Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Azungumza na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Simbachawene Ikulu Jijini Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhe. Goerg Simbachawene alipofika Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo na kujitambulia leo baada ya kuchaguliwa kushika wadhifa huo.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza haja kwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kuendelea  kusimamia amani na usalama wa wananchi pamoja na mali zao wakati wote.

Hayo aliyasema leo wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi George Boniface Simbachawene Ikulu Jijini Zanzibar alipofika kwa ajili ya kujitambulisha kufuatia kuteuliwa kushika wadhifa huo hivi karibuni.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alimueleza Waziri huyo kuwa ipo haja kwa Wizara hiyo ya kuendeleza kasi katika kushughulikia suala zima la kulinda amani na usalama kwa wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Vikosi vyake vyote vya ulinzi ili kuhakikisha amani, usalama na utulivu unaendelea kudumu hapa nchini.

Alieleza kuwa Serikali ya Mapnduzi ya Zanzibar kwa upande wake imekuwa ikiendelea kuhakikisha amani, usalama na utulivu unakuwepo kwa wananchi pamoja na mali zao na ndio maana imeanzisha mradi wa Mji Salama katika maeneo yote ya Jiji la Zanzibar ukiwemo Mji Mkongwe ambao umepata umaarufu sana kwa utalii.

Rais Dk. Shein  alieleza kuwa Mradi huo wa Mji Salama mbali ya kuhakikisha usalama kwa wananchi wa Zanzibar pia una lengo la kuhakikisha wageni wote wakiwemo watalii wanaotembelea Jiji la Zanzibar wako salama.

Hivyo, Rais Dk. Shein alisisitiza haja kwa vikosi vya ulinzi vya Jeshi la Polisi kuhakikisha linaendelea na utaratibu wake wa kuwalinda wananchi pamoja na mali zao kwa maeneo ya mjini na mashamba hasa zile sehemu za ukanda wa Utalii.

Aidha, Rais Dk. Shein ameeleza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Jeshi hilo la Polisi katika kusimamia ulinzi na usalama wa wananchi na mali zao pamoja na kusifu juhudi za Jeshi la Uhamiaji kwa kuendelea kudhibiti na kupambana na wahamiaji haramu hapa Zanzibar.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein ameendelea kulisisitiza Jeshi la Polisi kuendelea kusimamia vyema usalama wa barabarani kwa lengo la kuepuka ajali zisizo za lazima pamoja na kuhakikisha sheria na kanuni elekezi za barabarani zinafuatwa.

Aliongeza kuwa kutokana na juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kuimarisha  miundombinu ya barabara hatua hiyo imepelekea madereva wengi kuvunja sheria kwa kwenda mwendo wa kasi na hatimae kuhatarisha maisha kwa wananchi.

Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo kumpongeza Waziri Simbachawene kwa kuteuliwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli kushika wadhifa huo na kumuahidi kuwa yeye pamoja na Serikali anayoiongoza wataendelea kumsaidia na kuipa mashirikiano Wizara anayoiongoza hasa ikizingatiwa kuwa ni  Wizara ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili iendelee kufanya kazi zake vyema.

Nae Waziri George Boniface Simbachawene, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa atahakikisha amani na  usalama vyote kwa pamoja vinaendelea kudumishwa hapa nchini ili Tanzania iendelee kusifika ndani na nje ya Bara la Afrika.

Waziri Simbachawene alimueleza Rais Dk. Shein kuwa ni jukumu la Wizara hiyo la kuhakikisha usalama na amani kwa wananchi pamoja na mali zao unakuwepo wakati wote na kusisitiza kuwa kwa mashirikiano ya pamoja ya vikosi vya ulinzi na usalama jambo hilo litaendelea kutekelezwa.

Waziri huyo alitoa pongezi zake kwa mashirikiano makubwa kutoka Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inayoendelea kuyapata Wizara anayoiongoza pamoja na vikosi vyote vya ulinzi na usalama vilivyomo katika Wizara hiyo.

Aidha, Waziri Simbachawene alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Rais wa Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein kwa kupatiwa eneo la kujenga Ofisi za Idara ya Uhamiaji hapa Zanzibar.

Pamoja na hayo, Waziri huyo alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa juhudi za makusudi zitaendelea kuchukuliwa na Jeshi la Polisi katika kuhakikisha sheria na kanuni zinafuatwa hasa zile za usalama barabarani.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.