Habari za Punde

Wazee wa Mkoa wa Kusini Pemba Wampongeza Dk.Shein Kwa Kutekeleza Ahadi na Ilani ya Uchaguzi Kwa Vitendo.


WAZEE wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa Mkoa wa Kusini Pemba wamempongeza Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein kwa kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 kwa vitendo.
Kwa nyakati tofauti wazee hao waliyasema hayo katika mikutano ya Makamu Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar ambaye pia, ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyoifanya katika Mkoa huo.
Wazee hao wa Mkoa huo walieleza kuwa juhudi alizozichukua Rais Dk. Shein katika kutekeleza kwa vitendo na kwa kasi kubwa Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2015-2020 ni za kupigiwa mfano kwani mafanikio yaliopatikana ni makubwa.
Walieleza kuwa Makamu Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar ameweza  kuiletea maendeleo makubwa Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuiimarisha na kuiendeleza miradi ya maendeleo ikiwemo miradi ya maji, elimu, afya, miundombinu ya barabara, usafiri na usafishaji, ujenzi wa ofisi za Serikali.
Waliongeza kuwa maendeleo makubwa yameendelea kupatikana chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein katika ujenzi wa barabara zenye viwango, upandishaji wa bei za karafuu, fedha za kila mwezi kwa wazee wa umri wa miaka 70 ambao miongoni mwao wanafaidika, ongezeko la fedha kwa wastaafu na uwekaji wa umeme na maji salama katika visiwa vya Unguja na Pemba na mengineyo.
Pamoja na hayo, wazee hao walieleza hatua anazozichukua Rasi Dk. Shein katika kuwajengea uwezo vijana, wanawake sambamba na kuwawekea mazingira mazuri wazee wa Unguja na Pemba abapo wazee hao walitumia fursa hiyo kumuahidi kushirikiana nae bega kwa bega.
Wazee hao walimpongeza Rais Dk. Shein na kueleza kuwa kitendo cha kwenda kukutana nao ni kielelezo kuwa anawajali na kuthamini juhudi zao ama mchango wao ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Aidha, wazee hao walimpongeza Rais Dk. Shein kwa jinsi alivyoweza kudumisha amani na utulivu nchini jambo ambalo limemfanya aweze kutekeleza kwa ufanisi Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020.
Wazee hao pia, walitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Shein kwa kuendelea kuyaenzi Mapinduzi matukufu ya Zanzibar kwa vitendo kwa kuendeleza kwa kasi matunda yake kama vile kuendeleza huduma za afya na elimu bure kwa wananchi.
Sambamba na hayo, wazee wa Makongwe kwa upande wao walitoa pongezi zao za pekee kwa Rais Dk. Shein kwa kuwapelekea umeme katika kisiwa hicho ambapo  wananchi wa kisiwa hicho wamekuwa wakifaidika na huduma hiyo muhimu katika maisha ya mwananadamu ikiwa ni pamoja na kufanya biashara kwa ufanisi mkubwa.
“Tunafahamu kuwa hichi ni kipindi chako cha kumalizia muda wa uongozi wako kwa nafasi ya urais ahadi yetu kwako tutakuwa na wewe bega kwa bega kuhakikisha Chama Cha Mapinduzi (CCM), kinaendelea kushika Dola na kuwaletea maendeleo wananchi wote”, walieleza wazee hao wa CCM wa Mkoa wa Kusini Pemba.
“Sisi Wazee tunakutakia kila la kheri katika maisha yako Mwenyezi Mungu akuzidishie hekma uvumilivu na upendo kwa unaotuongoza tutaendelea kuchota na kufuata nyayo zako katika yote mazuri kutoka kwako sisi pamoja na vizavi vyetu”, waliongeza wazee hao.
Nae Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kununua boti mpya ili kuwasaidia wananchi wakiwemo wazee wanaoishi katika visiwa vidogo vidogo vya Unguja na Pemba waweze kuvuka kwa uhakika.
Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar tayari imeshaanza mchakato huo ambao utakapokamilika utawasaidiaa kwa kiasikikubwa wananchi wanaoishi visiwani.
Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alivitaja visiwa sita ambavyo vimelengwa kupata boti hizo mpya na za kisasa ili ziwe msaada mkubwa kwao katika kuwasaida kuwavusha kikiwemo Kisiwa Panza, Makongwe, Fundo, Uvinje, Kokota na Tumbatu.
Aidha, Rais Dk. Shein amesisitiza haja ya kufanya kazi pamoja na wazee kwani ni watu muhimu sana katika jamii ambao bado mchango wao unahitajikakatika maendeleo ya kisiasa, kiuchumi na kijamii.
Alisisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini na inazijali juhudi za wazee walizozichukua hadi kupelekea kupatikana kwa uhuru wa Tanganyika na uhuru wa Zanzibar kupitia vyama vya siasa vya ASP na TANU wakati huo.
Rais Dk. Shein alisema kuwa miongoni mwa mambo ambayo wazee waliyapakipaumbele ni kujitolea na ndio maana uhuru kwa Tanganyika na Zanzibar ukapatikana pamoja na mambo mengine makubwa ya kujenga nchi yaliyofanyika baada ya kupatikana uhuru huo ambayo hayo yote yalitokanana falsafa ya kujitolea.
Katika mazungumzo hayo na wazee wa Mkoa wa Kusini Pemba ambapo Mama Mwanamwema Shein alishiriki kikamilifu, Dk. Shein alisema kuwa CCM ndio chama kinachowatetea wanyonge hivyo, ni lazima kitegemee nguvu za wanachama wake katika kufikia malengo yao waliyoyakusudia ikiwa ni pamoja na kuendelea kuongoza Dola na kuwaletea maendeleo endelevu wananchi wote.
Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Abdalla Juma Mabodi alisema kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) bado kinaendelea kuwatunza, kuwaenzi na kuwathamani wazee na ndio maana wameingizwa katika taratibu zote za chama hicho.
Aliongoza kuwa hikma za kuwaenzi wazee zimeanza kabda ya Mapinduzi chini ya Jemedaru Hayati Mzee Abeid Amani Karume na hadi hivi leo hikma na busara hizo zinaendelea kutumika ikiwa ni pamoja na kuwatuza wazee wote wa Unguja na Pemba tena bila ya ubaguzi.
Nao viongozi wa CCM Mkoa wa Kusini Pemba walieleza kufarajika kwao na juhudi za makusudi anazozichukua Rais Dk. Shein katika kuwahudumikia wananchi wa Zanzibar wakiwemo wazee ambao amewawekea mazingira mazuri katika maisha yao jambo ambalo bado nchini nyingi ndani nan je ya Bara la Afrika halijafanya la kuwapatia wazee waliotimia umri wa miaka 70 pencheni jamii  kwa kila mwezi.
Viongozi hao walitumia fursa hiyo kwa kumpongeza Rais Dk. Shein kwa kutekeleza kwa vitendo Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.