Habari za Punde

SEMINAR YA UMOJA WA AFRIKA(AU-UTUMISHI NA UTAWALA)

Na.Abraham Nyantori -MAELEZO
Wajumbe kutoka Nchi 18 za Afrika zilizoridhia Mkataba wa Misingi ya Kanuni za Utawala na Utumishi wa Umma wameanza semina ya siku tatu leo, jijini Dar es salaam, Tanzania, lengo la semina likiwa ni kupeana uzoefu wa kila nchi, pia ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango Kazi wa Kamati ndogo ya Kisekta Namba Nane inayoratibu masuala ya Utumishi wa Umma na Utawala barani Afrika.

Akifungua semina hiyo katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere kwa niaba ya Mwenyekiti wa kamati Ndogo, Utumishi na Utawala (AU-STC 8) George Mkuchika, ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora) Tanzania, Naibu Waziri, Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora) Dkt Mary Mwanjelwa, amesema ni wakati wa kuzikabili changamoto zinazokwamisha maendeleo ya nchi za Afrika.

Akasema, “Ni muda mzuri sasa kukaa na kuangalia namna bora ya kuzishughulikia (changamoto),” pia akazitaja baadhi ya changamoto hizo kama upungufu wa mifumo na miundo ya utawala, upungufu wa maadili, mifumo ya kilimo, mfano, changamoto za kilimo zikitatuliwa zitaongeza usalama wa chakula.

Naibu Waziri amezitaja changamoto nyingine ni kusimamia ukuaji wa idadi ya watu, kuongeza makusanyo ya mapato ya ndani ili kupunguza utegemezi wa wafadhili, kuimarisha uwajibikaji katika kusimamia mapato ya asili, kutengeneza fursa za ajira na kuwawezesha vijana.

Kadhalika kuongeza ushiriki wa wananchi kuanzia ngazi ya chini katika maamuzi, kuboresha utoaji huduma kwa umma kwa kutumia TEHAMA, kuzirejesha katika amani nchi za Umoja wa Afrika zinazoingia katika mgogoro wa ndani na raia na kuimarisha uchumi wa Jumuiya za Kikanda kwa kuzingatia kanuni ya kuzinufaisha nchi wanachama zote.

“Ni matumaini yangu kuwa mtatumia vizuri fursa hii kujadili masuala muhimu yatakayosaidia kuboresha na kuimarisha Usimamizi wa huduma za umma ili kukabiliana na changamoto zinazoikabili Afrika na kuelekea Afrika tuitakayo.” Mhe. Dkt. Mwanjelwa amesisitiza.

Naye Mwakilishi wa Kurugenzi ya Masuala ya Kisiasa ya Umoja wa Afrika, Issaka Garba Abdou, katika hotuba yake ya utangulizi, ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa kukubali semina hiyo kufanyika Tanzania.

Amesema ni wakati muafaka kuona Afrika inakuwa na Mikataba yake inayokidhi malengo na mipango ya kila nchi mwanachama wa Umoja wa Afrika pasipo kuathiri makubaliano ya kimataifa na mipango ya maendeleo ya kila nchi.

Semina hiyo imeandaliwa na Kamisheni ya Umoja wa Afrika na imeshirikisha wajumbe kutoka nchi 18 zilizoridhia Mkataba wa Misingi ya Kanuni za Utawala na Utumishi wa Umma ambazo ni Tanzania, Algeria, Burkina Faso, Burundi, Cameroon, Ivory Coast, Kongo, Kenya, Comoros, Malawi, Mali, Msumbiji, Mauritius, Namibia, Rwanda, Afrika ya Kusini, Sao Tome&Principe na Zambia.

Aidha, ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango Kazi wa Kamati ndogo ya Kisekta Namba 8 inayoratibu masuala ya utumishi wa umma na utawala katika Bara la Afrika. Waziri wa Utumishi na Utawala Bora ni Mwenyekiti wa Kamati.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.