Habari za Punde

Maadhimisho ya kimataifa ya siku ya kujua kusoma na kuandika



NA ABDI SHAMNAH

Jamii yakumbushwa umuhimu wa kusoma vitabu

L  Huduma za maktaba zina mchango mkubwa kitaaluma

ILIKUWA ni asubuhi tulivu, jua likiwaka bila kuathiri shughuli za kibinadamu, huku pepo mwanana za bahari zikivuma na kupunguza makali ya  joto, ambalo yumkini tayari limeanza kuvinyemelea visiwa vya Zanzibar.

Shamra shamra, chereko chereko, nderemo na hoi hoi zilihanikiza katika viunga vya Ofisi za Shirika la Hudma Maktaba, ziliopo Maisara, kuashiria kuna jambo kubwa linalojiri.

Hakika ilikuwa ni tukio la kihistoria, ni muendelezo wa matukio yanayojiri takriban kila mwaka, kwani kilichofanyika viwanjani hapo kililenga kumuelekeza, kumfahamisha na kumtanabahisha Mzanzibari, juu ya umuhimu wa kutumia huduma za maktaba.

KUANZISHWA HUDUMA ZA MAKTABA ZANZIBAR

Mnamo miaka ya 1980, Huduma za Maktaba zilianzishwa rasmi hapa Zanzibar, na ilipofika mwaka 1993 Baraza la Wawakilishi likapitisha Sheria Nam.7 ya 1983 uanzishaji wa Bodi ya Huduma za Maktaba (ZLSB).
Aidha, mnamo mwaka 2009, huduma hizo ambapo kabla zilikuwa katika Jengo Serena, Shangani mjini hapa,  zikahamishiwa katika jengo jipya na la kisasa Zaidi liliopo Maisara.

Lengo likiwa ni kuwa na taasisi inayotowa huduma bora za kimaktaba mijini na vijijini , ili wanafunzi wa nagzi zote pamoja na jamii kwa ujumla , ipate huduma hizo na kujifunza bila malipo,  ili hatimae kuwa na kizazi kilichoelimika.
Katika makala hii, mwandishi anangalia vipi Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kupitia Shirika la Huduma za Maktaba lilivyoungana na jumuiya ya kimataifa, kuadhimisha siku hii   muhimu  na adhimu kwa lengo la kuhakikisha jamii ya Wazanzibari inahamasika katika matumizi bora ya huduma za maktaba.

YALIYOJIRI KATIKA MAADHIMISHO

Maadhimisho yam waka huu yalitanguliwa na maandamo yaliyoongozwa na watoto wanaotumia huduma za maktaba, wakiwa na mabango yenye kaulimbiu inayosomeka ‘kusoma na kuendeleza ujuzi’.

 Aidha,  yalipambwa kwa aina tofauti za maonyesho, ikiwemo yale ya  vitabu , usomaji wa tenzi, nyimbo  na onyesho maalum la ‘English-Debate’, ambapo kundi moja la wanafunzi kwa mtazamo wao wanahisi lililo  bora kwao katika matumizi ya vita bu ni kurudufu nakala za vitabu (kutowa kopi), huku kundi jingine likisisitiza umuhimu wa kununua vitabu, kama njia sahihi ya kufikia azma  ya kujifunza.

Hata hivyo, kupitia onyesho hilo lililoendeshwa kwa lugha ya kiingereza, ufumbuzi sahihi ukafikiwa kuwa njia ilio bora ni ‘kwenda maktaba pekee, mahala ambapo huduma za vitabu, majarida, magazeti na machapisho mengine hupatikana na mtu kujisomea bila malipo’.

Suluhisho hilo likabainishwa kwa hoja, kuwa utaratibu wa  kutowa kopi nakala za vitabu una changamoto zake, ikiwemo Haki miliki ya muandishi, jambo ambalo lapaswa kufanyika kwa ridhaa ya muandishi. Lakini pia hoja  ya kununua vitabu vipya, nayo ikabainishwa changamoto zake ikiwemo ya kuwa na uwezo wa kutosha kwa maana ya fedha nyingi, kwa kuzingatiwa  muhusika atakuwa na mahitaji ya vitabu zaidi ya kimoja.

Kuambatana na onyesho hilo ufafanuzi ukatolewa kuwa Huduma za Maktaba hutolewa bure kituo hapo, ambapo kimsingi kinachohitajika ni kujisajili.

Imeelezwa kuwa kwa mwanafunzi wa skuli ya msingi itamlazimu kulipia shilingi 1,000/-, mwanafunzi wa Sekondari shilingi 3,000/- na kwa wale walioko  Vyuo vikuu wanahitajika kulipia shilingi 5,000, ambapo fursa kubwa watakayoipata ni pamoja na kujisomea vitabu hivyo nyumbani.

NASAHA ZA WADAU

Sichana Haji Foum ni Mkurugenzi wa Shirika la Huduma za Maktaba Zanzibar, anasema mkusanyiko huo unalenga kuwakutanisha wadau na kuwahamasiha umuhimu wa kupenda kusoma na kuandika.

Anabainisha kuwa Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa (UNESCO) mnamo mwaka 1965 lilibaini kuwepo kwa tatizo kubwa la watu kutokujua kusoma na kuandika, hivyo mnamo mwaka 1966 maadhimisho hayo yalianza.

Anasema lengo ni kutathmini mafanikio na changamoto zinazoikabili jamii katika kufanikisha dhana ya kujua kusoma na kuandika.

Aidha anasema  kwa vile Shirika la Huduma za Maktaba Zanzibar ni wadau, hivyo  kuna kila sababu za kujumuika na kuadhimisha siku hiyo.

Kwa mnasaba huo, analitolea pongezi Shirika la Book Aid International kutoka nchini Uingereza kwa misaada mbali mbali inayotowa kwa shirika hilo, ikiwemo uaptkanji wa vitabu, ambavyo hatimae husambazwa skuli mbali mbali Unguja na Pemba, ambapo nao huanzisha maktaba zao.

“Sio rahisi kwa wazazi kuwa na uwezo wa fedha za kutosha kununua vitabu kwa ajili ya wanafunzi, hivyo wenzetu hawa wamekuwa wakiondowa hiyo ‘gape’ iliopo  kati wenye  nacho na wasio nacho”, anasema.

Aidha, anasema ni jambo gumu kwa mwanafunzi au jamii kwa ujumla kujifunza iwapo haiwezi kusoma, na kubainisha kuwa wale wanaosoma wanakuwa katika nafasi nzuri ya kuendeleza ujuzi walionao.

“Iwe mwanafunzi, iwe mwalimu, iwe mkulima au jamii kwa jumla, shughuli zako utazifanya kwa ufanisi”, anaongeza.
Mkurugenzi Sichana akawakumbusha wadau, jinsi kitabu kitakatifu cha Qoraan kilivyokuja na kuhimiza umuhimu wa suala la kusoma, ikiwa ni njia ya kupanuwa wigo wa ufahamu kwa binadamu.

Akatowa wito kwa wadau wote kuishajiisha jamii kujenga utamaduni wa kupenda kusoma na kuandika, sambamba na kuzitumia kikamilikfu huduma za maktaba ili kujiongezea maarifa.

Nae, Mwalimu Ali mwalimu, Katibu wa Jumuiya ya Waandishi wa Vitabu Zanzibar, akabainisha shughuli zinazofanywa na jumuiya hiyo, kuwa ni pamoja na kuihamasisha jamii ya Wazanzibari na Watanzania kwa ujumla, umuhimu wa kusoma vitabu.

Anasema chanzo cha kuanzishwa Jumuiya hiyo kuliotokana na changamoto iliyokuwepo ya wananchi kutokuwa na utamaduni wa kupenda kusoma vitabu, hivyo kuundwa kwake kulilenga kumuamsha Mzanzibari  juu ya umuhimu wa jambo hilo.

Anasema, “kuanzia hapo tulianza kufanya juhudi za kuandika na ndio leo hii unakuta kuna vitavu vingi vilivyoandikwa na Wazanzibari”.

“Hivi sasa kuna umuhimu kwa wadau kukaa na kutafakari, kwani hali ya usomaji wa vitabu haiko vyema, hakuna utamaduni wa kusoma vitabu’, anasema.

Amewataka wadau walioshiriki katika maadhimisho hayo 
kutumia fursa hiyo kuishajiisha jamii kujenga utamaduni wa kusoma vitabu, akibainisha jinsi Jumuiya yake, ilivyojidhatiti katika jambo hilo, kwani ina kipindi maalum kupitia Shirika la Utangazaji Zanzibar( ZBC TV).

Anaedelea kuitanabahisha jamii kuwa suala la matumizi yaa huduma za mkataba, hayapo kwa ajili ya wanaafunzi pekee, bali ni kwa ajili ya watu wote.

Aidha, anashauri kuziunga mkono na kuziimarisha maktaba za skuli, kwa kigezo kuwa haziko vyema na zinakabiliwa na chanagmoto kadhaa, ikiwemo ukosefu wa vitabu, sambamba na maktaba za Wilaya ambazo bado hazijaanzishwa.

“Kuna maktaba za wananchi, ni mfano ule ule utakuta kwenye majumba yetu, mtu kaweka ‘shockest’ lake ukumbini, kuna vitu kadhaa vya thamani……..vikombe, visahani na vingine kadha wa kadha, lakini huwezi kukuta vitabu………”, anaonyesha mshangao.

