Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, Azindua Programu ya Pamoja ya Zanzibar na UN.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt Ali Mohamed Shein na Mkurugenzi Mkaazi wa UN Tanzania Mr. Alvaro Rodriguez wakipiga makofi baada ya kuondoa kipazia katika Bunner ya Uzinduzi wa Programu ya Pamoja na Zanzibar katika Kuwaendeleza Wajasiriamali na Wakulima Wanawake wa Mwani Zanzibar na Vijana, Hafla hiyo ya Uzinduzi imefanyika katika Ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdulwakil Kikwajuni Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na wananchi wake inatambua mchango mkubwa wa Umoja wa Mataifa (UN) pamoja na Mashirika yake katika kuimarisha maendeleo endelevu ya Zanzibar.

Dk. Shein aliyasema hayo leo katika uzinduzi wa “Programu ya Pamoja ya Zanzibar” (ZIP), hafla iliyofanyika huko katika ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil, Kikwajuni Mjini Zanzibar ambayo ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd.

Katika hotuba yake, Rais Dk Shein alisema kuwa program hiyo sio tu itasaidia kuimarisha maendeleo ya Zanzibar bali itasaidia sana katika kufikia malengo ya maendeleo yaliyowekwa na Umoja wa Mataifa (UN).

Rais Dk. Shein alisema kwamba, malengo ya Mashirika ya Umoja wa Mataifa kwa Zanzibar yako wazi katika kila sekta na yanafahamika kwa wananchi wote wa Zanzibar jinsi yalivyolenga katika kuimarisha sekta za maendeleo.

Alisema kuwa UN imekuwa ikifanya kazi na kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali  za maendeleo ikiwemo elimu, afya, upatikanaji wa maji safi na salama, utawala bora, uimarishaji wa haki za binaadamu, uwezeshaji, mapambano ya udhalilishaji wa kijinsia pamoja na uhifadhi wa mazingira.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa Mashirika ya Umoja wa Mataifa (UN) kwa mashirikiano inayotoa katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo hapa Zanzibar.

Alisema kuwa programu ya pamoja inalenga zaidi kushirikiana na Serikali katika kupunguza vifo vya uzazi, ukatili dhidi ya wanawake na watoto, uwezeshaji wa kiuchumi kwa wanawake kupitia zao la mwani pamoja na uratibu wa utekelezaji wa malengo ya dunia.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein aliongeza kuwa programu hiyo itasaidia zaidi kuimarisha uhusiano uliopo pamoja na kuiwezesha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kufikia malengo yake ya maendeleo ya muda mrefu na muda mfupi uliojiwekea.

Dk. Shein aliuhakikishia Umoja wa Mataifa (UN) kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itahakikisha kuwa kila sekta inayohusika katika utekelezaji wa mpango huo inatekeleza majukumu yake ipasavyo.

Aidha, Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itahakikisha kwamba kwa pamoja inazifanyia kazi changamoto mbali mbali zinazoweza kujitokeza katika programu hiyo mpya.

Aliongeza kuwa Serikali kwa kushirikiana na Mashirika ya UN itatumia uzoefu ulionao katika  kutekeleza programu na miradi mbali mbali iliyofanywa hapo siku za nyuma baina ya Serikali na Mashirika hayo ili kutekeleza vyema progamu hiyo.

Katika hotuba yake hiyo, Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya wafanyakazi kuleta mabadiliko ya fikra na mawazo na kuacha kufanya kazi kwa mazoea kama anavyosisitiza mara zote ili kuweza kuifanikisha progamu hiyo kwa ufanisi mkubwa.

Rais Dk. Shein alitilia mkazo haja ya kuwa wabunifu katika kubuni na kutekeleza miradi ya maendeleo yenye tija na inayokwenda sambamba na mazingira pamoja na mahitaji halisi ya wananchi wa Zanzibar badala ya kusubiri wataalamu kutoka nje waje kubuni miradi kwa ajili ya Zanzibar.

Alisisitiza kuwa Zanzibar kwa kuweza kubuni miradi yake wenyewe itakuwa ni rahisi kwa Umoja wa Mataifa kutoa ushirikiano wake kwa Zanzibar kwa kuzingatia mipango na mahitaji yaliyopo.

Dk. Shein alisisitiza umhimu wa ushirikiano baina ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, sekta binafsi na asasi za kiraia katika utekelezaji wa miradi mbali mbali inayotekelezwa na mashirika ya Umoja wa Mataifa kwa kuzingatia kwamba mashirikiano ya pamoja yanahitajika.    

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alisisitiza umuhimu wa kuwepo suala zima la uwajibikaji, uwazi pamoja na kujidhatiti katika kufikia malengo yaliyowekwa.
Nae
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.