Muonekano wa chumba cha
upasuaji katika kituo cha afya Bunda mjini baada ya kuboreshwa na Serikali ya Awamu ya Tano kwa gharama ya shilingi milioni
500 kwa kujengewa majengo mapya na vifaa tiba vya kisasa.
Sehemu ya majengo ya kituo
cha Afya Bunda mjini mkoani Mara baada ya kuboreshwa na kuanza kutoa huduma za upasuaji kwa wananchi wa mji huo na maeneo ya jirani.
(Pichana MAELEZO)
Na.Jonas
Kamaleki, Bunda
Utoaji
wa huduma za Afya umeboreshwa baada ya Serikali kutoa milioni 500 kwa ajili ya
ujenzi wa Kituo cha Afya Bunda, mkoani Mara.
Baadhi
ya wakazi wa Bunda wameipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuwaboreshea na
kuwasogezea huduma za afya hivyo kuwaondolea adha walizokuwa wakizipata kabla
ya hatua hiyo ya Serikali.
Mkazi
wa Kijiji cha Nyasula, Elizabeth Madimanya amesema kuwa Kituo kinatoa huduma
nzuri na mandhari ya hospitali ni nzuri.
Naye
Rehema Malila, mkazi wa Kijeti, Bunda ametoa pongezi kwa Mhe. Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuboresha huduma za afya.
“Zamani
tulikuwa tunahangaika kupata huduma za afya mbali sana na kwetu hadi mtoto
wangu alifia tumboni kwa kukosa huduma ya karibu, Kituo kinatoa huduma nzuri,
watumishi ni wazuri, utadhani wote ni wachaMungu”, alisema Malila.
Kituo
cha Afya Bunda kimekuwa msaada mkubwa kwa wakazi wa maeneo hayo ambao walikuwa
wanafuata huduma za afya umbali mrefu zaidi ya kilomita 17.
Muuguzi
Kiongozi wa Kituo hicho, Dorcas Makaya anasema Kituo cha Afya Bunda kinahudumia
takriban akina mama watano kwa siku kwa ajili ya huduma za kujifungua.
Anaelezea kuwa wanajitahidi kuwahudumia wananchi kwani dawa na vifaa tiba
vinapatikana kwa uhakika.
“Nawashukuru
viongozi wa Halmashauri ya Bunda Mji kwa ushirikiano wanaotupatia kiasi kwamba
tunatoa huduma bila wasiwasi, pia namshukuru Mhe. Rais John Pombe Magufuli kwa
kutujengea Kituo hiki”, anaongeza Makaya.
Kituo
hicho baada ya ujenzi wake kukamilika, kilianza kutoa huduma moja kwa moja
baada ya Halmashauri ya Bunda kupata vifaa vya hospitali hiyo kutoka kwa
wahisani toka nje.
“Hatukusubiri
Serikali kutuletea vifaa ilibidi tujiongeze wenyewe kwa kuwasiliana na wahisani
toka nje ili huduma zianze”, anaeleza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya
Bunda Mji, Janeth Mayanja.
Kwa
mujibu wa Mayanja Kituo hicho kimekuwa msaada mkubwa kwa wakazi wa Bunda Mjini
na maeneo ya jirani kwa kusogeza huduma za afya karibu.
Serikali
ya Awamu ya Tano imedhamiria kuboresha huduma za afya kwa kujenga zaidi ya
vituo vya afya 362, hospitali za wilaya 67 ambazo hivi karibuni zimeagizwa na
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, Suleiman Jafo kuanza kutoa huduma mara
moja baada ya kukamilika ujenzi wake.
Mhe.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli amekuwa
akisikika akisema kuwa Serikali yake imejipanga kuboresha huduma za afya kwa
kuongeza bajeti ya Dawa na vifaa tiba kutoka Shilingi bilioni 31 hadi bilioni 270.
“Tumeajiri
watumishi wa kada mbalimbali za 11,152, tumejenga nyumba za watumishi 306 na
pia tumeboreshana kuimarisha huduma za kibingwa katika Hospitali yetu ya Taifa
Muhimbili na Hospitali za Rufaa za Bugando, KCMC na Mbeya. Hivi sasa watu toka
nchi jirani wanakuja nchini kupata matibabu ya magonjwa ya moyo, figo,kansa,
mifupa ubongo na kadhalika”, anasema Rais Magufuli.
Hakika
huduma za afya zimeboreshwa na kusogezwa karibu na wananchi hivyo kuwaongezea
matumaini ya kuishi wakiwa na afya bora. Karibu wilaya zote hapa nchini licha
ya kuwa na hospitali za wilaya, vituo vya afya na zahanati vimejengwa na
vingine kuboreshwa.
No comments:
Post a Comment