Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akikata utepe kuashiria kuifungua Skuli ya Sekondari ya Kijiji Wilaya ya Kaskazini "A" Unguja iliojengwa na Kampuni ya Island Lodge, inayomilika Hoteli ya Mnemba.Matemwe Mkoa wa Kaskazini Unguja, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Balozi Seif Ali Iddi akishuhudia uzinduzi huo uliofanyika leo 17-2-2019.
Na.Abdi Shamnah. Ikulu Zanzibar.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi, Dk. Ali Moahmed Shein amesema uzinduzi wa Mabanda ya madarsa ya
skuli ya Sekondari Kijini, una mnasaba mkubwa na utekelezaji wa Ilani ya CCM ya
2015 – 2020.
Amesema wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa
2015, Viongozi wa Chama hicho waliahidi kuwaletea wananchi maendeleo ya
kiuchumi na kijamii, ikiwemo uimarishaji wa sekta ya elimu,
Dk. Shein amesema hayo katika hafla ya uzinduzi
wa madarasa manne (4) ya kusomea katika skuli ya Sekondari Kijini, Mkoa wa
Kaskazini Unguja, yaliojengwa na Mwekezaji kutoka Kampuni ya “AndBeyond”
iliyowekeza katika Hoteli ya Mnemba Lodge.
Ujenzi wa mabanda hayo ulioanza February 2018 hadi Octoba, 2018
umegharimu zaidi ya shilingi Milioni 148.5 hadi kukamilika kwake, ikiwa pamoja
na ununuzi wa samani za walimu na wanafunzi.
Dk. Shein alimpongeza mwekezaji huyo na kusema
ameonyesha njia kuelekea maendeleo ya
kielimu nchini, sambamba na kuahidi Serikali kuendeleeza juhudi hizo ili
kuimarisha sekta hiyo.
Akigusia sekta ya elimu kabla ya Mapinduzi, Dk.
Shein alisema hadi kufikia mwaka 1948, Zanzibar ilikuwa na skuli chache za
msingi na sekondari , wakati ambapo Mkoa wa Kaskazini ulikuwa na skuli ya
Mkwajuni pekee.
Alisema Wazanzibari wanyonge walishindwa kupata
elimu, kwa vile ilikuwa ikitolewa kwa misingi ya matabaka na uwezo wa mtu.
Aidha alisema wananchi wa Nungwi walinyimwa haki
ya kupata elimu baada kupotoshwa juu ya faida zake, sambamba na kuharibu
utamaduni wao.
Alisema Mapinduzi ya 1964 yalikuja kumkomboa
Mzanzibari, baada ya elimu kutolewa bure, ikiwa ni utekelezaji wa sera ya Chama
cha ASP iliyowekwa wakati wa kupigania uhuru.
Alisema hivi sasa sekta ya elimu imeimarika
nchini na imekuwa ikipatikana katika
ngazi zote kuanzia ngazi ya shina, wadi, Wilaya hadi Mikoa.
Alisema mnamo mwaka 2014, Serikali ilipanga
kuandikisha wanafunzi wa elimu ya msingi kwa asilimia mia moja hadi kufikia
mwkaa 2020, jambo ambalo limetekelezwa kabla ya wakati, ambapo hivi sasa tayari
wanafunzi walioandikishwa wamefikia asilimia 116 (116%), huku elimu ya
sekondari wakifikia asilimia 86 (86%).
Dk. Shein, alisema hivi sasa Serikali
inakamilisha ujenzi wa skuli tisa za Ghorofa katika maeneo mbali mbali Unguja na Pemba, wakati ambapo kuna Vyuo Vikuu vitatu vya elimu yajuu, kimojawapo
kikiwa cha serikali.
Alisema lengo la serikali ni kuwaandaa wanafunzi
ili kuwa na wataalamu katika fani tofauti, kwa lengo la kulisaidia Taifa pamoja
na kuwasaidia wazazi wao.
Alisema Jimbo la Kijini lina bahati kubwa, hivyo
linapaswa kuendelea kuimarishwa kielimu, akibainisha matarajio yake katika
kipindi cha miaka kumi ijayo ya jimbo hilo kupata Chuo Kikuu.
Aidha, Dk. Shein aliwataka wazee na wazazi wa
kijiji hicho kuwa imara na kuwaelimisha watoto wao, sambamba na kuepuka
upotoshaji na udanganyifu unaosambazwa na watu wasiowatakia mema.
Katika hatua nyengine Dk. Shein aliwahakikishia
wananchi wa Kijini na maeneo jirani kuwa barabara ya Mkwajuni – Kijini hadi
Mbuyutende itajengwa mwaka ujao, mara tu baada ya barabara ya Bububu –
Mkokotoni kumalizika ujenzi wake.
Alisema maandalizi ya ujenzi wa barabara hiyo
unaendelea vyema ,ambapo tayari serikali
imeagiza vifaa vinavyohitajika.
Mapema, Makamo wa Pili wa Rais wa Mapinduzi
ya Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd,
aliwataka wawekezaji wengine wenye miradi katika maeneo hayo kuiga mfano wa
kampuni ya Andbeyond’ ili kuisaidia
jamii inayowazunguka.
Alisema kuna wawekezaji wengi katika maeneo hayo,
hivyo akataka kutumia sehemu ya faida wanayopata kusaidia huduma za kijamii.
“Kutokana na uwekezaji Serikali hunufaika
kutokana na kupata mapato sambamba na wananchi kunufaika kutokana na faida
kupitia sekta za kijamii kama vile upatikanaji wA huduma za maji, afya na
barabara”, alisema.
Aliwataka wananchi hao kushirkiana na wawekezaji
wa maeneo hayo ili hatimae waweze kunufaika na matunda yatokanayo na uwekezaji.
Nae, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Riziki
Pembe Juma aliishukuru Kampuni ya ‘Andbeyond’ kwa misaada mbali mbali inayotowa
kwa wananachi wa maeneo hayo, ikiwemo uimarishaji wa elimu.
Alisema misaada hiyo inakuja kutokana na
mazingira bora yaliowekwa na Serikali kupitia sekta ya uwekezaji na kutoa fursa
kwao ya kuisaidia jamii.
Aliwataka wazazi kutumia vyema fursa zinazotolewa
na serikali na kushirikiana nayo ili kufanikisha dhana ya uimarishaji wa sekta
ya elimu nchini.
Aidha, Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Elimu
naMafunzo ya Amali Madina Mjaka alisema ujenzi wa madarasa hayo utapunguza
msongamano wa wanafunzi madarasani, hadi
kufikia wanafunzi 45 kwa darasa moja.
Aliwashajiisha wazazi na walezi wa maeneo hayo
kuthamini juhudi zinazochukuliwa kwa kuandikisha wanafunzi wote wanaopasa
kuanza masomo.
Naibu Katibu Mkuu huyo alitoa shukurani kwa
kampuni iliyofanikisha ujenzi huo kwa juhudi kubwa iliyofanya, sambamba na kushirikiana
vyema na wananchi wa eneo hilo.
No comments:
Post a Comment