Habari za Punde

Makamu wa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Aitaka WCF Kuendelea Kuwabana Waajiri Kujisajili.


NA K-VIS BLOG/Khalfan Said
MAKAMU wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, ameuagiza uongozi wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), kuendelea kuwafuatilia waajiri ambao bado hawajajisajili ili waweze kufanya hivyo.
Makamu wa Rais alitoa wito huo leo Oktoba 29, 2018 alipotembelea banda la Mfuko huo kwenye maonesho ya viwanda Mkoa wa Pwani kwenye viwanja vya CCM-Sabasaba, Picha ya Ndege Mkoani humo.
Alisema viwanda vimeongezeka nchini na kwamba huduma za WCF zitahitajika sana kwa wakati huu na hivyo kuutaka uongozi wa Mfuko, kuhakikisha unaendelea na ufuatiliaji kwa waajiri wa zamani na wapya ambao bado hawajajisajili na kuwasilisha michango kwenye Mfuko watekeleze takwa hilo la kisheria ili mfanyakazi anapoumia aweze kupata haki yake ya fidia.
“Waajiri wao muwabane wajisajili na mfuko na waweze kuwasilisha michango ili Mfuko uendelee kuwa na uwezo wa kulipa fidia, pale watoto wetu (wafanyakazi) wanapokatika vidole au kuumia waweze kupata haki zao.” Alisisitiza.
Katika hatua ya kuimarisha Hifadhi ya Jamii, Tanzania, Serikali ilianzisha Mfuko wa Fidia Kwa Wafanyakazi kwa mujibu wa kifungu namba 5 cha sheria ya Fidia kwa Wafanyakazi,  kipengele cha 263 kilichofanyiwa marejeo mwaka 2015 ili kuhakikisha kila mfanyakazi Tanzania Bara kutoka sekta ya umma na binafsi anapata fursa ya kuwekewa bima na mwajiri wake ili anapopata majeraha au magonjwa awapo kazini basi aweze kufidiwa kwa mujibu wa sheria.
Katika hatua nyingine, WCF imekuwa miongoni mwa taasisi zilizotunukiwa vyeti vya shukrani kwa kuwezesha maonesho hayo kufanyika. 
Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi unashiriki maonesho hayo ya kwanza ya viwanda kufanyika Mkoani Pwani ambapo waajiri, wafanyakazi na wananchi wamekuwa wakipita kwenye banda la Mfuko huo kupata elimu kuhusu shughuli za Mfuko.
 Makamu wa Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan, akimkabidhi cheti cha shukrani Mkurugezni Mkuu wa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw.Masha Mshomba kutokana na Mfuko huo kuwa miongoni mwa taasisi zilizowezesha kufanyika kwa maonesho ya kwanza ya viwanda Kibaha kwenye viwanja vya Sabasaba-Picha ya Ndege Mkoani Pwani, Oktoba 29, 2018.  
 Makamu wa Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan, akihutubia wakati wa ufunguzi wa maonesho hayo.
 Makamu wa Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan, akizungumza na Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Bw. Masha Mshomba, alipotembelea banda la Mfuko huo.
Bw. Mshomba (wapili kushoto), akimsikilizia kwa makini Mwenyekiti Mtendaji wa IPP., Dkt. Reginald Mengi, mmoja wa waajiri wakubwa hapa nchini, wakati alipokuwa akitembelea mabanda ya makampuni mbalimbali (waajiri), kwenye maonesho ya viwanda Kibaha kwenye viwanja vya Sabasaba, Picha ya Ndege Oktoba 29, 2018.
Makamu wa Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan, akipeana mkono na  Mkurugenzi wa Huduma za Fedha na Uwekezaji, Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi (WCF), Bw.Bezil Ewala, alipotembelea banda la Mfuko huo. Wapili kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Bw. Mshomba.
 Wananchi wakipatiwa maelezo na Afisa Uhusiano Mwandamizi wa WCF, Bw. Sebera Fulgence walipofika kwenye banda la Mfuko huo.
 Mgeni rasmi katika picha ya pamoja na wawezeshaji wa maonesho hayo.
Kikundi cha ngoma cha JKT

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.