Habari za Punde

Mchakato wa Kumpata Mgombea Urais Umekwenda Vizuri - Dk. Shein.


Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akihutubia Wajumbe wa Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM Taifa katika ukumbi wa White House Jijini Dodoma leo 10/7/2020. 
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein ambaye pia, ni Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar amesema kuwa mchakato wa kumpata mgombea wa nafasi ya Rais wa Zanzibar umekwenda vizuri tokea ulipoanza hadi kukamilika hivi leo.
Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati akitoa salamu zake katika Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa CCM “White House” Jijini Dodoma.
Makamo Mwenyekiti huyo alieleza kuwa mchakato wa kuwapata wagombea hao  umekwenda vizuri kwa mujibu wa Katiba ya CCM, Kanuni na taratibu zote za chama hicho chini ya uongozi wake.
Akizungumza kabla ya kufanyika kwa uchaguzi huo wa kumpata mgombea wa nafasi ya Urais wa Zanzibar, Rais Dk. Shein alisema kuwa kilichofanyika Zanzibar katika vikao vya chama hicho ni kutafuta wagombea ili kuendeleza mchakato huo wa kumpata mgombea mmoja atakaepeperusha bendera ya CCM.
Alisisitiza kuwa lengo la chama hicho ni kutafuta ushindi katika uchaguzi mkuu ujao wa mwaka huu na kusisitiza kuwa CCM itashinda.
Katika salamu zake hizo, Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alieleza uzoefu wake ndani ya chama hicho ambapo amekitumikia kwa takriban  miaka 51 hivi sasa.
Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuepuka maneno yasiokuwa na msingi katika kukiimarisha chama hicho na kwuataka kuwa waungwana ikiwa ni pamoja na kukemea vikali kauli za kubeba  mgombea katika mchakato huo wa kumpata Rais wa Zanzibar.
Katika Kikao hicho cha Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), majina matatu yalipigiwa kura baada ya wagombea hao mapema kutoa salamu zao na kuomba kura kwa wajumbe  wa mkutano huo.
Waliopigiwa kura katika kikaohicho ni Shamsi Vuai Nahodha aliyepata kura 16 sawa na asilimia 9.75, Dk. Khalid Salum aliyepata kura 19 sawa na asilimia 11.58 na Dk. Hussein Mwinyi aliyepata kura 129 sawa na asilimia 78.65 kati ya wapiga kura 166 na hatimae kuibuka kidedea katika uchaguzi huo.
Aidha, katika kikao hicho kilipitisha jina la mgombea wa nafasi ya CCM katika nafasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Joseph Magufuli ambaye atakwenda kupigiwa kura katika Mkutano Mkuu wa CCM hapo kesho.
Pamoja na hayo, Rais Magufuli alimpongeza Rais Dk. Shein kwa umakini wake mkubwa katika kuiongoza Zanzibar sambamba na mafanikio makubwa yaliyopatikana katika sekta mbali mbali za maendeleo.
Rais Magufuli ambaye pia, ni Mwenyekiti wa CCM Taifa aliwapongeza viongozi wote wa CCM pamoja na wale wote waliomdhamini huku akiwataka Wazanzibari kuwa wamoja katika kuiimarisha CCM na hatimae kuhakikisha inapata ushindi wa kishindo katika uchaguzi Mkuu ujao.
Mapema wagombea wote watano wa nafasi ya Urais wa Zanzibar na wakiwemo wale watatu waliopitishwa katika Kamati Kuu ya chama hicho walitumia fursa hiyo kutoa salamu zao ikiwa ni pamoja na kutoa shukurani kwa (CCM) kwa kuweza kupata nafasi ya kugombea nafasi hiyo muhimu.
Nae Katibu Mkuu wa CCM Taifa Dk. Bashiru Ali Kakurwa alieleza mafanikio yaliyopatikana katika uongozi wa Rais Magufuli katika uongozi wake wa kipindi cha Kwanza cha miaka mitano huku wajumbe wa mkutano huo walitoa pongezi kwa Rais Magufuli pamoja na Rais Dk. Shein kwa mafanikio hayo.
Baada ya kutangazwa kuwa mshindi wa kura hizo Dk. Hussein Mwinyi ambaye alikuwa Mbunge wa Kwahani na pia, Waziri wa Ulinzi aliwashukuru wajumbe wote kwa kuonesha imani kwake na kuahidi kufanya kazi na kulitumikia Taifa kwa uwezo wake wote. "Hizi ni kura nyingi sana...nikuahidini kuwa tutakuwa pamoja tukatafute ushindi wa Chama Cha Mapinduzi,"
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.