Anasema kuna haja kwa skuli kuanzisha maktaba zao ili wanafunzi watumie fursa ya kujifunza kikamilifu.

Nae, Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Huduma za Maktaba 
Fatma Hassan Kingwaba, akaitanabahisha jamii juu ya thamani ya elimu na gharama zinazowakabili wazazi katika kufanikisha azma ya kuwapatia elimu bora watoto wao.

Anasema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kulifahamu hilo, imelazimika kuanzisha miundombinu ya elimu, ikiwemo Shirika la Huduma za Makatba, kwa lengo la kusaidia juhudi za wananchi/wazazi kuwapatia elimu watoto.

“Ninaiomba jamii ithamini juhudi za Serikali za kuanzisha huduma hizi za maktaba tofauti, ikiwemo za shule. Tujenge utamaduni wa kupenda kusoma vitabu, kuna vitabu vimetungwa na watunzi wetu; vimezingatia lugha, mila, silka na maadili yetu”, anafafanuwa.

Hudhaifa Haji ni Mkutubi katika Shirika la Huduma za Maktaba Zanzibar, anasema huduma hizo zinapatika kwa watu wa aina zote, ikiwemo wanafunzi wa skuli za msingi, sekondari, vyuo vikuu pamoja na wananchi wengineo.

Anasema kuna utaratibu uliopangwa kwa watoto wanaosajiliwa kujifunza katika siku za ijumaa, ambapo hupata fursa ya kufundishwa namna bora ya kusoma, kuchora, kuimba pamoja na kushiriki michezo mbali mbali inayolenga kuimarisha uwezo wao wa akili.

Anatowa wito kwa wazazi na walezi kuwapeleka watoto wao katika shirika hilo ili kupata mwanga na kuwa na msingi bora wa kielimu.

“Tunaiomba jamii ihamasike na kuwaleta watoto wao hapa, angalau kwa siku ya Ijumaa, ili kuwafanya watoto wajenge utamaduni wa kupenda kusoma na kuandika”, anasema 
Hudhaifa.

Katibu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Dk. Muslih Hijja ambae alikuwa mgeni rasmi katika maadhimisho hayo akimuwakilisha Naibu Waziri wa Wizara hiyo. Anasema, kwa mujibu wa Shirika la Kimataifa la UNESCO katika taarifa iliyotolewa mwaka 2016, inakadiriwa zaidi ya watu Milioni 775 hawajui kusoma wala kuandika Duniani kote.

Akinukuu takwimu za Shirika hilo anasema kila penye watu wazima watano (5), basi kuna mtu mmoja ambae hajuwi kusoma na kuandika, ambapo miongoni mwao, asilimia  sitini na sita (66%) ni wanawake.

“Hii inaonyesha kwa kiasi gani tatizo hilo lilivyo kubwa na juhudi madhubuti zinazohitajika kuchukuliwa ili kupunguza au ikiwezekana kuliondosha kabisa tatizo la kutojua kusoma na kuandika”, anasema. 

Aidha, anasema  maktaba zina  mchango mkubwa sana kwa jamii katika kuhakikisha wananchi wanapata fursa za kusoma kupitia vitabu na machapisho mengine kama vile magazeti, majarida na huduma za mitandao (internet).

Anasema kuna muhimu kwa Shirika hilo kuendelea kuihamasisha jamii kuchangamkia fursa hizo, kwa kigezo kuwa kuna nafasi kubwa ya kuwanyanyuwa kiuwezo katika nyanja za kiuchumi, kijamii, kisiasa na kiutamaduni na pia kwenda sambamba na maendeleo ya Ulimwengu wa Sayansi na Teknolojia.

Anaeleza kuwa katika kuhakikisha wananchi wa Zanzibar wanaweza kusoma na kuandika, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inafanyakazi kwa karibu na wadau mbali mbali wa elimu ndani na nje ya nchi.

Akatumia fursa hiyo kulipongeza Shirika la ‘Book Aid International’ la Uingereza, kwa kuwa mstari wa mbele kusaidia juhudi za Zanzibar na Tanzania kwa ujumla katika kupunguza tatizo la kutokujua kusoma na kuandika.

“Serikali yetu inapenda kulishukuru sana Shirikia hili kutokana na jitihada zake ambazo leo hii sote ni mashahidi kwamba Shirika la Maktaba, lililo chini ya Wizara Elimu na Mafunzo ya Amali limekuwa likipokea msaada wa vitabu vipya na vizuri ambavyo husaidia kuendeleza maktaba za Jamii, skuli na hata  maktaba za Vyuo”, anasema.

Anasema hayo yanafanyika kwa lengo la kuyabadili maisha ya wananachi , akiamini kuwa mtu asiyejuwa kusoma na kuandika ni sawa na yule anaeishi gizani.

