Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Ujumbe wa UWT Ikulu leo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akimsikiliza Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Tanzanbia (UWT) Mhe.Gaudensia Kabaka, alipofika Ikulu Zanzibar, kujitambulisha leo akiongozana na Uongozi wa UWT.kulia Makamu Mwenyekiti wa UWT Mhe. Thuwaiba Kisasi na Bi Queen Mlozi Katibu Mkuu wa UWT, wakiwa katika ukumbi wa mkutano huo.

RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa wanawake wa Tanzania ndio waliokuwa mstari wa mbele katika kupigania uhuru wa Tanzania Bara na Zanzibar hivyo ni vyema wakapewa kipaumbele ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na uongozi wa Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Taifa, ulioongozwa na  Mwenyekiti wa Umoja huo Gaudensia Kabaka ambao ulifika Ikulu kwa ajili ya kujitambulisha kwa Rais.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein ambaye pia, ni Makamo Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, aliueleza uongozi huo kuwa wanawake wana nafasi maalum katika Chama na Serikali kutokana na majukumu yao sambamba na juhudi zao.

Rais Dk. Shein alisema kuwa bila ya akina mama mafanikio zaidi hayatofikiwa katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ndani ya (CCM) hasa ikizingatiwa kuwa wana umuhimu mkubwa katika jamii.

Alieleza kuwa kina mama ni vyema wakapewa nafasi katika kukitumikia chama chao na Serikali yao na ndio maana (CCM) ikaunda Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT), ambao tokea kuasisiwa kwake umepata mafanikio makubwa na umekuwa muhimili muhimu wa (CCM).

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza matumaini yake makubwa kuwa uongozi huo mpya wa (UWT) chini ya Mwenyekiti wake Gaudensia Kabaka utafanya vizuri kwa azma ya kuendeleza mafanikio katika Umoja huo na CCM kwa ujumla.

Akitoa wito kwa Umoja huo, Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuendeleza umoja, mapenzi na  na mshikamano miongoni mwa Wanajumuiya sambama na kufanya kazi wakiwa wamoja.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alisisitiza haja kwa uongozi huo kuwaandaa vijana kushika nafasi za uongozi katika Umoja huo wa (UWT) hapo baadae hasa ikizingatiwa kuwa kiongozi huandaliwa hivyo ni vyema wakaandaliwa vijana watakao kitumikia chama chao cha (CCM).

Nae Mwenyekiti wa (UWT) Taifa Gaudensia Kabaka alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa kutekeleza vyema Ilani ya Uchaguzi ya (CCM) ya mwaka 2015-2020 huku akitumia fursa hiyo kumpongeza Dk. Shein kwa kupata kura zote katika mkutano mkuu  wa chama hicho uliofanyika Disemba mwaka 2017.

Mwenyekiti huyo alieleza kuwa kupata kura zote kwa Rais Dk. Shein ambaye ni Makamo Mwenyekiti wa (CCM) Zanzibar kunatokana na kuwa (CCM) inamkubali na inazikubali kazi zake anazozifanya katika kuiongoza Zanzibar na watu wake pamoja na chama hicho.

Aidha, Mwenyekiti huyo alizipongeza juhudi za Rais Dk. Shein kutokana na mafanikio makubwa yaliopatikana katika kuendeleza na kuimarisha miradi ya maendeleo Unguja na Pemba sambamba na hatua alizozichukua za kuwaenzi wazee wa Zanzibar na kuwapa nafasi za uongozi akina mama katika Serikali anayoiongoza.

Pia, Mwenyekiti huyo alieleza azma, malengo pamoja na mikakati iliyowekwa katika Umoja huo katika kuhakikisha (CCM) inaendelea kushinda katika chaguzi zote ukiwemo uchaguzi ujao wa mwaka 2020 sambamba na kusisitiza mchakato wa ziara watakazozifanya Zanzibar ambazo zitaanzia kisiwani Pemba mara tu baada ya sherehe za miaka 55 za Mapinduzi mwaka huu.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.