RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amewataka wananchi wa
Zanzibar kuendelea kuidumisha hali ya amani na utulivu ambayo ndio msingi wa
mafanikio yanayoendelea kupatikana hivi sasa na yatakayopatikana hapo baadae.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo katika risala yake ya kuukaribisha mwaka mpya wa 2019
aliyoitoa kupitia vyombo vya habari, Ikulu mjini Zanzibar.
Rais Dk. Shein alisema
kuwa katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya mwaka 2018 mafanikio makubwa
yamepatikana ambayo yamechangiwa na kuwepo kwa amani, mshikamano, umoja na
mapenzi yaliopo.
Katika risala yake
hiyo Rais Dk. Shein alieleza kuwa hali ya amani, umoja na mshikamano uliopo
nchini ni jambo muhimu linalowavutia Washirika wa maendeleo ambao wanaridhika
na jitihada zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na ndio maana
wanaiunga mkono katika mipango yake ya maendeleo.
Alisema kuwa hapana
shaka kwamba iwapo amani, usalama na utulivu vitadumishwa na kufanya kazi kwa
bidii Washirika wa Maendeleo watakuwa pamoja na Zanzibar katika kuisaidia ili
kuweza kutekeleza malengo yaliyopangwa.
Rais Dk. Shein alitoa shukurani
kwa wananchi wote kwa kuunga mkono juhudiza serikali za kuiletea maendeleo
Zanzibar na kueleza kuwa moyo wao huo wa umoja na mshikamano umewezesha
kuimarisha vizuri hali ya uchumi wa Zanzibar.
Hata hivyo, Dk. Shein
alitoa shukurani nyingi kwa wananchi wote kwa kuunga mkono juhudi za Serikali
za kuiletea maendeleo Zanzibar ambapo moyo wao huo wa umoja na mshikamano
umewezesha kuimarisha vizuri hali ya uchumi wa Zanzibar.
“Tukiwa tunaukaribisha
mwaka mpya wa 2019, nachukua fursa hii kwa niaba ya wananchi wote wa Zanzibar kuwashukuru kwa dhati Washirika wetu wa Maendeleo kwa kuendelea
kutuunga mkono, tunathamini mikopo, misaada na ushauri tulioupata kutoka kwao”,
alisema Dk. Shein.
Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza
kuwa wakati unakaribishwa mwaka 2019 ni wajibu wa kila Taasisi ya Serikali
ikajipima namna inavyoendelea kutekeleza mambo yaliyoagizwa katika Ilani ya CCM
ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015-2020.
“Nawakumbusha viongozi
wenzangu viongozi wenzangu wote wa CCM tuliochaguliwa na wananchi katika
Uchaguzi Mkuu wa 2015, uliorudiwa mwezi Machi, 2016. Kadhalika jukumu hili
wanapaswa walizingatie na wale wote niliowateua katika nyadhifa mbali
mbali”,alisema Dk. Shein katika risala yake hiyo.
Katika risala yake
hiyo Rais Dk. Shein alizitaja kumbukumbu za matukio yalitokea katika mwaka 2018
ikiwa ni pamoja na utiaji wa saini wa Mkataba wa Mgawanyo wa Uzalishaji wa
Mafuta na Gesi Asilia (PSA), baina ya Kampuni ya Maendeleo ya Mafuta na Gesi
Asilia na kampuni ya RAK GAS ya Ras Al Khaimah.
Aliongeza kuwa tukio
jengine la kihistoria ni kufanyika kwa Tamasha la Utalii la Kimataifa ambalo
lilihudhuriwa na Makampuni 150 ya Utalii ya ndani na nje ya nchi ambalo
lilileta mafanikio katika kuwaunganisha wafanyabiashara wa utalii wa Zanzibar
na wale wa Kimataifa na kuitangaza Zanzibar katika masoko ya Kimataifa.
Alieleza kuwa mwaka
2018 umefungua milango katika utekelezaji wa dhamira ya kuendeleza kilimo cha
mpunga kwa njia ya umwagiliaji maji na utumiaji wa zana za kisasa ambapo tarehe
6 Disemba, 2018 Serikali ilitiliana saini Mkataba wa Ujenzi wa Miundombinu ya
Kilino cha Umwagiliaji maji na Kampuni ya Kokon Hansol JV ya Jamhuri ya Korea
kupitia Shirika la Maendeleo la nchi hiyo.