Dk. Muslih anasema kuna kila sababu ya Serikali kuwahimiza wananchi wake kuongeza bidii katika kusoma pamoja na matumizi ya maktaba.

Akiziainisha sababu hizo, anasema ni pamoja na ukweli kuwa kusoma ndio msingi mkuu katika mafanikio ya kielimu na katika maisha.

Anasema kusoma kunaongeza uwezo wa ubongo kufanya kazi, kama ilivyo kwa wanaofanya mazoezi ambapo huongeza uwezo wao wa misuli.

Anasema pia kusoma kunaongeza ukwasi wa misamiati, “ kadri unavyosoma vitabu vingi kutoka kwa waandishi mbali mbali, ndivyo unavyojitajirisha katika suala la misamiati”.

Aidha, anasema hatua ya kuwa na  misamiati mingi kunasaidia sana katika maisha ya kila siku, kwani humfanya mtu kujiamini na kujenga uwezo mzuri wa kuzungumza mbele ya hadhira.

“Kusoma kunaimarisha stadi za uandishi, waandishi mahiri ni wale waliopata msukumo kutokana na usomaji wa kazi za waandishi wengine hususan waliobobea”, anaeleza.

Katika hatua nyengine, anasema kusoma kunaongeza maarifa, ambapo humpa mtu taarifa mpya, jambo linalomfanya mtu kuwa na utajiri wa maarifa, ikiwa nyenzo muhimu katika kukabiliana na changamoto zinazojitokeza maishani mwake.

Katibu Mkuu huyo, akatanabahinisha jinsi kusoma kunavyoweza kuongeza uwezo wa kufikiria na kupambanuwa mambo, sambamba na kuleta burudani isiyo na gharama.

“Ni kweli vitabu vingi vizuri huuzwa kwa bei ghali, lakini usisahau kuwa unaweza kupata burudani ya karibu ya bure kupitia vitabu, kwa kujenga mazoweya ya kutembelea maktaba katika eneo lako”, anabainisha.

Anaeleza kuwa Maktaba huwa na mchanganyiko wa vitabu vya kila aina, kuanzia riwaya hadi taaluma mbali mbali.

Katika hatua nyengine Injinia huyo anatowa wito kwa wazazi, walezi na jamii kwa ujumla kuhakikisha watoto wote waliofika umri wa kusoma wanapatiwa fursa endelevu za kielimu ili kuondokana na tatizo sugu la kutojua kusoma na kuandika kwa maslahi ya Taifa.

“Wazazi na walezi ni watu muhimu sana katika kuwasimamia watoto kujua kusoma na kuandika, suala hili si la walimu peke yao, ila ni la jamii nzima, tushirikiane pamoja ili tuweze kulipatia ufumbuzi wa kudumu”.

Dk. Muslih anabainisha njia za kufuatwa na wazazi pamoja na walezi katika kumsaidia mtoto ili kumuwezesha kujua kusoma na kuandika, kuwa ni pamoja na kusoma pamoja na watoto hao na kuwasikiliza wanaposoma, sambamba na kuweka vitabu nyumbani.

Aidha, anawataka wazazi/walezi kufanya ushawishi  kwa kuwapeleka watoto maktaba ili waweze kusoma vitabu pamoja na kuchukuwa nyumbani kwa ajili ya kujisomea.

Anasema endapo kutakuwa aa usimamizi mzuri, bila shaka watoto na jamii kwa ujumla itajenga utamaduni imara wa kupenda kusoma na kuongeza ufaulu katika masomo yao, sambamba na kuwa na uwezo wa kuendeleza ujuzi katika mambo mbali mbali.

Nidhahiri kuwa suala la kubadili mitizamo kwa wanafunzi na jamii ya Wazanzibari kwa ujumla, hususan katika suala zima la kutumia huduma za maktaba linahitajika.

Kuna ukweli kuwa bado jamii ya Wazanzibari haina utamaduni wa kutumia huduma za maktaba, kwa kile kinachoonekana kutokuwepo utamaduni wa kupenda kusoma na kuandika.

Hivyo ni wakati sasa kwa Wazanzibari kubadilika na kuhamishia nguvu zao katika kujenga utamaduni wa  kupenda kusoma vitabu, ikizingatiwa kuna vipaji vingi vya waandishi mahiri wa vitabu, hususan vya Kiswahili  hapa nchini.

Wakati Wazanzibari wakiungana na Jumuiya za Kimataifa kuadhimisha siku ya Kujua kusoma na kuandika, ni wakati pia wa kutafakari kwa kiasi gani tunachukuwa hatua maridhawa katika kuwasaidia watoto na jamii kwa ujumla kujua kusoma na kuandika.   

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.