Muonekano wa nje wa jengo la Ofisi ya Madini na Kituo
cha Umahiri, mkoani Simiyu, Wilaya ya
Bariadi ikiwa ni jitihada za Serikali za kuimarisha sekta ya madini nchini,
kupitia Mradi wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini. (Picha na Mpigapicha
Wetu)
Na: Mwandishi wetu.
Serikali kupitia Mradi wa
Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Madini (SMMRP), imeendelea kunufaisha
wachimbaji wadogo wa madini kwa kuanzisha na kuboresha mifumo mbalimbali
itakayosaidia kukuza sekta ya madini pamoja na kutatua changamoto zinazowakabili
wachimbaji wadogo.
Ujenzi wa Kituo cha
Umahiri kilichopo katika Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu kunatokana na Sera ya
Madini ya Mwaka 2009 ambayo inasisitiza sana juu ya uendelezaji wa sekta ya
madini na hasa wachimbaji wadogo, ni hatua itakayosaidia kutatua changamoto za
wachimbaji wadogo wa madini.
Mnamo Septemba
05, 2018 Kituo cha Umahiri cha Bariadi kilianza kujengwa na Kampuni ya Ujenzi ya SUMA
JKT na kusimamiwa na Kampuni ya
Sky Actate Consultants, kilikamilika
Oktoba 16 mwaka huu na kugharimu shilingi
bilioni 1.308, kitasaidia
kutoa mafunzo na maarifa kwa
wachimbaji wadogo kuhusu sera ya madini, sheria, kanuni, taratibu na miongozo
mbalimbali ya kiutendaji katika shughuli za madini.
Aidha, kituo
hicho kitasaidia kutoa elimu kuhusu ujasiriamali, utafutaji madini, uchimbaji
madini, uchorongaji miamba, mazingira, afya na usalama migodini, pamoja na
kutoa elimu juu ya mfumo wa kutathmini mashapo ya madini yaliyopo ili kufanya
uchimbaji uwe na tija.
Akizungumza hivi karibuni, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka alisema ujenzi wa kituo
hicho utajibu mahitaji ya mkoa katika kuwasaidia wachimbaji wadogo kuondokana
na uchimbaji wa kienyeji na kwenda kwenye uchimbaji wa kisasa.
"Wachimbaji wetu wadogo wamekuwa wakifanya shughuli zao
kienyeji lakini uwepo wa kituo hiki utajibu mahitaji yao kwa sababu kitakuwa ni
sehemu sahihi ya wao kupata elimu juu ya uchimbaji bora, pamoja na uwepo wa wataalam
wa madini karibu na maeneo yao”, alisema Mtaka.
“ Sisi kama mkoa tuna faida
ya uwepo wa rasilimali madini tuna nikeli, shaba, dhahabu, cobalt, tuna chumvi
katika wilaya ya Meatu lakini pia tuna madini ya ujenzi kama kokoto, mchanga na
mengine, hivyo uwepo wa kituo cha umahiri kutasaidia wachimbaji kufanya kazi
zao katika utaalamu ili uchimbaji ufanyike kwa ufanisi na uwe na tija”,
alisisitiza Mtaka.
Naye, mchimbaji mdogo wa madini kutoka mkoa wa Simiyu, James
Bundala, anasema kituo hicho cha umahiri ni kituo cha msaada katika kazi zao,
na wanatarajia kitasaidia kuongeza tija na kukuza kipato kwa vile watafanya kazi
kisasa zaidi.
“Imani yetu ni kuwa kituo hiki kitatusaidia kutatua migogoro
ya uchimbaji madini inayojitokeza, pamoja na kupata elimu kuhusu uongezaji
thamani madini na upatikanaji wa masoko, na haya yote yatatusaidia kufanya biashara
yetu vizuri zaidi na kukuza vipato vyetu”, alisema Bundala.
Vile vile, kituo
hicho kitasaidia katika usimamizi na uratibu wa shughuli mbalimbali zinazohusu
madini, pamoja na kuwezesha wachimbaji wadogo kupata taarifa sahihi za maeneo
yaliyotengwa kwa ajili yao.
Katika kipindi
cha miaka minne ya utawala wa Serikali ya Awamu ya Tano, inayoongozwa na Dkt.
John Pombe Magufuli, sekta ya madini imetekeleza hatua mbalimbali zenye lengo
la kuimarisha sekta ya madini nchini kwa kuboresha maisha ya wachimbaji wadogo,
sambamba na kuongeza pato la taifa.
Aidha, Serikali imefanikiwa kuifanya sekta ya madini kuwa moja ya
vyanzo vikubwa vya mapato kwa kuwekeza utaalam wa rasilimali watu, majengo,
upimaji na utaalam mbalimbali wa kusaidia wachimbaji wadogo. Waziri wa
Madini, Dotto Biteko, wakati alipokuwa akiwasilisha bungeni makadirio ya mapato
na matumizi ya fedha kwa mwaka 2019/20 alisema kuwa mchango wa sekta ya madini kwenye pato la
taifa kwa mwaka 2018/19 umeendelea kuimarika na kufikia asilimia 5.07 mwaka
2018.
Mchango huo
ulitokana na kuongezeka kwa uelewa kwa wadau wa sekta ya madini na kuwepo kwa
uwazi katika shughuli zao, ukuaji wa sekta, kuimarisha usimamizi wa shughuli za
madini kwa kudhibiti utoroshwaji, kuimarisha ukaguzi katika sehemu za uzalishaji
na biashara ya madini, kuongezeka kwa viwango vya mrabaha na kuanzishwa kwa ada
ya ukaguzi wa madini kupitia Marekebisho ya Sheria ya Madini Sura ya 123
yaliyofanyika mwaka 2017.
Aidha, Biteko
amesema kuwa kuhusu uendelezaji wa uchimbaji mdogo wa madini, Serikali
imeendelea kuhakikisha kuwa changamoto za sekta ya madini zinapatiwa ufumbuzi
na hivyo kuwafanya wadau kufanya shughuli zao za uchimbaji na biashara ya
madini katika mazingira ya kibiashara yanayovutia.
Mkakati mwingine uliofanywa na Serikali ili kuimarisha sekta ya madini nchini ni pamoja na Rais Dkt. John Pombe
Magufuli, kufanya mkutano na wachimbaji, wafanyabiashara na wadau wa sekta ya madini
Januari 22 na 23 mwaka huu, kwa lengo la
kuondoa changamoto zilizokuwa zikiikabili sekta hiyo.
Katika mkutano
huo, Serikali ilipokea kero na hoja mbalimbali zikiwemo, kupunguzwa kwa kodi na
tozo zinazotozwa kwa wachimbaji wadogo wa madini, kufutwa kwa maeneo ya leseni
za madini zisizoendelezwa na kuwekwa kwa maafisa madini kwenye maeneo ya
machimbo ya madini.
Hoja nyingine
katika mkutano huo zilikuwa, kudhibiti utoroshwaji wa madini, kuimarisha
utunzaji wa mazingira katika maeneo ya uchimbaji madini, ukosefu wa
miundombinu, tozo na ada kulipwa kwa fedha za kigeni, pamoja na kuondoa kodi ya ongezeko la thamani
(VAT) asilimia 18 na kodi ya zuio (withholding tax) asilimia 5 kwa wachimbaji
wadogo. Hii inafanya jumla ya kodi zote zilizofutwa kufikia asilimia 23.
Ni dhahiri kuwa,
katika kipindi cha miaka minne, Serikali ya Awamu ya Tano inaimarisha sekta ya
madini na kuneemesha wachimba madini kwa kuanzisha masoko ya madini na kujenga
vituo vya mfano na umahiri ambavyo wachimbaji wadogo wanapata fursa ya
kujifunza teknolojia na mbinu bora na za kisasa za uchimbaji na uchakataji
madini, utunzaji wa mazingira, pamoja na kuanzisha mfumo wa masoko ya madini
katika mikoa yote yenye madini ya metali na vito yaani metallic minerals and gemstones.
No comments:
Post a Comment