Habari za Punde

MAAMUZI YA TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI KUHUSU RUFAA MOJA YA UCHAGUZI MDOGO WA TAREHE 19 JANUARI, 2019 KWA KATA YA MAGOMENI JIMBO LA KINONDONI

Tume ya Taifa ya Uchaguzi ilipokea Rufaa moja (1) kutoka kwa Mgombea Udiwani wa Kata ya Magomeni katika Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni. Tume imepokea rufaa hiyo kwa kuzingatia kifungu cha 44(5) cha Sheria ya Uchaguzi ya Serikali za Mitaa, Sura ya 292, kikisomwa pamoja na kanuni ya 28(1) ya Kanuni za Uchaguzi wa Serikali za Mitaa (Uchaguzi wa Madiwani) za mwaka 2015,

Rufaa hiyo iliwasilishwa na mgombea Udiwani wa Chama cha Wananchi (CUF) Ndg. Ngude Athumani Yusuph akitaka arejeshwe kuwa mgombea udiwani katika Kata ya Magomeni kupitia chama hicho.

Kuenguliwa kwake kulitokana na pingamizi lililowekwa na mgombea mwenzake kwa madai kuwa Sio Raia wa Tanzania, hakudhaminiwa na chama chake cha siasa kugombea udiwani na fomu yake ya uteuzi haikujazwa kikamilifu. Msimamizi wa Uchaguzi alikubaliana na pingamizi hilo, hivyo kumuengua mgombea.

Tume katika kikao chake cha tarehe 24 Disemba 2018, ilipitia vielelezo vilivyowasilishwa na kujiridhisha kuwa mrufani ni Raia wa Tanzania na kwamba alidhaminiwa na chama chake cha siasa na kwamba fomu yake ya uteuzi ilijazwa kwa ukamilifu na hivyo, kuelekeza arejeshwe kuendelea kuwa mgombea udiwani katika Kata ya Magomeni, Halmashauri ya Manispaa ya kinondoni
Aidha, Tume ilipokea malalamiko kutoka kwa Ndg. Ngulangwa Eng Mohamed Mshamu wa Chama cha Wananchi (CUF) akipinga  uamuzi wa Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Temeke kumuondoa kwenye orodha ya wagombea Ubunge na kumtangaza Mgombea wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Ndg. Abdallah Ally Mtolea  kuwa amepita bila kupingwa.

Kwa mujibu wa kifungu cha 44 cha Sheria ya Taifa ya Uchaguzi, Sura ya 343, Mgombea akitangazwa kuwa amepita bila kupigwa Tume haina mamlaka juu ya uamuzi wa Msimamizi wa Uchaguzi. Hivyo, malalamiko hayo yaliyowasilishwa na Ndg. Ngulangwa Eng. Mohamed Mshamu na pia hayana sifa ya kuwa rufaa.
Taarifa za maamuzi ya rufaa na malalamiko, zimetumwa kwa wahusika kupitia kwa Wasimamizi wa uchaguzi wa Halmashauri husika.

Imetolewa leo  tarehe  24 Disemba, 2018 na:


Giveness Aswile
 MKURUGENZI WA HABARI NA ELIMU YA MPIGA KURA

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.