wasikilizaji wa wananchi ikiwa ni pamoja na kuwasikiliza wale wote wanaowaongoza pamoja na wananchi wengine katika jamii.

“Nimeshuhudia uwezo mkubwa mlionao wafanyakazi wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na nimethibitisha hili kwa kufuata ule msemo usemao  ukitaka kuwajua wafanya kazi wa Ikulu wape kazi”,alisema Rais Dk. Shein.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuzipongeza  Wizara nyengine zote zilizowasilisha Mpango kazi wao kwa kufanya vizuri kazi hiyo na kuonesha mafanikio makubwa jambo ambalo limeendelea kumpa moyo katika kuhakikisha malengo yaliokusudiwa yanafikiwa.  

Dk. Shein aliueleza uongozi wa Ofisi hiyo ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kuwa  katika kuongoza ni lazima kuwepo na mashirikiano ili ufanisi uweze kupatikana hivyo ni vyema wakaimarisha mashirikiano waliyonayo kwa lengo la kupata ufanisi huo.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alisisitiza haja ya viongozi kusimamia vyema majukumu yao na kuwajibika ili kutela ufanisi zaidi huku akieleza umuhimu wa kufanya utafiti jambo ambalo ni muhimu katika utendaji wa kazi huku akisisitiza haja ya kiongozi kuwa mbunifu.

Aidha, Dk. Shein alieleza haja ya kuwepo mpango wa masomo kwa muda mrefu na muda mfupi  kwa watendaji wa Ofisi hiyo na kusisitiza kuwapangia nafasi za kazi walizozisomea mara baada ya kuhitimu masomo yao huku akieleza umuhimu wa kuwepo kwa Kamati ya Mafunzo ndani ya Wizara ili kurahisisha shughuli hizo.

Kwa upande wa Wazanzibari wanaoishi nje ya nchi yaani Diaspora, Rais Dk. Shein alieleza kuwa hatua kubwa zimefikiwa katika kutekeleza dhamira hiyo kwa upande wa Zanzibar.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliupongeza uwasilishaji Mpango Kazi na utekelezaji mzuri uliowasilishwa na Ofisi hiyo huku akieleza lengo kuu la zoezi hilo ni kupanga kwa ajili ya kuona mbele na kutoa wito kwa kila kiongozi kujua wajibu na majukumu yake.

Dk. Mzee aliwapongeza watendaji wa Ofisi hiyo kwa kufanya kazi kwa kasi na ari kubwa na kuwataka kuendelea kuwa mfano mzuri na kuwa kioo kwa jamii pamoja na kwa watendaji wengine wa Serikali huku akimpongeza Dk. Shein kwa niaba ya Wafanyakazi wote wa Ofisi hiyo kutokana na kujifunza mambo mengi kutoka kwake.

Mapema Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Ussi Haji Gavu akisoma utangulizia wa Mpango kazi wa Ofisi hiyo alitoa shukurani za dhati kwa Rais Dk. Shein kwa kuendeleza utaratibu wa kukutana na watendaji wa Mawizara ili kuwasilisha kwake taarifa za utekelezaji wa Mpango Kazi.  

Waziri Gavu alielezea kuwa uwasilishaji huo wa taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kazi umekuwa dira katika kuonyesha na kuelekeza njia bora zaidi za utekelezaji wa majukumu  ya kila siku.

Alieleza kuwa katika programu ya kusimamia huduma na shughuli za Rais na kuimarisha Mawasiliano Ikulu,  shughuli za Rais zimefanyika vizuri na wananchi wameeleweshwa juu ya shughuli kadhaa za Serikali zikiwemo maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

Aliongeza kuwa kupitia ziara anazofanya Rais katika Mikoa yote ya Zanzibar, wananchi hupata fursa ya kuelezea changamoto zinazowakabili ambazo hutolewa ufafanuzi na Mawaziri wanaofuatana naye katika ziara hizo.

Vile vile, alieleza kuwa jarida la Ikulu pamoja na vipindi mbali mbali vya Redio na Televisheni vilitayarishwa na kurushwa hewani ambapo pia, mitandao ya kijamii na magazeti yalitumika katika kuwapatia taarifa wananchi na watu mbali mbali.

Pamoja na hayo, Waziri Gavu alieleza kuwa kupitia Programu ya Kuratibu Ushirikiano wa Kikanda, Mashirika ya Kimataifa na Wazanzibari Wanaoishi Nje ya Nchi, ushiriki wa Zanzibar umekuwa ni wenye tija katika Jumuiya za Mtangamano wa Kikanda za SADC, EAC,IORA na Jumuiya ya Utatu (EAC-SADC-COMESA).

Aidha, alieleza kuwa mahusiano mazuri yameimarika zaidi baina ya Serikali na Wazanzibari wanaoishi nje ya nchi yaani Diaspora ambapo Serikali imeendeleza dhamira yake ya kuwashajiisha Wanadiaspora kushiriki katika kuiletea Zanzibar maendeleo ya kiuchumi na kijamii kupitia Kongamano la Nne la Wanadiaspora.

 Nao Washauri wa Rais wa Zanzibar walimpongeza Rais Dk. Shein kwa juhudi kubwa alizozifanya katika kuipaisha Zanzibar kimaendeleo ikiwa ni pamoja na kutekeleza vyema Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 kwa vitendo.

Walieleza kuwa Zanzibar imeweza kupiga hatua kubwa katika kukuza uchumi wake sambamba na kupunguza umasikini.

Walimpongeza kwa kasi nzuri ya kuongoza nchi pamoja na juhudi zake  za kusisitiza na kuazisha suala zima la utafiti katika taasisi za Serikali huku wakieleza umuhimu wa watendaji wa Serikali kupelekwa katika vyuo vyenye sifa na vinavyotambulikana.

Mshauri wa Rais Ushirikiano wa Kimataifa na Uchumi Balozi Mohamed Ramia Abdiwawa  alieleza kuwepo kwa Kitengo cha kufuatilia maagizo na maelekezo ya Serikali ambacho tayari kimeshaanza  kazi na kutoa wito kwa uongozi wa Ofisi hiyo kumsaidia Waziri ili aweze kufanikisha malengo yaliokusudiwa na Kitengo hicho.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.