Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein,
akikabidhiwa picha ya Siti Binti Saad, “ikimoonesha Bi. Siti Bint Saad na Bwa.
Ali Muhsin, aliyemuibua katika fani ya uimbaji ” akikabidhi Katibu wa Taasisi hiyo
Dkt. Mohammed Omar na (kushoto kwa Rais) Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwanaharakati
Bibi Siti Bint Saad.Bi.Nasra Mohammed Hilal, hafla hiyo imefanyika leo
10-3-2020,Ikulu Jijini Zanzibar.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameitaka Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti
bint Saad kumtangaza mwanaharakati huyo pamoja na kuzitangaza kazi zake ili
zifahamike ndani na nje ya Zanzibar.
Hayo ameyasema leo, Ikulu Jijini Zanzibar
alipokutana na uongozi wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi Siti bint Saad ukiongozwa
na Mwenyekiti wa Taasisi hiyo Bi Nasra Mohamed Hilal pamoja na Mshauri wa
Taasisi hiyo Bwana Abdalla Mwinyi Khamis.
Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein aliueleza
uongozi huo kuwa Mwanaharakati Bibi Siti bint Saad amefanya mambo mengi ambayo
yanapaswa jamii iyafahamu na hilo litafanikiwa iwapo Taasisi hiyo itachukua
jukumu lake hilo na kulifanyia kazi ipasavyo.
Rais Dk. Shein alieleza kuwa mengi aliyoyafanya
Bibi Siti Bint Saad hayaonekani hivi sasa na mengine yamebakia kwenye picha za
kubuni pamoja na kuandikwa vitabuni tu, hivyo, ni jambo jema Taasisi hiyo
ikafanya juhudi za makusudi katika kuhakikisha Mwanaharakati huyo
anatambulikana ndani na nje ya Zanzibar.
Aliongeza kuwa Taasisi hiyo ni vyema ikachukua
juhudi za makusudi katika kuhakikisha kazi pamoja na shughuli za Mwanaharakati
huyo alizozifanya katika uhai wake zinajulikana na jamii iliyopo pamoja na
vizazi vijavyo.
Aidha, Rais Dk. Shein ambaye pia, ni Mshauri Mkuu
wa Taasisi hiyo alisema kuwa katika suala zima la kumtangaza Bibi Siti binti
Saad ni vyema zikatumika kazi zake alizozifanya ikiwa ni pamoja na nyimbo zake
ambazo zilikuwa na sifa, mvuto, ghaiba na elimu kubwa kwa jamii wakati huo na huu
uliopo.
Rais Dk. Shein alieleza kuwa nyimbo za Bibi Siti
Binti Saad zimeweza kuelemisha, kuburudisha, kuadabisha na kufunza jamii kwani
ziligusa katika mambo ya kisiasa, kiuchumi na kijamii.
Rais Dk. Shein alieleza kuwa iwapo kazi za Bibi
Siti binti Saad zitasambazwa zikiwemo CD za nyimbo zake zitapata soko kubwa
sana katika ukanda wa Pwani ya Afrika Mashariki, Kaskazini na Kusini mwa Afrika
pamoja na nje ya Bara hilo.
Alisisitiza kuwa hatua hiyo ni nzuri ambayo mbali
ya kumuenzi Mwanaharakati huyo pia, itasaidia kuzitangaza kazi zake sambamba na
kuongeza mtaji kwa Taasisi hiyo.
Alieleza kuwa soko la nyimbo za Bibi Siti bint
Saad litapatikana kutokana na historia ya msanii huyo ambaye alikuwa ni
mwanamke jasiri na aliyekuwa na kipaji cha sanaa na sauti nzuri iliyowavutia
watu wengi ambayo bado watu wanatamani kuisikia na kumfahamu vilivyo
Mwanaharakati huyo.
Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein aliipongeza Taasisi
hiyo kwa kuendelea na harakati za kuzitunza kazi za Mwanaharakati huyo huku
akisisitiza haja ya kuongeza kasi ya kumtangaza msanii huyo ambaye alipata
umaarufu mkubwa ndani na nje ya Zanzibar.
Pia, Rais Dk. Shein alisisitiza haja kwa Taasisi
hiyo kuandaa Mpango maalum wa muda mrefu, wakati na muda mfupi katika
kumtangaza Mwanaharakati huyo ili historia yake iendelee kutambulika.
Rais Dk. Shein aliutaka uongozi wa Taasisi hiyo
kutovunjika moyo kwa yale yote ambayo yalibuniwa na bado hayajafikia malengo
yaliokusudiwa na kueleza kuwa waendelee na subira huku wakipanga mipango na
mikakati ya kuyafanikisha.
Nae Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwanaharakati Bibi
Siti bint Saad, Bi Nasra Mohamed Hilal alimueleza Rais Dk. Shein mafanikio
yaliopatikana katika Taasisi hiyo pamoja na malengo yaliyowekwa.
Katika maelezo yake Mwenyekiti huyo alimueleza
Rais Dk. Shein kuwa Taasisi hiyo imeweza kufanya mambo mengi ikiwa ni pamoja na
kufanya tafiti mbali mbali zinazohusiana na Mwanaharakati Bibi Siti binti Saad
pamoja na makongamano ya Kiswahili, kutoa mafunzo ya uchoraji, kutoa vyeti vya
uwanachama na mengineyo.
Aidha, Mwenyekiti huyo alieleza kufarajika kwake
kwa kuwa na vijana waliojiunga katika Taasisi hiyo wenye fani mbali mbali ambao
wamekuwa wakitoa msaada mkubwa kwa kuiendeleza na kuiimarisha Taasisi hiyo.
Pia, Mwenyekiti huyo alieleza miradi mbali mbali
ambayo imeandaliwa na Taasisi hiyo yenye lengo la kuongeza kipato kwa Taasisi
pamoja na kuitangaza Taasisi hiyo kwa kuanzisha tovuti yake, kuanzisha vijarida
na mambo mengineyo.
Pia, uongozi huo ulieleza azma ya kuanzisha redio
ya ‘Siti Redio fm” kwa ajili ya kuzitangaza kazi za Taasisi hiyo sambamba na
hivi sasa kumiliki Televisheni Mtandao.
Bibi Siti Binti Saad
alizaliwa katika kijiji cha Fumba mnamo mwaka 1870 na kuishi miaka 80 ambayo
iligawika kwa miaka 40 ya kwanza ya uhai wake akiwa kwa jina la Mtumwa Binti
Saad wakati huo akiwa mfinyanzi wa vyungu vya kupikia na kazi nyengine za
usanii wa mikono.
Miaka 40 ya mwisho wa
maisha yake kuanzia mwaka 1910 hadi 1950 alipofariki alikuwa msanii na muimbaji
kwa hivyo alikuwa maarufu kwa jina la Bibi Siti bint Saad ambapo nyimbo zake
zilipata umaarufu mkubwa kwa kua alikuwa muimbaji wa kwanza wa kike kuimba nyimbo
za taarab tena kwa lugha ya Kiswahili.
Taasisi ya Mwanaharakati
bibi Siti bint Saad ilizinduliwa rasmi Januari 7 mwaka 2014 na Rais wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein.
Wakati huo huo, Taasisi hiyo ilimkabidhi Rais Dk. Shein ambaye
pia, ni Mshauri Mkuu wa Taasisi hiyo kadi yake ya uwanachama, ripoti ya miaka
mitano, kazi inazozifanya taasisi hiyo pamoja na picha yenye maelezo kuhusu
kuibuliwa kwa muimbaji Siti bint Saad na bwana Muhsin Bin Ali.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment