Habari za Punde

Tanzania Kunufaika na Fursa za Uchumi Endelevu wa Bahari

Naibu Katibu Mkuu Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Maliasili na Utalii, Uvuvi na Mifugo kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Dkt. Islam Seif Salum akifungua mkutano wa wadau uliojadili masuala ya uchumi endelevu wa Bahari ‘Sustainable Blue Economy’ unaotarajiwa kufanyika Nchini Kenya. Kulia ni Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga Bi. Zena Said.
Prof. Kassim Kulindwa kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam akitoa majumuisho ya mkutano huo ulifanyika katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam.
Mmoja wa washiriki wa Kikao hicho Balozi Celestine Mushi kutoka Sekretarieti ya Mkoa wa Mtwara akichangia jambo katika mkutano wa wadau uliojadili masuala ya uchumi endelevu wa Bahari ‘Sustainable Blue Economy’

Na.lulu mussa..
Katika jitihada za kujenga uelewa juu ya dhana nzima ya uchumi endelevu utokanao na rasilimali za  bahari, mabwawa na mito Ofisi ya Makamu wa Rais imeendesha kikao cha wadau kutoka taasisi mbalimbali zinazojishughulisha na sekta ya uvuvi na mazingira kutoka Tanzania Bara na Zanzibar ili kwa pamoja kuandaa msimamo wa Nchi katika Mkutano unaotarajiwa kufanyika Nchini Kenya hivi karibuni.
Akifungua kikao hicho Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo, Maliasili na Utalii, Uvuvi na Mifugo kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Dkt. Islam Seif Salum amesema kuwa ni muhimu kwa Tanzania kama nchi kunufaika ipasavyo na fursa za uchumi endelevu wa bahari katika nyanja za uvuvi, utafiti na uchimbaji wa mafuta na gesi na katika sekta ya utalii.
“Tuko hapa kujadiliana na kuweka mikakati ya pamoja kama nchi katika kuelekea Mkutano mkubwa wa masuala ya kunufaika na rasilimali za uvivu katika bahari, mito, maziwa na mabwawa, dhana hii ni mpya hapa nchini kwetu ingawa tunatekeleza kwa kiwango kidogo.” Alisisitiza Dkt. Salum.
Dkt. Salum amesema kuwa mkutano huo utajenga fursa zaidi za kuwekeza katika rasilimali za baharini ili kutimiza lengo la kukuza uchumi na kuendeleza Tanzania ya Viwanda.
Kwa upande mwingine Afisa Uvuvi Mkuu kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Bi. Emelda Teikwa amesema kuwa dhana ya ‘Blue Economy’ ni ngeni hapa nchini ila ni muhimu sana katika uchumi. “Tunaangalia namna ambavyo Uchumi wa bahari unaweza kuchangia katika kukuza pato la Taifa, kwa kuwa na uvuvi endelevu na kukuza sekta ya utalii”. Alisisitiza Bi. Teikwa.
Tanzania ni miongoni mwa nchi zitakazoshiriki katika Mkutano Mkubwa wa uchumi endelevu wa Bahari ‘Sustainable Blue Economy’ unaotarajiwa kufanyika Nchini Kenya mwishoni mwa mwezi huu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.