Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Mwakilishi wa FAO Nchini Tanzania na Mwenyekiti wa Washirika wa Maendeleo ya Sekta ya Kilimo Tanzania Mr. Fred Kafeero, alipofika Ikulu Zanzibar na Ujumbe wake kwa mazungumzo leo.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein ameeleza dhamira ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika
kuimarisha sekta ya kilimo na kuwapongeza Washirika wa Maendeleo wa sekta hiyo waliopo
nchini kwa kuiunga mkono dhamira hiyo.
Rais Dk. Shein
aliyasema hayo leo alipokutana na kufanya mazungumzo na Washirika wa Maedeleo
wa Sekta ya Kilimo Tanzania wakiongozwa na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa
Mataifa linaloshughulikia Chakula na Kilimo Duniani (FAO) ambaye pia, ni
Mwenyekiti wa Washirika hao hapa nchini
Fred Kafeero.
Katika Mazungumzo hayo,
Dk. Shein alipongeza hatua kubwa zilizochukuliwa na Washirika hao wa Maendeleo
wa sekta ya Kilimo kwa kufika Zanzibar na kuja kuona juhudi zinazochukuliwa na
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika sekta hiyo na hatimae kupata upeo
mpana wa kupata kujua mafanikio na changamoto zilizopo.
Rais Dk. Shein
alieleza matumaini yake kutokana na azma
na mikakati iliyowekwa na Washirika hao wa Maendeleo katika kuiunga
mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya kilimo hasa katika programu kuu ya
Sekta ya Kilimo hapa Zanzibar ambayo ipo katika hatua ya mwisho ya matayarisho.
Alieleza kuwa hatua za
Washirika hao wa Maendeleo ya kuja Zanzibar kwa muda wa siku mbili kwa lengo na
azma ya kutembelea maeneo mbali mbali ya sekta ya Kilimo pamoja na kuwepo
rasimu ya programu ya sekta ya kilimo ili kuona maeneo ambayo watashirikiana ni
jambo jema na linatoa mwanga wa matumaini katika sekta hiyo.
Aidha, Rais Dk. Shein
alisisitiza haja kwa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi kuhakikisha
Programu Kuu ya Sekta ya Kilimo Zanzibar ambayo itakuwa ndio Dira katika
mashirikiano ambayo Zanzibar itaonesha mipango ya sekta ya kilimo kwa hivi sasa
na miaka mengine ijayo.
Katika maelezo yake,
Rais Dk. Shein aliwapongeza Washirika wote wa Maendeleo wa sekta ya Kilimo Tanzania na kulipongeza Shirika la (FAO), kwa
kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya kilimo na kuifanya
izidi kuvutia kwa kutoa ajira kwa vijana sambamba na kuimarisha uchumi wa nchi.
Rais Dk. Shein pia, alitumia
fursa hiyo kutoa pongezi kwa Jumuiya ya Ulaya (EU), kwa kuendelea kushirikiana na Zanzibar katika
kuendeleza miradi mbali mbali ya maendeleo hasa katika kufanya utafiti wa
kutafuta nishati mbada.
Alieleza kuvutiwa
kwake na juhudi zinazochukuliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa
linaloshughulikia Viwanda Duniani (UNIDO) kwa kuendeleza viwanda vidogo vidogo
hapa Zanzibar kwa lengo la kusaidia sekta ya ajira sambamba na matumizi bora ya
bidhaa za kilimo.
Pamoja na hayo, Rais
Dk. Shein alieleza haja kwa Shirika la Maendeleo ya Kilimo la Umoja wa Mataifa (IFAD)
kuhakikisha linaendelea kufanya kazi kwa karibu zaidi na Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar ili Zanzibar iweze kunufaika na miradi inayoendeshwa na Shirika
hilo.
Nao Washirika hao wa
Maendeleo wa Sekta ya Kilimo Tanzania wakiongozwa na Mwenyekiti wao Fred
Kafeero ambaye pia ni Mwakilishi wa (FAO) nchini Tanzania walimpongeza Rais Dk.
Shein kwa kuiendeleza sekta ya kilimo na kuiunganisha na sekta nyengine ili
ziweze kwenda sambamba na mipango ya maendeleo iliyopangwa na Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar.
Walieleza kwamba kasi
ya uchumi inaimarika zaidi pale sekta zote muhimu za kiuchumi na kujamii zinapofanya
kazi kwa kasi ya pamoja kama alivyoamua kufanya hivyo Rais Dk. Shein katika
sekta hiyo ya kilimo.
Aidha, viongozi hao
walieleza kufurahishwa kwao kwa kupata fursa ya kuitembelea Zanzibar na kujua
mafanikio na changamoto zilizopo katika
sekta ya kilimo na kuahidi kuendelea kuiunga mkono Zanzibar.
Viongozi hao waliahidi
kutoa ushirikiano wao katika uhamasishaji na ushahijishaji katika kutafuta rasilimali
muhimu zinazohitajika katika kuendeleza sekta ya kilimo hapa Zanzibar sambamba
na kuhakikisha programu kuu ya Sekta ya Kilimo Zanzibar inafanikiwa.
Sambamba na hayo,
walieleza haja kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuzichangamkia na
kuzitumia vyema fursa zilizopo kutoka kwa Wasirika wa Maendeleo wa Sekta ya
Kilimo Tanzania hasa katika suala zima
la upatikanaji wa misaada na mikopo.
Walieleza kuwa nchi
nyingi wameweza kupata mafanikio na kuendeleza sekta ya kilimo kwa kuzitumia
vizuri fursa za mikopo na misaada inayotolewa huku kiongozi wa Umoja wa Ulaya
aliyekuwemo katika ujumbe huo Bi Jenny Correian Nunes akiahidi Jumuiya hiyo
kuendelea kutoa ushirikiano wake kwa Zanzibar.
Viongozi hao walieleza
kuvutiwa kwao na kauli ya Rais Dk. Shein anayoitoa mara kwa mara juu ya
utendaji wa kazi kwa kuwataka watendaji kwenda kwenye maeneo ya kazi badala ya
kukaa maofisini kauli ambayo walieleza kuwa ndio Dira kubwa katika utekelezaji
wao wa kazi.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment