Habari za Punde

Serikali ya Oman Yakabidhi Vifaa Idara ya Nyaraka Zanzibar.


Mwenyekiti wa Mamlaka ya Uhifadhi Nyaraka na Kumbukumbu katika serikali ya Oman Dk. Hamed Mohammed Al Dhawaiyan (mwenye kanzu katikati), akikabidhi vifaa vya kisasa vya kutunzia nyaraka kwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Nyaraka na Kumbukumbu Zanzibar Salum Suleiman Salum (kulia), nje ya jingo la ofisi hizo Kilimani mjini Unguja. 
Mwenyekiti wa Mamlaka ya Uhifadhi Nyaraka na Kumbukumbu katika serikali ya Oman Dk. Hamed Mohammed Al Dhawaiyan (mwenye kanzu katikati), akikabidhi vifaa vya kisasa vya kutunzia nyaraka kwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Nyaraka na Kumbukumbu Zanzibar Salum Suleiman Salum (kulia), nje ya jingo la ofisi hizo Kilimani mjini Unguja. (Picha na Salum Vuai, WHUMK). 

Na Salum Vuai, ZANZIBAR
SERIKALI ya Oman imeanza kutekeleza kwa vitendo makubaliano iliyofikia na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, katika kusaidia teknolojia ya kisasa ya uhifadhi wa nyaraka.

Septemba 3, 2018, ujumbe wa Idara ya Nyaraka na Kumbukumbu ya Mambo ya Kale kutoka nchi hiyo, umekabidhi mashine za kisasa za kutunza nyaraka na kumbukumbu kwa mfumo wa kidijitali kuzuia kuharibika.

Makabidhiano hayo yalifanyika katika ofisi za taasisi ya Nyaraka na kumbukumbu Zanzibar zilizopo Kilimani mjini Unguja.

Vifaa hivyo ni mashine ya kurudufu nakala na nyengine kwa ajili ya kuhifadhia nyaraka kwa njia ya kidijitali.

Mwenyekiti wa Mamlaka ya Nyaraka na Kumbukumbu wa Oman Dk. Hamed Mohammed Al Dhawiyan ndiye aliyekabidhi vifaa hivyo kwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Nyaraka na Kumbukumbu Zanzibar, Salum Suleiman Salum.

Akizungumza baada ya kukabidhi mashine hizo, Dk.  Al Dhawiyan, alisema msaada huo wameutoa ikiwa ni sehemu ya makubaliano kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na ile ya Oman, wakati wa ziara ya Waziri wa Habari, Utalii na Mambo ya Kale Mahmoud Thabit Kombo na ujumbe wake nchini Oman mwishoni mwa mwezi Aprili mwaka huu.

Alifahamisha kuwa, nyaraka za nchi ni vitu muhimu ambavyo vinahitaji kushughulikiwa na kuthaminiwa, ili zidumu kwa miaka mingi na kutumiwa kwa tafiti mbalimbali.

“Ni vyema jambo hili lifanyiwe kazi kikamilifu kutokana na umuhimu wake kwa taifa, wananchi, wageni na wasomi wanaohitaji kumbukumbu kwa ajili ya tafiti zao,” alieleza Mwenyekiti huyo.

Alieleza kuwa, vifaa hivyo ni hatua ya awali katika misaada wanayokusudia kuipatia Zanzibar, na kuongeza kuwa, vyengine vitaendelea kuletwa.

Aidha, alisema katika ujumbe wao uliowasili nchini Septemba 1 na 2, wamo wataalamu maalumu waliobobea katika matumizi ya vifaa hivyo, ambao wamekuja kwa lengo la kutoa mafunzo kwa wafanyakazi wa taasisi hiyo ya Zanzibar ili wapate maarifa ya kutumia mashine hizo.

Dk. Al Dhawiyan alifafanua kwamba, ni fahari kwa Oman ambayo imepiga hatua kubwa ya maendeleo katika sekta mbalimbali, kutoa mchango wake katika kuzisaidia nchi nyengine ili nazo zipate mabadiliko na ufanisi wenye tija kiuchumi na kijamii.

Mbali na ujuzi wa kuhifadhi nyaraka kisasa, pia alisema nchi yake ina ujuzi wa kuziharibu kitaalamu  kumbukumbu zilizopitwa na wakati ambazo hazihitajiki tena, na ziko nchi nyingi zikiwemo Urusi, Iran na Belarusia zinazoomba kufanyiwa kazi hiyo.

Alieleza kuwa, katika ulimwengu wa sasa, nyaraka zinakuwa siri kwa muda maalumu na baadae hutangazwa ama kuwa huru kwa watu mbalimbali kuziona kwa shughuli zao, au kuwa hazihitajiki tena.

Akizungumza katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Taasisi ya Nyaraka na Kumbukumbu Zanzibar Salum Suleiman Salum, alibainisha changamoto kadhaa zinazowakabili, ikiwemo hali ya joto ambayo baadhi ya nyaraka haziwezi kuihimili kwa muda mrefu.

Kutokana na sababu hiyo, alisema nyingi kati ya nyaraka zilizopo zimeshaanza kupoteza hadhi na uhalisia wake, kwa hivyo alishauri uwezekano wa Oman kuliangalia pia eneo hilo kwa msaada stahiki.

Mbali na hayo, alisema kwa sasa jengo lao limekuwa dogo kulingana na wingi wa shughuli na halikidhi matumizi ya taasisi hiyo kwa sasa.

Alisema pamoja na kuwepo uwezekano wa kulitanua, lakini ni vizuri zaidi kujenga jengo jipya, kubwa na la kisasa litakalokuwa na  mahitaji yote ya msingi kwa shughuli za uhifadhi wa kumbukumbu, pamoja na mazingira rafiki kwa watu wenye ulemavu.
IMETOLEWA NA WIZARA YA HABARI, UTALII NA MAMBO YA KALE ZANZIBAR- SEPTEMBA 3, 2018

CAPTION
MWENYEKITI wa Mamlaka ya Uhifadhi Nyaraka na Kumbukumbu katika serikali ya Oman Dk. Hamed Mohammed Al Dhawaiyan (mwenye kanzu katikati), akikabidhi vifaa vya kisasa vya kutunzia nyaraka kwa Mkurugenzi wa Taasisi ya Nyaraka na Kumbukumbu Zanzibar Salum Suleiman Salum (kulia), nje ya jingo la ofisi hizo Kilimani mjini Unguja. (Picha na Salum Vuai, WHUMK). 


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.