Habari za Punde

HOTUBA YA RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI, MHESHIMIWA AL-HAJJ DK. ALI MOHAMED SHEIN, KATIKA BARAZA LA IDD EL FITRI, MWEZI MOSI MFUNGUO MOSI, 1440 HIJRIYA - JUNI, 2019


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Alhajj Ali Mohamed Shein, akihutubia Baraza la Eid El Fitry katika ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil Kikwajuni Zanzibar. 

BISMILLAHI RAHMANI RAHIM
Assalam Aleikum Warahmatullahi Wabarakatuh

IDD MUBARAK
Kwa hakika, ni wajibu wetu kumshukuru Mwenyezi Mungu; Subhanahu wa Taala, Mwingi wa Rehema na Utukufu.  Mola ambaye kwa rehema na utukufu wake ametujaaliya neema ya uhai na afya njema tukaweza kuifikia sikukuu hii ya Idd el Fitr, tukiwa salama na wenye amani na furaha.  Kwa mapenzi na rehema zake Allah, tumeweza kuikamilisha ibada ya saumu ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na kuifikia siku hii ya Idd. Tumsalie na tumtakie rehema na amani Mtume wetu Muhammad (S.A.W), yeye na ahli zake, Masahaba, Maulamaa na Wafuasi wake wote walioongoka kwa kufuata mwendo na miongozo yake.

Katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani tulioumaliza jana, kuna ndugu, jamaa na Waislamu wenzetu ambao tulianza kufunga pamoja nao na hivi sasa wameshafika mbele ya haki. Kwa hivyo, sisi tulio hai hadi leo, tunapaswa kuzitafakari rehema za Mwenyezi Mungu kwa mazingatio makubwa. Tunamuomba Mwenyezi Mungu awarehemu Waislamu wenzetu wote waliokwishatangulia mbele ya haki na sisi atujaalie khatma njema.

Kwa baraka za siku hii, namuomba Mola wetu Mtukufu awape subira wale wote walioondokewa na ahli zao, wazazi, ndugu, watoto na wahisani ambao walitegemea kula nao sikukuu pamoja. Kadhalika, tunamuomba Mwenyezi Mungu awajaalie afya njema wagonjwa wetu walioko hospitali na nyumbani.  Vile vile, na sisi na familia zetu atujaalie sikukuu njema na kila lenye kheri. Aizidishie nchi yetu amani na utulivu, na atudumishe katika mapenzi na mshikamano zaidi baina yetu.

Ndugu Wananchi,
Natoa salamu zangu za Idd kwenu nyote mliohudhuria kwenye Baraza hili, wale wanaotufuatilia katika vyombo vya habari, kwa wananchi na Waislamu wote duniani katika kuisherehekea siku hii. Leo tumekusanyika katika Baraza la Idd kwenye ukumbi huu wa Marehemu Sheikh Idris Abdulwakil, tukiungana na Waislamu wote duniani kwa ajili ya kuisherehekea Sikukuu ya Idd el Fitr.  Shughuli hii ilitanguliwa na sala ya Idd wakati wa asubuhi, ambayo Kitaifa kwa upande wa Zanzibar ilisaliwa katika viwanja vya Maisara na vile vile, ilisaliwa katika misikiti mbali mbali.  Kwa hakika, Mwenyezi Mungu ametuwekea siku hii, ili iwe ya furaha baada ya kukamilisha utekelezaji wa maamrisho yake ndani ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Tunamuomba Mola wetu Mtukufu azikubali saumu zetu tulizozitekeleza pamoja na ibada zote tulizozifanya katika mwezi wa Ramadhani tukitaraji malipo kutoka Kwake, ikiwa ni pamoja na kutusamehe makosa yetu mapya na yaliyotangulia kabla. Imepokelewa hadithi ya Mtume wetu Muhammad (S.A.W), kutoka kwa Imaam Al-Bukhariy na Muslim inayosema:   
“Atakayefunga Ramadhani kwa imani na kutaraji malipo, ataghufuriwa madhambi yake yaliyotangulia”.

Inshaallah Mwenyezi Mungu, atujaalie tuwe ni miongoni mwa watu hao, atulipe fadhila nyingi pamoja na kutusamehe makosa yetu kwa baraka na utukufu wa mwezi wa Ramadhani.
Ndugu Wananchi,
Baraza la Idd ni kikao chenye haiba na umuhimu mkubwa.  Haiba ya mkusanyiko huu inadhihirika katika nyuso zetu za furaha na mavazi yetu ya kupendeza katika siku hii. Kadhalika, hafla hii inatupa wasaa wa kukutana  na ndugu,  jamaa, marafiki na  viongozi mbali mbali, kwa pamoja, ili tuweze kukumbushana na kubadilishana mawazo  juu ya mambo  mbali mbali  yenye mnasaba na siku hii, yaliyopita na yaliyopo ambayo yanahusiana na ustawi wa maendeleo ya nchi yetu.

Ilivyokuwa ni jana tu Mwenyezi Mungu ametujaalia tumeikamilisha funga ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, kwa hivyo, ni vyema tukaendelea kukumbushana  na kuhimizana juu ya umuhimu wa kuyadumisha tuliyojifunza katika mwezi wa Ramadhani na tufungamane nayo, ili iwe ni tabia itakayojengeka katika kuyaendesha maisha yetu. Kwa hakika, tukifanya hivyo ndipo tutakuwa tumehitimu vyema kwenye mafunzo tuliyoyapata na tutaweza kutimiza lengo la kuumbwa kwetu hapa duniani, ambalo ni kumuabudu Mwenyezi Mungu mmoja Subhaanahu wa Taala, bila ya kumshirikisha na chochote. Mwenyezi Mungu ametaja uovu wa kumshirikisha katika aya kadhaa ndani ya Kitabu Chake kitakatifu cha Qurani, na miongoni mwao ni Aya ya 13 ya Surat Luqman ambayo tafsiri yake inasema:
“Na (wakumbushe), Luqmani alipomwambia mwanawe, na hali ya kuwa anampa nasaha. Ewe mwanangu! Usimshirikishe Mwenyezi Mungu maana shirki ndio dhulma kubwa”.

Ndugu Wananchi,
Katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani tulizidisha uchamungu wetu kwa kufanya vitendo vingi vyenye kheri. Kama kawaida, ibada zetu za saumu zilifuatiwa na sala za faradhi na sunna, ambapo misikiti ilifurika waumini kwa sala na darsa zilizoongozwa na Maimamu, Mashehe na Walimu wetu. Tulisimama imara kwa umoja wetu bila ya kujali muda katika sala za tarawehe. Tulijenga mapenzi na huruma kwa kupeana sadaka mbali mbali, kupelekeana vyakula vya tunu, kuftari pamoja na kusaidiana katika njia za kheri. Tumejifunza mengi juu ya kuishi kwa umoja na mshikamano.
Vile vile, tuliendeleza kusoma sana Qurani na tulishuhudia mashindano ya kuhifadhi Qurani yaliyowashirikisha watoto wetu wa umri tafauti. Kadhalika, waumini wengine waliushindikiza Mwezi wa Ramadhani kwa kukaa itikafu misikitini. Mambo haya yote yalikuza imani zetu na kumcha Mwenyezi Mungu.  Vile vile, yalituwezesha kurejesha mwenendo na utamaduni mzuri wa maisha yetu. 

Ni dhahiri mambo hayo yote mazuri tuliyoyafanya yalikuwa ni kwa lengo la kufuata sheria za dini yetu, ili kutafuta radhi, fadhila na baraka za Mwenyezi Mungu katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani. Mwenyezi Mungu Inshaallah atutakabalie ibada zetu, ili ziwe ni sababu ya kupata malipo ya daraja ya juu, kama ambavyo Mwenyewe Azza wa Jalla alivyotuahidi katika Aya ya 20 ya Suratul Muzammil, ambayo tafsiri yake ni kama ifuatavyo:

 “Na chochote mnachokitanguliza kwa (ajili ya) nafsi zenu katika mambo ya kheri (basi) mtakikuta kwa Mwenyezi Mungu kikiwa bora (zaidi) na malipo makubwa (zaidi)”. 

Ndugu Wananchi,
Ibada ya saumu ilitufunza kuwa watiifu kwa kujiepusha na mambo yote ambayo yangeweza kuzibatilisha funga zetu.  Tulijitahidi sana kujiepusha na vitendo vya dhulma, wizi, kusema uongo, kusengenya na maasi mengine. Mwenendo huu ulichangia kutufanya tuwe waumini wazuri na raia wema.  Kwa hivyo, ili tuongeze ufanisi katika maendeleo ya jamii yetu, nasisitiza kwamba tuendelee na mwenendo mzuri wa kutafuta radhi za Mola wetu hata katika miezi mingine baada ya kumalizika kwa mwezi Mtukufu wa Ramadhani.  Bila ya shaka, kuuendeleza mwenendo huo baada ya mwezi wa Ramadhani ni jambo muhimu, kwani kutaiwezesha jamii yetu isiwe na vitendo vya uvunjaji wa sheria na ukiukaji wa maadili, silka na utamaduni tulioachiwa na wazee wetu.


