Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Autawa Uongozi wa ZSSF Kuwa Waadilifu Katika Kutumia Fedha za Mfuko.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein ameutaka uongozi wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF) kufanya kazi kwa uadilifu kwa kuyatekeleza maagizo ya Serikali katika ukodishaji nafasi za kufanyia biashara katika jengo la Jumba la Treni “Chawl” lililofanyiwa ukarabati mkubwa.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hafla ya ufunguzi wa jengo la Jumba la Treni “Chawl building”, lililopo Darajani Mjini Unguja, ambalo limefanyiwa ukarabati mkubwa na Srikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF).

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein aliutaka uongozi huo wa (ZSSF) kuwa wawazi, wasiwe na muhali na wala wasimpendelee mtu yeyote katika ukodishwaji wa nafasi za kufanyia biashara katika jumba hilo la maduka.

Rais Dk. Shein pia, alisisitiza haja kwa uongozi huo wa (ZSSF) kutofanyabiashra kirafiki wala kujuana kwani biashara ni heshima, hivyo ni vyema wakafanya biashara kwa lengo la kupata faida.

Aliongeza kuwa ni vyema watu wote wakazingatia kuwa nafasi na fursa zilizopo katika jengo hilo ni chache na kwa hivyo, haitowezekana kila mtu anayehitaji apewe sehemu ya kufanyia shughuli zake katika jengo hilo.

Alieleza matumaini ya Serikali kuwa kukamilika kwa mradi wa matengenezo ya nyumba ya treni kutachochea kasi ya ukuaji wa shughuli za biashara katika mji wa Zanzibar.

Dk. Shein aliwashangaa wale wote wanaokasirika na kununa wakati Serikali ikifanya mambo mazuri kwani lazima Serikali itekeleze mambo yake ikiwa ni pamoja na kujenga miundombinu yake ya kihistoria kwa madhumuni ya kuienzi historia ya Zanzibar.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa kuna baadhi ya miji mikubwa ulimwenguni nje ya Afrika, ambayo inasifika kwa usafi ukiwemo mji wa Singapore, Honolulu, Copenhagen, London, Geneva, Stockholm na mengineyo, hivyo ni vyema na mji wa Zanzibar ukafuata mkondo huo.


Alieleza kuwa hivyo, ni jambo la busara sana na Zanzibar ikaiga tabia ya kuvitunza vitu vyake katika hali zote ikiwemo usafi ili maeneo  yake nayo yasifike kwa kuwa na mazingira safi yanayovutia.

Alisisitiza suala la usafi kwa miji yote ya Unguja na Pemba na kueleza haja ya jengo hilo ya kulitunza na kuliweka katika hali ya usafi ili lizidi kudumu kwa miaka mengine 200 ijayo.

Akitoa historia fupi ya jumba hilo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa Jumba hilo ambalo kwa lugha ya Kiengereza linaitwa “Chawl Building” ambalo neno Chawl linatokana na moja ya lugha za Kihidni inayoutwa Marati (Marathi) ambayo inazungumza na takriban watu 68 milioni wa Mashariki ya India.

Alisema kuwa historia inaeleza kuwa majengo kama hayo yalianza kujengwa mwishoni mwa karne 18 kuingia 19 ambayo ni majengo marefu yanayofikia ghorofa 4 mpaka 5 ambapo wka upande wa Zanzibar jumba hilo lilijengwa mnamo mwaka 1880.

Kwa mujibu wa Maelezo ya Dk. Shein aliyejenga Jumba hilo alikuwa ni mtawala wa Kisultani wa Zanzibar aliyeitwa Barghash bin Said ambalo alijenga kwa dhamira ya kwua chanzo cha kuzalisha mapato katika kuanzisha na kuendeleza mradi wa maji  safi na salama ndani ya mji wa Zanzibar.

Aliongeza kuwa kodi zilizokusanywa kutokana na jumba hilo ndizo zilizokamilisha miundombinu ya maji safi na salama katika mji mkuu wa Zanzibar, lakini miundombinu hiyo haikutosheleza kusambaza maji kwa mahitaji ya sehemu zote za Unguja.

Kuhusu ujenzi wa maduka ya kisasa katika eneo la Darajani kwenye mradi uliopewa jina la “Darajani Corridor”, Dk. Shein alieleza kuwa inayochelewesha sio Serikali bali ni Shirika la UNESCO kutokana na taratibu za Mamlaka ya miji mikongwe duniani lakini alieleza kuwa hata hivyo wapo baadhi ya watu kutoka Zanzibar ambao walipeleka fitna juu ya ujenzi wa sehemu hiyo huko UNESCO.

