Habari za Punde

UNFPA na Benki ya Dunia Zaahidi Kusaidia Sensa ya Watu na Makazi mwaka 2022


Mkuu wa Wilaya ya Bahi Mwanahamisi Munkunda akielezea mtawanyiko wa huduma za jamii katika wilaya wakati wa maonesho ya ramani za huduma za jamii za wilaya hiyo pamoja na maeneo ya kuhesabiwa watu kwa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022. 
Mrasimu ramani kutoka NBS Jerve Gasto akiwaonesha viongozi wa Halmashauri ya Bahi, wageni waalikwa wakiwemo wadau Maendeleo maeneo ya kuhesabia watu katika halmashauri hiyo.




Na.Said Ameir.                                                                                                                                   

Shiriki la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Idadi ya Watu (UNFPA) na Benki ya Dunia zimeeleza kuendelea kusaidia uzalishaji wa Takwimu nchini ikiwemo Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022.
Taasisi hizo zimetoa ahadi hiyo wiki hii wakati wa hafla ya Kutangaza Matokeo ya Zoezi la Kutenga Maeneo katika Wilaya ya Bahi na Uzinduzi wa Kitabu cha Taarifa za Kiuchumi na Kijamii cha Halmashauri ya Bahi kwa Mwaka 2019 huko Bahi mkoani Dodoma.  
Naibu Mwakilishi wa Shirika la UNFPA nchini Dk. Wilfred Ochan alieleza kuwa shirika lake linaisaidia Tanzania sio tu katika maandalizi ya awali ya Sensa bali katika uchambuzi wa data, kutoa matokeo hadi kuyasambaza matokeo hayo ya Sensa kwa wadau.
Alibanisha kuwa shirika lake lina historia ya muda mrefu ya ushirikiano na Tanzania katika kutekeleza Sensa za Watu Makazi pamoja na uzalishaji wa Takwimu nyingine.
“UNFPA inajivunia mchango wake katika mafaniko ya Tanzania kutekeleza Sensa za Watu na Makazi katika miongo iliyopita, katika kuimarika kwa uwezo wa Tanzania wa kuzalisha takwimu za msingi na zile tafiti za kitakwimu zinazowahusu wananchi” Dk. Ochan alieleza.
Aliongeza kuwa anaamini fika kuwa kutokana na uzoefu wa Ofisi za Takwimu nchini (NBS na OCGS), sifa za kitaaluma walizonazo watumishi wa Ofisi hizo pamoja dhamira na utashi wa serikali, Sensa ya mwaka 2022 itakuwa ya mafanikio makubwa.
Dk. Ochan alieleza kuwa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 itakuwa ya kipekee kwa kuwa kwa mara ya kwanza Tanzania itatumia tekinolojia mpya za kisasa tangu maadalizi ya mwanzo hadi mwisho wa utekelezaji wake.
“Matumizi ya simu janja, vishikwambi (tablets) na mifumo ya inayotumia mitandao katika kuhesabu watu ambayo ni sehemu ya mapinduzi ya data katika mukhtadha wa Sensa za miaka 2022 naamini kila mmoja wetu atakuwa anajivunia kuona sehemu ya mapinduzi haya yanaongozwa na Ofisi yetu ya Taifa ya Takwimu” Mwalikishi huyo alieleza.
Kabla ya uzinduzi huo viongozi wa wilaya ya Bahi wakiongozwa na Mkuu wa wilaya hiyo Mwanahamisi Munkunda, wageni waalikwa wakiwemo wadau wa Maendeleo waliangalia ramani zinazoonesha mtawanyiko wa huduma mbalimbali za jamii katika wilaya hiyo pamoja na ramani za kuhebia watu kwa ajili ya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022.
Kwa upande wake, Benki ya Dunia imeahidi kuendelea kuisaidia Tanzania kuimaisha maendeleo mfumo wa Taifa wa Takwimu nchini.
Bi Elizabeth Talbert aliyeiwakilisha benki hiyo katika hafla hiyo alieleza kuwa benki hiyo imekuwa mstari wa mbele kuisaidia Tanzania kuimarisha mfumo wa taifa wa Takwimu.
“Tunashirikiana na Tanzania katika miradi na programu mbali mbali za maendeleo katika sekta nyingi ikiwemo uimarishaji wa sekta ya Takwimu” Alisema Bi Talbert.
“Ramani tulizozishuhudia hapa zinaeleza picha halisi ya hali ya huduma za jamii katika wilaya hivyo zinasaidia kutuongoza katika mikakati yetu ya kusaidia wilaya hii” alisema mwakilishi huyo.
Bi Talbert aliwapongeza watumishi wa NBS na OCGS kwa kazi nzuri wanayoifanya katika kutenga maeneo na uzalishaji wa ramani hizo na kusisitiza kuwa kufikia Agosti, 2019 ni lazima nchi nzima iwe imegawanywa katika maeneo ya kuhesabia watu ili Sensa ifanyike kwa muruwa.
“Tumeona hapa kazi nzuri na kubwa iliyofanywa kwa wilaya hii. Fikirieni kuna wilaya ngapi hapa Tanzania Bara na Zanzibar. Tunataka kila mtu ahesabiwe mwaka 2022. Hakuna kumuacha mtu nyuma” Alisisitiza Mwakilishi huyo wa Benki ya Dunia Elizabeth Talbert. 
Kwa upande wake Mtakwimu Mkuu wa Serikali Dk. Albina Chuwa alieleza kuwa Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 ina umuhimu wa kipekee kwa kuwa Takwimu zitakazokusanywa zitatumika kupima mafanikio ya Dira ya Maendeleo 2025 na Utkelezaji wa Malengo Endelevu ya Dunia Mwaka 2030”Mtakwimu Mkuu wa Serikali Dk. Albina Chuwa.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.