RISALA YA MWENYEKITI WA TUME YA
TAIFA YA UCHAGUZI MHE. JAJI (R) SEMISTOCLES S. KAIJAGE KUHUSU UPIGAJI KURA
KATIKA UCHAGUZI MDOGO WA UBUNGE KATIKA JIMBO LA BUYUNGU NA UDIWANI KATIKA KATA THELATHINI
NA SITA (36) TANZANIA BARA
TAREHE 12 AGOSTI, 2018
Ndugu
Wananchi;
Awali
ya yote, kwa niaba ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi nachukua fursa hii kuvipongeza
Vyama vya Siasa vilivyojitokeza kushiriki uchaguzi huu mdogo kwa kuwadhamini
Wagombea waliochukuwa fomu na hatimaye kuteuliwa kuwania nafasi hizo zilizo wazi
za Ubunge na Udiwani.
Nitumie
nafasi hii pia kuwapongeza wananchi wote katika Jimbo
la Buyungu na Kata Thelathini na Sita (36) zinazohusika na uchaguzi huu, kwa
utulivu mliouonyesha wakati wote wa kipindi cha Kampeni.
Ndugu
Wananchi;
Kesho
Jumapili tarehe 12 Agosti, 2018, ni Siku ya kupiga kura katika Uchaguzi Mdogo
wa Ubunge wa Jimbo la Buyungu katika Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko Mkoani Kigoma.
Vile vile, Uchaguzi mdogo wa Madiwani
katika Kata Thelathini na Sita (36) zilizopo katika Halmashauri 29, za mikoa 19,
ya Tanzania Bara. Uchaguzi huu Mdogo wa Ubunge na Udiwani Tanzania Bara, utahusisha jumla ya Wapiga Kura 485,203
walioandikishwa katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na kutakuwa na Vituo vya Kupigia Kura 1,314.
Ndugu
Wananchi;
Tume ya
Taifa ya Uchaguzi inapenda kutumia nafasi hii kuwakumbusha wapiga kura wa Jimbo
la Buyungu na kata zote zitakazoshiriki Uchaguzi
huu kuzingatia mambo muhimu yafuatayo:-
i)
Mosi, Upigaji kura utafanyika katika
vituo vile vile vilivyotumika wakati wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 na vitafunguliwa
saa moja kamili (1:00) asubuhi na kufungwa saa kumi kamili (10:00) jioni. Iwapo, wakati wa kufunga kituo watakuwepo wapiga
kura katika mstari ambao wamefika kabla ya saa kumi jioni na hawajapiga kura,
wataruhusiwa kupiga kura. Mtu yeyote
hataruhusiwa kujiunga katika mstari wa wapiga kura baada ya saa kumi kamili (10:00)
jioni.
ii)
Pili, watakaoruhusiwa kupiga kura ni
wale tu ambao wamo kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwenye Jimbo au Kata
husika na wana kadi ya mpiga kura. Hata hivyo, Tume kwa kuzingatia masharti ya kifungu
cha 61(3) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, pamoja na kifungu cha 62(1) cha
Sheria ya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa,
imeruhusu wapiga kura ambao ama kwa bahati mbaya wamepoteza kadi zao za kupigia
kura au zimeharibika au zimechakaa watumie mojawapo ya vitambulisho vifuatavyo;
wanaweza kutumia Pasi ya Kusafiria, Leseni ya Udereva au Kitambulisho cha Uraia
kinachotolewa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA).
iii)
Tatu, mpiga kura aliyepoteza kadi
yake ya kupigia kura au kadi hiyo kuharibika au kuchakaa ataweza kuruhusiwa
kutumia Vitambulisho hivyo mbadala, iwapo tu; atakuwa aliandikishwa kwenye
Daftari la Kudumu la Wapiga Kura mwaka 2015, jina lake liwe katika orodha ya
Wapiga Kura katika kituo anachokwenda kupiga Kura na majina yake yaliyopo
katika Daftari la Mpiga Kura yafanane kwa herufi, maneno na tarakimu na majina
yaliyopo katika kitambulisho mbadala.
iv)
Nne, katika zoezi la upigaji kura,
na kwa kadri itakavyowezekana kipaumbele kitatolewa kwa wagonjwa, watu wenye
ulemavu wa aina mbalimbali, wanawake wajawazito au wenye watoto wachanga, na wazee.
v)
Tano, mpiga Kura mwenye ulemavu wa
kutoona, ataruhusiwa kwenda kituoni na mtu atakayemchagua mwenyewe kwa ajili ya
kumsaidia kupiga kura yake.
vi)
Sita, ni wajibu wa Vyama vya Siasa
vinavyoshiriki katika uchaguzi kuweka Mawakala katika vituo vyote vya Kupigia
na Kujumlishia Kura kwa utaratibu ambao tulikubaliana wakati wa Mkutano wa Tume
na Vyama vya Siasa tarehe 10/07/2018 uliofanyika katika ukumbi wa Kimataifa wa
Mikutano wa Mwalimu Nyerere Jijini Dar es Salaam, na nakala ya utaratibu huo
kutumwa kwa Wasimamizi wa Uchaguzi.
vii)
Saba, mawakala hao wanaruhusiwa
kuwepo katika Vituo vya Kupigia Kura na wanatakiwa kufuata na kuzingatia Sheria,
Kanuni na taratibu zinazoongoza Uchaguzi katika kipindi chote cha kupiga, kuhesabu
na kujumlisha kura na kutangaza matokeo.
Pamoja
na kuwakumbusha mambo machache yanayopaswa kufanywa na kufuatwa siku ya
Uchaguzi, Tume pia inapenda kusisitiza mambo yafuatayo:-
Kwanza, mwisho wa mikutano ya kampeni
ni leo saa kumi na mbili kamili (12:00) jioni. Baada ya muda huo, Vyama, wagombea
na mashabiki wasifanye kampeni za aina yoyote, kama vile kutumia alama za Vyama
zinazoashiria kampeni, vipeperushi, bendera, mavazi n.k kwa kuwa kesho ni siku
ya Uchaguzi. Aidha, wananchi waheshimu Sheria
za Nchi wakati wote wa upigaji, kuhesabu, kujumlisha kura na kutangaza matokeo.
Pili, pale panapokuwa na malalamiko
yoyote ya ukiukwaji wa Sheria na Taratibu za Uchaguzi, malalamiko hayo yafikishwe
kwenye mamlaka inayohusika kwa utaratibu uliowekwa kwa mujibu wa Sheria. Vivyo
hivyo, Viongozi wa Vyama vya Siasa, Wagombea au wafuasi wao na wananchi kwa
ujumla wajiepushe na vitendo vinavyoweza kusababisha fujo au vurugu katika
vituo vya Kupigia, Kuhesabia na Kujumlishia Kura.
Tatu, kwa kuzingatia tafsiri sahihi ya Kifungu cha 104 (1) kikisomwa pamoja
na Kifungu cha 72(1) cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi iliyotolewa na Mahakama Kuu
ya Tanzania kwenye Shauri la Madai Anuai (Misc. Civil Cause No. 37 la mwaka
2015) mpiga kura anatakiwa kuondoka kituoni na kwenye maeneo ya kituo cha
kupigia kura mara baada ya kupiga kura yake. Aidha, mbali ya wale ambao Sheria
za Uchaguzi zinawaruhusu kuingia na kuwepo kwenye Vituo vya kupigia kura, wananchi
wanatakiwa kujiepusha na mikusanyiko au mikutano katika maeneo ya Vituo vya
kupigia kura. Vyama vya Siasa vimeweka mawakala vituoni ambao watalinda maslahi
ya vyama husika na wagombea wao.
Nne, wanaoruhusiwa kuingia kwenye Vituo vya kupigia, kuhesabia na
kujumlishia kura ni wale tu walioainishwa kwenye kifungu cha 72(1) cha Sheria
ya Taifa ya Uchaguzi na kifungu cha 63(2) cha Sheria ya Uchaguzi wa Serikali za
Mitaa.
Tano, Vyama vya Siasa, Wagombea, Wananchi na Watendaji wa Uchaguzi kwa
ujumla wanakumbushwa kuzingatia na kuheshimu matakwa na masharti ya Sheria za
Uchaguzi, Sheria za Nchi na Maadili ya Uchaguzi wakati wa Upigaji Kura, Kuhesabu,
Kujumlisha hesabu za Kura, na Kutangaza matokeo.
Ndugu
Wananchi;
Kwa
kumalizia, Tume ya Taifa ya Uchaguzi inawasihi tena Wapiga Kura wote
waliojiandikisha kwenye Daftari la Kudumu la Wapiga Kura na wanaoishi kwenye
maeneo yanayofanya Uchaguzi Mdogo, kujitokeza kwa wingi kupiga kura ili
kuwachagua Viongozi wanaowataka wawaongoze kwa kipindi cha takribani miaka miwili
ijayo. Wananchi wafanye na kutekeleza
zoezi la kuwachagua wawakilishi wao bila hofu, woga, wasiwasi au ushawishi
kwani chini ya Kanuni ya 3.1 (b) ya Maadili ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na
Madiwani ya mwaka 2015, Serikali imepewa wajibu wa kuhakikisha kuwa kuna hali ya
usalama, amani na utulivu katika kipindi chote cha Uchaguzi.
Ni
matumaini ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuwa, hali ya Amani na Utulivu kwenye maeneo ya Uchaguzi ambayo imekuwepo hadi hivi
sasa, itaendelea kudumishwa ili kuhakikisha Uchaguzi huu mdogo unafanyika na
kumalizika salama kwa Ustawi wa Taifa letu.
Aidha,
kila Mwananchi, Vyama vya Siasa na wadau wote wa uchaguzi tushirikiane, ili
kuhakikisha kuwa viashiria vya kuvunjika kwa amani na utulivu vinaepukwa ili uchaguzi
utakaofanyika uwe huru, wazi na wa haki.
KUMBUKA, KUPIGA KURA NI HAKI YAKO YA MSINGI
KWA MUSTAKABALI WAKO NA WA NCHI YAKO,
NENDA UKAPIGE KURA.
MUNGU
IBARIKI TANZANIA.
Ahsanteni kwa kunisikiliza.
No comments:
Post a Comment