Naibu Waziri wa Habari,Utamaduni, Sanaa na
Michezo, Mhe. Juliana Shonza akizungumza alipokuwa mgeni rasmi katika hafla ya
ufunguzi wa awamu ya pili ya mafunzo ya Mawasiliano ya Kimkakati kwa Maafisa
Habari kutoka wizara, taasisi, mashirika ya umma na
halmashauri nchini leo tarehe 02 Desemba 2019 Jijini Dodoma.
Na Anitha Jonas & Shamimu Nyaki -
WHUSM Dodoma.
Naibu Waziri Wizara ya Habari
Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe.Juliana Shonza amewataka Maafisa Habari nchini
kuwa vinara katika kutangaza shughuli mbalimbali za serikali ikiwemo
miradi inayotekelezwa.
Mhe.Shonza ametoa kauli hiyo leo
Jijini Dodoma alipokuwa akifungua mafunzo ya awamu ya pili ya Maafisa Habari
nchini yanayofanyika kwa siku tano yenye lengo la kuwajengea uwezo.
‘Katika kutangaza habari za serikali
kwa umma kila Afisa Habari ni lazima kutumia vyanzo vyote kusambaza habari
ikiwemo mitandao ya kijamii kwa sababu inasambaza habari kwa haraka zaidi na
kufikia watu wengi,’alisema Mhe.Shonza.
Akiendelea kuzungumza katika ufunguzi
huo Naibu Waziri Shonza alisisitiza kuwa kwasasa waandishi wa habari
wanatakiwa kuwa na elimu kulingana na Sheria ya Huduma za Vyombo vya
Habari ya mwaka 2016 kwani tasnia hii inatakiwa kuondokana na makanjanja.
Kwa Upande wake Msemaji Mkuu wa Serikali
Dkt.Hassan Abbasi amesisitiza kuwa Maafisa Habari wanapaswa kuandika na
kutangaza habari za kimkakati zinazotekelezwa na serikali ili wananchi wafahamu
maendeleo yanayofanywa na serikali.
"Nawapongeza kwa kazi nzuri
mnayoifanya ya kutangaza shughuli mbalimbali za serikali lakini wapo baadhi
hawafanyi vizuri na ndiyo maana tumeona tuwape mafunzo haya ili kurekebishana katika utendaji,"alisema Dkt.Abbasi.
Naye Katibu wa Chama cha Mawasiliano
Serikalini (TAGCO) Bw. Abdul Njaidi amesihi Maafisa hao kuzingatia elimu
watakayoipata katika mafunzo hayo ili waweze kutangaza vizuri utekelezaji wa
Serikali katika maeneo yao.
Pamoja na hayo mmoja wa Maafisa Habari Bibi.Nuru Mfaume kutoka Ofisi ya Mkuu
wa Wilaya ya Bunda alitoa shukrani zake kwa Msemaji Mkuu wa Serikali na uongozi
wa TAGCO kwa mafunzo hayo ambayo yatawaongezea ujuzi.
"Kweli kabisa mafunzo haya
yametusaidia kujitathimini utendaji wetu na kugundua makosa yetu na baada ya
hapa hakika kutakuwa na mabadiliko katika utendaji ikiwemo uandishi wa habari
zetu"alisema Bibi.Nuru.
Mafunzo hayo yanahudhuriwa na Maafisa
Habari mia moja kutoka Wizara,Taasisi,Mashirika,Mikoa na Halmashauri za
Tanzania Bara ambapo mada mbalimbali zitatolewa.
No comments:
Post a Comment