Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Atowa Salamu za Mwaka Mpya Kwa Wananchi wa Zanzibar. Mwaka Mpya 2020



RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewapongeza wananchi wa Zanzibar  kwa kushirikiana na Serikali zao zote mbili ile ya Jamhuri ya Mungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuidumisha amani na utulivu kwa kipindi chote cha mwaka 2019.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo katika risala yake aliyoitoa kwa wananchi kupitia vyombo vya habari katika kuukaribisha mwaka mpya wa 2020, risala aliyoitoa huko ofisini kwake Ikulu mjini Zanzibar.

Katika risala yake hiyo, Rais Dk. Shein alisema kuwa wananachi wameonesha mapenzi makubwa, umoja na mshikamano baina yao na miongoni mwa wageni wanaokuja kuitembea nchini.

Aliongeza kuwa amani, utulivu na umoja vilivyoendelezwa vimewezesha kuitekeleza mipango ya maendeleo kwa mafanikio makubwa ambapo umepelekea uchumi wa Zanzibar kuendelea kukua kwa asilimia 7.1 kwa mwaka 2018 ikilinganishwa ma asilimia 6.8 kwa mwaka 2016.

Rais Dk. Shein alisema kuwa hali ya amani na utulivu iliyopo nchini imeongeza mshikamano na mapenzi baina ya wananchi na kusisitiza kuwa nchi iko salama na kila mwananchi anafanya shughuli zake bila ya bughudha.

Aliongeza kuwa hali ya amani na utulivu imechangia katika kuimarika kwa sekta ya utalii ambapo watalii na wageni mbali mbali walitembelea Zanzibar katika mwaka 2019 ambapo jumla ya watalii 477,579 walitembelea Zanzibar katika kipindi cha Januari hadi Novemba 2019.
Alieleza kuwa kuimarika kwa amani na utulivu nchini pia, kulipelekea Taasisi na Mashirika mbali mbali ya Kikanda na Kimataifa yalivutiwa sana kuja kufanya mikutano yao hapa Zanzibar katika mwaka 2019 ukiwemo Mkutano wa Jumuiya ya Majaji na Mahakimu wa Afrika Mashariki, (EAMJA) Mahakama ya Afrika ya Haki za Binaadamu na Watu na Mkutano wa Wabunge wa Jumuiya ya Madola.

Alisema kuwa utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya 2020 ya Zanzibar ambayo sambamba na Ilani ya Uchguzi Mkuu ya CCM ya 2015/2020 umefanyika kwa ufanisi na kupelekea kukaribia kukifikia kiwango cha chini cha nchi za kipato cha kati cha USD 1,040 kwa mujibu wa vigezo vya Kimataifa.

“Tumemaliza mwaka bila ya shida yoyote ya upatikanaji wa bidhaa za chakula na bidhaa nyengine muhimu kwa maisha ya kila siku ya wananchi wa Zanzibar”,alisema.

Aidha, alisema kuwa miongoni mwa mafanaikio makubwa yaliopatikana katika mwaka uliopita ni kuimarika kwa sekta ya kilimo, uvuvi na ufugaji ambapo jitihada za Serikali na wakulima zimewezesha kupata mafanikio makubwa katika sekta ya kilimo kwa kuongeza mavuno ya mazao ya chakula hasa mpunga, mboga, na matunda.

Alisema kuwa kwa mwaka 2018/2019 wakulima walivuna tani 47,507.1 za mpunga kutoka tani 39,682.7 mwaka 2017/2018 ambapo mafanikio hayo kwa jumla yamewezesha kujitosheleza kwa chakula kwa asilimia 60 kutoka asilimia 51 mwaka 2011.

Kwa upande wa sekta ya uvuvi, Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali imeanza hatua za awali za kuanzisha Kampuni ya Uvuvi ya Zanzibar (ZAFICO), kushika nafasi ya Shirika la Uvuvi lililokuwepo kabla.