Dk. Shein alieleza kuwa hata hivyo, ujenzi wake upo pale pale ambapo mradi huo utatekelezwa baada ya kupokea maoni ya UNESCO ambayo yanategemewa yataletwa baada ya Serikali kuwasilisha kwao maelekezo waliyoyatoa takriban miaezi sita iliyopita na kueleza matarajio yake juu ya ujenzi huo kuanza mara tu kukamilika mipango hiyo, hivyo aliwataka wananchi kuendelea kuwa wavumilivu na lolote litakalokuwa watajuulishwa.

Kwa upande wa Skuli ya Darajani, Dk. Shein alisema kuwa skuli hiyo haitovunjwa kama wanavyoeleza watu wasiojua ukweli na badala yake jengo hilo litatumika kwa ajili ya matumizi mengine na wanafunzi wake watahamishiwa katika skuli mpya inayojengwa huko Rahaleo pamoja na wale wa skuli ya Vikokotoni ambao jengo lao hilo la skuli litavunjwa kwani halimo katika historia na wao pia watahamia Rahaleo.

Akieleza kuhusu ujenzi wa maduka makubwa “Shopping Malls” katika eneo la Michenzani nao upo pale pale ambapo Taasisi ya Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (ZSSF) ndio utakaojenga maduka hayo ambapo ujenzi wake hauna muda mrefu utaanza.
Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kwa kuwashukuru na kuwapongeza wananchi kwa kustahamili wakati wote wa ujenzi wakiwemo wale wote waliokuwa wakiishi na kufanya biashara katika Jumba hilo na kuipongeza Kampuni ya ujenzi ya CRJE East Afrika, wakandarasi wasadidi, Mshaidizi Ujenzi Kampuni ya CONS Africa na wengineo.

Aliipongeza (ZSSF),Bodi yake kwa kuyawezesha kwa ufanisi matengenezo ya jengo hilo na kuupongeza uongozi wa Wizara ya Fedha na Mipango kwa usimamizi wao mzuri wa kuhakikisha ujenzi huo unakamilika.

Nae Waziri Fedha na Mipango Dk. Khalid Salum Mohamed alitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa Rais Dk. Shein kwa ushauri wake, maelekezo na usimamizi sambamba na utekelezaji wake wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM katika kuhakikisha ahadi za ujenzi wa jengo hilo inatekelezwa.

Alisema kuwa dhamira ya Rais Dk. Shein ni kuhakikisha mji wa Zanzibar unarejea kwenye haiba yake na unaendelea kuwa kivutio kwa wageni na wenyeji wa Zanzibar.

Katika maelezo yake Dk. Khalia alieleza miradi mbali mbali ambayo imetekelezwa na mengine inaendelea kutekelezwa katika uongozi wa Ras Dk. Shein ambayo imeleta faida kuwa kwa ile ambayo imeshatekelezwa ukiwemo mradi wa ZUSP katika mji wa Unguja na Pemba huku akieleza azma ya kuutengeza mji mpya katika maeneo ya Chumbuni na Kwahani mjini Unguja.

Pamoja na hayo, alieleza hatua za ujenzi wa hoteli ya Bwawani ambao utaanza hivi karibuni pamoja na ujenzi wa jaa la kisasa katika maeneo ya Kibele, Mkoa wa Kusini Unguja.

Mapema Mkurugenzi Mwendeshaji wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF) Sabra Issa Machano alieleza kuwa ujenzi wa Jumba hilo hadi kumalizika kwake umegharimu TZS Bilioni 11.5.

Aliongeza kuwa Jumba hilo lina milango ya maduka ya biashara 52, sehemu ya IT, eneo la kusalia kwa wanawake, nyumba 10 za kuishi, mkahawa, sehemu ya mazoezi, duka la mahitaji mbali mbali ‘supermarket’ ambapo pia, jengo hilo limezingatia watu wenye mahitaji maalum pamoja na lifti kwa ajili ya kuwafikisha wananchi sehemu walinazokusudia.

Alisisitiza kuwa katika malengo hayo ni katika kuhakikisha mahitaji yanapatikana kiuchumi, kijamii na kiuchumi na kueleza kuwa ndani ya miaka 10 fedha za ujenzi huo Serikali itajilipa huku akitumia fursa hiyo kwa kupongeza Rais Dk. Shein kwa uwamuzi wake wa kulikarabati jengo hilo.


Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.