Habari za Punde

Wananchi Visiwani Zanzibar Waipongeza Hutuba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.

WANANCHI wameipongeza hotuba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyeitoa katika kilele cha kuadhimisha miaka 56 ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 hivi karibuni.

Wakiwa katika maeneo mbali mbali kwa nyakati tofauti wananchi hao wameipongeza hotuba ya Rais Dk. Shein na kumpongeza yeye mwenyewe binafsi kwa yale yote aliyoyasema katika hotuba hiyo ambayo wamesema ni dira katika maendeleo ya Wazanzibari.

Wananchi hao walisema kuwa mbali ya kueleza katika hotuba hiyo juhudi za Serikali anayoiongoza pamoja na hatua kubwa zilizofikiwa katika kukuza uchumi pia, wameunga mkono kauli yake ya kutochelea kumchukulia hatua mtu yeyote atakayejaribu kuhatarisha amani iliyopo hapa nchini.

Walieleza kuwa juhudi anazozichukua Rais Dk. Shein kwa kushirikiana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli za kuhakikisha amani na utulivu vinadumishwa nchini ni hatua madhubuti ya kuungwa mkono na kila Mtanzania.

Wananchi hao wamepongeza maneno ya Rais Dk. Shein katika hotuba yake hiyo jinsi ya viongozi hao wanavyotekeleza wajibu wao wa Kikatiba na Kisheria katika kutekeleza amani, utulivu na kulinda maisha ya wananchi pamoja na mali zao.

Wananchi hao walieleza na kuponmgeza jinsi hotuba hiyo ilivyotilia mkazo suala la Muungano na hasa pale Rais Dk. Shein aliposema kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Serikali ya Jamhauri ya Muungano wa Tanzania katika kuendeleza na kudumisha Muungano.

Aidha, wananchi hao walimpongeza Rais Dk. Shein kwa kutekeleza vyema majukumu yake katika Awamu yake hii ya Saba katika kipindi cha miaka tisa cha uongozi wake kwa kuendelea na juhudi za kutekeleza mipango ya mageuzi ya kiuchumi ili kuhakikisha kwamba uchumi na ustawi wa wananchi wa Zanzibar unaimarika.

Wananchi hao walieleza kufurahishwa na juhudi hizo ambazo ni pamoja na kuhakikisha hali ya amani na utulivu inaimarika hatua ambayo zimepelekea kuongezeka kwa pato halisi la Taifa kwa mara 1.6 zaidi ya kutoka thamani ya TZS Bilioni 1,768 mwaka 2010 hadi kufikia thamani ya TZS Bilioni 2,874 mwaka 2018.

Sambamba na hayo, wananchi hao walipongeza hatua zilizochukuliwa na uongozi wa Rais Dk. Shein katika kuimarisha uchumi kulikopelekea ongezeko la ukusanyaji wa mapato mwaka hadi mwaka ambapo kwa mwaka wa fedha 2018/2019 mapato ya ndani yalifikia TZS Bilioni 748.9 ikilinganishwa na jumla ya TZS Bilioni 181.1 zilizokusanywa mwaka 2010/2011.

Katika maelezo yao wananchi hao walimpongeza Rais Dk. Shein kwa juhudi alizozichukua katika kuimarisha sekta za maendeleo zikiwemo elimu, afya, maji safi na salama, ajira kwa vijana, biashara, viwanda, utalii, uvuvi na ufugaji pamoja na sekta ya kilimo, mafuta na gesi, nishati ya umeme, miundombinu ya barabara.

Pia, Rais Dk. Shein alipongezwa kwa mikakati yake ya ujenzi wa bandari mpya ya Mpigaduri pamoja na Mangapwani, Mradi wa Kamera za uangalizi (CCTV), Mahakama, mazingira, Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Kuhujumu Uchumi (ZAECA), kuanzisha mfumo wa Ugatuzi wa madaraka kwa wananchi na kuimarisha sekta michezo.

Kwa upande mwengine  waliipongeza hotuba hiyo ya Dk. Shein kutokana na juhudi zilizochukuliwa kuimarisha sekta ya habari na kuongeza ufanisi ikiwa ni pamoja na kuliimarisha Shirika la Utanzagazi la Zanzibar (ZBC) na Shirika la Magazeti la Zanzibar huku wakiahidi kuufanyia kazi wito wake wa kwensda kujiandikisha kwa ajili ya uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Walisema kuwa hotuba hiyo imeeleza azma ya Serikali anayoingoza Rais Dk. Shein  katika kuziimarisha huduma za Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume zikiwemo ujenzi wa jengo la abiria “Terminal 3” pamoja na ujenzi wa uwanja mpya wa kisasa wa Pemba kwa mashirikiano kati ya Serikali na Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB).

Walieleza kuwa hawatokuwa wachoyo wa shukurani kwa kumshukuru Dk. Shein kwa kurekebisha maslahi ya Wafanyakazi ya mishahara aliyoyafanya mwaka 2011, 2013, 2015 na mwaka 2017 kwa lengo la kuwapa motisha kwa kuzingatia ukuaji wa mapato.

Aidha,  walitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Shein kwa kuwaahidi Watumishi wa Umma kuwa anamatumaini makubwa kwamba kutokana na hali ya uchumi unavyoendelea wasishangae kuwa mwaka huu akaongeza chochote.

Walieleza kuwa kauli hiyo imewapa faraja na kueleza kuwa Rais Dk. Shein ni kiongozi wa pekee anaewajali wananchi wake wakiwemo wafanyakazi wa sekta za umma.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Kija Kijitu Makame  wa Majenzi Makunduchi  alipongeza Rais Dk. Shein kwa hotuba yake ambayo alisema imejaa kila kitu kuanzia masuala ya uchumi, maji, elimu, kilimo, mishahara, majenzi, barabara pamoja na umuhimu wakuendeleza amani na utulivu.

“Helikwacha kitu, kwa msingi uno Mheshimiwa Rais kwake mambo yoti ni vipaumbele maana kana tazama watu wanachaka nini, jambo lino tunamshukuru sana maana ni ishara ya kiongozi msikivu na mwadilifu” , alisema Kija Kijitu Makame.

Aliendeleza pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa kuonesha kuwajali wananachi wake “Suwe wa njia ya kusini tunamshukuru sana kutujali kwa kutuwishia shida iliyowaja Kibonde Mzungu kila ikanya vua mtihani mpaka watu kufya, akajenga daraja zuri na katii taa vazuri hamba Ulaya” alisisitiza Kijitu.

Aliongeza kuwa “Kigezo chengine cha kuonesha jinsi Rais Dk. Shein anavyowajali watu ni valya Amani wakati kana hutubia, kono jua kali sana na joto jingi basi akaamua asiisome yoti hotuba yake ili watu wasikae too”.

“Bali yalya ya muhimu mfano kuongeza mshahara, kuongezeka kwa uchumi na jinsi miradi ya maendeleo ilivyoimarika kono aseme kabisa tukampigia makofi, Mungu alijaalie tuvate kiongozi mwengine ja yeye ili tuvate maendeleo zaidi na zaidi”, alimalizia Kijitu.

Ali Hamad Ali mkaazi wa Pembeni Wilaya ya Wete Pemba, anasema kwamba hotuba ya Dk. Shein ilisheheni kila kitu ambacho kilichofanyika ikiwemo, ukuwaji wa Uchumi, uwajibikaji wa Serikali, maendeleo yaliofikiwa sambamba na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi  (CCM) ya mwaka 2010-2020.

Alieleza kuwa hotuba hiyo, ilikuwa na mchanganuo wa mambo mbali mbali, ikiwemo elimu, afya, barabara mambo ambayo ni ya uhakika kwani kila mmoja anayaona ambayo ni tofauti sana na miaka iliopita kabla ya Mapinduzi ya mwaka 1964.

Alifahamisha kuwa kubwa ambalo halijawahi kutokea katika historia ya Zanzibar, ni pale hotuba inavyoelezea jinsi Serikali inavyoendelea kulishughulikia suala la  Mafuta na Gesi Asilia jambo ambalo likifanikiwa litakuza uchumi wa Zanzibar maradufu.

Nae Massoud Ali Mohammed mkaaazi wa Ndagoni Wilaya ya Chake Chake Pemba, anasema kwamba hotuba aliyoitoa Rais Dk. Shein inaeleza ukweli mtupu kwani kila liliomo ndani ya hotuba  liko wazi na linaonekana na kilichobakia kwa wananchi wa Zanzibar ni kushirikiana na Viongozi pamoja na Serikali yao.

Alisema suala la kuwaenzi Wazee ambalo ni moja ya hatuba alioitowa Rais katika kilele cha sherehe za Miaka 56 ya Mapinduzi ni ukweli usiopingika ambapo wazee sasa hivi wanafaidika na huduma ya malipo ya Pencheni Jamii “Kwa kweli nikiwa  mwananchi wa Zanzibar naiopongeza sana hatuba ya Dk. Shein”,alisema Masoud Ali.

Kwa upande wake, Omar Mjaka Ali, Mbunge Mstaafu wa Jimbo la Vitongoji ambalo hivi sasa ni Jimbo la Wawi aliipongeza hotuba ya ya Rais Dk. Shein aliyoitowa katika kilele cha Sherehe za miaka 56 ya Mapinduzi Zanzibar, kwa kusema ilikuwa imesheheni kila kitu na aliyoeleza yote ni ya kweli kabisa na yamefanywa kwa vitendo.

Nae Muhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agostino (SAUT), kiliopo Mwanza Dk. Zakayo Bernad aliipongeza hotuba aliyoitoa Dk. Shein ambayo ilionekana na kusikika katika vyombo vya habari mbali mbali nchini na kusema kuwa hotuba hiyo ni kitabu rejea ambacho  wanafunzi wanaweza kukitumia katika ufanyaji wa tafiti zao.

Mkurugenzi  wa Chuo cha Utawala wa Umma (IPA) Dk. Mwinyi Talib kwa upande wake alieleza kuwa hotuba hiyo ni ushahidi wa kutosha kuwa Rais Dk. Shein anaongoza kwa kufuata misingi ya Katiba, Sheria na Utawala Bora na ndio maana mafanikio makaubwa yameweza kupatikana katika uongozi wake.

Bi Rahma Abasi Madeweya mkaazi wa Fuoni Michenzani alieleza kuwa kwa upande wake amefarajika sana na hotuba ya Rais Dk. Shein hasa pale aliposisitiza kutoa elimu bure tena bila ubaguzi hatua ambayo itawapunguzia mzigo wazee na walezi sambamba na kuendeleza malengo ya Bwana Abeid Karume ya kutoa matibabu bure.

Akieleza kuhusu mafanikio makubwa  katika sekta ya utalii, Muhidini Kutengwa ambaye ni Mtembezaji watalii alikiri kuwa azma ya Rais Dk. Shein kama alivyoeleza katika hotuba yake jinsi Serikali ilivyoweka mikakati ya kuimarisha viwanja vya ndege na bandari itaimarisha uchumi na kukuza pato la Taifa. “Nathubutu kusema kuwa Rais Dk. Shein ni ‘baba lao’ kwa maendeleo Zanzibar”alisisitiza Kutengwa.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.