Ndugu Wananchi,
Mwezi wa Ramadhani ni mwezi mtukufu wenye ubora wa pekee kwa wanaadamu hasa kwa Waislamu.  Kila Muislamu ana wajibu wa kuuheshimu kutokana na ubora wake. Miongoni mwa mambo yanayoufanya mwezi wa Ramadhani kuwa bora ni kwamba ndani ya mwezi huu iliteremshwa Quran tukufu.  Mwenyezi Mungu ametueleza  katika Suratul Qadr aya 1 na ya 3, katika tafsiri isemayo:-
1.   “hakika tumeiteremsha (Qurani) katika Laylatul - Qadr (usiku wenye hishima kubwa), (usiku  wa mwezi wa Ramadhani).
3.“huo usiku wa hishima (huo) ni bora kuliko miezi elfu”.

Kwa mnasaba wa  aya hizi, tunatakiwa tuuheshimu na tufanye ibada kwa wingi na kwa nia safi,  ili tufaidike na baraka na neema za Mola wetu. Mwenyezi Mungu ameendelea kuonya juu ya kwenda kinyume na maamrisho yake.  Mwenyezi Mungu ametutaka tutoe neema alizotupa kwa njia ya kutafuta radhi Zake na tuepukane kabisa kuzitumia neema hizo kwa njia isiyofaa kama alivyosema katika aya ya 195 ya Suratul Baqarah; yenye tafsiri isemayo:-
Na toeni katika njia ya Mwenyezi Mungu, wala msijitie kwa mikono yenu katika maangamizo. Na fanyeni wema, hakika Mwenyezi Mungu huwapenda wafanyao wema”.

Inasikitisha kuona kwamba pamoja na nasaha mbali mbali kutoka kwa Mola wetu kuhusu kuzitumia kwa njia sahihi neema alizotupa, nasaha ambazo sisi waumini tumekuwa tukizikariri, ili kutanabahisha juu ya kuuenzi mwezi wa Ramadhani, bado tulisikia vikiripotiwa vitendo viovu  vilivyoashiria baadhi ya watu kutouheshimu mwezi huo. Yaliripotiwa matukio ya wizi madukani unaofanywa na watu wasio waaminifu. Kuliripotiwa vitendo vya baadhi ya vijana kukutwa wakivuta sigara mchana hadharani. Vile vile, tumesikia matukio yanayohusiana na matumizi ya dawa za kulevya.  Zaidi ya yote, bado taarifa za kuendelea kwa vitendo vya ubakaji vilisikika katika mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
Kwa hakika, hayo si mambo ya kuridhisha hata kidogo. Vitendo vya aina hii sio tu vinaiaibisha jamii yetu, bali, vilevile, vinakwenda kinyume cha maadili mema  ambayo Mola wetu ametuamrisha tuwe nayo hasa katika Mwezi wa Ramadhani.  Natoa wito kwa wananchi wote waviache vitendo vya aina hio ambavyo ni kinyume na maamrisho ya Mwenyezi Mungu. Nawanasihi Mashekhe na Walimu wetu waendelee kutoa mawaidha juu ya umuhimu wa kuyaheshimu maamrisho ya Mwenyezi Mungu kwa kufuata mwenendo wa maadili mema na kubainisha madhara ya kuhalifu maamrisho ya Mola wetu Subhanahu Wataala.  Mategemeo yangu ni kuwa nasaha hizo zitasaidia kuiepusha jamii yetu na mitihani ya aina hio kwa sasa na baadae.

Ndugu Wananchi,
Nnawanasihi wananchi wenzangu kuwa tunapaswa tuzitii sheria za nchi yetu, ili na wageni wanaoitembelea nchi yetu waweze kuuiga mfano wetu, na hatimae tuendelee kuishi katika hali ya salama na amani. Nchi inayothamini na kufuata misingi ya utawala bora, watu wake huwa na uvumilivu maalum wa kuishi pamoja katika jamii yenye watu wenye imani tafauti za kidini na kiutamaduni. Watu wa Zanzibar na Watanzania kwa ujumla, tumekuwa ni kigezo kizuri miongoni mwa nchi kadhaa duniani katika kuuendeleza ustaarabu huo wa uvumilivu tangu hapo kale na dahari. Kwa hakika uvumilivu ni miongoni mwa sababu zinazotuepusha na migogoro ya wenyewe kwa wenyewe nchini mwetu. Tumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa tunu hii, tutahakikisha kwamba tunailinda amani na usalama nchini mwetu kwa kila hali.

Ni jukumu letu kwamba kila wakati tutafakari hali za wenzetu waliokosa amani katika baadhi ya nchi duniani. Tunayaona na tunayasikia katika  vyombo vya habari madhila na mateso wanayoyapata watu wa nchi hizo. Kuna Waislamu wenzetu ambao wametekeleza ibada ya saumu katika hali dhalili ya taharuki na unyonge kutokana na tatizo la kukosa amani na usalama, tena wakiwa katika nchi zao wenyewe.  Tunamuomba Mwenyezi Mungu atuepushie mbali na hayo na wao awaondoshee mtihani huo.

