Habari za Punde

Zanzibar Yathamini Mashirikiani Kati yake na Jamhuri ya Watu Cuba.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk.Ali Mohamed Shein, akiwa katika mazungumzo na mgeni wake Naibu Waziri wa Kwanza wa Mambo ya Nje Jamhuri ya Cuba Mhe.Marcelino Medina Gonzalez, yaliofanyika Ikulu Zanzibar leo,8, Septemba 2019.

JAMHURI ya Watu wa Cuba imepongezwa kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya na kuelezwa haja ya kutoa nafasi za masomo ya Udaktari Bingwa kwa Madaktari wa Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo wakati alipofanya mazungumzo na Naibu Waziri wa Kwanza  wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Watu wa Cuba Marcelino Medina Gonzalez, Ikulu mjini Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dk. Shein alizipongeza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Cuba katika kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo ikiwa ni pamoja na kuiunga mkono Zanzibar katika sekta mbali mbali za maendeleo ikiwemo sekta ya afya.

Hivyo, Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa Zanzibar inathamini sana mashirikino hayo yaliopo hasa katika sekta ya afya ambapo nchi hiyo imo katika mashirikiano na Zanzibar ya kusomesha Madaktari ambapo tayari kuna Madaktari 15 wa Zanzibar wanasoma nchini humo hivi sasa katika Chuo Kikuu cha Mantanzas.

Kutokana na juhudi hizo, Rais Dk. Shein alieleza haja ya kuendelezwa mashirikiano zaidi kwa Jamhuri ya Watu wa Cuba kutoa nafasi ya masomo ya Udaktari Bingwa kwa Madaktari wa Zanzibar hasa ikizingatiwa kuwa Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) kimeshaanza kutoa wahitimu mabali mbali wa fani hiyo.

Aidha, Rais Dk. Shein aliipongeza Cuba kwa kuendelea kushirikiana na Zanzibar kwani pande mbili hizo zina historia kubwa hasa ikizingatiwa kuwa  nchi hiyo ni miongoni mwa nchi za mwanzo kuyatambua Mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya Januari 12, 1964.

Alieleza kwamba mbali ya Cuba kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya, elimu na sekta nyenginezo pia, Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuendeleza uhusiano na ushirikiano katika sekta ya utalii hasa ikizingatiwa kuwa Cuba imepiga hatua kubwa katika sekta hiyo.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza mafanikio makubwa yaliofikiwa na Cuba katika sekta ya utalii hasa katika eneo la Ukanda wa Utalii unaojulikana kwa jina la Varadero, ambao unavivutio kadhaa vya kitalii zikiwemo hoteli za kisasa za hadhi ya juu, maeneo ya kihistoria na fukwe za kuvutia.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa Jamhuri ya Watu wa Cuba na Tanzania ikiwemo Zanzibar ni marafiki wa damu ambapo urafiki wao huo umekuwa ukiimarika kila uchao hivyo kuna kila sababu za kuuimarisha zaidi kwa manufaa ya pande zote mbili.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumueleza kiongozi huyo jinsi ya Muungano uliopo kati ya Zanzibar na Tanganyika ambao uliasisiwa Aprili 26 mwaka 1964 kuwa ni wa kihistoria na wapekee hadi hivi sasa kwa nchi za Bara la Afrika.

Nae Naibu Waziri wa Kwanza  wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Watu wa Cuba Marcelino Medina Gonzalez alimueleza Rais Dk. Shein jinsi ya nchi yake inavyofarajika na uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati yake na Zanzibar na kuahidi kuuendeleza.

Naibu Waziri Conzalez ambaye alifuatana na Balozi wa Cuba katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Profesa Lucas Domingo Hernades alimueleza Rais Dk. Shein kuwa ujio wake hapa Zanzibar umezidi kutoa fursa ya kuendelezwa kwa mashirikiano katika sekta mbali mbali za maendeleo ambapo umeweza kuwakutanisha na viongozi kadhaa na hatimae kujadiliana juu ya  sekta hizo.

Alisema kuwa miongoni mwa sekta hizo ni sekta ya afya, elimu, utalii, kilimo na biashara ambapo alisisitiza kuwa iwapo mashirikiano zaidi yataendelezwa kupitia sekta hizo mafanikio zaidi yataendelea kupatikana kwa pande zote mbili.

Kiongozi huyo alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Jamhuri ya Watu wa Cuba itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya ikiwa ni pamoja na kuendeleza mashirikiano ya kuwasomesha madaktari wazalendo nchini Cuba katika vyuo vyake mbali mbali kikiwemo Chuo Kikuu cha Mantanzas.

Sambamba na hayo, Naibu Waziri huyo aliyapongeza mapokezi mazuri aliyoyapata hapa nchini na kusisitiza kuwa Jamhuri ya Watu wa Cuba inathamini uhusiano na ushirikinao na Jamahuri ya Watu wa Tanzania katika nyanja zote zikiwemo za kiuchumi, kijamii na kisiasa.

Alieleza kuwa mbali ya uhusiano katika nyanja za kiuchumi na kijamii, pia, Jamhuri ya Watu wa Cuba ina mlahaka mzuri kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama Cha Kikomunisti cha Cuba (CPC) na kuahidi kuwa mahusiano yaliopo yataendelezwa kama walivyoanzwa na waasisi wa Mataifa hayo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.