Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akihutubia Wajumbe wa Baraza la Tisa la Wawakilishi Zanzibar kabla ya kulivunja rasmin, hafla hiyo imefanyika katika ukumbi wa mkutano wa Baraza Chukwani Jijini Zanzibar.
Mheshimiwa
Zubeir Ali Maulid; Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar,
Mheshimiwa
Balozi Seif Ali Iddi; Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar,
Mheshimiwa
Job Ndugai; Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa
Kassim Majaaliwa Majaaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mheshimiwa
Omar Othman Makungu; Jaji Mkuu wa Zanzibar,
Mheshimiwa Mgeni Hassan Juma; Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi,
Waheshimiwa Wenyeviti wa Baraza la Wawakilishi,
Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi,
Waheshimiwa Mabalozi Wadogo mlioko Zanzibar,
Wawakilishi
wa Mashirika mbali mbali ya Kimataifa,
Makamanda
wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama na Idara Maalum za SMZ,
Waheshimiwa
Viongozi wa Vyama vya Siasa,
Ndugu
Wageni Waalikwa,
Mabibi na
Mabwana
Assalam Aleikum
Mheshimiwa Spika,
Tuna wajibu wa kumshukuru Mwenyezi
Mungu Mtukufu Subhanahu Wataala, kwa kuendelea kutupa neema ya uhai na afya
njema tukaweza kukutana katika hadhara hii tukiwa salama na kutuwezesha
kuishuhudia siku hii muhimu katika historia ya Baraza hili. Namuomba Mola wetu atuwezeshe kuutekeleza
wajibu wetu huu wa kikatiba kwa ufanisi na aupe kheri na baraka mkusanyiko wetu
huu.
Mheshimiwa
Spika,
Nnakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii
ya kulihutubia Baraza hili la tisa kabla
ya kulivunja. Kwa hivyo, kikao hiki cha
leo kimeitishwa kwa ajili ya kutekeleza matakwa ya kikatiba kwa mujibu wa
mamlaka niliyopewa katika kifungu cha 91(2)(a) cha Katiba ya Zanzibar ya
1984. Kadhalika, kikao hiki, ni
utekelezaji wa kifungu cha 92(1) cha Katiba ya Zanzibar kuhusiana na uhai wa
Baraza la Wawakilishi kuwa ni kipindi cha miaka mitano tangu ulipoitishwa
mkutano wa kwanza na leo tarehe 20 Juni, 2020 ndio nalihutubia Baraza la tisa
kwa mara ya mwisho kabla ya kulivunja, ili kupisha Uchaguzi Mkuu wa mwezi
Oktoba, mwaka 2020.
Mheshimiwa Spika,
Kwa hakika nimeridhishwa sana na kazi
nzuri iliyofanywa na Baraza hili la Tisa la Wawakilishi, kwa utekelezaji mzuri
wa jukumu lenu hili la Kikatiba katika kipindi chote tangu pale nilipolizindua
rasmi tarehe 5 Aprili, 2016. Kwa nyakati
mbali mbali kwenye hotuba zangu nimekuwa nikieleza wazi wazi kuridhishwa kwangu
na kazi nzuri inayofanywa na Wajumbe na wafanyakazi wa Baraza hili. Hivyo, basi, natoa shukurani zangu za dhati
kwako Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid, Spika wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar
kwa umahiri na uongozi wako bora na kazi kubwa uliyoifanya ya kuliongoza Baraza
hili, kwa kipindi chote kuanzia tarehe 5 Aprili, mwaka 2016 hadi sasa. Hapana shaka kwamba umeliongoza Baraza hili
na kuziendesha shughuli zake zote kwa mafanikio makubwa, ingawa nnafahamu
kwamba kazi hio haikuwa rahisi, kwani ilihitaji ujasiri, uvumilivu na hekima
kubwa. Kama nitaimithilisha kazi hio
uliyoifanya na unahodha wa meli, basi meli hio umeifikisha bandarini na kufunga
gati; salama usalimini. Nakupongeza
kwa dhati na nasema hongera sana.
Mheshimiwa Spika,
Kadhalika, natoa shukurani zangu za
dhati kwa Mheshimiwa Mgeni Hassan Juma, Naibu Spika, Mheshimiwa Mwanaasha
Khamis Juma na Mheshimiwa Shehe Hamad Mattar, Wenyeviti wa Baraza, Wenyeviti
wote wa Kamati za Baraza na kwenu nyote Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza la
Wawakilishi, kwa namna tulivyoshirikiana na tulivyosaidiana, kwani bila ya
kufanya jitihada hizo, tusingeweza kuyapata mafanikio tunayoyaelezea hivi
leo. Mmeyatekeleza vyema majukumu yenu
kwa moyo wa kizalendo na kwa ari kubwa mlioionesha na bila ya juhudi zenu
mafanikio haya tusingeyapata. Wakati
wote mmeweka mbele maslahi ya wananchi kwa kutambua kuwa tunawatumikia wao na
sote na tunawajibika kwao. Hapana
shaka, wananchi wameridhishwa na kazi
mliyoifanya na wamejenga imani kwenu kwa kuwawakilisha vyema kwenye Baraza hili
muhimu la kutunga sheria.
Nnakupongezeni kwa dhati kutokana na kazi nzuri mlioifanya ya kuijadili;
kuichangia na baadae mkayakubali na kuyapitisha mapendekezo ya bajeti za Wizara
mbali mbali za Serikali na hatimae bajeti ya Serikali (Makadirio ya Mapato na
Matumizi) kwa mwaka wa Fedha 2020/2021; ambazo jumla ya TZS Trilioni 1.579.2 zimeidhinishwa. Hongereni sana. Hiki ni kiwango cha historia ambacho Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar haijapata kuleta katika Baraza hili la kutunga sheria.
Mheshimiwa Spika,
Nilipolizindua Baraza la Nane la
Wawakilishi la Zanzibar hapo tarehe 11 Novemba, 2010, nilielezea mtazamo wangu
uliotokana na misingi ya Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka 2010 na MKUZA
II na nikaelezea kazi iliyokuwa mbele yetu.
Niliyataja majukumu na
vipaumbele vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba katika sekta
zote za maendeleo ya nchi yetu.
Niliahidi kuwatumikia wananchi wote wa Zanzibar bila ya woga wala
ubaguzi wa aina yoyote na kwa kuzingatia misingi ya haki na utawala bora
inayotokana na Katiba ya Zanzibar ya 1984 na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania ya 1977.
Nilipolihutubia
Baraza la Wawakilishi hapo tarehe 26 Juni, 2015, kwa madhumuni ya kutoa tamko
la kulivunja Baraza hilo hapo tarehe 13 Agosti, 2015; nilielezea kwa urefu
mafanikio tuliyoyapata na changamoto tulizokabiliana nazo, katika kipindi cha
miaka 5 ya mwanzo ya uongozi wangu.
Mheshimiwa
Spika,
Vile vile, kwa wale mliokuwepo katika
Baraza hili, mtakumbuka kuwa katika hotuba yangu ya uzinduzi wa Baraza la Tisa
la Wawakilishi, niliyoitoa tarehe 5 Aprili, 2016, nilielezea mwelekeo wa
mipango ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kipindi cha pili cha uongozi wa
Awamu ya Saba. Kwa mara nyengine, natoa
shukurani kwa Chama changu, Chama cha Mapinduzi, kwa kuniamini na kunipa
heshima kubwa ya kugombea nafasi ya Urais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza
la Mapinduzi, kwa vipindi vyote viwili.
Kadhalika, nawashukuru wananchi wa Zanzibar kwa kunichagua kwa kura
nyingi mimi na wagombea wengine wa Chama cha Mapinduzi na kutuwezesha kupata
ushindi mkubwa. Ushindi huo ulitupa
uwezo wakikatiba wa kuiongoza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba,
ambayo imepata mafanikio makubwa katika nyanja zote za kiuchumi, kijamii na
kisiasa.
Katika muda wote wa uongozi na utendaji
kazi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Awamu ya Saba, tumekuwa
tukiwashukuru na kuwapongeza viongozi wa Awamu zilizopita. Katika uongozi wetu huo, tulizingatia namna
ya kuyafikia matumaini na matarajio ya wananchi ya kuyaendeleza mafanikio
yaliyotokana na utendaji wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Awamu
zilizotangulia. Wakati wote tulizingatia malengo na misingi madhubuti ya
Mapinduzi Matukufu ya tarehe 12 Januari, 1964 na utekelezaji wa Sera na Mipango
mikuu ya maendeleo yenye lengo la kukuza uchumi na kuimarisha ustawi wa jamii.
Katika vipindi vyote viwili vya
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Awamu ya Saba, niliiongoza kwa kuzingatia
utekelezaji wa Mipango Mikuu ya Kitaifa ambayo ni Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM
ya Mwaka 2010 na 2015, Dira ya Maendeleo ya 2020, MKUZA Awamu ya Pili na ya
Tatu na Malengo Endelevu ya Dunia.
Pamoja na mipango hio, vile vile tumezingatia utekelezaji wa ahadi
nilizozitoa katika kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010 na 2015 pamoja na
vipaumbele vyengine ambavyo Serikali iliona kuna haja ya kuvizingatia na
kuvitekeleza kwa lengo la kuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar.
Mheshimiwa Spika,
Kwa hakika sote
tumefanikiwa na tumeridhika na mafanikio makubwa tuliyoyapata katika
utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya vipindi vyote viwili (2010 na
2015). Mafanikio hayo ni makubwa ya kupigiwa mfano tuliyoyapata ambayo
yametokana na jitihada mbali mbali za pamoja zinazofanywa na Serikali,
Mashirika na Taasisi mbali mbali za Kitaifa na Kimataifa, zinazotuunga
mkono. Vile vile, utendaji mzuri wa
viongozi wa ngazi mbali mbali, kwenye jamii yetu, watumishi wa umma pamoja na
wananchi waliovinjari kushirikiana na Serikali yao, nao wameongeza nguvu na ari
ya mafanikio haya. Ni dhahiri kuwa
mafanikio ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM, ambayo ni mkataba
baina ya Serikali yetu na wananchi, yamezidi kukijengea heshima chama chetu na
kimezidi kuaminika kwa wananchi. Hivyo
basi, nna matumaini makubwa kuwa katika Uchaguzi utakaofanyika baadae mwaka
huu, bila ya shaka, wananchi wataendelea kukichagua Chama cha Mapinduzi na
wagombea wake wote watakaowasimamisha, ili kiweze kuongoza Serikali na
kuwaletea maendeleo zaidi.
Mheshimiwa
Spika,
Tuliianza Awamu ya Saba ya Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar tukiwa tumebeba dhima ya matumaini makubwa ya Wazanzibari
ya kuwaunganisha kama Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilivyoelekezwa na Ilani
ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya Mwaka 2010, kwenye kifungu cha 171 (a-c); ukurasa wa
212-213 na kuhusu Ulinzi na Usalama katika kifungu cha 191 ukurasa
230-231. Kwa hivyo, nilifahamu kwamba
dhima tuliyoibeba; mbali ya kuwatumikia wananchi wa Zanzibar, kwa kuwatatulia
shida zao na kero zao zitakazowakabili haitotosha bila ya kuendeleza na
kuimarisha amani, utulivu na mshikamano wa kitaifa miongoni mwa Wazanzibari na
Watanzania kwa jumla.
Niliahidi na nilijidhatiti katika
kipindi cha uongozi wangu kufanya kila nililoweza, ili kuendeleza amani, umoja
na mshikamano, ili Wazanzibari tuendelee kuwa wamoja, tunaopendana,
tunaoshirikiana na tunaosaidiana; bila ya ubaguzi wa aina yoyote au tafauti
ziliopo baina yetu. Niliahidi kwa kusisitiza katika uongozi wangu wote kwamba
Zanzibar itaendelea kuwa nchi ya amani, usalama na utulivu. Leo nnapolihutubia Baraza hili, ili baadae
tuagane, kwa kuzingatia utaratibu uliowekwa, hapana shaka sote ni mashahidi
kwamba nchi yetu iko salama, yenye amani na utulivu na bado tungali
wamoja. Kwa hakika haya ni mafanikio makubwa tuliyoyapata katika uongozi wa
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Awamu ya Saba, ingawa yalikuwepo baadhi ya
matukio yaliyotishia kuudhoofisha umoja wetu na hata kutaka kuhatarisha amani
ya nchi yetu, katika kipindi cha mwanzo na mwanzoni mwa kipindi cha pili cha
Awamu ya Saba ya Serikali nnayoiongoza.
Mheshimiwa Spika,
Katika vipindi
vyote hivyo viwili, walikuwepo baadhi ya wananchi wenzetu waliojaribu
kupandikiza chuki za kila aina na kuleta fadhaa na vurugu miongoni mwa ndugu na
watu wamoja wanaopendana. Vile vile,
walikuwepo baadhi ya watu walioonesha dharau na kejeli kwa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, ili wananchi waichukie, waibeze na waione Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar si Serikali yao.
Zaidi ya hayo, ziliandaliwa njama, hila na mazingira ambayo hayakupaswa
yawepo, ili utokee mtafaruku. Lakini kwa
uwezo wake Mwenyezi Mungu na mapenzi yake kwa Zanzibar, uwezo wa viongozi wa
Serikali, Vikosi vyetu vya Ulinzi na Usalama, ari na imani ya wananchi kwa nchi
yao, Mwenyezi Mungu ametujaalia hali ya amani, umoja, mshikamano na utulivu, hadi hii leo kwa
viwango vile vile tunavyovitarajia na Ishaallah, amani, umoja na utulivu
vitaendelea kudumu hapa Zanzibar.
Kutokana na
jitihada za viongozi wa Serikali, uongozi wao bora na msimamo wao wa dhati na
kwa kushirikiana na viongozi wengine wa jamii, viongozi wa dini na wananchi
wenyewe tumefanikiwa kupambana na changamoto zilizojitokeza na tukaweza kuzishinda
kwa kuzingatia Katiba yetu na Sheria zilizowekwa. Kadhalika, navipongeza vikosi vyetu vya
Ulinzi na Usalama vya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Idara Maalum za SMZ,
kwa kazi nzuri wanazozifanya za ulinzi wa nchi yetu. Hongereni sana.
Mheshimiwa
Spika,
Nawashukuru viongozi wote pamoja na
wananchi kwa kuiendeleza na kuiimarisha amani, umoja na mshikamano, kwa sababu
haya ni mambo muhimu na ya lazima katika kuwaletea wananchi maendeleo. Hapana mbadala wa mambo haya muhimu, kwa
hivyo ni lazima wakati wote tuwe makini na tuchukue tahadhari dhidi ya wenye
nia mbaya na Serikali yetu.
Mheshimiwa
Spika,
Niliahidi kuisimamia amani, umoja na
mshikamano, kuidumisha na kuiendeleza katika kipindi chote cha uongozi wangu;
ikiwa ni misingi madhubuti ya maendeleo yetu. Serikali imeweza kuyatekeleza
majukumu yake katika sekta zote, kutokana na ahadi nilizozitoa, nilipowaomba
wananchi ridhaa yao ili wanichague, mimi na Chama changu Chama cha Mapinduzi
pamoja na wagombea wenzangu wa CCM.
Mheshimiwa
Spika,
Leo ni siku ya
mwisho kwa Baraza la Tisa la Wawakilishi la Zanzibar, ambapo linamaliza uhai
wake katika kufanya kazi zake. Kwa
hivyo, natumia fursa hii kuelezea majukumu ya Serikali ya Awamu ya Saba, namna
yalivyotekelezwa.
Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba, tangu ilipoingia madarakani tarehe 3
Novemba, mwaka 2010 hadi hivi sasa, imeendelea na juhudi za kuitekeleza mipango
mbali mbali ya kiuchumi, ili kuhakikisha kwamba uchumi na ustawi wa wananchi wa
Zanzibar unaimarika. Ilani ya Uchaguzi
Mkuu ya CCM ya mwaka 2010 kifungu cha 123 (a,b,c, na d) ukurasa wa 157-158 na
Ilani ya mwaka 2015 kifungu cha 68 (a,b,c, na d) ukurasa wa 123-124 iliielekeza
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ijenge mazingira yatakayouwezesha uchumi wa
Zanzibar ufikie kiwango cha uchumi wa nchi zenye kipato cha kati, mfumko wa bei
ubaki katika tarakimu moja na wastani wa pato la kila mwananchi liongezeke.
Vile vile, mapato yaendelee kudhibitiwa pamoja na nidhamu ya matumizi ya
Serikali, kupunguza utegemezi kwa Wahisani wa Maendeleo, misamaha ya kodi
isiyokuwa na tija na kuongezeka kwa kiwango cha ukusanyaji wa mapato ya ndani.
Mheshimiwa
Spika,
Katika kipindi cha mwaka 2010 hadi
2019, Pato la Taifa limeweza kukua kutoka thamani ya TZS Bilioni 1,768 mwaka
2010 hadi kufikia thamani ya TZS Bilioni 3,078 mwaka 2019. Ongezeko
hilo ni sawa na mara 1.74 zaidi ya wakati Awamu ya Saba inaingia
madarakani. Kasi ya ukuaji wa uchumi
imeongezeka kutoka asilimia 4.3 mwaka 2010 hadi kufikia asilimia 7.0 mwaka
2019. Vile vile, Pato la Mwananchi nalo
limeongezeka kutoka TZS 942,000 sawa na USD 675 mwaka 2010, hadi kufikia TZS
2,549,000 sawa na USD 1,114 mwaka 2019.
Ongezeko hilo ni kubwa sana ambalo tumefikia sawa na asilimia 170.59.
Kadhalika, mfumko
wa bei nao kasi yake imeshuka kutoka asilimia 14.7 mwaka 2011 hadi asilimia 2.9
mwaka 2019. Kwa hakika hali hii imetoa
faraja sana kwa wananchi kuweza kupata bidhaa muhimu kwa bei ya kuridhisha. Hatua
ya kukua kwa uchumi imeiwezesha Serikali kupata ongezeko la mapato mwaka
hadi mwaka. Katika mwaka 2019/2020,
mapato ya ndani yalifikia TZS Bilioni 748.9 ikilinganishwa na jumla ya TZS
Bilioni 181.1 zilizokusanywa mwaka 2010/2011.
Kadhalika, hali ya utegemezi wa bajeti imepungua kutoka wastani wa
asilimia 30.2 mwaka 2010/2011 na kufikia wastani wa asilimia 5.7 mwaka
2018/2019. Hatua hio, imeiwezesha
Serikali kutekeleza Mipango yake ya Maendeleo kwa kutumia fedha zake yenyewe za
mapato inazokusanya, kwa kiasi kikubwa. Nazipongeza Taasisi zetu za kukusanya
mapato; Bodi ya Mapato ya Zanzibar (ZRB) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)
kwa kuweza kuyatekeleza kwa ufanisi majukumu yao na tukaweza kuyafikia
mafanikio haya ya kuridhisha katika kipindi
cha uongozi wa Awamu ya Saba.
Mheshimiwa Spika,
Hivi sasa, tumedhamiria
kuwekeza zaidi katika kuwejengea uwezo wafanyakazi, ili tuwe na wataalamu wa kutosha katika sekta
mbali za uchumi na kijamii, ikiwa ni pamoja na kuendeleza Uchumi wa Buluu ambao
umejumisha uvuvi, utalii, usafiri wa
bahari, mafuta na gesi asilia, ufugaji wa mazao ya baharini. Tumejidhatiti katika kuwawezesha wajasiriamali na kukuza Maendeleo ya viwanda kwa kushirikiana na sekta
binafsi. Tutaongeza nguvu katika kuunganisha sekta ya utalii na sekta nyengine
za uzalishaji, ili utalii uweze kuwa na manufaa zaidi.
Mheshimiwa
Spika,
Katika kipindi kilichofikia Disemba
2010, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iliidhinisha miradi 648 yenye mtaji wa
makisio wa TZS bilioni 5.9 na kutarajiwa kutoa ajira zipatazo 51,822 kwa
wazalendo. Katika kipindi chote cha Awamu ya Saba, Serikali imefanya jitihada
kubwa za kushajiisha na kuendeleza uwekezaji nchini. Idadi ya miradi
iliyoidhinishwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba kupitia
Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA), hadi kufikia Juni mwaka 2020,
imefikia jumla ya miradi 749 yenye mtaji wa makisio wa TZS bilioni 6.7 na ajira
kwa wazalendo zinazotarajiwa kupatikana ni 55,888.
Mheshimiwa
Spika,
Katika kipindi hiki, Serikali
imetayarisha sera ya ardhi, ili kusimamia na kutekeleza mipango ya matumizi
bora ya ardhi. Katika kipindi cha miaka
kumi iliyopita tulikamilisha Mkakati wa Matumizi ya Ardhi Zanzibar (National
Spatial Development Strategy - 2015).
Katika Mkakati huu, Miji Kumi na Nne (14) ilipangwa, ikiwemo Mji wa
Zanzibar, Chake-Chake, Wete, Mkokotoni, Konde na Kengeja. Kati ya Miji hiyo,
Serikali imekamilisha mipango ya miji mitano ambayo ni Mji wa Zanzibar, Nungwi,
Mkokotoni, Chwaka na Makunduchi. Matayarisho ya mipango ya miji ya Chake-Chake
na Wete imeshaanza.
Kadhalika,
katika mwaka 2014, Serikali ilikamilisha Mpango Mkuu wa Mji wa Zanzibar. Katika Mpango huo, Serikali imeamua kuanzisha
eneo jipya la Biashara na Utamaduni.
Eneo lote kutoka Darajani hadi Kariakoo na kutoka Maisara hadi Kinazini
litapangwa upya, ili kuanzisha ujenzi wa nyumba za ghorofa, kuweka kituo kipya
cha mabasi, kuongeza sehemu mpya za maduka na biashara na kujenga sehemu mpya
za bustani. Aidha, Mji wa Zanzibar utakuwa na miji mitatu mipya; Chuini kwa
upande wa Kaskazini, Tunguu kwa upande wa Mashariki na Fumba kwa upande wa
Kusini. Mipango hii inafanywa kuhakikisha kuwa Zanzibar inaendelea ikiwa
na uwiyano wa kiuchumi, kijamii na kimazingira, ili kufikia lengo lake la
Milenia na kuelekea katika Malengo Mapya ya Maendeleo Endelevu (Sustainable Development
Goals).
Katika Awamu hii ya Saba, Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, iliandaa na kutekeleza miradi mbali mbali ya kimkakati
ikiwemo kuanzisha Idara ya Mipango Miji na Vijiji mwaka 2013. Mpango Mkuu Mpya
uliandaliwa wa kuliendeleza Jiji la Zanzibar (Zanzibar City) pamoja na miji
yetu mingine iliyopo Zanzibar. Uamuzi
huo ulianzisha Mpango Mkuu wa Matumizi ya Ardhi kwa kuweka maeneo maalum ya
makaazi, biashara na shughuli nyengine zikiwemo za kilimo na ufugaji. Katika utekelezaji wa azma hio, kwa
kushirikiana na Sekta Binafsi, Serikali ikahamasisha miradi ya ujenzi wa nyumba
za kisasa za makaazi, biashara na za kutoa huduma nyengine mbali mbali. Serikali ilifunga mkataba na Bakhresa “Group
of Companies”, ili kujenga miundombinu katika Maeneo Huru ya Uchumi ya
Fumba. Jumla ya kilomita 12.7 za
barabara zimejengwa, umeme umefikishwa na maji yamesambazwa.
Hadi sasa jumla ya nyumba 200
zimejengwa pamoja na kiwanda cha maziwa na maeneo ya kupumzikia watu. Vile vile Kampuni ya SS Bakhresa “Group of
Companies” imekamilisha ujenzi wa Hoteli ya Verde huko Mtoni, iliyowekwa jiwe
la msingi tarehe 3 Januari, 2017 na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi na ilifunguliwa rasmi tarehe 11 Januari, 2020 na Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Ujenzi huo pia ulijumuisha maeneo ya michezo
ya maji (water park) na “Marina”.
Mradi wa Ujenzi wa Mji wa Kisasa wa
Kibiashara pamoja na hoteli kubwa ya nyota tano ulioanza kutekelezwa na Kampuni
ya “Pennyroyal” ya Gibralter kwa gharama ya USD Milioni 800, ulioanza katika
mwaka 2013. Ujenzi wa hoteli uko katika
hatua ya maandalizi hadi leo.
Mradi mwengine wa nyumba za makaazi
unaendelea kutekelezwa huko Nyamanzi na
Kampuni ya CPS, ambapo hadi mwaka huu wa 2020, jumla ya nyumba za makaazi 465
zimejengwa. Nyumba 169, miongoni mwao
zimeshamalizika na 120 zimeshakabidhiwa kwa wenyewe waliozinunua na
naamini miongoni mwa Wajumbe wa Baraza hili mtakuwemo. Nakupongezeni sana.
Hatua za ujenzi wa nyumba nyengine zinaendelea. Vile vile, Serikali kupitia
Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (ZSSF) imekamilisha ujenzi wa majengo 15 ya nyumba za kisasa za ghorofa 7 zenye jumla ya
fleti 210 huko Mbweni, ambapo fleti 146 tayari zimeuzwa na zilizobakia zimo
katika utaratibu wa kuuzwa.
Hivi sasa, Mfuko huo unaendelea na
ujenzi wa majengo mawili yenye fleti 28 na kuanza ujenzi wa sehemu za michezo
na biashara kwenye eneo hilo. Hivi
sasa, Serikali inaendelea na ujenzi wa
nyumba za kisasa kwa ajili ya wananchi
katika eneo la Kwahani, ambapo majengo 3
ya ghorofa sita yenye fleti 70,
yanaendelea kujengwa na Kampuni inayojenga itaikabidhi Serikali katika mwezi wa
Septemba, 2020. Hatua hii ya ujenzi
ni Awamu ya Kwanza, ambapo ujenzi huu
utaendelea katika awamu mbali mbali hapo baadae, hadi nyumba zote
zitakapokamilika kujengwa katika eneo hilo.
Kwa upande wa
majengo ya biashara na kuimarisha haiba ya Jiji la Zanzibar, Serikali kupitia
Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF) inakamilisha mradi wa ujenzi wa
majengo mawili ya kisasa katika eneo la Michenzani na itajenga jengo jengine
kwa ajili ya maegesho ya gari (car park).
Jengo la kwanza
linalojulikana kwa jina la “Michenzani Shopping Mall” na jengo la pili la
biashara ambalo limepewa jina la Marehemu “Sheikh Thabit Kombo Mall”, ujenzi wake unatarajiwa kukamilika hivi
karibuni. Hapana shaka majengo haya yatabadilisha kabisa haiba ya eneo la
Michenzani na vile vile yataendeleza dhamira ya Mwasisi wa Mapinduzi ya
Zanzibar ya tarehe 12 Januari, 1964, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume ya kuupa
hadhi mtaa wa Michenzani na kuliendeleza Jiji la Zanzibar kwa kujenga majengo
ya kisasa.
Mheshimiwa
Spika,
Katika kipindi hiki cha Awamu ya Saba,
ilikamilisha ujenzi wa nyumba za fleti za Mpapa, ambapo jumla ya nyumba 24
zilikamilishwa na kupewa wananchi.
Pamoja na kuzifanyia matengenezo nyumba kadhaa za maendeleo za Mtemani
Wete Pemba na Madungu Chake Chake Pemba kwani
nyumba hizo zilikuwa katika hali mbaya.
Kazi hii itaendelezwa na Shirika la Nyumba kwenye Miji mingine, hatua
kwa hatua.
Pamoja na hatua hio, Serikali pia
imelifanyia matengenezo makubwa jengo maarufu la “Chawl”, maarufu Jumba la
Treni liliopo Darajani, lililojengwa mwaka 1880, ili kulipa haiba nzuri jengo
hilo muhimu la biashara. Sasa
linaonekana vyengine na biashara zimepamba moto.
Mheshimiwa
Spika,
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya
Awamu ya Saba, inaendelea kuimarisha mazingira ya biashara kwa kushirikiana na
sekta binafsi. Licha ya kwamba hatujaweza kuuweka vyema uwiano na urari wa
biashara, usafirishaji wa bidhaa ndani na nje ya Tanzania unaendelea kuimarika.
Katika kipindi cha miaka kumi iliyopita, jumla ya tani 2,937,198.4 za bidhaa
zenye thamani ya TZS Bilioni 4,120.25 ziliingizwa nchini ikilinganishwa na
bidhaa zenye thamani ya TZS Bilioni 769.85 zilizosafirishwa kwenda nje ya nchi.
Jumla ya bidhaa zenye thamani ya TZS Bilioni 1,997.88 zilisafirishwa kwenda
Tanzania Bara na bidhaa zenye thamani ya TZS Bilioni 1,245.62 ziliingizwa
Zanzibar kutoka Tanzania Bara katika kipindi hicho.
Mheshimiwa
Spika,
Kuhusu biashara ya karafuu, katika
kipindi hiki cha miaka kumi, Serikali imenunua jumla ya tani 37,995.60 za
karafuu, zenye thamani yaTZS Bilioni 511.27 kutoka kwa wakulima na kati ya hizo
jumla ya tani 37,782.2 za karafuu zenye thamani ya TZS Bilioni 614.86, sawa na
USD Milioni 324.37 ziliuzwa nje ya nchi.
Kwa kipindi cha miaka tisa mfululizo,
Serikali ilimlipa mkulima kiwango cha
asilimia 80 ya bei ya karafuu katika soko la dunia, ambayo ni sawa na TZS
14,000; kwa kilo moja ya karafuu kavu za daraja la kwanza. Vile vile, TZS
12,000 kwa kilo moja yya karafuu kavu za daraja la pili na TZS 10,000 kwa kilo
moja ya karafuu za daraja la tatu. Mkakati hii imelenga katika kumnufaisha
mkulima na kuhakikisha kwamba zao la karafuu linazidi kuimarishwa kwa hali
yoyote. Vilevile, Serikali ilianzisha bima maalum kwa wachumaji wa karafuu
wanaopata ajali na kuwazawadia wakulima bora. Hatua hizo ziliongezea wakulima
ari na juhudi za kukiendeleza kilimo cha karafuu.
Mheshimiwa
Spika,
Mpango Mkakati wa Miaka Kumi wa
Kuliendeleza Zao la Karafuu umefanikiwa sana. Jumla ya miche milioni 3,465,034
imetolewa kwa wakulima katika kipindi hiki ambapo baadhi ya mikarafuu hio hivi
sasa imeanza kuzaa. Aidha, jumla ya Vituo vipya 22 vya kisasa vya kununulia
karafuu vilijengwa huko Pemba. Shirika la Biashara la Taifa (ZSTC), lilifanyiwa
mageuzi makubwa, ili lijiendeshe kibiashara.
Kwa hakika, nawashukuru wakulima wa
karafuu wa Unguja na Pemba kwa kuziuza karafuu zao katika vituo vya ZSTC.
Kadhalika, nawapongeza wananchi, ZSTC, Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na
Uvuvi na Idara Maalum za SMZ kwa kuliendeleza na kuliokoa zao la karafuu kiwa
ni pamoja na kupambana na magendo ya karafuu na kuyadhibiti.
Sheria ya Viwango
Namba 1 ya mwaka 2011 ililenga kuimarisha sekta ya biashara na viwanda kwa
Zanzibar na Sheria ya Ushindani Halali wa Biashara na Kumlinda Mtumiaji Namba 5
ya 2018 zimeanza kutekelezwa kwa mafanikio makubwa.
Mheshimiwa
Spika,
Sekta ya Viwanda imeendelea kutoa
mchango mkubwa katika kipindi hiki cha Awamu ya Saba. Mchango wa Sekta hio
katika Pato la Taifa umeongezeka kutoka asilimia 8.2 mwaka 2013 hadi 17.8 mwaka
2018. Katika kuimarisha Soko la Ajira,
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba, imeandaa mipango mbali mbali
yenye lengo la kukuza sekta ya viwanda. Utengenezaji wa bidhaa katika baadhi ya
viwanda vilivyokuwapo awali na vyengine viliyoanzishwa katika miaka ya karibuni
umezidi kuimarika. Jumla ya viwanda 340 vilianzishwa katika kipindi cha miaka
10 iliyopita.
Mheshimiwa
Spika,
Serikali imeanzisha Wakala wa Maendeleo
ya Viwanda Vidogo Vidogo na vya Kati (Small and Medium Industries Development
Agency - SMIDA) kwa mujibu wa sheria Namba 2 ya mwaka 2018. Wananchi waliojiajiri wenyewe katika sekta
hii hadi mwishoni mwa 2018 wamefikia watu 180,851. Nawapongeza wawekezaji wote
waliowekeza katika sekta ya viwanda, kwa kuitikia wito wa Serikali na
kuimarisha maendeleo ya sekta hii.
Serikali imeendelea kushirikiana na
Sekta Binafsi katika kuimarisha sekta ya viwanda na biashara pamoja na kwa
kuyafanyia kazi mapendekezo yanayotolewa na Baraza la Biashara la Zanzibar
(ZNBC), katika mikutano ya kila mwaka tunayoifanya pamoja na kuendeleza Tamasha
la biashara.
Mheshimiwa Spika,
Serikali ya Awamu
ya Saba iliahidi kuwa itauimarisha utalii, ili uwe ni kichocheo cha maendeleo
ya sekta ya biashara, usafirishaji na uchukuzi wa barabara, baharí na anga na
kuujenga utalii wenye kuheshimu mila zetu, desturi na utamaduni wa Mzanzibari.
Mheshimiwa Spika,
Katika kipindi hiki cha miaka kumi
Serikali imetekeleza kwa mafanikio makubwa Mpango wa Utalii kwa Wote (Tourism
for All) tulioutangaza rasmi tarehe 16 Oktoba, 2011 katika ukumbi wa Salama,
Bwawani. Tumefanya jitihada kubwa za kuitangaza
Zanzibar katika masoko mapya ya Bara la Asia na Ulaya na jitihada zetu za
kushajiisha uwekezaji na ujenzi wa hoteli kwa ajili ya maendeleo ya sekta ya
utalii zilifanikiwa sana.
Hadi kufikia mwezi
Novemba, 2019, Zanzibar ilikuwa na hoteli zilizosajiliwa na kutoa huduma
zipatazo 509 za madaraja mbali mbali, ambapo 26 kati yao ni za nyota 5 na 20 ni
za nyota 4 na nyengine ni za daraja mbali mbali. Takwimu zinaonesha kuwa idadi ya watalii
walioitembelea Zanzibar imeongezeka kutoka 133,000 katika mwaka 2010 hadi
kufikia 538,264 mwaka 2019, ikiwa ni sawa na ongezeko la mara 4 katika miaka
kumi iliyopita. Mipango mbali mbali
imeandaliwa ya kuongeza idadi ya watalii watakaoitembelea Zanzibar katika siku
zijazo. Serikali imechukua hatua madhubuti kuhusu ulinzi na usalama kwa watalii
kwenye maeneo mbali mbali wanayotembelea na kwenye hoteli wanazoishi.
Mheshimiwa
Spika,
Serikali
imeziimarisha huduma za makumbusho na mambo ya kale kwa kuipa umuhimu unaostahiki historia ya
Zanzibar na kuimarisha utalii. Majengo
ya kihistoria yakiwemo magofu na majengo ya makumbusho na mapango mbali mbali
ya kihistoria yaliopo katika Mikoa yote ya Unguja na Pemba yameanza kufanyiwa
matengenezo makubwa. Majengo ya historia
ya Bungi Miembe Mingi; kwa Bi. Khole, Fukuchani, Kaskazini na mingine yameanza
kufanyiwa ukarabati na tayari yanatembelewa na watalii.
Katika kipindi
hiki jumla ya wageni 24,863 waliyatembelea maeneo yetu ya historia kwa mwaka
2019, ikilinganishwa na wageni 13,251 waliotembelea mwaka 2010.
Mheshimiwa
Spika,
Natoa wito kwa wananchi wote wa
Zanzibar na Tanzania kwa jumla waendelee
kuyahifadhi maeneo ya historia na mambo ya kale, ambayo ni muhimu kwa utamaduni wetu na ni hazina muhimu
kwa historia na nnawahimiza wayatembelee
maeneo yetu ya historia, kwa lengo la
kuuimarisha utalii wa ndani.
Mheshimiwa Spika,
Kwa lengo la
kukuza uchumi, kupata lishe bora na kuwa na usalama wa chakula nchini, Serikali
imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha kilimo cha mazao mbali mbali. Katika
kipindi hiki Serikali imeendelea kuimarisha kilimo cha mpunga kwa kutoa ruzuku
kwa wakulima ya asilimia 75 ya pembejeo za kilimo pamoja na huduma za matrekta
wao wenyewe wanatoa 25% tu. Teknolojia ya kisasa ya kilimo cha mpunga shadidi
ilitumika kupitia Mradi wa Kuongeza Uzalishaji na Tija (ERPP), na imechangia
kuongezeka mavuno ya zao la mpunga.
Jitihada hizo
zimepelekea kuongezeka kwa mavuno ya mpunga kutoka tani 21,014 mwaka 2010 hadi
tani 47,507 mwaka 2019. Mazao mengine ya chakula,
matunda na mboga nayo yaliongezeka kutoka tani 289,481 mwaka 2010 hadi kufikia
tani 404,285 mwaka 2019, sawa na ongezeko la asilimia 30. Mafanikio hayo, yameiwezesha Zanzibar
kujitosheleza kwa chakula kwa asilimia 60 mwaka 2018, kutoka asilimia 51 mwaka
2011.
Mheshimiwa
Spika,
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
imetekeleza Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa 2015, kifungu 72(c) kwa kuanzisha
ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji
maji katika hekta 2,200 za mabonde ya Cheju, Kibokwa, Kilombero kwa Unguja na
Mlemele pamoja na Makwararani kwa Pemba, ili kuimarisha na kukiendeleza kilimo
cha mpunga. Mradi huo ulizinduliwa tarehe 2 Januari, 2020 huko Kisongoni na
umegharimu USD Milioni 50, ambazo ni mkopo kutoka Benki ya Exim ya Jamhuri ya
Korea na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imechangia USD Milioni 14. Kadhalika, hivi sasa, Serikali imeanza
kutekeleza Mpango wa Maendeleo ya Sekta ya Kilimo ya Zanzibar (ASDP) wa miaka
kumi, unaogharimu USD Milioni 148 kwa kushirikiana na Washirika wa Maendeleo.