Ndugu Wananchi,
Kuwepo kwa amani na utulivu nchini kumetuwezesha kuzidi kupiga hatua za ufanisi za utekelezaji wa mipango yetu mikuu ya maendeleo ambayo ni MKUZA III, Dira ya Maendeleo ya 2020, Mpango wa Dunia wa Maendeleo Endelevu na Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya Mwaka 2015-2020.  Utekelezaji wa mipango yetu hio umetuwezesha kupata mafanikio katika ukuaji wa uchumi na uimarishaji wa huduma mbali mbali.  Katika hali hii ya kupata mafanikio makubwa, tunapaswa tumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kuyafikia mafanikio haya.

Katika Aya ya 7 ya Suratul Ibrahim, Mwenyezi Mungu ameahidi kutuzidishia neema tutakapomshukuru aliposema:
“Na (kumbukeni) alipotoa tangazo Mola wenu (kwamba), iwapo mtanishukuru (kwa neema nilizokujaalieni), basi nitakuzidishieni (neema hizo); (lakini) iwapo mtazikufuru (neema hizo) basi hakika adhabu yangu ni kali (kabisa)”.

Kutokana na aya hii, sote tuna wajibu wa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia kuwa na uchumi unaokua mwaka hadi mwaka. Katika mwaka wa fedha wa 2018 uchumi wetu ulikua kwa asilimia 7.1, kutoka asilimia 7.0 na  mfumko wa bei uliendelea kushuka; kutoka kasi ya asilimia 5.6 mwaka 2017 hadi kufikia  asilimia 3.9 mwaka 2018.

Katika kuimarika kwa uchumi wetu,  makusanyo ya mapato yameongezeka na kufikia TZS bilioni 668.70 mwaka 2017/2018 kutoka TZS bilioni 181.48 mwaka 2010/2011.  Hii ni sawa na ongezeko la mara 3.7.   Kadhalika, pato la mtu binafsi ambalo lilikuwa TZS 942,000 mwaka 2010, limeongezeka na kufikia TZS 2,323,000 mwaka 2018 ikiwa ni sawa na ongezeko la asilimia 146.7 

Kasi yetu hio ya makusanyo na utekelezaji wa mipango yetu ya maendeleo, inatupa matarajio ya kukua kwa uchumi wetu kufikia asilimia 7.8 katika mwaka wa fedha wa 2019/2020. Kwa hivyo hapana shaka kwamba Zanzibar itafikia nchi yenye uchumi wa kati ifikapo mwaka 2020, kama ilivyolengwa katika Dira ya Maendeleo ya Zanzibar ya 2020.

Mafanikio hayo makubwa tuliyoyapata katika kuongeza mapato na kukuza uchumi wetu, yametokana na jitihada za pamoja za Viongozi, Wizara, Washirika wa Maendeleo, Taasisi mbali mbali za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikiwemo Mamlaka ya Mapato ya Tanzania (TRA) na Bodi ya Mapato ya Zanzibar (ZRB), Wakulima, Wafanyakazi pamoja na wananchi wote kwa jumla.  Natoa shukurani kwenu nyote kwa ushirikiano wenu.  Ni dhahiri kuwa tuna wajibu wa kuongeza bidii katika kutekeleza majukumu yetu, ili tuendelee kupata ufanisi na kupiga hatua zaidi za mafanikio.

Ndugu Wananchi,
Historia ya Uislamu inaeleza kwamba katika matayarisho ya vita vya Taabuk ambavyo jeshi la Warumi lilipanga kupigana na jeshi la Waislamu, Bwana Mtume Muhammad (S.A.W) aliwatangazia Waislamu kuchangia, ili kuliongozea nguvu jeshi hilo liweze kuelekea katika mapambano kwa uhakika na ufanisi.

Tukizingatia mantiki ya historia hii kwa mnasaba wa maendeleo ya nchi yetu na watu wake, tutaihusisha na ulipaji wa kodi.  Serikali haina uwezo wa kumpa kila mtu mmoja mmoja pesa za matumizi katika kuendesha maisha yake, ila humlipa kupitia huduma mbali mbali Serikali inazozitoa kwa wananchi. Kwa hivyo, kila kiongozi, kwa nafasi aliyo nayo, itamlazimu asimamie suala la ulipaji kodi pamoja na utoaji wa risiti. Tuendelee kushajiishana juu ya utoaji na uchukuaji wa risiti, ili kuhakikisha kwamba kila senti inayopaswa kukusanywa na Serikali inakusanywa. Hata Uislamu umetufundisha haja ya kuandikiana mahali ambapo miamala ya pesa inafanyika, kwa sababu kuwepo kwa stakabadhi ya maandishi ni ushahidi madhubuti. Aya ya 282 ya Suratul Baqara inatoa taswira ya mafundisho haya.

Natoa wito kwa wafanyabiashara wetu watambue umuhimu wa kutoa risiti zilizo halali katika biashara zao na kulipa kodi kwa mujibu wa sheria. Ni dhahiri kuwa sehemu kubwa ya mapato yetu inatokana na kodi.  Kwa hivyo, nawahimiza wafanyabiashara wauendeleze utaratibu huo kwa imani na mapenzi kwa kutambua kuwa huo ni wajibu wao wa kisheria, ili Serikali ipate fedha za kutolea huduma na kuiendeleza miradi mbali mbali ya maendeleo. Serikali ni sisi wenyewe wananchi. Tunapokuwa tayari kuichangia Serikali, huwa tunaharakisha maendeleo ya nchi yetu ambayo yanafanywa kwa lengo la kuleta ustawi wetu kwa wananchi wote.

Ndugu Wananchi,
Katika kusimamia utekelezaji wa kazi za Serikali pamoja na kusimamia mapato na matumizi ya fedha za Serikali, kuanzia tarehe 13 Mei, 2019 hadi tarehe 27 Mei, 2019, niliendelea na utaratibu wetu wa vikao vya uwasilishaji wa utekelezaji wa Mipango Kazi kwa kila robo mwaka (maarufu kwa jina la Bango Kitita). Wizara zote za Serikali na Taasisi zake, ziliwasilisha kwa mujibu wa malengo na majukumu ya msingi ya kila Wizara. Vikao hivyo huwa vinafanyika Ikulu.  Kwa jumla, Wizara zote zimeonesha ufanisi mkubwa katika kuhakikisha fedha zilizoidhinishwa kwa matumizi ya robo tatu ya mwaka kuanzia Julai, 2018 hadi Machi, 2019 zimetumika vyema na mafanikio makubwa ya utekelezaji wa kazi zilizopangwa yamepatikana.

Miongoni mwa mambo yaliyochangia mafanikio yetu ni umakini tulioutumia na usimamizi madhubuti katika kudhibiti  uvujaji wa mapato pamoja na matumizi ya fedha za Serikali na wahisani wetu wa maendeleo kwa mujibu wa bajeti na mipango tuliyojipangia kuitekeleza.  Serikali imeridhika na kiwango cha uwajibikaji kilichooneshwa na Wizara zetu zote na Taasisi zake katika kutumia fedha zilizoidhinishwa na Baraza la Wawakilishi kwa mujibu wa sheria na taratibu za matumizi zilizopo.

Kwa mnasaba huu, natoa pongezi kwa Mawaziri, Manaibu Mawaziri, Watendaji na Watumishi wote wa Serikali na Taasisi zake kwa mafanikio hayo na ufanisi tunaoendelea kuupata katika kukuza uchumi, kuimarisha huduma za wananchi na kuwapatia huduma mbali mbali wananchi kwa ufanisi.  Natoa wito kwa viongozi wote katika Wizara na Taasisi za Serikali waendelee kusimamia vizuri utekelezaji wa shughuli zao, na watendaji wengine waongeze bidii, ili tupate mafanikio zaidi.  Ni vyema tukaiga mbinu za mwanariadha mzuri ambaye huwa anaongeza kasi na bidii kwa kadiri anavyokaribia mfundani. Maendeleo ya nchi hayana kikomo, kwani kadri miaka inavyoingia na kutoka huwa inakuja na mambo na taratibu mpya, kwa sababu ulimwengu unasonga mbele. Na sisi, ili tusiachwe nyuma inatulazimu twende na kasi ya maendeleo duniani kwa mujibu wa uwezo tulio nao. Kwa hivyo, mfunda wetu ni ile mipango yetu tunayoipanga kuitekeleza katika kipindi cha mwaka mmoja lazima tuitekeleze. Ni wajibu wetu tukaze kamba, ili tuweze kufika kwa ufanisi katika mfunda huo. Nna matumaini makubwa kuwa tunaweza kufanya vizuri zaidi iwapo kila mmoja wetu atatimiza wajibu wake kwa uzalendo mkubwa.

Ndugu Wananchi,
Ushirikishwaji wa wananchi katika mipango na shughuli zao za maendeleo ni miongoni mwa nguzo za utawala bora. Kwa kuzingatia ukweli huu, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuanzia mwezi Julai, 2017, ilianzisha rasmi mfumo wa ugatuzi, ili kushusha madaraka kwa wananchi kutoka Serikali kuu na kuyaweka katika usimamizi wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.  Kwa hatua za awali, tumeanza na sekta tatu ambazo ni elimu ya msingi na maandalizi, afya ya msingi na kilimo katika huduma za ugani.  Mfumo huu ni mpya hapa petu, lakini ni mfumo unaotumika katika nchi mbali mbali ambazo zimepata mafanikio makubwa.

