Habari za Punde

Zanzibar Kuadhimisha Siku ya Takwimu Afrika.















Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Bi. Mayasa Mahfudh Mwinyi akizungumza na Waandishi wa habari wa vyombo mbalimbali vilioko Zanzibar kuhusiana na maandalizi ya Maadhimisho ya Siku Takwimu Afrika.i

Na Faki Mjaka-Maelezo Zanzibar 16.11.2018
Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imeandaa Mdahalo mkubwa utakaofayika Novemba 19, kwa lengo la kuongeza uelewa wa Wananchi juu ya umuhimu wa Takwimu katika maendeleo ya Taifa.
Mtakwimu Mkuu wa Serikali Mayasa Mahfudh Mwinyi aliyasema hayo alipokuwa akizungumza na Waandishi wa habari ofisini kwake Mazizini kuhusu shamrasharma za maadhimisho ya siku ya Takwimu Afrika.
Amesema Takwimu zina umuhimu mkubwa katika kupanga maendeleo ya Taifa hivyo wananchi wanapaswa kujua kwa undani wake ili kutoa mashirikiano kwa ofisi hiyo.
Amesema Ofisi ya Takwimu itaendelea na jukumu lake la kufanya Tafiti katika nyanya mbalimbali ikiwemo za kiuchumi, kimaendeleo na kijamii na kuishauri Serikali na Taasisi binafsi kuhusu mwelekeo wa kiuchumi.
Aidha amezishauri Taasisi za Serikali na binafsi kuzitumia Takwimu zinazotolewa na ofisi hiyo ili zipige hatua mbele kimaendeleo na kukabiliana na changamoto zao.
Alisisitiza wadau wote wanaotaka kufanya tafiti rasmi kwenda katika Ofisi yao kuomba ushauri wa kitaalamu ili Takwimu watakazozipata katika tafiti zao ziwiane na Takwimu ya Ofisi yake.
“Ili kuepuka mgongano wa Kitakwimu nawaomba Wadau wote wanaofanya Tafiti basi waje ofisini tuwasiliane kuboresha Takwimu badala ya takwimu hizo kugongana” alisisitiza Mtakwimu Mkuu.
Mbali na kilele Mtakwimu Mayasa alielezea mambo watakayoyafanya ikiwa ni pamoja na kutoa msaada katika nyumba za kulelea watoto Mazizini ambapo Jumapili kutakuwa na Mchezo wa Mpira wa Miguu kati ya Ofisi ya Mtakwimu na Ofisi ya Mdhibiti Mkuu wa Serikali.
Awali Mtakwimu Mwandamizi kutoka Ofisi ya Mtakwimu Abdulmajid Jecha alisema kulingana na Takwimu za uwezekano wa umri wa kuishi kwa Mzanzibari ni miaka 67.
Alisema miaka hiyo imeongezeka kutokana na uimarishwaji wa huduma za Afya Zanzibar na matumizi madogo ya ulevi ikiwemo Pombe kwa Wanzanzibari.
Hali hiyo ni tafauti kidogo kwa Tanzania Bara ambapo Makadirio ya kuishi ni miaka 66.
“Sababu zinazofanya Makadirio ya kuishi kwa Wazanzibari kuwa juu ukilinganisha na Bara ni uimarishwaji wa huduma za Afya kwa mfano kupungua kwa Malaria  ikilinganishwa na Bara lakini hata Ulevi ambao ni chanzo cha magonjwa Zanzibar ni kidogo ukilinganisha na Bara ” alibainisha Abdulmajid Jecha
Hivyo Jecha alishauri watu wazidi kuzitumia Takwimu sahihi zinazotolewa na Ofisi hiyo ili kujipangia mipangilio yao ya maendeleo.
Kila ifikapo November 18 ni siku ya Takwimu Afrika ambapo kwa Zanzibar itaadhimishwa November 19 katika viunga vya Ofisi hiyo Mazizini, ili kufikisha ujumbe kwa wananchi wengi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.