Mheshimiwa
Spika,
Jambo moja la kufurahisha sana ambalo
limefanywa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kupandisha hadhi Kituo cha
Utafiti wa Kilimo Kizimbani kuwa Taasisi ya Utafiti wa Kilimo ya Zanzibar, kwa
mujibu wa Sheria Namba 8 ya mwaka 2012. Kituo hiki kina historia kubwa kwani ni
kituo cha kwanza kabisa Afrika Mashariki kilichoanzishwa katika miaka ya 30. Watu walikuja kujifunza kilimo hapa Zanzibar
miaka hio. Tafiti mbali mbali za mbegu
za mazao ya chakula, biashara, mboga na matunda zimefanywa katika Taasisi hio
na matokeo yake yanatumika kwa kukiendeleza kilimo.
Mheshimiwa
Spika,
Vile vile, Serikali imeanzisha maonesho
ya kilimo, uvuvi na ufugaji kila mwaka, tangu mwaka 2018. Maonesha hayo
yanafanyika huko Chamanangwe kwa Pemba na Langoni kwa Unguja. Kadhalika, Serikali imenunua matrekta mapya 30 kutoka katika Kampuni
ya Mahindra Mahindra ya India, ambapo matrekta 20 yameshawasili nchini na
mengine kumi yako njiani yataletwa. Katika jitihada za kukiendeleza Kituo chetu
cha Matrekta cha asili kule Mbweni,
Serikali imeanzisha Wakala wa Serikali wa Huduma za Matrekta na Zana za Kilimo
kwa mujibu wa Sheria Namba 2 ya mwaka 2019; kwa ajili ya kuyahudumia matrekta
na zana zote za kilimo hapa Zanzibar.
Mheshimiwa Spika,
Katika mwaka 2017, Serikali ilianzisha
Taasisi ya Utafiti wa Mifugo kwa mujibu wa sheria Namba 7 ya mwaka 2020,
inayoshughulikia na kuzipatia ufumbuzi changamoto za wafugaji. Vituo vya huduma za mifugo Unguja na Pemba,
vimeimarishwa, ili viweze kutoa huduma kwa ufanisi. Jumla ya ng’ombe 110 aina
ya Fresian na Jersey Unguja na Pemba, wamepandishwa kwa njia ya sindano, ambayo
ni sawa na asilimia 200 ya lengo. Kadhalika, jumla ya vijana 224 wamepatiwa
mafunzo ya kinga na tiba na huduma za ugani, ili kuendeleza shughuli za ufugaji
kwa ufanisi. Vile vile, vikundi mbali mbali vya ufugaji
vimeanzishwa na vimepewa ng’ombe
wa maziwa bure 368 na mbuzi wa maziwa
720, ili waendeleze ufugaji.
Mheshimiwa
Spika,
Katika Kuendeleza Sekta ya Uvuvi,
Serikali ilianzisha upya kampuni
ya Uvuvi (ZAFICO). Kampuni hio tayari
imenunua boti ya kisasa ya uvuvi iitwayo Sehewa II ambayo ilizinduliwa tarehe 2
Disemba, 2019. Boti hio tayari imeanza kazi kwa ajili ya uvuvi wa Bahari Kuu na
imetoa mafunzo kwa wafanyakazi wake.
Boti nyengine ya pili itawasili nchini mwezi wa Septemba, 2020. Boti zote mbili kila moja ina uwezo wa
kuchukua tani 40 za samaki kwa wakati mmoja.
Kadhalika, Serikali kupitia ZAFICO imeanza mradi wa ujenzi wa chelezo na
mtambo wa kusarifu samaki kwenye bandari ya Malindi na shughuli za wavuvi
wadogo zimeimarishwa. Jitihada hizi za Serikali zimewezesha kuongezeka kwa
kiwango cha samaki waliovuliwa kutoka tani 25,396 mwaka 2010 hadi kufikia tani
36,728 mwaka 2019. Sambamba na hatua hizi, Serikali imeanzisha Taasisi ya
Utafiti ya Uvuvi na Mazao ya Baharini, ambayo nayo imeanza kazi vizuri
sana. Jengo la Taasisi hio jipya
linaendelea vizuri pale Maruhubi.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa kushirikiana
na Shirika la Kimataifa la Kilimo na Chakula (FAO), Serikali imeanzisha mradi
wa ujenzi wa kituo cha kutotolea vifaranga wa samaki huko Beit Ras, uliogharimu USD Milioni 3.23,
zilizotolewa na Serikali ya Korea, kupitia Shirika la Ushirikiano wa Maendeleo
la Kimataifa la Korea (KOICA). Lengo la mradi huu ni kuzalisha vifaranga
milioni moja kwa mwaka, vya samaki, kaa, majongoo na kuvigawa kwa wananchi wa
Unguja na Pemba. Tayari vifaranga
195,000 vya samaki vimegaiwa kwa
wafugaji wa samaki.
Mheshimiwa
Spika,
Hatua za kuliongezea tija zao la mwani
zimechukuliwa. Ahadi ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kuwapa wakulima wa
mwani Unguja na Pemba, vihori 500 kwa kwa ajili ya kubebea mwani tayari
imetekelezwa, kama ilivyoelekezwa katika kifungu cha 76(c) cha Ilani ya CCM ya
Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015. Kwa kushirikiana na wataalamu na wawekezaji wa
Kampuni za “Ocean Fresh” na “Kaappa Carrageenan Nusantaran” za Indonesia,
kiwango cha ubora wa mwani wa Zanzibar kimeongezeka sana kutokana na mafunzo
yaliyotolewa kwa wakulima wa mwani na tunatarajia kujenga Kiwanda cha Mwani
huko Chamanangwe, Wete Pemba, kuanzia mwezi wa Agosti, 2020. Fedha kwa ajili ya ujenzi wa kiwanda hicho,
tayari tunazo, eneo la ujenzi limesafishwa na michoro iko tayari. Muda wetu
ukifika mwezi wa nane tutaanza kazi.
Hawa ni watu wa kweli.
Tutaendelea kushirikiana nao.
Wakulima wa mwani wawe na subira mambo yao yatakuwa
mazuri. Matumaini yangu bei ya mwani
itapanda mara 3 au 4. Wakulima wa mwani
wasivunjike moyo. Kampuni ya Kaappa
Carageenan watanunua mwani huo.
Mheshimiwa Spika,
Serikali iliandaa
Sera Mpya ya Mazingira ya mwaka 2013 yenye kutoa muongozo wa shughuli za
uhifadhi wa mazingira hapa Zanzibar na Sheria mpya ya Usimamizi wa Mazingira
Namba 3 ya mwaka 2015. Kutokana na Sera
na Sheria ya mazingira, Serikali imesimamia kwa ufanisi mkubwa upigaji marufuku
wa uingizaji na utumiaji wa mifuko ya plastiki kuanzia mwaka 2011. Hadi kufikia mwezi wa Mei 2020, jumla ya tani
9.30 za mifuko ya plastiki zilikamatwa na watuhumiwa waliopatikana na makosa
walitozwa faini ya jumla ya TZS Milioni 86.40.
Nimethibitishiwa kwamba fedha hizo walizilipa.
Kadhalika,
Serikali imeendelea kuwaelimisha wananchi kuhusu umuhimu wa kuyatunza na
kuyaendeleza mazingira, kuzitunza raslimali
zisizorejesheka hasa mchanga, mawe, kokoto na kifusi pamoja na kuzuia
ukataji ovyo wa miti na kuwahamasisha wananchi wapande miti kwa wingi
sana. Naipongeza Ofisi ya Makamo wa Pili
wa Rais kwa kazi nzuri wanayoifanya.
Serikali inakabiliana na athari za
mabadiliko ya tabianchi kwa kutekeleza
mpango mkakati wa miaka mitano, kwa mafanikio makubwa. Kadhalika, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,
Awamu ya Saba imelisimamia kwa mafanikio makubwa suala la maafa, kwa kuzingatia
sheria Namba moja ya 2015.
Katika kukabiliana na maafa, jitihada
mbali mbali zimechukuliwa na Serikali zikiwemo ujenzi wa misingi ya kupitisha
maji ya mvua ambayo husababisha maafa ya mafuriko katika makaazi ya watu kwenye
maeneo mbali mbali ya Jiji la Zanzibar.
Serikali ilibuni na ilitekeleza Mradi wa Huduma za Jamii Mijini (ZUSP)
uliofanikiwa kuliondoa tatizo hilo la mafuriko ya maji ya mvua, katika maeneo
mbali mbali.
Mheshimiwa
Spika,
Katika vipindi vyote wiwili vya
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu ya Saba, imeelekeza juhudi kubwa
katika kupambana na usafirishaji na matumizi ya dawa za kulevya. Hatua hizo ni pamoja na kuwakamata
na kuwachukulia hatua wale wanaofanya kazi hii ya haramu ya kusafirisha dawa za
kulevya.
Kadhalika, mafanikio yamepatikana
katika kuvivunja vikundi vingi vilivyokuwa vikitumia dawa za kulevya. Vile vile, kwa lengo la kuwarekebisha
watumiaji wa dawa za kulevya, Serikali imewaweka kwenye nyumba maalum za nafuu
(Sober Houses), vijana wapatao 9,030, ambapo kati ya hao vijana 3,161 sawa na
asilimia 35, walifanikiwa kuachana kabisa na dawa hizo.
Vile vile, Serikali ya Awamu ya Saba,
imejenga kituo cha tiba na marekebisho ya tabia kwa waathirika wa dawa za
kulevya kilichopo Kidimni, Wilaya ya Kati Unguja. Ujenzi huo umo katika hatua za mwisho
kukamilika na ununuzi wa vifaa mbali mbali vya tiba na kurekebisha tabia za
vijana hao umekamilika. Kituo cha
dharura cha tiba na marekebisho, kwa hivi sasa kimefunguliwa katika Hospitali
ya Wagonjwa wa Akili, Kidongo Chekundu.
Vile vile, katika jitihada za kupambana na janga hili, jumla ya
watuhumiwa 398 wametiwa hatiani katika kipindi hiki, wakiwemo raia wa kigeni.
Idadi ya kesi za dawa za kulevya
imekuwa ikiongezeka mfululizo kutoka kesi 183 kwa mwaka 2015, kesi 354 kwa mwaka 2016, kesi 694
kwa mwaka 2017, kesi 654 kwa mwaka 2018 na kesi 503 kwa mwaka 2019. Vile vile, kuna ongezeko la kiwango cha dawa
zinazokamatwa, kimebainika ambapo katika mwaka 2015, zilikamatwa kilogramu
68.6, mwaka 2016 kilogramu 45.28, mwaka 2017 kilogramu 138.94, katika mwaka
2018 zilikamatwa kilogramu 722.22 na
mwaka 2019 zilikamatwa kilogramu 701.73 za dawa za kulevya. Hali hio si nzuri sana.
Ni dhahiri kuwa ongezeko hilo la kasi
na kiwango cha dawa za kulevya zilizokamatwa pamoja na wahalifu
waliohusika limetokana na jitihada za
Serikali kupitia vyombo vyake pamoja na
raia wema katika kukabiliana na janga hili.
Leo tumetoa taarifa hizi rasmi, ili wananchi wajue tulikuwa
hatukulala. Tulikuwa tunangoja tu muda
ufike tuwaeleze.
Natoa wito kwa viongozi na wananchi
kuendelea kushirikiana na Tume ya Taifa ya Kuratibu na Udhitiiti wa Dawa za
Kulevya na vyombo vyengine vya ulinzi katika kufanikisha mapambano dhidi ya
usafirshaji na matumizi ya Dawa za
Kulevya, ambazo huathiri zaidi vijana ambao ni nguvu kazi ya Taifa letu. Sheria mpya tuliyoitunga inafanya kazi vizuri
sana.
Mheshimiwa
Spika,
Wananchi wamefaidika sana na juhudi
zetu za kuhamasiha uanzishwaji na uendelezwaji wa vyama vya ushirika na SACCOS
kwa lengo la kujipatia ajira na mikopo ya kujiendeleza.
Mheshimiwa
Spika,
Kipindi cha miaka kumi si kidogo, ndio
maana tumefanya mambo mengi na makubwa.
Baraza hili ndilo yaliyoyafanikisha maendeleo haya ambayo mimi leo naona
raha na furaha kuyaelezea. Naamini na nyinyi mnaona raha hivyo hivyo; kwa hivyo,
endeleeni kunivumilia.
Katika hotuba yangu ya ufunguzi wa
Baraza la Tisa la Wawakilishi nilitoa ahadi kuhusu azma ya Serikali katika
kipindi hiki, ya kuviendeleza vikundi vya ushirika kwa kuvipatia mafunzo,
mikopo na kuvifanyia ukaguzi kwa lengo la kuviimarisha. Leo nataka nieleze bayana kwamba, jumla ya
vyama vya ushirika 39 vya Akiba na Mikopo na vyengine 1,652 vya uzalishaji mali
vimesajiliwa. Hatua hio imefanya idadi
ya vyama vya ushirika vilivyosajiliwa hadi mwezi Oktoba, 2019 kufikia
3,676. Vile vile, mwamko wa wananchi
kujiunga na SACCOS umewezesha kuongezeka kwa mitaji ya Taasisi hizo kutoka TZS
Bilioni 3.5 mwaka 2013 na kufikia TZS Bilioni 14.3 mwaka 2019.
Mheshimiwa
Spika,
Mafanikio yameendelea kupatikana katika
kuimarisha huduma za Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi na kukabiliana na
tatizo la ajira. Tangu mikopo hio yenye
masharti nafuu na isiyo na riba ilipoanza kutolewa mwaka 2014 hadi tarehe 31
Machi 2020 imefikia jumla ya mikopo 3,758 yenye thamani ya TZS Bilioni 5.684
imetolewa na imewanufaisha wananchi 51,973 wa Unguja na Pemba kati yao wakiwemo
wanawake 27,992 ambao wapo wengi kuliko wanaume ambapo wanaume 23,981. Kinamaa
oyee!
Kadhalika, kwa lengo la kuwawezesha
vijana kiuchumi, katika mwezi wa Septemba, 2019 Serikali ilianzisha Mfuko wa
Vijana wenye mtaji wa USD Milioni 20 sawa na TZS Bilioni 46, ikiwa TZS Bilioni
23 kutoka kwenye Khalifa Fund (Mfuko wa Mtawala wa Jumuiya ya Falme za Kiarabu
UAE) na TZS Bilioni 23 kutoka SMZ.
Juhudi hizi za Serikali zitaongeza fursa za ajira na kuimarisha
maendeleo ya vijana. Matayarisho ya
matumizi ya fedha hizo yanaendelea na utekelezaji wake utaanza muda wowote
kuanzia sasa.
Mheshimiwa
Spika,
Katika kipindi hiki, Serikali
iliuendeleza Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, tuliviendeleza vituo vya
mafunzo ya amali, tuliyaimarisha mazingira ya uwekezaji na shughuli za utalii;
ili maeneo hayo yaongeze fursa za ajira nchini hasa kwa vijana. Katika mwaka 2014, tuliuanzisha na
tuliuzindua Mpango Mkakati wa Ajira kwa Vijana, ulioweka vipaumbele katika
sekta za ujasiriamali, elimu ya amali na ufundi stadi.
Serikali ya Awamu ya Saba, imeweza
kutoa nafasi 21,850 za ajira kwa wazalendo na
ajira 20,394 zimetoka kwenye sekta binafsi, ambazo kati ya hizo 13,248
ni za ndani na 7,146 ni ajira za nje.
Naipongeza sana sekta binafsi kwa mchango wao muhimu katika kuongeza
fursa za ajira kwani Serikali haiwezi kukabili changamoto ya ajira bila ya
kushirikisha sekta binafsi. Wataalamu wanasema “private sector is the engine of growth” tafsiri sekta binafsi ndio
injini ya kuufufua uchumi.
Mheshimiwa
Spika,
Katika hotuba
yangu ya ufunguzi wa Baraza la Tisa
niliahidi kuchukua hatua mbali mbali za kuimarisha mazingira ya kufanya
kazi kwa kuzingatia sheria na sera ya utumishi, maslahi ya watumishi,
kuimarisha fursa za mafunzo, usalama kazini na upatikanaji wa vifaa vya kazi na
nyenzo, ili kuongeza ufanisi katika sehemu za kazi. Katika kuyafikia
malengo hayo, kama tulivyoahidi, Serikali ilifanya mageuzi makubwa ya Utumishi
wa Umma baada ya kutungwa kwa Sheria ya Utumishi wa Umma Namba 2 ya mwaka 2011
na Kanuni za Utumishi wa Umma za mwaka 2014. Ofisi ya Rais inayohusika na
Utumishi wa Umma na Utawala Bora imeanzishwa pamoja na kuandaa mpango wa
maendeleo ya wafanyakazi na Miundo ya Utumishi “ Scheme of Service” ya kila
Wizara, Idara, Mashirika na Taasisi zake na kuandaa Miundo na Mifumo ya Taasisi
zote hizo. Suala la mgawanyo wa mamlaka
na dhamana, nidhamu na uwajibikaji wa kazi na kufanya kazi kwa mujibu wa kanuni
ya utumishi yote yametekelezwa kama nilivyoahidi.
Marekebisho ya mishahara ya wafanyakazi
yalifanywa mara nne kuanzia mwaka 2011, 2013, 2015 na 2017, kwa lengo la kuwapa
motisha wafanyakazi kwa kuzingatia mapato yetu wenyewe. Haya yote ni kwa mapato yetu yenyewe. Haijapata kutokea. Awamu ya Saba tumeweza. Viwango vya mishahara
ya wafanyakazi wa ngazi mbali mbali, wataalamu na mabingwa wa fani mbali mbali;
vilibadilishwa na viliimarishwa. Hivi
karibuni, Serikali imekamilisha kazi muhimu ya kuweka viwango vya mishahara na
maposho ya Mashirika yote ya Serikali yenye mfumo mmoja unaolingana na Idara ya
Serikali. Kazi hii imefanyika vizuri na
taarifa nilizoletewa ni kwamba uongozi wa Mashirika, Idara za Serikali na watumishi
wao wameridhika na wamefurahi sana. Ni matumaini yangu kwamba tatizo lililokuwepo la muda
mrefu la kila Shirika la Serikali kufanya utaratibu wake wa mishahara na
maposho, halitotokea tena. Tatizo la
mishahara na mapato leo halipo tena.
Mheshimiwa
Spika,
Hatua ya kupandisha mishahara ililenga
kuwapa motisha na ari watumishi, ili waongeze juhudi na ufanisi katika kazi
zao, kwa lengo la kuwatumikia wananchi kwa nidhamu kubwa na uadilifu. Haikuwa ruzuku ni wajibu wao. “Mchezo
kwao hutunzwa”. Vile vile, hatua hio ni matokeo ya ukuaji mzuri wa uchumi
wetu na kuongezeka kwa mapato. Kwa
uamuzi huo wa Serikali, matumizi ya Serikali kwa ajili ya mishahara
yakaongezeka hadi kufikia TZS Bilioni 417.9 kwa mwaka 2018/2019, sawa na
ongezeko la asilimia 48. Kiwango cha malipo ya mishahara katika mwaka 2010/2011
kilikuwa ni TZS Bilioni 83.1. Hata
hivyo, licha ya ongezeko hilo, Serikali imemudu kulipa mishahara kwa wakati kwa
kipindi chote cha miaka kumi na inaendelea kumudu, kwa vile uchumi wetu
umeendelea kukua kwa kasi na kiwango cha kuridhisha.
Sambamba na
kuimarishwa kwa mishahara ya watumishi wa umma,
vile vile, Serikali katika kipindi hiki imeongeza kwa vipindi viwili
malipo ya pencheni za wastaafu, katika
mwaka 2011 na mwaka 2017. Kadhalika, Serikali imewatayarishia watumishi
mazingira bora ya kufanyia kazi, kwa kujenga majengo mapya yaliyo bora kwa
ajili ya Ofisi mbali mbali za Serikali kwa Unguja na Pemba nyote mashahidi
mnayaona. Miongoni mwa majengo ya ofisi
hizo ni pamoja na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu
wa Serikali, Wizara ya Katiba na Sheria, Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za
Nishati Zanzibar (ZURA) na majengo ya wizara za Serikali yaliyopo Gombani huko
Chake Chake Pemba yanayotumika kwa Wizara sita na mengineyo. Baada ya kuyasimamia mabadiliko makubwa ya
utumishi wa Umma yaliyotekelezwa, tumeshuhudia kuongezeka kwa ufanisi wa kazi
na uwajibikaji kazini, ingawa bado bidii zaidi inahitajika. Sijayataja yale ya Idara Maalum ambayo nayo
yako mengi sana. Kazi nyengine muhimu
tuliyoifanya, ni ya mishahara inayoitwa “mishahara hewa”. Nyinyi Wajumbe wa
Baraza mlilizungumzia hili humu Barazani, na mimi nikamtaka CAG alete ripoti
yake ya mishahara hewa. Kwa hivyo ripoti
ile ni ya kwangu mimi, na nikaifanyia kazi.
Nikaunda timu nzuri ya watu waliokuwa na nidhamu na wanaojua kuwajibika
wakaziangalia wizara tano zilizodhaniwa kuwa na matatizo ya mishahara
hewa. Mbili kati ya hizo hazikuwa na
matatizo makubwa, kwa hivyo tukazitaka fedha wazirudishe.
Tatu miongoni mwao
zilihitaji matatizo yao kuzungumzwa na kuzingatiwa. Taarifa hizi tukazizungumza Serikalini na
tukawajibisha. Walikuwa wakichukua
mishahara kwa ghilba na hila. Nikamwambia Katibu wa Baraza la Mapinduzi na
Katibu Mkuu Kiongozi atangaze katika vyombo vya habari mambo tuliyoyaona na
nyie mkayasikia. Kisha wengine tukawafuza kazi na wengine tukawabadilisha
wizara kwa sababu ya heshima ya Serikali.
Haya lazima myajue Waheshimiwa Wawakilishi kwamba hali yaikuwa
nzuri. Sie tunachuma tupate sote, lakini
wenzetu, tena wengine wako nchi za nje, huku fedha zinaingia katika akaunti
zao. Akhasi kuliko zote ilikuwa Wizara
ya Elimu. Mwenyewe Waziri shahidi
anajua. Yeye hakuhusika aliyakuta mengine
lakini ndio uongozi. Kwa hivyo
tumechukua hatua madhubuti. Udanganyifu si mzuri, na kwa kweli huu ni wizi si
udanganyifu.
Ni wazi kwamba
katika mfumo wowote wa maisha, hata kwa wanyama panakuwa na uongozi; na uongozi
unakuwa na heshima na thamani yake.
Lakini unapoitwa kiongozi unakuwa na kitu cha ziada ambacho watu
wanakiratajia. Hali hii inathibitika
katika ile hadithi ya bwana muuza kasuku.
Kuna bwana mmoja
alikwenda kwa wauza ndege kutika kununua
kasuku. Akakuta kasuku wa rangi tatu, mmoja mwekundu, mmoja wa
kijani na mmoja manjano. Akaulizwa
unataka kununua?. Akasema ehee.
Akaambiwa chagua. Akachagua
mwekundu akauliza kiasi gani?. Akaambiwa
Dola 500. Akauliza huyu wa kijani kiasi
gani?. Akaambiwa Dola 500,000, na huyo ya mwisho Dola Milioni Moja. Akauliza sasa wanatafauti gani?, mbona huyu
ghali zaidi?. Akaambiwa hawa wote
wanamwita huyu bosi. Kila mtu anataka ubosi lakini, ili uupate ubosi ni lazima
ufanye kazi.
Mheshimiwa Spika,
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Awamu
ya Saba ilitambua kuwa lengo lake la kukuza uchumi wa Zanzibar halitaweza
kufanikiwa bila ya kwenda sambamba na
uimarishaji wa barabara, bandari, viwanja vya ndege pamoja na kuwa na nishati
ya uhakika ya umeme. Kwa hivyo, katika kipindi cha miaka kumi iliyopita,
jitihada kubwa zimefanywa na Serikali katika kuimarisha miundombinu hio.
Mheshimiwa
Spika,
Kuhusu miundombinu ya barabara,
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Awamu ya Saba, hadi kufikia mwezi Disemba 2019, imejenga
jumla ya kilomita 129 za barabara kwa kiwango cha lami kwa Unguja na Pemba. Kiwango hiki ni kikubwa cha Zanzibar. Miongoni
mwa barabara hizo ni barabara ya Jendele-Cheju-Kaebona (km 11.7), barabara ya
Njia nne hadi Umbuji (km5), Mwanakwerekwe-Fuoni (km5), Mfenesini-Bumbwini (km
13.6) Magogoni-Kinuni (km 2.15) na barabara ya Bububu-Mahonda-Mkokotoni (km
31), Matemwe-Muyuni (km 7.6), Pale-Kiongele (km 4.6) kwa Unguja. Kwa upande wa Pemba ni barabara tano katika
Mkoa wa Kaskazini Pemba zenye urefu wa km 34.85 nazo ni Wete-Konde (km 15),
Wete-Kando (km 13) Bahanasa-Daya-Mtambwe (km 13.6), Mzambarautakao-Pandani-Finya
(km 8) na Mzambarau Karimu-Mapofu (km 8.6). Nyengine ni barabara ya
Mkanyageni-Kangani (km 6.5) na barabara ya Mgagadu-Kiwani (km 7.6). Tumefanya mambo makubwa sana na yote haya
yametokea hapa hapa katika Baraza lenu, na Baraza hili ndio chem chem ya
maendeleo yetu. Anayesema vyengine hiari yake, lakini wananchi wote wanajua
hivyo.
Mheshimiwa
Spika,
Vile vile, Serikali imejenga daraja na
barabara kwa kiwango cha lami, yenye urefu wa mita mia nne katika eneo la
Kibondemzungu pamoja na kuweka taa za barabarani. Ujenzi huo umekamilika na daraja hilo
lililopewa jina la “Daraja la Dk. Ali Mohamed Shein” ambalo lilifunguliwa rasmi
tarehe 9 Januari, 2020. Hivi sasa kazi za ujenzi wa barabara zinaendelea katika
maeneo mbali mbali ya Unguja na Pemba.
Kwa upande wa Unguja, ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami unaendelea
kwa barabara kutoka Kibondemzungu hadi kituo cha Polisi Fuoni (km 1.6),
Koani-Jumbi (km 6.3), Fuoni-Kombeni (km8.59), na barabara ya
Jozani-Charawe-Ukongoroni-Bwejuu (km 23.3).
Kwa upande wa Pemba, kazi ya ujenzi wa barabara ya Ole-Kengeja (km 35)
upo hatua ya mwisho kukamilika na ianze kutumika rasmi. Naipongeza kwa dhati Wizara ya Ujenzi,
Mawasiliano na Usafirishaji kwa kazi nzuri wanayoifanya.
Mbali ya ujenzi wa barabara unaofanywa
na Wakandarasi, Serikali iliamua kununua zana na vifaa vipya vya kisasa vya
kutengenezea barabara, ili kazi hio ifanywe na Wakala wa barabara. Vifaa hivyo viligharimu jumla ya TZS Bilioni
14. Vile vile, katika kipindi hiki cha miaka kumi, zimewekwa taa za barabarani
na za kuongozea vyombo vya moto katika barabara zetu kwenye maeneo mbali mbali
ya Jiji la Zanzibar na katika manispaa za mji wa Chake Chake, Wete na
Mkoani. Kazi inaendelea vizuri, lakini
juzi nimepata taarifa mbaya za kunitia huzuni na kunifadhaisha. Nimeambiwa taa mpya tulizozitia kule Pemba
kuna watu wanaojidhania kuwa mashujaa wamezing’oa. Mimi nataka niwambie waliofanya kazi hio ya
kuharibu taa zetu, wende wenyewe wakajisalimishe vituo vya polisi, maana
tutawakamata na tumeanza kuwajua. Ni
vyema wende wenyewe kabla ya hatujenda kuwakamata sisi. Tukiwashika sisi yatakuwa mengi sana. Nawanasihi ndugu zangu wa Pemba wasiwe na
ghulka hii ya kuharibu mtu kitu chake.
“Chako ni chako”, lazima ukithamini.
Tabia ya kuvuruga vitu vya Serikali vyenye manufaa na wananchi wengi, ni
jambo la kishetani sana. Nawaambia ndugu
zangu wa Chake na Wete kuwa hili liwe la mwisho.
Mheshimiwa
Spika,
Uimarishaji wa usafiri wa anga ni
miongoni mwa masuala yaliyozingatiwa na Serikali ya Awamu ya Saba, kama
nilivyoahidi wakati nilipoingia madarakani mwaka 2010 ni kuikamilisha kazi ya
ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Abeid Amani Karume, iliyoanzishwa na Serikali yetu
ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Mstaafu Dk. Amani Abeid Karume. Wakati wetu wa Awamu ya Saba, tumejenga njia
za kupitia ndege (taxi ways) kutoka mita 1,805 hadi kufikia mita 3,427.
Tumenunua vifaa vya kisasa kadhaa, kwa mfano mashine mpya tano za kisasa za
ukaguzi wa abiria na mizigo. Kadhalika,
tumejenga uzio wenye urefu wa kilomita 11 unaozunguka eneo lote la uwanja kwa
lengo la kuuhifadhi uwanja huo. Katika
uwanja wa ndege na sehemu nyengine za mji wetu tumeshughulikia ulinzi kwa
kufunga kamera za usalama CCTV, ili kujihami na matukio ya ujambazi ndani ya
uwanja wa ndege na sehemu nyengine.
Kiwanja cha ndege cha Zanzibar sasa ni miongoni mwa viwanja virefu
katika Afrika ya Mashariki ni kiwanja chenye njia ndefu za kurukia ndege kuliko
viwanja vyote vya Afrika Mashariki. Ndege yoyote inatua Zanzibar. Uwanja wa
Abeid Amani Karume ni kiwanja cha Kimataifa.
Hivi sasa Serikali
inakamilisha ujenzi wa jengo jipya la abiria la Terminal III ambalo
litakapomalizika mwezi wat isa mwaka huu, tutakapokabidhiwa, litafikia gharama
za USD Milioni 128.4 badala ya USD 70.4, za mkataba wa mwanzo. Tuliongeza mkataba na mambo kadhaa, ili kuupa
hadhi ya juu uwanja huu. Jengo hili
litaongeza huduma na haiba ya uwanja huo na linatarajiwa kuwahudumia kiasi cha
abiria 1,600,000 kwa mwaka. Tumepiga
hatua kubwa sana.
Mheshimiwa
Spika,
Kuhusu kiwanja cha
ndege cha Pemba, Serikali imechukua hatua za kuimarisha huduma za kiwanja hiki
kwa kuweka taa, ili kuziongoza ndege kuruka na kutua kwa usalama. Kadhalika,
jengo la abiria limefanyiwa matengenezo makubwa na eneo la ziada la maegesho ya
ndege limeongezwa. Serikali inaendelea na hatua za kukiimarisha kiwanja cha
ndege cha Pemba kwa ufadhili wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB),
iliyosaidia kufanywa kwa upembuzi yakinifu pamoja na kuandaa mahitaji yote
yanayohusu ujenzi wa kiwanja kipya cha kisasa cha Pemba. Ripoti ya upembuzi yakinifu tayari
imeshakabidhiwa kwenye Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), kwa ajili ya kuomba
mkopo wa fedha za ujenzi kwa kuzingatia taratibu ziliopo. Tunatarajia kwamba
ujenzi wa Uwanja huu mpya utaanza mara tu baada ya mkopo huo kupatikana. Mimi na Rais John Pombe Magufuli tumeiomba
Benki ya Maendeleo (AfDB) kujenga uwanja wa ndege mpya wa Pemba.
Mheshimiwa
Spika,
Juhudi hizo za
Serikali zimeleta mafanikio katika usafiri wa anga ambapo safari za ndege kwa
Unguja na Pemba zimeongezeka kutoka safari 42,733 mwaka 2010 hadi kufikia
safari 66,393 mwaka 2019. Vile vile, abiria wanaotumia viwanja vya ndege vya
Zanzibar wameongezeka kutoka abiria 596,252 mwaka2010 hadi kufikia abiria
1,426,866 mwaka 2019 na mizigo iliyopitia katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Abeid
Amani Karume imeongezeka kutoka tani 584 mwaka 2010 hadi kufikia tani 2,538
mwaka 2019.
Mheshimiwa
Spika,
Serikali imezingatia umuhimu wa bandari
ikiwa ni lango kuu la biashara na uchumi. Katika hotuba yangu ya ufunguzi wa
Baraza la Tisa la Wawakilishi, niliahidi kuwa Serikali itatekeleza mradi wa
ujenzi wa bandari mpya ya kisasa ya kuhudumia mizigo katika eneo la Mpigaduri.
Bandari ya Malindi itaendelezwa kwa kuiongezea vifaa vya kisasa vya kutolea
huduma za abiria na mizigo nalo hili limeanza kutekelezwa pamoja na bandari ya
Mkoani Pemba. Vile vile, Serikali
iliahidi kujenga gati ndogo ya Mkokotoni na Tumbatu, ili kurahisisha huduma za
usafiri hasa kwa wananchi wa Tumbatu.
Gati ndogo ya Tumbatu tayari imejengwa na ile ya Mkokotoni ujenzi wake
utaanza hivi karibuni.
Jitihada hizo za kuimarisha bandari na
usafiri wa baharini zilifanikiwa katika kipindi hiki cha takriban miaka kumi,
ambapo zana na vifaa vya kisasa vya kazi vilinunuliwa kwa ajili ya kuimarisha
huduma katika bandari zetu za Unguja na Pemba.
Kwa upande wa bandari ya Malindi, utoaji wa huduma hivi sasa umeimarika
sana, ambapo meli kubwa zinazofika katika bandari hio zenye uwezo wa kuchukua
makontena 6,000, sasa zinahudumiwa kwa siku tatu tu badala ya wiki moja kama
ilivyokuwa hapo kabla.
Katika kipindi
hiki majengo manne ya kuwahudumia abiria yamejengwa katika bandari ya Malindi,
Wete na Mkoani ambapo majengo mawili yenye uwezo wa abiria 1,085 wanaweza
kuhudumiwa kwenye bandari ya Malindi, abiria wapatao 300 wanaweza kuhudumiwa
kwenye bandari ya Mkoani na abiria 200 wanaweza kuhudumiwa katika bandari ya
Wete. Vile vile, bandari ndogo ya
Mkokotoni imeimarishwa kwa kujengwa ofisi ya Shirika la Bandari pamoja na
kukamilika kwa ujenzi wa gati ndogo ya Tumbatu.
Bandari za
Zanzibar zimetoa huduma kwa meli za kigeni 1,509 na kuhudumia mizigo
mchanganyiko yenye uzito wa tani milioni 2.6.
Vile vile, jumla ya abiria 20,499,164 walihudumiwa katika bandari ya
Unguja na abiria 9,541,686 walihudumia katika bandari za Pemba. Haya ni mafanikio makubwa sana yaliyopatikana
kwa kipindi cha miaka kumi.
Mheshimiwa
Spika,
Uamuzi wa Serikali wa kujenga Bandari
ya Mpigaduri upo pale pale kama ilivyoelezwa kwenye Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya
2010/2015 katika kifungu cha 90(a) ukurasa wa 151. Hata hivyo, ujenzi huo umechelewa kuanza
kutokana na sababu zifuatazo:- Kwanza, gharama za ujenzi zilizokisiwa na
Kampuni iliyokubaliwa ijenge bandari hio; hapo mwanzo zilibainika kuwa kubwa na
ilichukua muda Serikali kujadiliana juu ya namna ya kupata mkopo wa ujenzi huo. Pili, michoro na ramani ya ujenzi huo
haikutayarishwa katika makisio yaliyofanywa mwanzo, hivyo ilikuwa ni vigumu
kuuendeleza mkopo huo na ujenzi wake.
Kwa hivyo, Serikali ililazimika ichukue hatua za kuandaa mpango kamili
ikiwemo michoro, ramani za ujenzi na gharama halisi kwa awamu ya kwanza ya
ujenzi wa Bandari ya Mpigaduri. Kazi hio sasa inaendelea vizuri pamoja na kutafuta mkopo
wa bei nafuu kwenye benki ya Exim ya Indonesia na Benki ya Exim ya Afrika. Tunatarajia ujenzi huo utaanza baadae mwaka
huu. Hata hivyo, ujenzi wa mradi huo tutauanza kuutekeleza kwa fedha zetu
wenyewe za ndani, ambazo tumezitenga kwenye bajeti ya 2020/2021.
Katika ziara yangu ya mwezi wa Aprili,
2019 nilipokitembelea kisiwa cha Uzi-Ngambwa, nililiona tatizo la usafiri wa
kwenda na kurudi huku na niliahidi kulifanyia kazi suala hili. Kwa hivyo, Serikali imeanza maandalizi ya
ujenzi wa daraja la Unguja Ukuu na Uzi Ng’ambwa. Ujenzi huo utaendelea kutekelezwa kwenye
bajeti ya 2020/2021. Ninaamini kwamba
Serikali ya Awamu ya Nane itamaliza ipasavyo kazi hii.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa lengo la kuimarisha usafiri wa
baharini kati ya Unguja na Pemba na bandari za mwambao wa Afrika ya Mashariki,
Serikali ilinunua meli mpya ya Mapinduzi II yenye uwezo wa kuchukua abiria
1,200 na tani 200 za mizigo na meli mpya ya mafuta inayoitwa MT Ukombozi II
yenye uwezo wa kuchukua tani 3,500 za mafuta.
Meli zote mbili
zilianza kazi mara tu baada ya kuwasili katika mwaka 2015 na 2018. Kadhalika,
hivi sasa Serikali inashughulikia matengenezo makubwa ya meli ya MV Maendeleo
iliyopelekwa Chelezoni huko Mombasa.
Vile vile, Serikali inashughulikia ununuzi wa boti tano za kisasa za
kusafirishia abiria wanaoishi katika visiwa vidogo vidogo.
Jitihada hizi za
kuimarisha usafiri wa baharini zimeweza kupata mafanikio zaidi kwa kuungwa
mkono na wawekezaji wazalendo ambao wamechukua hatua ya kuleta nchini meli za
kisasa na boti zinazokwenda kwa kasi zinazotoa huduma kwa abiria na mizigo
katika bandari ya Unguja, Pemba, Dar es Salaam, Tanga na bandari nyengine za
ukanda huu wa Afrika Mashariki. Hatua ya
wawekezaji hawa zimerahisisha sana kuwepo kwa huduma za uhakika za usafiri wa
bahari, na vile vile kukuza shughuli za biashara, hasa biashara ya utalii hapa
Zanzibar.
Mheshimiwa
Spika,
Nishati ya umeme ni muhimu katika
kuimarisha ukuaji wa uchumi wa nchi na ustawi wa maendeleo ya wananchi wetu.
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, katika awamu zake mbali mbali imefanya
jitihada kadhaa za kuhakikisha kwamba Zanzibar inakuwa na huduma za nishati za
umeme za uhakika. Katika uongozi wa Awamu ya Saba, niliahidi kuendeleza
jitihada zilizoanzishwa na Awamu za Uongozi wa Serikali zilizotangulia katika
kusambaza na kuwafikishia wananchi huduma hizi popote walipo.
Nnafuraha kueleza kuwa hadi sasa
Serikali imeweza kuufikisha umeme katika shehia zote za Unguja na Pemba. Nishati hii inapatikana katika vijiji 2,882
kati ya vijiji 3,259 sawa na asilimia 88.43 vikiwemo vijiji 354 vilivyopatiwa
umeme katika kipindi hiki. Jumla ya
visiwa vidogo vidogo vitano (5) navyo vimepatiwa umeme ambavyo ni Kisiwa Panza,
Makoongwe, Shamiani (Mwambe), Fundo na Uvinje.
Jitihada za kuufikisha umeme katika kisiwa cha Kokota na Njau huko Pemba
zilipata changamoto na kusababisha kuchelewa kidogo. Hata hivyo, fedha kwa
ajili ya kazi hio zimeshatengwa na utekelezaji wa mpango huo utaendelezwa kama
nilivyoahidi. Nawanasihi wakaazi wa
kisiwa cha Kokota na Njau waendelee kuwa na subira, Mwenyezi Mungu atatujaalia
dhamira yetu hii njema itafanikiwa.
Naupongeza uongozi na wafanyakzi wa Shirika la ZECO pamoja na Wizara kwa
kazi kubwa ya kusambaza umeme hapa Zanzibar.
Kutokana na ongezeko la mahitaji ya
nishati ya umeme yaliyojitokeza pamoja na kupata msaada wa Kampuni ya MCC ya
Marekani kwa kuunganishwa waya wa baharini wa Megawati 100, mwaka 2010,
Serikali imeamua kuwa ipo haja ya kuwa na umeme wa uhakika na tayari ishaanza
kutafuta njia mbadala za kupata vyanzo vipya vya nishati ya umeme. Utafiti uliofanywa kwa kushirikiana na Umoja
wa Ulaya (EU) umeonesha kuwepo kwa uwezekano mkubwa wa Zanzibar kupata nishati
ya umeme kutokana na nishati ya jua. Kwa
hivyo, hivi sasa Serikali inaendelea kulifanyia kazi suala hilo na limefikia
hatua nzuri sana, kwa kushirikiana na Benki ya Dunia pamoja na sekta binafsi,
ili kuongeza upatikanaji wa uhakika wa nishati hii. Tumeambiwa kuwa Benki ya Dunia itatuunga
mkono kwa kuanzia kupata MW 35, lakini wapo wawekezaji walojiandaa kuwekeza zaidi
ya MW 70 na kadhalika.
Mheshimiwa
Spika,
Sekta ya Mafuta na
Gesi Asilia ni eneo jipya la nishati ambalo niliahidi Serikali italishughulikia
katika uongozi wa Serikali ya Awamu ya Saba. Kwa kushirikiana na Serikali ya
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
lilitunga Sheria ya Mafuta Namba 21 ya mwaka 2015 iliyoipa mamlaka Serikali
zetu mbili, kila moja itunge sheria yake ya Mafuta na Gesi Asilia. Kwa mara nyengine
tena, nataka nimpongeze kwa dhati Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kushirikiana nami kwa kuifanya kazi hii
kwa uzalendo mkubwa. Kwa hivyo, sheria ya Mafuta na Gesi Asilia Namba 6 ya
mwaka 2016 ya Zanzibar, ilitungwa hapa hapa Baraza la Wawakilishi na nyinyi ndio
mlioitunga, kwani bila ya nyie haya yasingelifanyika. Kutokana na sheria hio, Mamlaka ya Udhibiti
na Utafutaji wa Mafuta na Gesi Asilia Zanzibar (ZPRA) na Kampuni ya Mafuta na
Gesi Asilia Zanzibar (ZPDC) zilianzishwa rasmi. Lengo la kuanzishwa kwa Taasisi
hizo ni kuleta ufanisi zaidi katika usimamizi na udhibiti wa mafuta na gesi
hapa Zanzibar.
Baada ya kutiliana
saini Mkataba wa Uzalishaji na Mgawano wa Mafuta na Gesi Asilia baina ya ZPDC
na RAK GAS ya Ras Al Khaimah, hapo tarehe 23 Oktoba 2018, utafutaji wa Mafuta
na Gesi Asilia katika kitalu cha Pemba-Zanzibar zinaendelea na zimefikia hatua
kubwa sana. Nampongeza na namshukuru kwa
dhati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Joseph Magufuli
kwa namna tulivyoshirikiana katika kulifanikisha suala hili. Katika hatua hii tuliyoifikia, nawanasihi
wananchi waendelee kuwa na subira kuhusu jambo hili kwani watalaamu wa Kampuni
zetu mbili wanaendelea kushauriana juu ya namna ya kuziarifu Serikali, ili hatimae
wananchi waelezwe matokeo ya utafiti huo uliofanyika. Taarifa zilizopo nzuri. Tungoje kampuni zilizopewa majukumu
zitwambie, ili baadae tuwaeleze wananchi.
Mheshimiwa Spika,
Katika kuhakikisha
kwamba, tatizo la upungufu wa mafuta linapatiwa ufumbuzi wa kudumu, Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba inaendelea na azma ya ujenzi wa bandari ya
Mafuta na Gesi Asilia, Mangapwani, kwa ajili ya shughuli za upakuaji wa mafuta
na gesi. Serikali inakamilisha mradi
ujenzi wa nyumba 31, uliofikia asilimia 72, ambazo zinatarajiwa kupewa wananchi
waliohama katika eneo litakalojengwa bandari hio.
Mheshimiwa Spika,
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,
Awamu ya Saba, ilitambua wazi kuwa kuimarisha huduma za jamii ni jukumu lake la
msingi na hatua muhimu ya kuendeleza shabaha ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar
ya tarehe 12 Januari, 1964. Katika
kutekeleza azma hio, Serikali imechukua jitihada mbali mbali katika kuimarisha
upatikanaji wa huduma bora za Elimu, Afya na Maji Safi na Salama katika maeneo
yote ya Unguja na Pemba, mjini na mashamba.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa upande wa Sekta ya Elimu, Serikali
imeendeleza mafanikio ya elimu yaliyopatikana katika Awamu zote za Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar zilizotangulia.
Kadhalika, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, imeimarisha ubora wa elimu
inayotolewa katika ngazi zote kuanzia Maandalizi, Msingi, Sekondari, Elimu ya
Juu pamoja na Elimu ya Mafunzo ya Amali na Elimu Mbadala. Vile vile, Serikali imefanikiwa kuimarisha
masomo ya Sayansi hasa kwa watoto wa kike, mafunzo ya elimu maalum kwa watu
wenye ulemavu, kuimarisha maslahi ya walimu pamoja na kuyaimarisha mazingira ya
kusomea yakiwemo majengo na vifaa vya maabara na vitabu vya kiada na ziada.
Mheshimiwa
Spika,
Ni jambo la kufurahisha, kuona
mafanikio makubwa ambayo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba,
imeweza kuyapata katika utekelezaji wa malengo iliyojiwekea kwa upande wa Sekta
ya Elimu, ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu ya mwaka
2010-2015, Ilani ya mwaka 2015-2020, Dira ya Maendeleo ya 2020 na Mipango
mingine ya Kitaifa.
Wakati tukiwa katika mwaka wa kumi wa
uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba, tunafarajika kwa
mafanikio makubwa ya kuandikisha watoto wote waliofikia umri wa kusoma. Serikali imeondoa michango ya wazazi katika
elimu ya msingi katika mwaka 2015/2016 na kuondoa gharama za mitihani yote ya
skuli za Sekondari kuanzia mwaka fedha 2016/2017, ili kuwawezesha watoto wote
wapate elimu bure kwa shabaha ile ile ya tamko la Mwasisi wa Mapinduzi ya
Zanzibar Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, alilolitangaza tarehe 23 Septemba,
1964. Katika kipindi hiki cha miaka kumi, tumeweza kuongeza idadi ya wanafunzi
wapya wanaoandikishwa katika ngazi ya elimu ya lazima; Maandalizi, Msingi na
Sekondari kutoka jumla ya wanafunzi 317,278 mwaka 2010 hadi kufikia wanafunzi
529,688 mwaka 2020.
Mheshimiwa
Spika,
Ongezeko la idadi ya skuli, taasisi
nyengine za elimu na wanafunzi katika ngazi zote ni miongoni mwa mafanikio
yaliyofikiwa katika Sekta ya Elimu.
Idadi ya vituo vya “Tucheze Tujifunze” - (TUTU); vimeongezwa kutoka
vituo 178 kwa mwaka 2010 hadi kufikia vituo 366 mwaka 2020. Ongezeko hili ni sawa na asilimia 51. Vituo hivi vipo kwenye Wilaya zote za Unguja
na Pemba.
Hadi Disemba 2019, idadi ya skuli za
Maandalizi imefikia 382 zenye wanafunzi 85,974, ikilinganishwa na skuli 238,
zilizokuwa na jumla ya wanafunzi 29,732 katika mwaka 2010. Ongezeko la skuli ni asilimia 62.3 na
ongezeko la wanafunzi ni asilimia 6.
Mheshimiwa
Spika,
Skuli za msingi zimeongezeka na
zimefikia skuli 381 zenye wanafunzi 290,510 mwaka 2019, kutoka skuli 299,
zilizokuwa na wanafunzi 226,812 katika mwaka 2010. Ongezeko la skuli ni asilimia 27.4 na
ongezeko la wanafunzi ni asilimia 28.
Kwa upande skuli za sekondari, hivi
sasa zipo skuli 287 zenye wanafunzi 135,519, ikilinganishwa na skuli 105,
zilizokuwa na wanafunzi 80,008, katika mwaka 2010. Ongezeko la skuli ni asilimia 73.3 na ongezeko
la wanafunzi ni asilimia 69.4. Majengo
kadhaa ya ghorofa ya skuli za Msingi na Sekondari yamejengwa na Serikali katika
Wilaya zote za Unguja na Pemba. Vile
vile, katika kipindi hiki cha miaka kumi, zipo skuli za sekondari za ghorofa,
zilizojengwa na wafanyabiashara wazalendo.
Mheshimiwa
Spika,
Vile vile, Serikali imejenga vituo 22
vya ubunifu wa kisayansi (Hubs), (13 Unguja na 9 Pemba) ambavyo kwa jina la
kitaalamu vinaitwa “Hubs”. Vituo
hivi vyote vina maabara za sayansi, vyumba vya kompyuta, maabara za lugha, maktaba na vyumba vya kujisomea wanafunzi.
Kadhalika, katika mradi huu, zimejengwa skuli mbili za sekondari katika maeneo
ya Mwanakwerekwe kwa Unguja na Wingwi kwa Pemba.
Mheshimiwa
Spika,
Sambamba na hatua hizo, Serikali
imezipatia skuli vifaa vya kusomea vikiwemo vitabu vya masomo mbali mbali,vifaa
vya maabara za masomo ya sayansi, vitabu vya maktaba, kuongezeka kwa walimu,
mambo ambayo yameongeza ubora wa elimu kwa vigezo mbali mbali. Katika kulishughulikia tatizo la upungufu wa
madawati, katika skuli za Msingi na Sekondari, Serikali imenunua jumla ya seti
za viti na meza 44,620 kwa ajili ya skuli za Sekondari Unguja na Pemba na kwa
ajili ya wanafunzi 42,195 wa skuli za msingi ambavyo tayari vimewasili nchini
na vimeanza kutumika na vyengine vinatarajiwa kuwasili wakati wowote kuanzia
sasa kutoka nchini China. Mambo yetu
mazuri sana.
Mheshimiwa
Spika,
Katika kipindi hiki cha miaka kumi,
Serikali imejenga majengo mapya kwa ajili ya Mafunzo ya Amali, huko Makunduchi
Mkoa wa Kusini Unguja na Daya Mtambwe, katika Mkoa wa Kaskazini Pemba. Kwa kujengwa vituo hivi viwili mafunzo ya
amali sasa yatatolewa katika Mikoa yote mitano ya Zanzibar. Vile vile, katika kipindi hiki Taasisi ya Sayansi na
Teknolojia ya Karume, iliyopo Mbweni, imeimarishwa na imeanza kutoa Mafunzo ya
Shahada ya Kwanza, katika fani ya Urubani na Uhandisi wa Ndege, ambapo vijana
53 wamejiunga na masomo hayo na hapo baadae Taasisi hio, itatoa mafunzo ya
Shahada ya Kwanza ya Ujenzi, Usafirishaji na Umeme.
Mheshimiwa
Spika,
Mafunzo ya ualimu yanaendelea kutolewa
katika Chuo cha Kiislamu Mazizini, Chuo cha Kiislamu Micheweni pamoja na vyuo
vikuu vitatu vilivyopo Zanzibar; Chuo
Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), Chuo Kikuu cha Zanzibar (ZU) na Chuo cha
Al-Sumeit. Katika mwaka 2018/19 vyuo hivi vilikuwa na jumla ya wanafunzi 7,090
wanaochukua masomo ya fani mbali mbali kuanzia ngazi ya Cheti, Stashahada,
Shahada ya Kwanza, Shahada ya Uzamili na Shahada ya Uzamivu.
Katika kipindi cha Awamu ya Saba ya
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ilikiunganisha Chuo cha Afya, Chuo cha
Kilimo, Chuo cha Utalii, Chuo cha Fedha na Chuo cha Uandishi wa Habari na Chuo
Kikuu cha Taifa cha Zanzibar, SUZA.
Katika kuunganishwa huku vyuo hivi vimepewa hadhi ya kuwa skuli za SUZA
(Schools) na vinatoa shahada, stashahada na vyeti mbali mbali. Kwa mara ya kwanza wanafunzi 73 wamemaliza
masomo ya Udaktari (Doctor of Medicine) katika mikupuo miwili, katika mwaka
2017 na 2018. Kadhalika, mafunzo ya
Shahada ya Uzamivu katika lugha ya Kiswahili yanaendelea kutolewa ambapo
wanafunzi watano walifaulu katika mwaka 2017/2018 na mwanafunzi mmoja katika
mwaka 2018/2019. Vile vile, mafunzo ya
Shahada ya Uzamili yalianzishwa katika masomo mbali mbali. Idara za SUZA zimeongezeka kutoka 1 mwaka
2010 hadi 8 mwaka 2020.
Mheshimiwa
Spika,
Kama ilivyoagizwa katika Ilani ya CCM
ya Uchaguzi Mkuu wa 2015, kifungu 100(ii), ambacho nakinukuu kama ifuatavyo: “Kuongeza nafasi za masomo katika elimu ya
juu na kuimarisha mfuko wa Bodi ya Mikopo, ili kuongeza idadi ya wanafunzi watakaonufaika…..”.
Serikali imeunda Bodi ya Mikopo ya
Elimu ya Juu Zanzibar iliyoanzishwa kwa Sheria Namba 3 ya mwaka 2011 kwa lengo
la kuwasaidia vijana wetu kuendelea na masomo ya juu katika fani mbali mbali,
ili tupate wataalamu wetu wenyewe imetekeleza vyema majukumu yake. Bodi
hii imetumia jumla ya TZS Bilioni 60.2,
kwa ajili ya kuwadhamini wanafunzi 6,087
wa elimu ya juu katika vyuo vikuu
mbali mbali vya ndani na nje ya nchi. Sambamba na hili, Uongozi wa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba, umeanzisha utaratibu wa kuwalipia gharama
zote za masomo wanafunzi wanaofaulu daraja la kwanza katika mitihani ya kidato
cha sita. Utaratibu huu ulianza mwaka 2016 kwa wanafunzi 10 na kufikia
wanafunzi 60 katika mwaka 2019.
Mheshimiwa
Spika,
Wahenga wanasema, “Mti hawendi ila kwa
nyenzo”, na mafanikio yote yaliyopatikana katika Sekta ya Elimu, nyenzo tafauti
zimetumika zikiwemo nguvu kazi, vifaa mbali mbali vyakufundishia na kujifunzia,
mafunzo ya kuwajengea uwezo walimu na majengo mazuri ya kusomea. Mafanikio yote
yaliyopatikana yametokana na kuongezeka bajeti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya
Amali imeongezwa mara 3.8; kutoka TZS Bilioni 47.093 mwaka 2010/2011 na kufikia
TZS Bilioni 178.917 mwaka 2019/2020. Tumefanya
kazi kubwa sana.
Ndugu Wananchi,
Kadhalika,
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatekeleza kwa mafanikio makubwa Sera yake
ya kutoa matibabu bure kama ilivyoanzishwa mara tu baada ya Mapinduzi ya tarehe
12 Januari, 1964.
Kutokana na
kuongezeka kwa bajeti ya Wizara ya Afya kwa mara 9.6 kutoka TZS Bilioni 10.81
mwaka 2010/2011 hadi TZS Bilioni 104.24 mwaka 2019/2020, huduma za afya
zimeimarika sana na zinaendelea kutolewa bure. Ongezeko la fedha za bajeti
zimesaidia sana katika kuziimarisha
huduma za tiba na kinga katika hospital kumi, vituo vya afya na zahanati
zote za Serikali 158 kwa Unguja na Pemba.
Serikali imetekeleza Ilani ya CCM ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 kifungu
102(b) kwa kuziimarisha huduma za Hospitali ya Mnazi mmoja hadi kufikia hadhi
ya hospitali ya rufaa. Nanukuu kifungu hicho kama ifuatavyo: “Kuendelea kuifanya hospitali ya Mnazi Mmoja
kuwa ya rufaa kwa kuongeza huduma za matibabu ya saratani na kuimarisha huduma
za uchunguzi na ununuzi wa vifaa kama Magnetic Resonance Imaging (MRI)
……”. Kutokana na hatua hii, hivi
sasa hospital hio inatambuliwa rasmi kuwa ni hospitali ya kufundisha madaktari,
miongoni mwa hospitali za Jumuiya za Nchi za Afrika ya Mashariki. Hospitali ya
Abdalla Mzee ya Mkoani, imepandishwa daraja na kuwa hospitali ya Mkoa baada ya
kufanyiwa ukarabati mkubwa na kupatiwa vifaa, zana na nyezo mpya mbali mbali za
kisasa. Hospitali ya “Cottage” ya
Kivunge na Makunduchi zimepandiswa daraja na kuwa hospitali za Wilaya Januari,
2019 baada ya huduma zake kuimarishwa.
Jitihada za
Serikali za kusomesha madaktari, wakiwemo madaktari bingwa, zimewezesha
kuongeza idadi ya madaktari na watumishi wengine wa afya. Jitihada hizi zimeimarisha uwiano wa
madaktari na watu wanaohudumiwa. Hivi sasa daktari mmoja anawahudumia watu
6,276 (1:6,276) kutoka daktari mmoja kuwahudumia watu 31,838 (1:31,838), mwaka
2010. Kwa hivyo, kutokana na kuongezeka
kwa idadi ya madaktari na wataalamu wengine mbali mbali wa fani za afya, upatikanaji
wa vifaa vya kisasa vya uchunguzi wa maradhi na nyenzo mbali mbali za kufanyia
kazi, pamoja na kuimarishwa kwa maeneo ya kufanyia kazi kumepelekea huduma za
tiba na kinga zizidi kuimarika.
Jitihada za
Serikali za kupambana na Malaria zinaendelezwa na kasi ya kuenea kwake bado ipo
chini ya asilimia moja (0.4%), ingawa baadhi ya maeneo machache ya Mjini
yamebainika kuongezeka wagonjwa wa Malaria. Juhudi zinaendelezwa za utoaji
elimu kwa wananchi, ugawaji wa vyandarua vyenye dawa ya muda mrefu na upigaji
wa dawa za ndani ya nyumba na maeneo yenye mazalia ya mbu.
Ndugu Wananchi,
Kadhalika,
maambukizo ya UKIMWI yameendelea kushuka na
hivi sasa yamefikia kiwango cha asilimia 0.4 kutoka asilimia 0.6 mwaka
2010. Kuhusu vifo vinavyotokana na uzazi vimepungua na vimefikia 155 kwa kila
vizazi hai 100,000, ikilinganishwa na vifo 288 kwa kila vizazi hai 100,000
katika mwaka 2010. Jitihada za
kuwaelimisha wajawazito wajifungulie hospitali badala ya majumbani, zimesaidia
sana, ambapo mwaka 2010 wajawazito 51,912 walijifungulia majumbani ikilinganishwa
na 37,803 mwaka 2019.
Pamoja na
mafanikio niliyoyaelezea katika hotuba yangu hii, kwa kudhibitiwa kwa baadhi ya
maradhi, lakini zipo changamoto zilizobainika katika hospitali zetu za Unguja
na Pemba; ambazo ni kuongezeka kwa maradhi yasiyoambukiza kama vile maradhi ya
sukari, matatizo mbali mbali ya maradhi ya moyo, maradhi ya figo, saratani ya
shingo ya kizazi na saratani nyengine.
Matarajio yangu ni kwamba wataalamu wa Taasisi ya Utafiti ya Afya na
wengine waliopo katika Idara mbali mbali za hospitali zetu na kwa kuendelea
kushirikiana na wataalamu wengine wa Kimataifa; watafanya kazi zao za utafiti
kwa bidii, ili Serikali iweze kuchukua hatua za kukabiliana na maradhi hayo.
Mheshimiwa
Spika,
Sekta binafsi katika Sekta ya Afya
imesaidia sana kupunguza msongamano wa wagonjwa katika hospitali za Serikali.
Sekta hio inazo hospitali 3 na vituo vya afya 63 vya binafsi vilivyosajiliwa
kisheria. Natoa pongezi na shukurani kwa
uongozi wa hospitali hizo kwa kushirikiana na Serikali pamoja na wananchi
katika kuimarisha huduma za afya nchini.
Mheshimiwa
Spika,
Serikali imeendelea kuziimarisha huduma
za maji safi na salama katika Mikoa yote ya Unguja na Pemba kwa kuzingatia
maelekezo ya Ilani katika vipindi vyote viwili. Utekelezaji wa Mradi wa maji wa
Mkoa Mjini Magharibi, kwa mkopo wa Dola za Kimarekani Milioni 21.246 kutoka
Benki ya Maendeleo ya Afrika, umekamilika na umezinduliwa tarehe 6 Januari,
2020. Wananchi wanaoishi katika Shehia 11 za Mji Mkongwe na Shehia 16 za maeneo
mingine wananufaika na Mradi huu.
Kadhalika, mradi uliotekelezwa na
Kampuni ya “First Highway Engineering of China” uliokamilika mwezi Aprili, 2018
umewanufaisha wananchi 11,850 katika shehia 21 za Mkoa wa Kaskazini Unguja na
Kusini Unguja. Vile vile, Serikali ya Ras
Al Khaimah ilisaidia kuchimba visima 150, kati ya visima hivyo, visima
59 tayari vinafanya kazi na maji yanapatikana.
Katika visima hivyo, vinavyotoa maji, visima 32 vipo Unguja na 27 vipo
Pemba. Hivi sasa, kijiji cha Mtende na
Uroa vinapata maji asilimia mia moja na kijiji cha Michamvi kinakisiwa kinapata
maji asilimia 90. Kazi ya ukamilishaji
wa miundombinu inaendelea. Wastani wa
upatikanaji wa maji katika Mikoa mitano ya Zanzibar, hivi sasa imefikia wastani
wa asilimia 80 katika kipindi hiki cha miaka kumi iliyopita. Hivi sasa,
Serikali inaendelea na matayarisho ya kuanza mradi mwengine mkubwa kwa mkopo
nafuu wa Dola za Kimarekani Milioni 92, uliotolewa na Serikali ya India. Kadhalika, Serikali ya Japan imetoa msaada wa
Dola za Kimarekani Milioni 100 kwa ajili ya kuendeleza huduma za maji.
Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na
Nishati imeanzisha Chuo cha Kuwahudumia Wafanyakazi watakaoshughulikia huduma
za maji. Jumla ya wanafunzi 80
wamechaguliwa kuanza mafunzo hayo.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa lengo la kuziimarisha huduma za
mawasiliano, Serikali ilianzisha mradi wa serikali mtandao (e-government), ambao ulizinduliwa rasmi
mwezi Januari, mwaka 2013. Hadi hivi sasa jumla ya majengo 130 ya Serikali
yameunganishwa katika serikali mtandao na yananufaika kupata huduma za mtandao
bila ya malipo kipitia mradi huu. Huduma za mradi huu sasa zimeendelezwa kwenye
“e-Heath” na “e-Tax” kwa lengo la
kuongeza ufanisi na utendaji katika utumishi wa umma. Jumla ya hoteli 200 za
madaraja mbali mbali zimeshaunganishwa katika mfumo huo.
Mheshimiwa Spika,
Serikali ilianzisha Shirika ka
Utangazaji la Zanzibar (ZBC), lenye kushughulikia kwa pamoja matangazo ya redio
na televisheni ya Zanzibar. Juhudi kubwa
zimefanywa katika kuubadilisha mfumo wa urushaji wa matangazo ya redio na
televisheni kutoka kwenye analojia na kwenda dijitali, ambapo mitambo ya kisasa
ya TV na Radio ilinunuliwa na kufungwa na tayari inatumika. Kampuni ya Z-MUX imeanzishwa kwa ajili ya
kusimamia utekelezaji wa ZBC TV.
Hivi sasa Shirika
la ZBC linawahudumia wananchi kwa
kurusha matangazo saa 24, na linaongeza programu mpya za vipindi vinavyohusu
masuala muhimu ya kiuchumi na kijamii. Hatua nyengine ya mafanikio ni kuanza
kuonekana kwa ZBC TV kupitia king’amuzi cha DSTV katika chaneli ya 291, jambo
ambalo limeongeza idadi ya watazamaji wa televisheni ya ZBC katika nchi mbali
mbali za Afrika. Hongereni ZBC kwa
kuelimisha “Corona” nimeiona kali yenu!.
Kwa upande wa
Shirika la Magazeti la Zanzibar, Shirika limefanikiwa kulichapisha Gazeti la
Serikali la Zanzibar Leo, hapa hapa Zanzibar katika Wakala wa Serikali wa
Uchapaji. Gazeti hilo sasa linapatikana na kusambazwa kwa urahisi, ikiwemo
kupitia mitandaoni. Kuanzia mwezi Novemba 2019, Shirika limeanza kuchapisha
gazeti la Kiingereza liitwalo “Zanzibar Mail”, ili kuwawezesha watumiaji wa
lugha ya Kiingereza, wakiwemo watu mbali mbali pamoja na watalii, wanaokuja
Zanzibar, kufuatilia taarifa muhimu za maendeleo ya Zanzibar. Kadhalika, Wakala wa Serikali wa Uchapaji
Zanzibar umeimarishwa kwa kupatiwa mitambo na vifaa vya kisasa ya kuchapisha
nyaraka mbali mbali za Serikali zikiwemo vitabu vya hotuba, vitabu vya risiti
na kuchapisha gazeti la Zanzibar Leo.
Taasisi hii imesaidia sana kuwezesha gazeti la Zanzibar Leo kuchapishwa
hapa Zanzibar na kupatikana kwa urahisi.
Mheshimiwa Spika,
Kuhusu sekta ya utamaduni na sanaa,
studio mpya ya kisasa ilimezinduliwa Rahaleo mwaka 2016, iliyotokana na studio
ya zamani kwa ajili ya wasanii wa filamu na muziki ambayo inatumika vizuri.
Vile vile, kuanzia mwaka 2010 hadi sasa, bado wasanii wanaendelea kulipwa
mirabaha ambapo jumla ya TZS Milioni 402.80 zimekusanywa na kugawiwa kwa
wasanii na wabunifu. Kadhalika,Tamasha
la Filamu la Kimataifa (ZIFF), Sauti za Busara, Tamasha la Utamaduni la Mzanzibari
na mengine ya asili yamefanyika.
Kwa lengo la kuienzi na kuiendeleza
Lugha ya Kiswahili, jumla ya makongamano
matatu ya kimataifa ya Kiswahili yaliyowajumuisha washiriki 419 yamefanywa.
Makongamano hayo, yameleta hamasa katika
kuiendeleza lugha ya Kiswahili. Vile vile, Kikundi cha Taifa cha Taarab Asilia
kimeimarishwa kwa kupatiwa ofisi na vyombo vipya.
Mheshimiwa Spika,
Tumezindua rasmi uwanja wa michezo wa
Mao-Zedong tarehe 3 Januari, 2018 baada ya kufanyiwa matengenezo na Serikali ya
Jamhuri ya Watu wa China, na hivi sasa unatumika kwa michezo mbali mbali.
Kadhalika, mpango wa Serikali wa kujenga viwanja vya michezo vya wilaya hivi
sasa unaendelea vizuri, katika Wilaya
tano. Vile vile, Serikali imeweka nyasi
bandia na mpira wa kukimbilia katika uwanja wa
Amaan Unguja na Gombani Pemba.
Timu yetu ya mpira wa miguu ya Zanzibar
Heroes iliandaliwa vizuri na ilifanikiwa
kupata ushindi wa pili katika mashindano ya Chalenji ya Mpira wa Miguu mwaka
2017. Timu ya michezo ya watu wenye
ulemavu imefanya vizuri kwenye mashindano ya kimataifa ya michezo mbali mbali.
Nazipongeza timu zetu zote hizo.
Kadhalika, Serikali imeendelea
kuwahamasisha wananchi wafanye mazoezi ya viungo hasa baada ya kuitangaza
tarehe mosi ya Januari ya kila mwaka, kuwa siku ya mazoezi hayo kwa Unguja na
Pemba. Jumla ya mabonanza manane
yameshafanyika. Idadi ya vikundi vya mazoezi vinavyoshiriki Bonanza la Mazoezi
hapa Zanzibar vimeongezeka kutoka vilabu 12 mwaka 2010/2011 kutoka Unguja tu na
kufikia vilabu 82 kutoka Unguja, Pemba na Tanzania bara katika mwaka 2019.
Mheshimiwa
Spika,
Katika kipindi hiki, ushirikishwaji wa
wanawake katika ngazi mbali mbali za uongozi Serikalini pamoja na vyombo vya
utungaji wa sheria, sera na utoaji wa maamuzi umeimarishwa. Kwa mfano, katika
chombo hiki cha kutunga sheria, idadi ya wajumbe wanawake katika Baraza la Nane
walifikia 26, na katika Baraza hili la Tisa, idadi yao ni 32 ikilinganishwa na
wajumbe 20 waliokuwemo katika Baraza la Saba, mwaka 2005-2010. Kama lilivyokuwa Baraz la nane na la tisa
vijana wameliongezea ufanisi na haiba.
Vile vile, Serikali katika kipindi hiki
imeanzisha skuli za sekondari maalumu za watato wa kike na imevihamasisha
vikundi vya ujasiriamali kwa kuvipatia mafunzo pamoja na mikopo yenye masharti
nafuu. Kadhalika, imeanzisha kituo cha
kuwafundisha wanawake kutengeneza vifaa vinavyotumia umeme wa nishati ya jua
kwenye Chuo cha “Barefoot” Kibokwa, Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Mheshimiwa
Spika,
Serikali inapiga vita vitendo vya
udhalilishaji vya wanawake na watoto na inapambana dhidi ya vitendo hivyo kwa
kushirikiana na taasisi mbali mbali na wananchi. Kampeni ya Miaka Mitano wa Kupambana na
Vitendo hivyo ulizinduliwa tarehe 6 Disemba, 2014 na ule wa kupambana na
vitendo vya ukatili dhidi ya watoto na Mpango ulizinduliwa Agosti, 2017. Jitihada hizo za Serikali zimesaidia sana
dhidi ya vitendo hivyo kwa wanawake na watoto.
Jumla ya matukio 1,091 ya udhalilishaji
yaliripotiwa katika vituo vya Polisi Unguja na Pemba kwa mwaka 2017/2018
ikilinganishwa na matukio 2,449 yaliyoripotiwa mwaka 2016/2017. Vitendo hivyo vimepungua kwa zaidi ya nusu ya
idadi ya matukio yote. Kwa mwaka 2019, matukio
ya vitendo vya ukatili na udhalilishaji vilivyoripotiwa katika vituo vya polisi
vya Mikoa yote yalikuwa 941, sawa
na upungufu wa asilimia 61.6. Kampeni
iliyofanywa pamoja na programu hizi zimesaidia sana mapambano hayo, lakini
jitihada zaidi bado zinahitajika kwani vitendo hivi vinaendelea kuripotiwa na
vyombo vya habari kila baada ya muda.
Mheshimiwa
Spika,
Kuhusu maendeleo na ustawi wa watoto,
Sheria mpya Namba 6 ya mwaka 2011, inayozingatia utekelezaji wa haki zote za
msingi za watoto, ilianzishwa ambayo imeipatia sifa Zanzibar duniani kote. Kwa
dhamira ya kuwatendea haki watoto, Serikali ilianzisha mahakama ya watoto mwaka
2013. Vile vile, Serikali imevifanyia
matengenezo makubwa viwanja maalumu vya kufurahishia watoto vya Kariakoo
Unguja na Tibirinzi Pemba.
Mheshimiwa
Spika,
Bado lipo tatizo la ajira kwa vijana,
lakini Serikali inachukua hatua. Kwanza
imeandaa mafunzo ya Amali katika vituo vya Serikali, katika vituo vya amali na
katika Kituo cha Ukuzaji Wajasiriamali Mbweni.
Pili, wamepatiwa mikopo, ili waweze kujiajiri wenyewe kwenye shughuli
zao. Tatu, wamewezeshwa kwenye kilimo kama vile pilipili hoho, ufugaji na
ushoni. Vijana 39,499 wamepatiwa mikopo
wenye thamani ya TZS Bilioni 4.32 kwa jili ya kuwaendeleza katika kilimo,
ufugaji na ushoni.
Mheshimiwa
Spika,
Kuwatunza wazee katika maisha yao ya
kila siku kwa kuwapatia mahala bora pa kuishi, huduma za msingi za kila siku
katika maisha yao, Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar, Awamu ya Saba, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita ilikuwa
inawalipa wazee wote Unguja na Pemba, waliofikia umri wa miaka 70 na kuendelea
posho la TZS 20,000 kwa kila mwezi.
Uamuzi wa Serikali, sasa umetungiwa Sheria Namba 2 ya mwaka 2020, ambapo
utaratibu wa kisheria umewekwa kuhusu masuala ya wazee. Hivi sasa, jumla ya wazee 28,022 wamesajiliwa
katika programu hii ya Pencheni Jamii.
Mheshimiwa
Spika,
Katika kipindi hiki, Serikali iliamua
kuanzisha Idara ya Watu wenye Ulemavu chini ya Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais
wa Zanzibar. Sambamba na hatua hio, watu
wenye ulemavu wameshirikishwa katika vyombo vya uamuzi, na kuhakikisha kuwa
wanapata huduma zote muhimu zikiwemo elimu, afya, michezo, ajira na masuala
mengine ya maendeleo na ustawi wao. Vile
vile, Serikali katika mwaka 2012, ilianzisha Mfuko wa Watu wenye Ulemavu, kwa
kuanzia na jumla ya TZS Milioni 167 kwa lengo la kuwawezesha katika shughuli
zao mbali mbali.
Mheshimiwa Spika,
Umuhimu wa utawala bora umeelezwa kwa
ufasaha na kwa ufupi mno na Professor na Mwanasaikolojia,Bwana Amit Abraham
pale aliposema, “There should be only one political ideology and that is good
governance,” kwa maana ya kuwa,
inapaswa pawe na itikadi moja tu ya kisiasa, ambayo ni utawala bora. Katika kuhakikisha kuwepo kwa Utawala Bora, Serikali
ilianzisha Taasisi mbali mbali za kuusimamia mfumo huo.
Katika kupambana na vitendo vya rushwa na
ubadhirifu wa mali ya umma, Serikali ya
Mapinduzi ya Awamu ya Saba, imeanzisha Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu wa
Uchumi Zanzibar (ZAECA) chini ya Sheria
Nambari 1 ya mwaka 2012. Jumla ya tuhuma 950 za vitendo vya rushwa na
ubadhirifu wa mali ya umma zimefikishwa na Taasisi hii tangu ilipoanzishwa.
Tuhuma 751 kati ya hizo, bado zinachunguzwa na nyengine zimeshatolewa maamuzi.
Vile vile, Mamlaka imefanikiwa kuokoa na kurejesha Serikalini fedha na mali
zenye thamani ya TZS milioni 411.90 tangu kuanzishwa kwake.
Kadhalika, Tume ya Maadili ya Viongozi
wa Umma ilianzishwa kwa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma Nam 8 ya 2015.
Waheshimiwa Wajumbe, suala la maadili ni muhimu kwa sisi viongozi tuzingatie
maadili na kuwa wakweli, ili tujenge imani kwa wananchi tunaowaongoza na
tujiamini sisi wenyewe tunapoikabili jamii kwa masuala mbali mbali.
Tunapokuwa na tabia zisizopendekeza
kwenye jamii, huwa tunakosa kujiamini na mara nyingi huishi katika maisha ya
wasi wasi. Kipo kisa cha bwana mmoja
hakuwa na maadili bora huku akifuga kasuku.
Bwana huyu, alikuwa na tabia
zisizopendeza kwa jamii huku akifuga kasuku.
Siku moja alipofika nyumbani alimkuta kasuku wake hayupo, bila ya kujua
kama katoroka au kaibiwa. Kwa hivyo, kwa
kuwa yule bwana hakuwa na tabia nzuri, alitoka mbio kwenda kuripoti tukio hilo
moja katika kitengo cha usalama, ingawa alipaswa kuanza kuripoti tukio hilo
katika kituo cha polisi cha kawaida.
Kufika kituoni akaanza kusema huku anatetemeka. “My talking parrot has disappeared” . Kwa maana ya kwamba, kasuku
wangu ambae anazungumza ametoweka.
Askari wa kitengo cha usalama
wakashangaa na baadae wakamuuliza na kumueleza: “Why have you come here? Go to the regular police”. Kwa nini umekimbilia huku, nenda karipoti
kituo cha polisi cha kawaida!.
Yule jamaa, kutokana na wasi wasi
aliokuwa nao kutokana na tabia na vitendo visivyopendeza alivyokuwa akivifanya
kisiri siri, akaanza kujishtaki na kujitetea kabla hajaulizwa lolote kuhusu
tabia zake na mambo aliyokuwa akiyafanya kwa kusema; “I will, I’m just here to you that I disagree with whatever that parrot
is going to say”. Kwa maana kwamba,
nitakwenda, lakini nimeona kwanza nije hapa, kitengo cha usalama, kukwambieni
kwamba mimi sikubaliana na hata jambo moja ambalo kasuku wangu atakwambieni au
kusema.
Mkasa huu unatufundisha kwamba
unapokuwa na tabia zisizo za kupendeza katika jamii, unakosa kujiamini, na
unakuwa unaishi maisha ya wasi wasi kwa kila jambo unalohisi linaweza kuifanya
jamii kujuwa tabia na mwenendo wako. Mtu
kama huyu akiwa kiongozi ni hatari kwa jamii na watu anaowaongoza. Viongozi wenzangu lazima tuwe na tabia njema
na tuendelee kushikamana na maadili ya kazi na katika jamii tunazoishi.
Taasisi hizi ni muhimu katika
kuimarisha maadili ya viongozi na kuendeleza mapambano dhidi ya rushwa na
ubadhirifu wa mali ya umma. Sote tunatekeleza
vizuri, matakwa ya sheria ya maadili ya Viongozi wa Umma. Tuendelee kutimiza wajibu wetu na tujipambe
na sifa za uongozi bora unaofuata maadili.
Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP)
imeanzishwa kwa Sheria Namba 2 ya mwaka 2010. Serikali imeimarisha mfumo wa
haki jinai kwa kuiwezesha ofisi hio kusimamia utaratibu wa upelelezi na
utaratibu maalum wa uendeshaji wa kesi za udhalilishaji pamoja na dawa za
kulevya. Hali hii imepelekea kupunguza kwa kiasi kikubwa mrundikano wa kesi
mahkamani. Ofisi hii, inasimamia kituo
cha Mafunzo ya Sheria na Utafiti ambapo jumla ya washiriki 513 wamehitimu
katika kituo hicho. Natoa pongezi kwa Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza la
Wawakilishi kwa kupitisha Sheria zenye kuimarisha Utawala bora.
Kadhalika, Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi
Mkuu wa Hesabu za Serikali, katika kipindi hiki cha miaka kumi imeimarishwa na
kujengewa mazingira ya kuiwezesha kufanya kazi zake kwa uhuru zaidi. Ripoti za uchunguzi na ukaguzi wa hesabu za
Serikali zinawasilishwa katika Baraza la Wawakilishi kwa wakati kwa mujibu wa
ibara ya 112(5) ya Katiba ya Zanzibar ya 1984.
Kadhalika, wafanyakazi wa Ofisi hio wameendelezwa kwa kupatiwa mafunzo
ya kazi zao ikiwemo mafunzo ya ukaguzi yakinifu na ukaguzi wa kiuchunguzi
(forensic audit).
Kwa kipindi kirefu, Ofisi ya
Mwanasheria Mkuu ilikuwa ikifanya kazi zake kwa kuzingatia masharti ya Katiba
na yaliyomo katika sheria mbali mbali.
Mnamo mwaka 2013, Serikali ilianzisha rasmi Ofisi ya Mwanasheria Mkuu
kisheria, kwa Sheria Namba 6 ya mwaka 2013.
Ofisi hii imetekeleza vyema
majukumu yake ikiwemo kuzisimamia kesi za Serikali, kuandaa Miswada ya Sheria
na kutoa ushauri wa kisheria kwa Wizara na Taasisi mbali mbali za Serikali.
Mheshimiwa Spika,
Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba, ilianzisha Mamlaka ya Serikali za Mitaa
kwa Sheria Namba 7 ya 2014 na Tawala za Mikoa kwa Sheria Namba 8 ya 2014. Kufuatia kutungwa sheria mbili hizo, shughuli
zote zinazohusiana na elimu ya msingi, afya ya msingi (huduma zote za afya
katika vituo na wafanyakazi wake) na shughuli zote za kilimo za ugani
zimehamishiwa katika Halmashauri za Wilaya ya Unguja na Pemba.
Baada ya
kugatuliwa, Wizara hizi tatu, masuala ya
Uongozi, Utawala na Matumizi yamehamishiwa sasa katika Ofisi ya Rais
Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ. Kuhusu Idara Maalum za SMZ, katika kipindi
hiki, Idara hii imeimarishwa ambapo maslahi ya Makamanda na Wapiganaji wote
yameimarishwa, baadhi ya majengo ya makaazi yao yamejengwa upya na mengine
yamekarabatiwa kwenye Idara Maalum zake zote (KMKM), JKU, Valantia, Zimamoto na
Jeshi la Uokozi pamoja na Chuo cha Mafunzo.
Katika kipindi
hiki cha miaka kumi, Serikali imeanzisha mradi wa mji salama, unaosimamiwa na
Idara Maalum za SMZ ambao ulizinduliwa tarehe 3 Oktoba, 2018. Awamu hii ilihusisha ufungaji wa camera za
uangalizi (CCTV) katika maeneo mbali mbali ya mji wa Unguja. Sehemu ya pili ya mradi huo, ulihusisha
uokozi na uzamiaji wakati wa majanga ya baharini na ulizinduliwa rasmi tarehe 2
Januari, 2019. Miradi yote miwili hivi
sasa, inaendelea vizuri sana. Na kwa
upande wa Pemba, ujenzi wa mradi wa CCTV umeanza kutekelezwa hivi karibuni
katika mji wa Chake Chake.
Ili kuleta ufanisi
wa kuundeleza mji wa Zanzibar, jiji la Zanzibar (Zanzibar City) limeanzishwa
rasmi na umeandaliwa Manispaa zake tatu; ya Mjini, ya Magharibi “A” na
Magharibi “B”. Manispaa hizi na zile za
Pemba, zote zina uongozi wake kamili.
Mheshimiwa Spika,
Kwa upande wa
muhimili wa Mahkama, juhudi kubwa zimefanywa katika kuimarisha utendaji wa
muhimili huo. Tumeimarisha maslahi ya watumishi na kuongeza idadi ya Majaji,
Mahakimu na Makadhi. Vile vile, tumeyafanyia matengenezo majengo na Ofisi za
mahkama .pamoja na kuyapatia vitendea kazi. Idadi ya Majaji imeongezwa kutoka
wanne mwaka 2010 hadi wanane hivi sasa, ambapo watatu kati yao ni wanawake.
Idadi ya Mahakimu imefikia 65 kutoka 13 mwaka 2010 na Makadhi ni 14. Ongezeko la Majaji na Mahakimu, limesaidia
sana katika kuzidisha kasi ya kusikiliza
kesi na kurahisisha utoaji wa haki kwa
wananchi. Serikali imeanza hatua ya
ujenzi wa jengo la kisasa la Mahkama Kuu lenye thamani ya TZS Bilioni 16 huko
Tunguu, ili kukidhi mahitaji ya nafasi ya
Mahkama Kuu ya Zanzibar.
Katika kipindi
hiki, Sheria Namba 13 ya Mwaka 2019 ya
kuanzishwa kwa Skuli ya Sheria imeanzishwa pamoja na Sheria mpya ya Mawakili
Namba 2 ya 2020, imetungwa kwa ajili ya kuweka utaratibu mzuri wa Mawakili
Zanzibar.
Kuhusu kudumisha Mapinduzi Matukufu ya
Januari 12, 1964 nnafuraha kwamba wananchi wanaendelea kunufaika na matunda
yake kwa kuwa huru tukiwa na mihimili mitatu yenye uwezo kamili ambayo ni
Mamlaka ya Utendaji, Baraza la Wawakilishi na Mahakama. Kadhalika, wananchi wa Zanzibar wanaendelea
kufurahia uhusu wa kufanya maamuzi mbali mbali yanayohusu masuala yao ya
maendeleo, kiuchumi, kisiasa na kijamii pamoja na kupata huduma za kijamii
zikiwemo elimu, afya, maji safi na salama kwa misingi ya usawa. Hayo ndiyo matunda ya Mapinduzi ambapo Waasisi
wetu walijitolea kuyapigania na kuyajengea misingi imara kwa manufaa ya watu
wote. Kwa hivyo ni wajibu wetu sote
tuendelee kuyadumisha.
Mheshimiwa
Spika,
Suala la kulinda na kudumisha Muungano
wetu wa Serikali mbili, kwangu halina mbadala. Nitaendelea na juhudi za
kudumisha Muungano wetu wa Tanganyika na Zanzibar wa Serikali mbili,
ulioasisiwa mwaka 1964 na Marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage
Nyerere na Marehemu Mzee Abeid Amani Karume ambao unatimiza Miaka 56 ifikapo
tarehe 26 Aprili 2020.
Waheshimiwa Wajumbe, tuna wajibu wa
kuhakikisha kwamba Serikali zetu mbili, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zinaendelea kuimarisha
mashirikiano na kufanya kazi kwa umoja na ukaribu zaidi katika kupanga na kuitekeleza
mikakati ya uchumi na mipango mengine ya maendeleo. Nitaendelea kuhakikisha kwamba tunaimarisha
mashirikiano, udugu na mapenzi baina ya watu wa pande mbili hizi. Nitaendelea kushirikiana na Mheshimiwa Dkt.
John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kudumisha
hali ya amani na utulivu, iliyodumu tangu kuundwa kwa Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, tarehe 26 Aprili, 1964.
Mheshimiwa
Spika,
Kama mnavyofahamu kwamba Tume ya
Uchaguzi ya Taifa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Tume ya Uchaguzi ya
Zanzibar hivi sasa zinaendelea na matayarisho ya Uchaguzi Mkuu, utakaofanyika
hapo baadae mwezi wa Oktoba. Kwa hivyo,
ni imani yangu kwamba wananchi ambao wametimiza masharti na vigezo vya Tume kwa
ajili ya mpiga kura, wamejiandikisha na kuhakiki majina yao katika daftari la
kudumu la mpiga kura, ili waweze kuitumia haki yao ya kidemokrasia ya kupiga
kura, kwa kuwachagua viongozi wanaowataka, wakati wa kufanya hivyo utakapofika.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa mara nyengine tena natoa shukurani
zangu za dhati kwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi la Tisa kwa kuendelea
kuweka misingi ya Utawala Bora na Demokrasia.
Ni dhahiri kuwa baada ya Uchaguzi Mkuu nitakamilisha kipindi changu cha
Pili cha Urais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Si haba nimeitumikia nchi yangu. Sitaongeza hata nukta moja. Panapo uhai na
majaaliwa, nitamkabidhi Rais aje kama mie nilivyokabidhiwa. Matumaini yangu makubwa sana kwamba
nitamkabidhi mwana CCM mwenzangu. Nasema
hivyo kwa ushahidi, sisemi tu. Hii ni kutokana na utekelezaji huu wa Ilani
tulioufanya katika kipindi cha miaka kumi iliyopita.
Juzi tumemsikia Rais Magufuli mafanikio
aliyoyaeleza kwa miaka mitano pekee na haya ni ya miaka kumi. Chama gani kitafanya kama CCM? Atakaepinga
mwambieni hayo niliyoyasema mimi. Kwanza hakuna chama kilichofanya haya. Pili, hakitatokea. Katika kipindi hiki tumefanya kwa ari na kasi
kubwa tukijiamini katika Serikali hii ya Awamu ya Saba. Walidhani wananiacha Awamu ya Saba sehemu ya
pili ningeshindwa. Mawe! Wameniacha uporo nipo nadunda naiongoza Zanzibar. Kwa
hakika mmeweza kuutekeleza wajibu wenu wa kikatiba wa kutunga sheria na
kuisimamia Serikali kama ilivyoainishwa katika kifungu cha 5A(1) na
kufafanuliwa katika kifungu 5A(2) cha Katiba ya Zanzibar ya 1984.
Mheshimiwa
Spika,
Katika kipindi cha miaka kumi,
mmetekeleza majukumu yenu kwa kufanya mikutano yenu katika hali ya salama na
utulivu, mmeyajadili masuala muhimu na mmeweza kuipitisha miswada
ya sheria 128 na baadae iliwasilishwa kwa Rais kwa ajili ya kutiwa saini na
sasa imekuwa sheria kamili za Zanzibar.
Takwimu zinaonesha kuwa katika kipindi
hiki cha miaka kumi, maswali 3,468 ya msingi na maswali ya nyongeza 4,894
yameulizwa kwa Serikali na yalipata majibu sahihi. Kadhalika, Kamati za Baraza nazo zilitekeleza
majukumu yake kwa uadilifu na umakini mkubwa.
Nawapongeza wajumbe wote wa Kamati hizo kwa kufuatilia na kuibua masuali
juu ya mambo mbali mbali, kuyaleta Barazani kwa kujadiliwa na baadae kuishauri
Serikali juu ya mambo yaliyojitokeza.
Kadhalika, nalipongeza Baraza kwa kupokea na kujadili hoja binafsi mbali
mbali zilizowasilishwa.
Leo ni siku ya furaha kwa upande mmoja
na ni siku ya huzuni kwa upande mwengine.
Nnasema hivi kwa sababu tutalivunja Baraza hili kwa mbwembwe na madaha
kutokana na mafanikio makubwa tuliyoyapata
katika kujenga nchi yetu. Lakini
leo ni siku ya huzuni kwa sababu tunaagana na baadae nitalivunja rasmi Baraza
la Tisa na kwa hivyo, huenda ikapita kipindi bila ya baadhi yenu kuonana,
ingawa tunategemeana kwa kiasi kikubwa.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa wale wenye dhamira ya kurejea
majimboni, kwa ajili ya kutafuta ridhaa ya wananchi kwa mara nyengine,
nawatakia kila la kheri na mafanikio, ili warudi tena kwa miaka mitano
mingine. Kwa wale ambao wamefikia uamuzi
wa kutogombea tena, nawanasihi sana waendelee kutumia maarifa na uzoefu
walioupata katika Baraza hili, katika kuongoza, kuhamasisha na kushiriki
kikamilifu katika harakati za nchi yetu.
Naamini ndani ya nafsi yangu kuwa yote mtakuwa hazina kubwa katika
kupanga na kuitekeleza mipango ya nchi hii.
Hata hivyo, kwa wale mtakaojaaliwa
kuchaguliwa tena na wananchi na kurudi Barazani, nakunasihini na nakukumbusheni
kuwa mnapokuwa kwenye Baraza hili muendelee kuilinda, kutii na kuitetea kwa
vitendo Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, sheria ziliopo na kanuni za Baraza hili.
Mheshimiwa
Spika,
Baraza la Wawakilishi ni Muhimili
uliowekwa ndani ya Katiba. Hiki ni
chombo kikubwa, hakiendeshwi kwa ukaidi wala kwa ubabe na njia yoyote
inayolingana na haya mawili niliyoyaeleza.
Baraza hili ni chombo cha wananchi wa Zanzibar, kwa hivyo, suala lolote
lenye maslahi na wananchi, hapa ndipo pahala pa kisheria pakulizungumza jambo
hilo.
Waheshimiwa wajumbe nyinyi ndio
mnaotunga sheria za nchi, kwa hivyo, nnakunasihini sana mlizingatie jambo hili,
kwamba kila sheria iliyotungwa na Baraza hili, matumizi yake yapo wazi kwa
kupitia Taasisi iliyowekwa. Vile vile,
nataka mzingatie maadili ya Chama cha Mapinduzi na taratibu zake kwani nyinyi
ni wanachama wa CCM; kwani mmeupata uwakilishi kwa tiketi ya CCM na hamkua
wagombea binafsi. Zingatieni sana “Three
Whip Sytem” iliyopo inafanya kazi
vipi. “Whip” ni kiboko, kwa hivyo vipo
viboko vitatu. Nyinyi mkiwa wagombea
mliofaulu kuchukua majimbo ya CCM ni lazima mnajua. Mligombea kuja Barazani kwa tiketi ya CCM na
nyote nilikushikeni mkono, Wabunge na Wawakilishi wa CCM. Leo wengine mnaniachia peke yangu. Nataka niwe mwazi kabisa. Mengine mnayosema nyinyi mimi sisemi na mengine
mnayosema hayasemwi lakini nyinyi mnayasema.
Nasema tena msijisahau mkiwa
barazani. Mna chama chenu kilichokuleteni, kwa hivyo msifikiche pahala
mkakilazimisha chama kukushughulikieni.
Mheshimiwa
Spika,
Siri kubwa ya mafanikio yetu katika
sekta za maendeleo nilizozielezea ni kuendelea kuwepo na kuimarika kwa hali ya
amani na utulivu. Ndio maana katika
hotuba yangu ya leo nilianza kwa kulizungumzia suala hili kabla ya kuzielezea
sekta nyengine. Kwa hivyo, kwa mara
nyengine tena nataka nisisitize tena umuhimu wa amani, umoja, utulivu na
mshikamano kwamba si suala la Idara Maalum za SMZ na Vikosi vyetu vya Ulinzi na
Usalama vya SMT peke yao, lakini linatushirikisha wananchi sote kwa jumla wa
Tanzania na Zanzibar. Katika kipindi
chote cha miaka kumi cha uongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Awamu
ya Saba na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, vikosi vyetu vya Ulinzi
na Usalama vimetekeleza vyema majukumu yao kwa umahiri mkubwa na utulivu. Natumia fursa hii kuwapongeza sana kwa
utekelezaji mzuri wa dhamana zao hizo walizopewa na Taifa.
Mheshimiwa Spika,
Nimefarajika sana kwa mafanikio makubwa
tuliyoyapata katika kipindi cha miaka kumi ya uongozi wangu nikisaidiana na
viongozi wenzangu mbali mbali. Hata
hivyo, katika kipindi hiki tulikabiliwa na changamoto mbali mbali. Baadhi ya changamoto hizo, zipo ambazo
tulianza kuzitatua, lakini hazikumalizika,
zipo nyengine tulizifikisha hatua kubwa, lakini zipo nyengine ufumbuzi wake ni
mgumu. Changamoto hizo, sote
tunazifahamu lakini nitazitaja kwa ujumla wake.
Kwanza, ni tatizo la ajira kwa vijana.
Pili, ni tatizo la upungufu wa mchanga hapa Zanzibar. Tatu, ni tatizo la
udhalilishaji wa wanawake na watoto.
Nne, ni tatizo la uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi na Tano, ni tatizo la
janga la COVID-19.
Nataka niizungumzie kwa ufupi
changamoto iliyotukumba hivi karibuni, nayo ni kuzuka kwa maradhi ya homa ya
mapafu yanayosababishwa na virusi vya “Corona”.
Tatizo la COVID-19. Maradhi haya
yalipoingia Tanzania mwishoni mwa mwezi wa Machi, yametuletea madhara ya afya
zetu na changamoto za kiuchumi. Madhara
ya afya ya “Corona” tumeyashuhudia na sasa yanajulikana vizuri na
tutaendelea kuyafanyia kazi. Kuhusu
madhara ya uchumi ya COVID-19, kayaelezea vizuri Waziri wa Fedha na Mipango
Mheshimiwa Balozi Mohamed Ramia Abdiwawa, aliyoyaelezea katika hotuba yake ya Bajeti ya
Serikali. Serikali zetu mbili
tulishirikiana sana na tulijidhatiti kupambana nayo kwa moyo mkubwa na kwa
uwezo wetu wote. Pamoja na upya wa
COVID-19, hatukuyaogopa na wala hakutokea kiongozi hata mmoja wa Serikali
aliyekimbia kutekeleza wajibu wake. Hongereni sana.
Tuliandaa mipango yetu madhubuti na
tuliwaongoza wananchi kujikinga dhidi ya COVID-19. Mipango na maelekezo ya Serikali, mipango na
maelekezo ya madaktari na wataalamu wetu wengine wa afya, imani za wananchi kwa
Serikali zao yalikuwa na hamasa ya hali ya juu katika kupambana na
“Corona”. Mambo yote hayo tuliyafanya
kwa uhakika, kwa kujiamini na kwa uwezo mkubwa sana. Tuliamua wenyewe, tuliongozwa na nia thabit
na uzalendo mkubwa. Hatukuwa tayari
kuiga wala kuogopa. Hatua tulizozichukua
zilikuwa sahihi ambazo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ilitangaza mambo kumi
hapo tarehe 29 Machi, 2020 katika
kulishughulikia tatizo la COVID-19. Kila
mmoja wetu aliendelea kutekeleza wajibu wake na kazi hazikusitishwa,
ziliendelea kufanywa kila pahala, pamoja na miradi yote ya maendeleo. Tarehe 23 Mei, 2020 nilipotoa hotuba yangu ya
Sikukuu ya Idd el Fitr, nilielezea uamuzi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
wa kuregeza masharti yaliyowekwa dhidi ya “Corona” hatua kwa hatua, kutokana na
hali ya ugonjwa itakavyokuwa.
Hali ilivyo sasa ni shwari kuliko
ilivyokuwa mwezi wa Aprili, Mei na mwanzo wa wiki ya Juni. Kwa upande wetu, Unguja na Pemba hadi tarehe
10 Juni vituo vyetu vyote vilivyokuwa vikiwatibu wagonjwa wa COVID-19, havina
hata mgonjwa mmoja; leo ni siku 10 zimepita tangu alipotoka mgonjwa wa
mwisho. Kwa hivyo, hali yetu imekuwa
bora zaidi, nami nawatangazia wananchi kwamba tutazifungua skuli za Unguja na
Pemba za Maandalizi, Msingi na Sekondari kuanzia Jumatatu, tarehe 29 Juni,
2020. Kutokana na mazingira ya madrasa,
skuli za Maandalizi na Msingi za Zanzibar yalivyo, Wizara ya Elimu na Mafunzo
ya Amali iandae mpango madhubuti na kabambe wa namna bora zaidi kwa wanafunzi
watakapokwenda masomoni.
Boti na meli zinazofanya safari, baina
Unguja na Dar es Salaam, Unguja na Pemba, Pemba na Tanga, kuanzia tarehe 29
Juni, 2020 zitaruhusiwa kuchukua abiria kwa mujibu wa idadi ya viti vya vyombo
hivyo, vilivyosajiliwa. Abiria
hawatoruhusiwa kusimama au kukaa popote.
Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji, Mamlaka ya Usafiri wa
Baharini na Shirika la Bandari watapaswa wausimamie utekelezaji wa maagizo
haya. Manahodha na uongozi wa vyombo hivyo watapaswa wawajibike, endapo
watayakiuka maelekezo haya ya Serikali.
Vile vile, shughuli za jamii nazo ruhusa zifanyike isipokuwa ni lazima
zichukuliwe tahadhari zote za kinga kama tunavyoelekezwa na wataalamu. Tusifanye dharau, kwani COVID-19
haijamalizika kabisa.
Siku kumi hizi hazitoshi kuamini kwamba
maradhi haya yamemalizika kabisa, lazima tuendelee kuchukua tahadhari. Wizara ya Afya, Idara ya Kinga wahakikishe
tahadhari zote zinachukuliwa bila ya kuwasumbua na kuwazuia watu. Ni wajibu waendelee kuwaelimisha wananchi. ZBC TV na Redio pamoja na magazeti ya
Zanzibar Leo endeleeni kuwaelimisha watu juu ya maradhi haya. Hatutarajii hali hii ya “Corona” ije kurejea
tena. Hata hivyo, vilabu vya michezo
yote visubiri, tukiacha michezo ya ligi kuu ya mpira wa miguu.
Mheshimiwa
Spika,
Kadhalika, nawapa pole wale wote
walioathirika na maafa ya kipindi cha mvua kubwa za masika zilizonyesha hivi
karibuni, ambazo zinasemekana ziliungana na mvua za Vuli, pamoja na upepo
mkali; ambazo zilipelekea watu watano kupoteza maisha na wengine kupoteza mali
na uharibifu mkubwa wa nyumba na mazingira. Nawapa pole wananchi wenzetu walioathirika
afya zao kwa kuambukizwa virusi vya “Corona”.
Maradhi yaliwasibu, hali zao zilikuwa dhaifu, lakini, kwa uwezo wa
Mwenyezi Mungu, jitihada za Serikali yetu, madaktari na wataalamu wa afya,
ndugu zetu hawa wamepata nafuu na wamepona.
Nawapa pole wananchi wenzetu ambao
wamewapoteza ndugu, jamaa na marafiki kutokana na maradhi ya COVID-19
yanayosababishwa na virusi vya CORONA ambayo yameingia katika nchi yetu kama
yalivyozikumba nchi nyengine duniani.
Natoa shukurani kwa wananchi wote kwa kushirikiana na Serikali katika
kukabiliana na mitihani yote hii. Vile
vile, natoa shukurani kwa Taasisi mbali mbali na wale wote walioungana na
Serikali katika kuwafariji kwa kutoa misaada mbali mbali kwa familia
zilizofikwa na maafa. Natoa wito kwa wananchi
wote tuendelee kuwa na subira, tuwe wamoja na tuzidi kushirikiana katika
kuikabili mitihani mbali mbali inayotokea hapa nchini.
Nachukua nafasi hii kutoa pongezi zangu
za dhati kwa madaktari, wauguzi na watendaji wote wa sekta ya afya, kwa juhudi
walizoonesha katika mapambano hayo. Kwa mara nyengine, natoa pongezi zangu za
dhati kwa Mwenyekiti wa Kamisheni ya Kupambana na Maafa ya Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, ambaye ni Makamo wa
Pili wa Rais wa Zanzibar, pamoja na
wajumbe wote, na Mwenyekiti wa Kamati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ya Kupambana na Maradhi haya ya
COVID 19, Mheshimiwa Kassim Majaaliwa Majaaliwa, ambaye ni Waziri Mkuu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; pamoja na wajumbe wote, kwa kufanya kazi
nzuri, kwa ushirikiano na uzalendo wa
hali ya juu; mambo ambayo yametoa
matokeo mazuri.
Vile vile, kwa mara nyingine shukurani zangu ziende kwa
viongozi wa dini, vyombo vya habari, vyombo vya ulinzi na usalama, Wakuu
wa Mikoa na Wilaya, masheha, viongozi wa ngazi mbali mbali, wasanii, wamiliki
na madereva wa vyombo vya usafiri, wafanyabiashara, wakulima, wavuvi, na wananchi wote, kwa kila mmoja kutekeleza
jukumu lake ipasavyo kwa uzalendo na uadilfu.
Kwa pamoja, tunaendelea kuyatekeleza yale
mambo kumi (10) yaliyotangazwa na Serikali tarehe tarehe 19 Machi, 2020. Serikali itaendelea kuregeza masharti na kutoa miongozo
mipya kwa kutegemea hali ya maradhi hayo ilivyo. Serikali zetu zote mbili zitaendelea kuchukua
uamuzi kwa kuzingatia uwezo na maisha
halisi ya wananchi, bila ya kutaka kuiga maamuzi na mipango ya nchi, taasisi au
watu wengine.
Tuongeze nguvu
katika kufuata miongozo inayotolewa na Serikali huku tukiwa na subira. Tuendelee kumuomba na
tumshukuru Mwenyezi Mungu, atuvue na janga hili na majanga mengine. Kwa uwezo
wake Yeye, atatunusuru na atatuvusha kwa
salama hapa tulipo, ili maisha yetu yarejee katika hali ya kawaida na iliyo
bora zaidi.
Mheshimiwa
Spika,
Leo tunaagana, lakini itakuwa kwa kheri
ya kuonana. Tutaendelea kuonana, kwani
tuna kazi kubwa iliyotukabili sote ambayo ni kushiriki kwenye uchaguzi kwa
kupiga kura. Kwa hivyo, ni vyema
tukahakikisha kwamba kila mwenye sifa na haki ya kushiriki katika uchaguzi,
anafanya hivyo, akielewa kuwa kufanya hivyo ni msingi muhimu wa utawala bora na
demokrasia.
Ni wajibu wetu tuiheshimu kazi,
majukumu ya Tume zetu za Uchaguzi NEC na ZEC, vyombo ambavyo vimeundwa
kikatiba. Serikali imetunga Sheria ya
Uchaguzi Namba 4 ya mwaka 2018. Sheria
hii imelenga kuweka utaratibu bora wa uchaguzi na kuondoa kasoro zote
zilizojitokeza katika chaguzi zilizopita.
Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar itafanya kazi nzuri na kila mmoja atapata
haki yake. Kuchukua uamuzi kinyume na
utaratibu uliowekwa na sheria, itakuwa kusababisha zogo na kuanzisha fujo. Zogo na fujo ndio chanzo cha watu kugombana
na hatimae kuingiyana maungoni. Hayo si
madhumuni ya uchaguzi. Kwa hivyo,
uchaguzi wa Oktoba mwaka huu utakuwa huru na haki. Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, itaendelea
kuhakikisha kwamba hali ya amani na utulivu iliyopo nchini hivi sasa itaendelea
kudumu. Wale wenye nia au mawazo ya
kutaka kuuharibu uchaguzi kwa njia yoyote au kufanya fujo, jambo hilo
halitawezekana kwenye uchaguzi wa mwaka huu.
Nawathibitishia wananchi, sheria ya uchaguzi ipo, katiba ipo, fedha zetu
wenyewe za kuendesha uchaguzi zipo, vikosi vyetu vya Ulinzi na Usalama
vipo. Nawatangazia leo mimi na Dkt. John
Pombe Joseph Magufuli tupo macho, hatutasinzia, tutatekeleza wajibu wetu. Watakaofanya vituko dhidi ya sheria
tutawashughulikia.
Nawatakia kheri wale Waheshimiwa wote
ambao kwa sababu mbali mbali hawatokuwepo katika Baraza lijalo baada ya
Uchaguzi wa Oktoba, 2020. Wale wanaoomba
kurejea pamoja na wengine ambao sasa si wajumbe nawanasihi wazingatie kuitunza
amani na utulivu katika harakati za uchaguzi.
Huu ni wakati wetu sote tudhihirishe ustaarabu katika siasa zetu, umoja
wetu, mshikamano na utiifu wa sheria.
Kuitunza amani ni dhamiri yetu sote.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa mara nyengine tena nnakushukuru kwa
dhati Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid, kwa kuliongoza Baraza la Wawakilishi kwa
busara, haki, uadilifu na ufanisi mkubwa.
Umefanya kazi kubwa ya kuliendesha Baraza hili na umetoa mchango mkubwa
katika kukuza demokrasia na utawala bora.
Nakutakia kila la kheri katika maisha yako. Lakini nakushukuru wewe na
wajumbe wote kwa kupitisha azimio la kunipongeza. Ahsanteni sana. Lakini sifa hii tunastahiki sote.
Nampongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe
Joseph Magufuli kwa kuiongoza Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na namna
tunavyoendelea kushirikiana; anavyokiongoza Chama chetu, Chama cha Mapinduzi na
jitihada zake katika kuuendeleza na kuuimarisha Muungano wetu. Vile vile, natoa shukurani kwa Mheshimiwa
Samia Suluhu Hassan, Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa
Kassim Majaaliwa Majaaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana
nami nikiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na kwa juhudi
zao za kuuimarisha Muungano wetu. Vile
vile, namshukuru Mheshimiwa Job Ndugai, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania kwa kushirikiana nami katika shughuli mbali mbali za Chama na
Serikali.
Kadhalika, nampongeza na namshukuru
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa kazi kubwa
anayoifanya katika kunisaidia kuiongoza Zanzibar. Tumefanya mambo mengi sana
makubwa. Wakati mwengine huwa nashangaa
anafanikiwa vipi. Namwagiza afanye mambo
wakati mwengine najua namsumbua lakini ndiyo kazi yenyewe niliyompa
anisaidie. Hajanambia sifanyi hata siku
moja. Hajanung’unika kwa kazi hata siku
moja. Amekua mtiifu kwangu wakati wote.
Nakupongeza wewe Balozi Seif Ali Iddi na Mama Asha Suleiman Iddi. Hongereni sana. Nafahamu tuna muda mfupi kabla ya
kumaliza. Tutapongezana zaidi baadae Serikalini.
Mheshimiwa
Spika,
Nawapongeza viongozi wastaafu
niliofanya kazi nao katika Chama cha Mapinduzi (CCM) akiwemo Rais Mstaafu Mzee
Ali Hassan Mwinyi, nimefanya kazi na Rais Mstaafu Benjamin William Mkapa ambae
nimefanya kazi nae kwa miaka minne na nusu, nilipokuwa Makamo wake wa
Rais. Kwa furaha kubwa sana nampongeza
Dk. Jakaya Mrisho Kikwete, tangu yeye akiwa Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa. Nimefanya kazi
nae kwa miaka minne na nusu na baadae akiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania kwa muda wa miaka mitano. Nilifanya
kazi nae nikiwa Makamo wake wa Rais. Tumezoeana na tumeshirikiana vyema katika
kuwatumikia wananchi, tumekuwa na udugu na urafiki mkubwa sana. Kadhalika, nawapongeza na viongozi wengine wa
CCM na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania niliofanya nao kazi.
Vile vile, natoa shukurani kwa
Mheshimiwa Dk. Salmin Amour, Rais Mstaafu wa Zanzibar wa Awamu ya Tano ya
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa
kuniteuwa kuwa mjumbe wa Baraza la Wawakilishi na kisha kuwa Naibu Waziri wa
Afya katika mwaka 1995. Kadhalika,
namshukuru Mheshimiwa Dk. Amani Abeid Karume Rais Mstaafu wa Zanzibar wa Awamu
ya Sita ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuniteua kuwa Waziri wa Katiba
na Utawala Bora mwaka 2000. Nawashukuru
sana viongozi wote wawili kwa kuniamini na kuniteua kushika nyadhifa hizo. Nawashukuru kwa kushirikiana nami katika nafasi mbali mbali za uongozi wa
Serikali na Chama cha Mapinduzi.
Ushirikiano walionipa umetoa mchango mkubwa katika kufanikisha maendeleo
ya Zanzibar.
Mheshimiwa
Spika,
Pongezi zangu za dhati nazitoa kwa Mheshimiwa
Jaji Mkuu, Mawaziri na Manaibu Mawaziri
wote. Nampongeza Mheshimiwa Said Hassan Said Mwanasheria Mkuu, huyu ni Mheshimiwa
makini sana namuamini kama ninavyoiamini nafsi yangu. Hongera sana. Nampongeza Mufti wa Zanzibar na Kadhi
Mkuu. Vile vile, nampongeza kwa dhati
Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Dk. Abdulhamid Yahya
Mzee, ni mfanyakazi aliyebobea katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Uwezo wake wote sina shaka nao. Anaifahamu Serikali kweli kweli. Amekuwa Katibu Mkuu kwa miaka mingi.
Anaiheshimu Serikali na viongozi wake.
Miaka kumi yote amenisaidia sana. Wakati mwengine namuweka macho hadi
usiku mkubwa. Hajawahi kunung’unika hata
siku moja. Nampongeza kwa ustahamilivu
wake. Si mpole tu ndio alivyo ni mpole
kwa kufanya kazi. Dk. Abdulhamid,
hongera sana. Namshukuru Mheshimiwa
Pandu Ameir Kificho, Spika Mstaafu wa Baraza la Wawakilishi kwa kushirikiana
nami katika kipindi cha mwanzo cha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya
Saba.
Nawapongeza Washauri na Wasaidizi wa
Rais pamoja na wafanyakazi wote wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi, Makatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu na watumishi wote wa Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar. Kadhalika,
nawapongeza viongozi wote wa Serikali, Viongozi wa vyama vya siasa vya
upinzani, viliomo Barazani; TADEA, ADC, Chama cha Wakulima na wengine
wanaoiunga mkono Serikali hii, ambao hawapo Barazani. Nawashukuru wananchi wa Zanzibar kwa
kunichagua kwa kura za ushindi na kuwa Rais wa Zanzibar na kuendelea kuiunga
mkono Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba. Shukrani maalum nazitoa kwa uongozi wa CCM na
wana CCM wote kwa kunipa heshima kubwa ya kuniteua nikagombea Urais wa
Zanzibar. Hili ni deni kubwa kwangu na
katika familia yangu. Sina namna ya
kuelezea shukrani zangu na pongezi, nasema Ahsanteni sana wana CCM na viongozi
wote.
Kadhalika, nampongeza na namshukuru Mama
Mwanamwema Shein, mke wangu kwa kunisaidia, kuniunga mkono, kunistahamilia na
kunivumilia wakati wote katika maisha yetu na nikiwa katika utumishi wa
Serikali ya Mapinduzi na Serikali ya Muungano wa Tanzania. Vile vile naipongeza familia yangu yote, ndugu,
jamaa na marafiki zangu katika siku hii muhimu kwa nchi yetu.
Mheshimiwa
Spika,
Ili kutoa nafasi kwa matayarisho ya
mwisho kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka 2020, kwa madaraka niliyonayo
kama ilivyoelezwa katika kifungu cha 91(2)(a) cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka
1984, natamka kwamba tarehe ya kuvunjwa kwa Baraza la Tisa la Wawakilishi la
Zanzibar itatangazwa kwenye Gazeti Rasmi la Serikali hapo baadae.
Nakutakieni
kila la kheri.
MUNGU
IBARIKI ZANZIBAR
MUNGU
IBARIKI TANZANIA
MUNGU
IBARIKI AFRIKA
Ahsanteni
kwa kunisikiliza.
No comments:
Post a Comment