Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akiagana na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Balozi Seif Ali Iddi, Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume Zanzibar, akielekea Nchini Ras Al Khaimah kwa ziara ya wiki moja.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein anaondoka nchini leo kuelekea Ras Al Khaimah katika
Umoja wa nchi za Falme za Kiarabu (UAE) kwa ziara ya wiki moja kufuatia
muwaliko wa kiongozi wa nchi hiyo Sheikh
Saud Bin Saqr Al Qasimi.
Ziara hiyo ya Rais Dk.
Shein huko Ras Al Khaimah inatarajiwa kuanza kesho tarehe 23 na kumaliza tarehe
28 Septemba mwaka huu 2019 ambapo katika ziara hiyo pia, atapata fursa ya
kuzungumza na mwenyeji wake Mtawala wa Ras-Al-Khaimah Sheikh
Saud Bin Saqr Al Qasimi.
Dk. Shein akiwa Ras Al
Khaimah atakutana na uongozi wa Kampuni mbali mbali za nchi hiyo ikiwemo
Kampuni ya Kimataifa ya Utafiti na Uchimbaji wa Mafuta na gesi asilia ya Ras Al
Khaimah “Rak Gas”, Kampuni ya RAKEZ, Kampuni ya Mji wa Bahari wa Ras Al
Khaiman, Mamlaka ya Uendelezaji Utalii ya Ras Al Khaimah, Mji wa Kisiwa cha
Marjani pamoja na kukutana na Kampuni nyengine za mji huo ambayo yatapata fursa
kueleza shughuli wanazozifanya.
Rais Dk. Shein akiwa Ras
Al Khaimah atatembelea maeneo ya mji wa Ras Al Khaiman ikiwa ni
pamoja na maeneo mengine ya kitalii katika mji huo na eneo la Kampuni ya
Kimataifa ya Utafiti na Uchimbaji wa Mafuta na gesi asilia ya Rasyale ya
maendeleo.
Aidha, Dk. Shein atakwenda
Abu Dhabi kwa ajili ya kushuhudia utiaji wa saini Mkataba wa Mashirikiano kati
ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Abu Dhabi kupitia Mfuko wa
‘Khalifa Fund’ wenye makao makuu yake nchini humo.
Rais Dk. Shein pia,
ataungana na waumini wa Dini ya Kiislamu katika sala ya Ijumaa kwenye msikiti
wa Sheikh Zayed uliopo mjini Abu Dhabi ambao ni msikiti maarufu duniani.
Katika
ziara hiyo, Dk. Shein amefuatana na viongozi mbali mbali akiwemo Mke wa Rais wa
Zanzibar Mama Mwanamwema Shein, Waziri wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza
la Mapinduzi Issa Ussi Haji Gavu, Waziri wa Fedha na Mipango Balozi Mohamed
Ramia Abdiwawa, Waziri wa Ardhi, Maji, Nishati na Mazingira Salama Aboud Talib.
Wengine
ni Mwanasheria Mkuu wa Serikali Said Hassan Said, Balozi Mohamed Haji Hamza
Kaimu Mkurugenzi Idara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa
upande wa Zanzibar pamoja na watendaji wengine wa Serikali.
Rais
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein anatarajiwa
kurejea nchini Jumamosi ya tarehe 29 Septemba, 2019.
Katika
uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume Rais Dk. Shein aliagwa na viongozi
mbali mbali wa vyama vya siasa na Serikali pamoja na viongozi wa Vikosi vya Ulinzi na Usalama ambao
waliongozwa na Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment