Habari za Punde

Wizara Yatakiwa Kuvitumia Vyombo Vya Habari Kutangaza Mafanikio Iliyoyapata.


 
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, amesisitiza haja kwa uongozi wa Wizara ya Ardhi, Maji na Nishati kuvitumia vyombo vya habari kuyatangaza mafanikio iliyoyapata ili wananchi wapate kuyajua.

Hayo aliyasema leo, Ikulu mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Ardhi, Maji na Nishati wakati ilipowasilisha utekelezaji wa Mpango Kazi wa Julai  2018 hadi Juni 2019 sambamba na Mpango Kazi wa Utekelezaji kwa mwaka 2019/2020.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa ni vyema wananchi wakaambiwa mafanikio makubwa yaliopatikana kupitia Wizara hiyo kwa kuzungumza na waaandishi wa Habari ama kwenda studio kuyaeleza kwani watakapokwenda huko wananchi watapata kuyajua na watafurahi.

Amesema kuwa Serikali hii ni ya wananchi na ipo kwa ajili ya kuwatumikia wananchi, hivyo ni vyema wakapewa taarifa zote kuhusiana na shughuli mbali mbali zinazofanywa na serikali na hasa zile zinazogusa maisha yao ya kila siku.

Aliwasisitiza viongozi hao kuvitumia vyombo vya habari likiwemo Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) Redio na Televisheni kutoa taarifa kwa ajili ya kuwaelimisha wananchi na kuutaka uongozi huo kutoficha habari kwani Serikali imefanya mambo mengi lakini wananchi hawayajui.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuupongeza uongozi  wa Wizara hiyo kwa kuwasilisha vyema Mpango Kazi wao na kueleza kufarajika kwake kutokana na matumizi katika Wizara za Serikali kwa kutambua kuwa tatizo hivi sasa sio fedha bali ni matumizi.

Aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inazo fedha za kutosha kukidhi mahitaji ya Bajeti za Wizara zake kutokana na makusanyo mazuri yanayofanywa na Taasisi husika zinazokusanya mapato zikiwemo ZRB na TRA.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa Serikali inajitahidi kutekeleza wajibu wake katika kutafuta fedha kwa ajili ya kuendeleza mambo yake ikiwemo miradi ya maendeleo jambo ambalo limeweza kuleta faraja katika kutekeleza mipango ya nchi.

“Kuna mafanikio mengi yamepatikana katika miradi mbali mbali ya maendeleo ndani ya Wizara hii ikiwa ni pamoja na mambo yote manne na hivi karibuni limeingia la tano la mafuta na gesi asilia hivyo nina imani kwamba mafanikio makubwa yatapatikana sasa ni vyema tukayatangaza, tukawaambiwa wananchi wetu ili wayajue” alisema Dk. Shein.

Aliongeza kuwa katika Wizara hiyo kila Taasisi na Idara zake zinaongozwa na Sheria hivyo ni rahisi kuiongoza na kuutaka uongozi huo kufanya kazi kwa kuangalia sheria zilizopo hasa ikizingatiwa kwamba Zanzibar ni mabingwa wa sheria.

Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuimarisha mashirikiano yaliopo katika Wizara hiyo kwa lengo la kupata mafanikio makubwa zaidi na kuupongeza uongozi wa Wizara hiyo kwa kuzidisha ushirikiano walionao.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza kazi nzuri ya uwasilishaji iliyofanywa na Wizara hiyo huku akisisitiza haja kwa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) kutumia umeme wa jua ili kupunguza matumizi ya umeme uliopo ambao gharama yake ni kubwa.

Mapema, Waziri wa Wizara ya Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Salama Aboud Talib alieleza kuwa  Wizara hiyo inaendeleza juhudi na mikakati ya Serikali ya kuhakikisha kuwa wananchi kwa ujumla wao wanapata huduma bora za maji, nishati iliyo salama na endelevu, makaazi bora pamoja na matumizi mazuri ya ardhi.

Waziri Salama alieleza kuwa Wizara yake kupitia Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA),  imeendelea kusimamia shughuli za program za uhaulishaji na upanuzi wa shughuli za maji Mijini na usambazaji maji vijijini.

Aidha, kwa maelezo ya Waziri Salama Mamlaka ya Maji kupitia mradi huu imefanikiwa  kulaza mabomba kwa masafa ya kilomita 87.1 katika maeneo ya Bumbwisudi, Kizimbani, Kianga, Welezo, Mikunguni, Mwembemakumbi, Makadara, Mwembeladu, Rahaleo, Miembeni, Mkunazini na maeneo ya Mji Mkongwe.

Waziri huyo alieleza kuwa Wizara kupitia Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati (ZURA) imeendeleza juhudi za kuimarisha mazingira bora ya utendaji wa kazi kwa kutekeleza shuguliza ujenzi wa jengo la Ofisi Maisara ambapo ujenzi huo hadi kufikia Juni 2019 umekamilika kwa asilimia 60.

Aliongeza kuwa Wizara hiyo pamoja na Wizara ya Fedha na Mipango na Afisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zilikamilisha majadiliano na Kampuni ya RAKGAS kwa kitalu cha Pemba-Zanzibar na hatimaye Kampuni ya Maendeleo ya Mafuta na Gesi Asilia ilitia saini Mkataba wa kwanza wa Mgawanyo wa uzalishaji wa mafuta na gesi asilia Oktoba 28 mwaka jana 2018.

Mkataba huo kwa maelezo ya Waziri huyo unajumuisha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Kampuni ya Mafuta na Gesi Asilia Zanzibar na Kampuni ya RAKGAS kutoka Ras al Khaimah.

Alieleza kuwa Serikali inaendelea na azma yake ya kuhakikisha Zanzibar inazalisha umeme kwa kutumia nishati mbadala ya jua na imeshatoa maamuzi ya uzalishaji wa nishati mbadala ya jua kwa kutumia mfumo wa Mzalishaji wa kujitegemea ambapo bado Serikali inahusika kwa njia moja au nyengine katika aina ya uwekezaji huo.

Aliongeza kuwa hivi sasa Wizara hiyo kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango inaendelea na matayarisho ya kuangalia namna bora ya utekelezaji wa aina ya uwekezaji kwa kiwango cha Megawati 30 MV.  

Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Ali Khalil Mirza akieleza Utekelezaji wa Malengo kwa kipindi cha Julai 2018 hadi Juni 2019 na alifafanua juhudi zilizochukuliwa na Wizara kufanikisha miradi yake na kupongeza maelekezo ya Dk. Shein katika utekelezaji wa zoezi hilo.

Nao uongozi wa Wizara hiyo ulieleza jitihada zilizofanyika ikiwa ni pamoja na kutafuta mchanga na kufanikisha kuupata ambapo umepelekea kuendelea vyema na ujenzi wa matangi ya Saateni kwa asilimia 80 na Mnara wa Mbao asilimia 90 ambapo mradi huo unatarajiwa kukamilika mwezi Septemba na mwezi Oktoba mwaka huu 2019 utafanyiwa majaribio na kuzinduliwa katika sherehe za Mapinduzi zijazo

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.