Alisema kuwa mwaka 2019 boti ya kisasa ya uvuvi inayoitwa SEHEWA II imenunuliwa kwa TZS Bilioni 1.33 na tayari Kampuni ya (ZAFICO) imepanga kununua boti nyengine moja ya uvuvi.

Pia, kwa maelezo ya Rais Dk. Shein Serikali kwa kushirikiana na Washirika wa Maendeleo imo katika mipango ya kuongeza boti nyengine nne zenye thamani ya USD milioni 2.2 kwa ajili ya uvuvi wa bahari kuu huku Serikali ikinunua meli mpya ya mafuta.

Katika risala hiyo, Rais Dk. Shein alisema kuwa mwaka 2019 Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilieNdeleza juhudi za utafutaji wa Mafuta na Gesi Asilia juhudi ambazo zilijumuisha tafsiri za taarifa za mitetemo ambayo ndio itakayoonesha miamba au maeneo yanayosadikiwa kuwa na mafuta na gesi asilia.
Rais Dk. Shein alisema kuwa katika mwaka 2019 mafanikio makubwa yamepatikana katika sekta za jamii ikiwemo utekelezaji wa sera ya kutoa huduma za afya na elimu bure ambapo bajeti ya Wizara ya Afya imeongezeka mara 9.6 kutoka bilioni 10.81 mwaka 2010/2011 hadi TZS bilioni 104.24 mwaka 2019/2020.

Aliongeza kuwa kwa lengo la kuendeleza sekta ya elimu, katika mwaka wa fedha 2019/2020 Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeongeza bajeti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali mara 3.8 kutoka TZS bilioni 47.093 mwaka 2010/2011 ilipoanza Awamu ya Saba hadi TZS bilioni 178.917 mwka 2019/2020.

Alisema kuwa katika kuimarisha upatikanaji wa huduma za maji safi na salama katika mwaka unaomalzika Serikali imeendelea kutekeleza miradi ya maji safi na salama kwa mafanuikiio katika mkikoa yote ya Unguja na Pemba na wastani wa upatikanaji wa amaji umefikia asilimia 79.

Sambamba na hayo, alisema kuwa miradi ya ujenzi wa mji katika eneo la Fumba na Nyamanzi imeendelea vizuri katika mwaka 2019 ambapo pia katika mwaka huo umeanzwa mradi wa ujenzi wa maduka ya kisasa (shopping mall) katika eneo la Michenzani  na mradi wa ujenzi wa majengo ya kisiasa ya makaazi huko Kwahani.

Alieleza kuwa miradi ya ujenzi wa miundombinu ya barabara imeendelezwa katika maendeeo mbali mbali Unguja na Pemba sambamba na Serikali kununua vifaa vya kutengenezea barabara vyenye thamani ya TZS bilioni 14 ili kujeijengea uwezo Idara ya Utunzani Barabara (UUB).

Alieleza jinsi Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ulivyofanikiwa huku akitumia fursa hiyo kuwahimiza viongozi wenziwe hasa Waheshimiwa Wabunge na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na viongozi wote wa Serikali wa ngazi mbali mbali na watumishi wote wa umma kuongeza jitihada kwa kufanya kazi kwa bidii katika kuwatumikia wananchi na kuyatatua matatizo yao katika mwaka 2020.

Na kwa wale waliotoa ahadi ya kuyatekeleza mambo kadhaa ya maendeleo walipokuwa wakiomba kura za kutaka uongozi mnamo mwaka 2015, Dk. Shein alisisitiza kuwa  wanapaswa kuzingatia kwamba mwaka 2020 tayari ushawadia.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pole kwa wananchi wote waliopata maafa yaliyotokana na mvua iliyoambatana na upepo mkali iliyotokea usiku wa kuamkia Jumaamosi ya terhe 21 Disemba, 2019. Kadhalika alitoa pongezi kwa viongozi wa ngazi mbali mbali waliowatembelea wananchi walioathirika kwa ajili ya kuwafariji.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.