Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la MapinduziDk.Shein Awapongeza Wananchi wa Mkoa wa Mwanza


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohamed Shein akitoa nasaha zake mara baada ya kulizindua Rasmi Jengo Jipya la Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amezidua nyumba ya makaazi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza na kupongeza juhudi kubwa zilizochukuliwa katika ujenzi wa nyumba hiyo.
Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hafla fupi ya uzinduzi wa nyumba ya makaazi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza iliopo, Isamilo Jijini Mwanza.
Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alisema kuwa ujenzi huo wa nyumba ya makaazi ya Mkuu wa Mkoa huo yatasaidia kwa kiasi kikubwa katika kuhakikisha makaazi ya kiongozi huyo yanakuwa bora zaidi.
Alieleza kuwa juhudi hizo zilizochukuliwa katika ujenzi wa nyumba hiyo ya kisasa pia, itasaida kwa wageni watakaomtembelea Mkuu huyo wa Mkoa wa Mwanza pamoja na yeye mwenyewe kuishi na familia yake.
Rais Dk. Shein alipongeza juhudi zilizochukuliwa katika kuhakikisha nyumba ya Mkuu wa Mkoa iliyokuwa hapo kabla kwenye mtaa wa Machemba, Isamilo hivi sasa imegeuzwa Ikulu Ndogo.
Hivyo, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwapongeza wananchi wa Mwanza kwa kupata Ikulu Ndogo kwenye nyumba hiyo ambayo kwa maelezo ya Rais Dk. Shein ina historia kubwa.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa uongozi wa Mkoa huo pamoja na Mkandarasi wa nyumba hiyo.
Mapema Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza Christopher Kadio akitoa taarifa ya ujenzi wa nyumba hiyo alimueleza Rais Dk. Shein kuwa mradi wa ujenzi huo ulianza kutekelezwa katika bajeti ya mwaka 2017/2018 baada ya nyumba aliyokuwa akiishi Mkuu wa Mkoa huo kubadilishwa matimizi na kuwa sehemu ya Ikulu Ndogo.
Aidha, alisema kuwa Mkataba wa ujenzi ulisainiwa tarehe 13 Juni, 2017 kati ya Mkandarasi Wakala wa Majengo (TBA) na Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza kwa gharama ya TZS Milioni 660.
Aliongeza kuwa Mkataba wa ujenzi huo ulihusisha ujenzi wa nyumba kuu, nyumba ya wasaidizi, ujenzi wa uzio pamoja na kibanda cha walinzi.
Katibu Tawala huyo alieleza kuwa Mkandarasi alianza ujenzi mwezi Septemba 2017 baada ya malipo ya awali ya kiasi cha fedha TZS milioni 150 zilizokuwa zimepangwa  kwa ajili ya ukarabati wa iliyokuwa nyumba ya Mkuu wa Mkoa na kubadilishwa kuwa Ikulu Ndogo.
Hata hivyo, kwa maelezo ya Katibu Tawala huyo baada ya ongezeko la gharama za vifaa vya ujenzi Mkandarasi aliongezewa kiasi cha fedha TZS milioni 50 kukamilisha shughuli za ujenzi wa uzio na ununuzi wa baadhi ya vifaa.
Sambamba na hayo Katibu Kadio alieleza eleza kuwa kwa sasa ujenzi wa mradi huo umekamilika kwa zaidi ya asilimia 99 ambapo kazi ya ujenzi wa kibanda cha walinzi bado haujakamilika na unatarajiwa kukamilika hivi karibuni.
Nae Mkuu wa Wilaya ya Ilemela Dk. Severine Mathias Lalika kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa huo alimpongeza Rais Dk. Shein kwa kuwazinduliwa jingo lao hilo na kusema kuwa ujio wake umewasaidia kwa kiasi kikubwa katika kuhakikisha ujenzi huo unakwenda kwa kasi na kufikia malengo yaliokusudiwa.
Hafla hiyo pia, ni miongoni mwa shamrashamra za sherehe za kuadhimisha miaka 58 ya Uhuru wa Tanzania Bara na miaka 57 ya Jamhuri Tanzania Bara.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.