Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Azungumza na Mwakilishi wa UNESCO Tanzania.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akimsikiliza  Mwakilishi wa Shirika la UNESCO Tanzania Bw.Tirso  Dos Santos (kushoto) wakati wa mazungumzo yao yaliyofanyika leo alipofika Ikulu Mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha. 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza umuhimu wa kukuza uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulkia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) ili kuendeleza miradi kadhaa inayosimamiwa na Shirika hilo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar alipofanya mazungumzo na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) Tirso Dos Santos, wakati Mwakilishi huyo alipofika Ikulu kwa ajili ya kujitambulisha na kumsalimia Rais.

Rais Dk. Shein alimueleza Mwakilishi huyo wa (UNESCO) kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini sana uhusiano na ushirikiano uliopo kati yake na Shirika hilo, hivyo ni vyema hatua hiyo ikaendelezwa kwa azma ya kuimarisha miradi kadhaa iliyopo hapa nchini.

Alieleza kuwa Shirika hilo limeweza kushirikiana na Zanzibar kwa muda mrefu hatua ambayo imepelekea kuimarika kwa miradi kadhaa ambayo (UNESCO) inaiunga mkono ikiwemo miradi ya elimu, utamaduni, afya na mengineyo ambayo imepata mafanikio makubwa hapa Zanzibar.

Hivyo, Dk. Shein alisisitiza kuwa kutokana na uhusiano na ushirikiano huo wa muda mrefu ni vyema Shirika hilo likaendelea kuipa kipaumbele miradi inayoimarishwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hasa katika Mji Mkongwe wake ambao ni urithi wa dunia.

Aidha, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kulipongeza Shirika hilo kwa kuendelea kushirikiana  na Zanzibar na kuahaidi kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Shirika hilo ili kutekeleza malengo yaliokusudiwa.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein amepongeza hatua za Shirika hilo katika kusaidia uendelezaji wa miradi mbali mbali iliyopo Unguja na Pemba ikiwa ni pamoja na mradi wa uimarishaji mawasiliano kwa jamii kwa lengo la kutoa elimu kupitia redio Jamii iliyopo Micheweni Pemba.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliipongeza Shirika hilo kwa kuendeleza juhudi zake za kuwaunga mkono vijana kupitia miradi mbali mbali inayoendeshwa na Shirika hilo.

Mapema na Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) Tirso Dos Santos, alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Shirika hilo litaendelea kuiunga mkono Zanzbar katika kuimarisha na kuendeleza miradi mbali mbali ya maendeleo.

Mwakilishi huyo alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Shirika hilo linafarajika kwa kiasi kikubwa kwa kuona kwamba miradi mingi inayoianzisha hapa Zanzibar inakwenda vizuri na imekuwa ikipata mafanikio.

Aidha, aliahidi kuwa (UNESCO) itaendelea kutoa ushirikiano wake kwa Zanzibar sambamba na kuhakikisha miradi yote muhimu iliyoanzishwa na inayotaka kuanzishwa inakwenda vizuri na kupata mafanikio yaliokusudiwa.

Asema kuwa katika kuimarisha sekta ya elimu (UNESCO) kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Elimu ina azma ya kuanzisha  programu ya “03” ambayo ina maana ya “ our right, our lives and our future” ambayo itawasaidia vijana kutambua haki zao na kuwa na malengo juu ya maisha yao.

Kiongozi huyo alieleza kuwa mradi mwengine ni mradi wa KOICA ambao una malengo ya kusaidia sekta ya elimu na kuwajengea uwezo watoto wa kike na wanawake kwa jumla ambao utatekelezwa katika Wilaya nne za Tanzania ambapo Zanzibar kwa upande wake Wilaya ya Mkoani Pemba itahusishwa.

Wilaya nyengine ni Sengerema, Kasulu na Ngorongore kwa upande wa Tanzania Bara ambapo Mradi huu pia utayashirikisha mashirika ya UNESCO, UN WOMEN na UNFPA.  

Adha, Mwakilishi huyo aliitaja miradi mengine ikiwemo ule utakaolenga Vyuo vya Serikali vya Amali pamoja na Skuli za Ufundi hatua ambayo itakwenda sambamba na utoaji wa elimu na kujengea uwezo wa masoko na wafanyakazi.

Mwakilishi huyo pia, alieleza azma ya Shirika lake hilo katika kuiunga mkono Zanzibar kwa kupitia miradi yake ukiwemo mradi wa uimarishaji wa Redio Jamii Unguja na Pemba ambapo redio hizo husaidia kutoa elimu kwa jamii.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.