Sote tunafahamu kuwa “Mwanzo mgumu”. Kwa vile upya wa jambo lolote huwa na changamoto zake, bila ya shaka na hapa petu mfumo wa ugatuzi tumebaini tayari una changamoto kadhaa. Lakini nataka niwathibitishie wananchi kuwa tumeanza kupata mafanikio katika kuimarisha huduma za sekta zilizogatuliwa katika kuwatumikia wananchi.

Kwa hivyo, changamoto zinazojitokeza katika kipindi hiki cha mpito  kama vile uhaba wa baadhi ya wataalamu, ufinyu wa nafasi za ofisi  za kufanyia kazi, nyenzo za kufanyia kazi, na kadhalika.  Changamoto hizi zisiwe sababu ya kuturudisha nyuma na kuona kwamba mfumo wa ugatuzi haufai.  Natoa wito kwa mamlaka zinazohusika katika sekta zilizogatuliwa zikae pamoja na wazifanyie kazi kwa haraka changamoto hizo.

Ndugu Wananchi,
Hatuna budi tufahamu kwamba kujadili mambo yetu kwa kushauriana kwa  lengo la kutatua matatizo yetu, ni jambo tuliloagizwa katika Uislamu. Tukirejea katika Qurani Tukufu Suratul Shuuraa, Aya 38 inatwambia:
Na wale waliomwitikia Mola wao (kwa kila amri Zake) na wakasimamisha sala na wanashauriana katika mambo yao..”

Kwa hivyo, ni matumaini yangu kwamba tutaendelea kushauriana jinsi ya kutatua changamoto hizo, ili hatimae tuone jinsi utaratibu wa ugatuzi unavyoweza kuleta mafanikio tuliyoyatarajia kama zilivyofanikiwa nchi nyengine. Lengo letu ni lazima tuondokane na urasimu usio wa lazima katika kuwatumikia wananchi, kwani tunafahamu kwamba wananchi ndio waajiri wetu waliotupa dhamana ya kuwatumikia.  Tutaendelea kufanya kazi kwa uzalendo mkubwa na tutawajibika zaidi, tukiamini kuwa maendeleo yetu tutayaleta sisi wenyewe.

Natoa pongezi kwa wananchi kwa kuendelelea kushirikiana na  viongozi wa ngazi mbali mbali za Serikali za mitaa katika kuyatekeleza maagizo na miongozo inayoendelea kutolewa na Serikali Kuu, kuhusu kuyahifadhi  mazingira pamoja  na utunzaji na utumiaji wa rasilimali zisizorejesheka, hasa uchimbaji wa mchanga, mawe, kifusi na kadhalika. Mafanikio katika masuala haya, yatategemea sana juhudi za viongozi wa Mikoa, Wilaya na wa Serikali za Mitaa kwa kuzingatia kwamba utendaji wao unayagusa moja kwa moja maisha ya kila siku ya wananchi. Kwa pamoja tuendelee kushirikiana katika kuhakikisha kwamba tunakuwa na mipango madhubuti na endelevu ya kuzitunza vizuri rasilimali zetu kwa faida yetu na kwa vizazi vijavyo.  Lazima tufanye jitihada katika kuzuia uharibifu wa mazingira kabla ya uharibifu huo haujatokea.  Tukumbuke msemo maarufu usemao: “Kinga ni bora kuliko tiba”.
Ndugu Wananchi,
Kama tunavyoelewa kwamba mwezi Mtukufu wa Ramadhani uliingia katika msimu wa mvua za masika ambazo kwa kiasi fulani bado zinaendelea. Tumeshuhudia mvua kubwa zilizonyesha katika kipindi hiki cha mwezi wa Mei ambapo kituo cha Uwanja wa Ndege wa Kimataifa cha Abeid Amani Karume kimerikodi milimita 167.2 kwa muda wa saa 24, kwa mvua iliyonyesha tarehe 5 Mei, 2019.

Kutokana na mvua zilizonyesha katika siku chache kuanzia tarehe 5 Mei, Kamisheni ya Kukabiliana na Maafa Zanzibar iliripoti uharibifu wa miundo mbinu ya barabara katika sehemu mbali mbali za Unguja na Pemba, ikiwemo baadhi ya misingi inayoendelea kujengwa kupitia Mradi wa Uendelezaji wa Huduma za Miji (ZUSP). Kadhalika, katika ripoti hio ilielezwa kuwa nyumba zipatazo 2,120 zimeathiriwa na mvua hizo. Hata hivyo, katika baadhi ya maeneo ya Mji wa Zanzibar katika sehemu ambazo misingi hiyo imejengwa, imebainika kuwa hakukuwa na uharibifu na kwamba misingi hio ilileta nafuu kubwa.

