Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu akisalimiana na Balozi wa Italia Nchini Tanzania Mhe. Roberto Mengoni mara baada ya kuwasili katika Ofisi ndogo ya Makamu wa Rais, Mtaa wa Luthuli Dar es Salaam.kwa Mazungumzo baina yao yamejikita katika nyanja za kuhifadhi na kusimamia mazingira Nchini.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu pamoja na Balozi wa Italia Nchini Tanzania Mhe. Roberto Mengoni wakiwa katika kikao cha pamoja, (katikati) ni Bi. Haikael Shishirana Kisa Mwaseba maafisa kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Bi. Kemilembe Mutasa, Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Mazingira.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Azzan Zungu akizungumza na Balozi wa Italia nchini Tanzania Mhe. Roberto Mengoni katika Ofisi ndogo ya Makamu wa Rais Luthuli Dar es Salaam. Pamoja na mambo mengine, nchi hizi mbili zimekubaliana mikakati ya pamoja ya kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya Tabia nchi.
Na Lulu Mussa. Dar es Salaam
Waziri wa Nchi Ofisi ya
Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Mussa Zungu amesema Serikali ya
Tanzania iko tayari kuendeleza mashirikiano na Serikali ya Italia katika nyanja
za Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira.
Hayo ameyasema hii leo
Jijini Dar es Salaam mara baada ya kufanya mazungumzo na Balozi wa Italia hapa
nchini Mhe. Roberto
Mengoni katika Ofisi ndogo ya Makamu wa Rais Mtaa wa Luthuli Jijini Dar es
Salaam.
Amesema suala la Mabadiliko
ya Tabianchi ni changamoto kubwa duniani kwa hivi sasa na nchi zinazoendelea
ndio waathirika wakubwa kutokana na uchafuzi wa mazingira unaofanywa na nchi
zilizoendelea.
Waziri Zungu ametoa wito kwa
Serikali ya Italia kuendeleza mashirikiano katika nyanja za udhibiti wa taka na
kujenga uwezo katika uzalishaji wa nishati mbadala ili kukabiliana na uharibufu
wa mazingira unaotokana na ukataji wa miti kwa matumizi ya kuni na Mkaa.
“Serikali ya Rais John
Joseph Pombe Magufuli inatekeleza ujenzi wa mradi mkubwa wa kufua Umeme katika
maporomoko ya Mto Rufiji kwa lengo la kuongeza nishati ya Umeme na kukuza sekta
ya viwanda nchini” Zungu alisisitiza.
Amesema kukamilika kwa mradi
wa kufua umeme wa Mwalimu Julius Nyerere utachochea jitihada za Serikali za
kupambana na uharibifu wa mazingira utokanao na ukataji wa miti kwa matumizi ya
nishati ya kupikia. Ameongeza kusema kuwa jitahada za dhati zinatakiwa kuwepo
pia katika uzalishaji wa umeme wa nishati ya jua na upepo.
Kwa upande wake Balozi wa
Italia nchini Tanzania amesema kuwa nchi yake inalenga kutoa msukumo zaidi
katika mapambano dhidi ya athari za mabadiliko ya Tabianchi, kuhimiza kilimo
rafiki kwa mazingira, nishati mbadala na nishati jadidifu.
Waziri Zungu amemuhakikishia
Balozi Roberto ushirikiano wa dhati katika kupambana na uharibufu wa mazingira
nchini ili kuhakikisha Tanzania inabaki salama kwa taifa la sasa na vizazi
vijavyo.
No comments:
Post a Comment