Habari za Punde

ZAECA Yafanikiwa Kukamata Fedha Zinazosadikiwa Kuwa ni Feki.


Na.Mwandishi Wetu.
Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu wa Uchumi Zanzibar (ZAECA), imefanikiwa kukamata fedha mabunda zaidi ya  30 ya fedha za kigeni zinazosadikiwa kuwa ni feki.

Akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa ZAECA, Mkuu wa kitengo cha uchunguzi na operesheni, Makame Khamis Hassan, alisema fedha hizo zinazodaiwa kumilikiwa na Ndg.Khatibu Amini Makame (Nondo), wamefanikiwa kuzikamata baada ya kupata taarifa kutoka kwa wasamaria wema kutoa taarifa hiyo.

Mkuu huyo alisema tukio hilo limetokea katika maeneo ya baa ya sai iliyopo maeneo ya Kibonde mzungu wilaya ya Magharibi B Unguja.

Hili ni tukio la pili kukamata fedha kama hizo ambazo ni kosa kwa mujibu wa kifungu cha sheria 51, kinaeleza kwamba mtu yeyote atakae jihusisha au kujiingiza moja kwa moja katika vitendo vya kughushi bidhaa fedha au utambulisho wa bidhaa au huduma kwa manufaa ya kipato au faida kwa manufaa ya kibiashara ametenda kosa la kuhujumu uchumi chini ya sheria namba moja ya mwaka 2012, ya ZAECA.

Mkuu huyo alisema baada ya kupata taarifa hiyo walifanikiwa kuweka mtego na hatimae kufanikiwa kumkamata mtu huyo.

Alifahamisha kwamba mzigo huo na mtuhumiwa wanaendelea kumshikilia ili kuendelea na upelelezi ili kuweza kukamilisha tuhuma hizo.

Alibainisha kwamba kukamilika kwa hatua hiyo mtuhumiwa huyo atafikishwa katika vyombo vya sheria ili kuendelea na hatua nyengine za kisheria.

Aidha alitumia fursa hiyo kuitaka jamii kuacha kujihusisha na matukio kama hayo ambayo yanapelekea kuhujumu uchumi wa nchi, ameitaja jamii wakibaini vitende hivyo kutoa taarifa ZAECA ili kuwafichua wale wote wanaojihusisha na vitendo hivyo kwa namna moja ama nyengine.

Sambamba na hayo Mkuu huyo alisema kutokea kwa matukio kama hayo yanasababisha kwa kiasi kikubwa serikali kukosa uwezo wa kutekeleza huduma mbalimbali za kijamii, hivyo ushirikiano wao ndio chachu ya kutokomeza vitendo hivyo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.