Ndugu Wananchi,
Serikali inaendelea na jitihada zake za kuifanyia kazi changamoto inayoendelea kutukabili ya uharibifu wa miundombinu ya barabara pamoja na madaraja katika msimu wa mvua. tumepata matumaini makubwa kuona kwamba matengenezo yaliyofanywa yametuwezesha kuzitumia barabara hizo, licha ya mvua kubwa zilizokuwa zikinyesha. Bila ya shaka, ujenzi wa miundombinu ya baadhi ya barabara, madaraja na misingi utakapokamilika rasmi matatizo yaliyokuwa yanajitokeza katika maeneo hayo wakati wa mvua yataondoka.

Natoa pongezi kwa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji kwa kutekeleza agizo nililowapa la kulitafutia ufumbuzi wa kudumu tatizo la maji la Kibonde Mzungu kwa kujenga daraja la kisasa. Naiagiza Wizara hio iendelee na kazi ya kuiunganisha  barabara ya Fuoni kutoka kwenye kituo cha Polisi hadi ifike  Kibonde Mzungu. Vile vile, naithamini sana kazi inayofanywa na Wizara  hio kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha kupitia Mradi wa ZUSP  ya kutekeleza agizo  langu la  kuinyanyua barabara  katika eneo la Bwawa la Mwanakwerekwe. Vile vile, nakupongezeni kwa kazi nzuri mlioifanya ya ujenzi wa msingi mkubwa kwa ajili ya kuyaondoa maji yaliyokuwa yakituama katika eneo la Kiembesamaki.  Msingi huo uliopitia Mbweni hadi pwani ya Mazizini, umelipatia ufumbuzi wa tatizo la miaka mingi. Nakuhimizeni muharakishe mipango mliyonayo ya kuzifanyia matengenezo barabara zetu zilizoharibika kwa mvua mara baada ya mvua hizi zitakaposita kunyesha.

Natoa pole sana kwa wananchi wote waliopata athari kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha.  Serikali ilifanya tathmini ya athari hizo na hatua za kuwasaidia wananchi waliofikwa na maafa hayo zimeshaanza kuchukuliwa. Hata hivyo, kwa mara nyengine nawanasihi wananchi waache kujenga katika maeneo ya mabondeni na katika njia za maji, ili kuepuka hasara zinazotokana na mvua.  Wakati wote tuzingatie msemo mashuhuri usemao: “Tahadhari, kabla ya athari”.

Katika jitihada za kuimarisha miundombinu ya barabara, Serikali  imenunua mtambo wa lami wa kisasa  pamoja na kuagiza zana na vifaa vya kisasa kwa  ajili ya utekelezaji wa miradi  ya ujenzi wa barabara mpya pamoja na ukarabati wa baadhi ya barabara za zamani za Unguja na Pemba. Mtambo huo wa lami pamoja na vifaa vilivyoagizwa vimegharimu jumla ya TZS bilioni 14.8.  Kazi ya ufungaji wa Mtambo wa lami inaendelea wakati zana na vifaa tulivyoviagiza vinategemewa kuwasili nchini mwezi huu.  Kuwepo kwa vifaa hivi vya kisasa, kutapunguza utegemezi wa kampuni za kigeni katika kuendeleza na kuimarisha barabara zetu na kutatuwezesha kutekeleza miradi mingi ya bababara kwa wakati mmoja kwa Unguja na Pemba.

Ndugu Wananchi,
Wakati tulipokuwa katika mwezi Mtukufu wa Ramadhani, wenzetu Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wamekuwa wakiendelea na  vikao  kwa ajili ya kusoma, kujadili na kupitisha  bajeti za Serikali  kwa mwaka wa Fedha wa 2019/2020.  Nachukua fursa hii kumpongeza tena Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid, Spika wa Baraza la Wawakilishi,Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi, Wenyeviti wa Baraza, Viongozi wa Kamati za Kudumu za Baraza na Waheshimiwa Wawakilishi wote kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuwawakilisha wananchi na kuisimamia Serikali.  Nimekuwa nikifuatilia mijadala ya vikao hivyo na nimeridhishwa sana na michango ya Waheshimiwa Wajumbe ambayo inaonesha wazi kuwa ina lengo la kuendeleza jitihada za Serikali na kuongeza kasi yetu ya maendeleo.

Natoa shukurani kwa viongozi wa Serikali katika Baraza la Wawakilishi wakiongozwa na Makamo wa Pili wa Rais Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, kwa namna wanavyoiwakilisha Serikali na kujibu hoja za Waheshimiwa Wawakilishi.  Nalitakia Baraza letu kila la kheri na mafanikio katika kumalizia kazi yao hio ya kikatiba.

Ndugu Wananchi,
Ombi langu kwenu wananchi ni kuwa muendelee kuzisikiliza na kuzifuatilia Hotuba za Bajeti za Wizara mbali mbali za Serikali kadri zinavyoendelea kuwasilishwa katika Baraza la Wawakilishi. Hadi hivi sasa tayari Wizara kumi na moja zimeshawasilisha Hotuba zao za Bajeti na zimepitishwa na Baraza.  Hapana shaka wananchi mmekua mkiyafuatilia majadiliano yanayoendelea kuhusu Bajeti za Wizara za Serikali.

Vile vile, nataka nikukumbusheni wananchi nyote kwamba msikose kuisikiliza bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2019/2020 itakayosomwa na Waziri wa Fedha na Mipango inayotegemewa kuwasilishwa  tarehe 20 Juni, 2019, ili muweze kuijua mipango ya Serikali na fedha zitakazotumika katika kuitekeleza mipango hio kwa ajili ya maendeleo yetu.

Ndugu Wananchi,
Ni kawaida katika Baraza hili la Idd el Fitr kuwatakia kheri na matayarisho mema Waislamu wenzetu ambao Mwenyezi Mungu amewajaalia wasaa wa kwenda kuitekeleza ibada ya Hija huko Saudi Arabia.  Tunamuomba Mola wetu Mtukufu awape afya njema, ili waweze kuitekeleza vyema ibada hio. Tunawaombea safari yao ya kwenda na kurudi iwe ya salama na utulivu. Tunamuomba Mwenyezi Mungu azikubali ibada zao zote.  Mwenyezi Mungu awape uwezo, nguvu na hamu ya kuitekeleza ibada ya Hija Waislamu wenzetu ambao bado hawajajaaliwa kwenda kuitekeleza ibada hio.

Kadhalika, natoa shukurani kwa wafanyabiashara wote ambao waliitikia wito nilioutoa katika nasaha zangu za kuukaribisha mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa kuwapunguzia wananchi bei za bidhaa mbali mbali. Ndugu zetu wafanyabiashara wanapaswa wajue kuwa hawakupoteza kitu, ila wametoa sadaka na kufanya uadilifu, mambo ambayo yana malipo makubwa mbele ya Mwenyezi Mungu.

Katika kuwafikiria na kuwapa msaada watu wenye mahitaji, kuna hadithi ya Mtume Muhammad (S.A.W) iliyopokelewa na Imam Muslim inayosema:
     Mtu mwenye kujali haja za ndugu zake, basi Mwenyezi Mungu huzijali haja zake”.

Kwa hakika, wenzetu wafanyabiashara wana haja nyingi zenye mnasaba na mafanikio ya shughuli zao. Kwa hivyo, kutokana na hadithi hii bila ya shaka, Mwenyezi Mungu atawaongezea baraka na ufanisi katika biashara zao.

Ndugu Wananchi,
Natoa shukurani kwa uongozi na wafanyakazi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati na Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) kwa kuwapatia huduma ya maji wananchi wenzetu ambao huduma za maji hazipatikani vyema katika maeneo yao. Nnazo taarifa kwamba katika kipindi cha mwezi wa Ramadhani, huduma za maji safi na salama ziliimarika katika maeneo mengi ya Mkoa wa Mjini Magharibi. Mafanikio haya, yanatihibisha kwamba ZAWA wana uwezo mkubwa wa kuimarisha utoaji wa huduma za maji safi na salama. Juhudi hizi lazima ziendelezwe katika kipindi chote.

Natoa shukurani kwa vyombo vya Ulinzi na Usalama kwa ajili ya kusimamia ulinzi wa nchi yetu katika maeneo yote, kusimamia hali ya usalama wa wananchi na kukabiliana na madereva wanaovunja sheria za usalama barabarani.  Hata hivyo, polisi wa usalama barabarani waendeleze jitihada za kufanya wajibu wao, hasa katika kipindi hiki cha sikukuu ambapo wananchi wengi hutumia barabara zetu.  Vile vile, wazazi na sisi walezi tuendelee kusimamia malezi na usalama wa watoto wetu, ili tuwalinde na mambo ambayo yanaweza kuwadhuru na yanayoweza kutuondeshea furaha ya sikukuu.

Namalizia hotuba yangu kwa kukutakieni nyote sikukuu njema yenye furaha na amani.  Tumuombe Mola wetu Mtukufu atuzidishie amani, umoja na mshikamano.  Aizidishie neema nchi yetu na atupe uwezo mzuri wa kupanga na kuitekeleza mipango yetu ya maendeleo kwa ufanisi zaidi.  Mwenyezi Mungu atupe neema ya mvua yenye kheri na baraka ya mazao na atuondoshee mitihani na khofu, kwani Yeye peke yake ndiye tunaemtegemea.  Namuomba Mwenyezi Mungu aturudishe sote nyumbani kwa salama na amani.

IDD MUBARAK
WAKULU AAM WAANTUM BIKHEIR
Ahsanteni kwa kunisikiliza.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.