Pia, Rais Dk. Shein
alieleza kuwa katika lengo la kuungana na nchi nyengine katika kuendeleza
uchumi wa Bahari tarehe 26 hadi 28 aliongoza Ujumbe wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania katika mkutano wa Kimataifa uliofanyika Nairobi nchini Kenya.
Alisisitiza kuwa kwa
upande wa Zanzibar inauanza mwaka 2019 ikiwa imejipanga kwa kutafuta njia bora
za kutumia rasilimali za bahari kwa kuitumia vizuri bahari ya Hindi
iliyoizunguka kwani hili ni eneo muhimu kwa uchumi wa Zanzibar.
Akieleza jambo jengine
muhimu ambalo limefanyika katika mwaka 2018, Rais Dk. Shein alisema kuwa tukio
linalohusu jitihada za Serikali za kuwakinga wanawake wa Zanzibar na janga la
saratani ya shingo ya kizazi ambapo mnamo April 10 Mama Mwanamwema Shein
alizindua rasmi Mpango wa Chanjo dhidi ya Ugonjwa wa Saratani ya Shingo wa
Kizazi.
Vile vile, tarehe 5
Disemba 2018 alizindua Mpango wa Miaka Minne wa Uchunguzi wa Saratani ya Shingo
ya Kizazi ambao unawajumuisha wanawake wenye umri wa miaka 21 hadi 65 kazi
ambayo itafanywa kwa kushirikiana na Wataalamu kutoka Jamhuri ya Watu wa China
ambapo huduma zote pamoja na matibabu zitatolewa bure.
Rais Dk. Shein
alieleza kuwa Zanzibar inasifika kwa uzuri wake, historia yake na khulka nzuri
za watu wake na hali ya usalama iliyopo ambapo Serikali nayo inafanya jitihada
za kuhakikisha kwamba sifa njema ya Zanzibar ya kuwa ni sehemu salama yenye
utulivu inaendelea kwua ni kichocheo cha kuwavutia wageni, watalii na
wawekezaji sambamba na kurahisiha utekelezaji wa mipango ya kamedneleo.
Hivyo, mnamo tarehe 3
Novemba 2018 ulizinduliwa rasmi Mradi wa
Ulinzi wa Mji Salama ambao lengo lake ni kuhakikisha hali ya usalama kwa
kutumia CCTV na vyombo vyengine vya kisasa ambapo dhamira ni kuendeleza mradi
huu katika Mikoa mengine ya Unguja na Pemba hatua kwa hatua.
Licha ya mafanikio
hayo yaliopatikana mwaka 2018, Rais Dk. Shein alieleza kuwa bado kunahitajika
kuzidisha mapambano dhidi ya udhalilishaji wa wanwake na watoto na unyanyasaji
wa kijinsia kwa vile kesi za vitendo hivyo bado zinaendelea kuripotiwa kwenye
maeneo mbali mbali.
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein aliwaahidi wananchi wote kwamba wale wote watakaobainika kwamba
wamehusika kwenye tukio la uvujaji wa mitihani ya kidato cha Pili kwenye sekta
ya elimu watachukuliwa hatua kali za kisheria.
Aliongeza kuwa tukio
hilo ni la kusikitisha, linalokwenda kinyume na mipango ya maendeleo ya elimu
ambalo halijengi mustakbali mwema wa elimu kwa watoto na kuwataka wananchi
kujifunza athari za tukio hilo kwa Serikali, Wizara, Walimu, Wazazi, Wanafunzi
na nchi kwa jumla.
Akimalizia risala yake
hiyo, Rais Dk. Shein alitoa wito kwa wananchi wote kushiriki kwa wingi katika
shughuli mbali mbali za kuadhimisha miaka 55 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar
ya Januari 12, 1964 zitakazofanyika katika maeneo yao kwani hizo ni sherehe zao
kila mmoja ahakikishe anashiriki ipasavyo katika hatua zote.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment