Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Ametoa Mkono wa Pole Kwa Familia ya Marehemu Mzee Mkapa leo. it


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akitowa mkono wa Pole kwa Familia ya marehemu Rais Mstaaf wa Awamu ya Tatu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Benjamin William Mkapa, alipofika nyumbani kwa marehemu Masaki Jijini Dar es Salaam (kulia kwa Rais) Mjane wa Marehemu Mama Anna Mkapa na Mtoto wa Marehemu Nico Mkapa.   l
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, ametoa mkono wa pole kwa familia ya Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bejamin William Mkapa na kueleza kuwa kiongozi huyo atakumbukwa kwa mazuri mengi aliyoifanyia Tanzania.
Rais Dk. Shein alifika nyumbani kwa marehemu Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bejamin William majira ya saa tano za asubuhi katika Mtaa wa Masaki Jijini Dar es Salaam ambapo alitoa mkono wa pole kwa familia pamoja na kumpa  mkono wa pole Mjane wa Marehemu Mama Anna Mkapa.
Mapema mara tu baada ya kufika nyumbani kwa marehemu Rais Dk. Shein alitia saini kitabu cha maombolezi  na kutoa  pole kwa kifo cha Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Bejamin William Mkapa huku akimuomba  Mwenyezi Mungu aipe subira familia ya Rais Mkapa katika kipindi hichi kigumu cha msiba.

Akitoa mkono wa pole kwa familia ya Rais Mkapa, Rais Dk. Shein alieleza jinsi alivyoguswa na kifo cha Rais Mkapa na kuitaka familia hiyo kuwa na subira na kuendelea kumuombea Marehemu kutokana na mema mengi aliyoyafanya kwa wananchi pamoja na nchi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Mara baada ya matukio hayo, Rais Dk. Shein alipata fursa ya kufanya mahojiano na waandishi wa habari ambapo katika mazungumzo yake alimuelezea Rais Mkapa kuwa ni kiongozi mahiri aliyefanya kazi nae kwa muda wa miaka minne na nusu na kuweza kujifunza mambo mengi.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa Rais Mkapa aliweza kuifikisha Tanzania mahala pazuri sana kwa kusimamia misingi ya uchumi ambayo hatimae iliipelekeaTanzania kuimarika.

Aliongeza kuwa Rais Mkapa ameitumikia nchi kwa nidhamu kubwa sana ikiwa ni pamoja na kusimamia nchi kiuchumi na kimaendeleo sambamba na kuisimamia nchi kwa misingi yote ya amani na utulivu mkubwa

Alisema kuwa msiba huo ni wa Watanzania wote na kwa kila anaependa maendeleo wa ndani na nje ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania huku akisisitiza kumuombea ili apumzike kwa salama.

Katika kufuata misingi ya Rais Mkapa, Rais Dk. Shein aliwataka viongozi waliopo madarakani wazee na vijana kujifunza uongozi kutoka kwa Rais Mkapa kwani kiongozi huyo alikuwa ni mtu aliyeishi vizuri na watu wa maeneo yote tena bila ya kuwabagua.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa anayakumbuka mengi aliyoyafanya Rais Mkapa wakati anafanya kazi nae pamoja ikiwa ni pamoja na kusaidia sana kuibadilisha nchi kwa kufanya mabadiliko ya kiuchumi sambamba na kuimarisha utawala bora kwa kuanzisha Wizara ya Utawala Bora ambayo ilikuwa ndiyo Wizara ya mwanzo katika Serikali za  nchi za Bara la Afrika huku akisimamia kwa vitendo uchumi wa Tanzania.

Alisema kuwa wakati Rais Mkapa anaingia madarakani makusanyo yalikuwa madogo sana kwani yalikuwa ni wastani wa TZS Bilioni 1.7 mnamo mwaka 2005  lakini kutokana na juhudi zake makusanyo yaliimarika zaidi hatua ambayo pia ilipelekea kufanyika kwa mabadiliko ya sayansi na teknolojia.

“Ninayakumbuka mengi sana aliyoyafanya Rais Mkapa tukiwa pamoja Serikalini na ni muhali kuyasema hapa yote kwa muda huu mfupi kwani amefanya mambo mengi wakati nilishirikiana nae”, alisema Dk. Shein.

Alieleza kuwa kubwa kabisa na la muhimu alilofanya Rais Mkapa ni kusimamia mwenendo mzuri wa uchumi wa nchi kwani hilo linatokana na uzoefu wake wa uongozi kwani awali aliwahi kuwa Waziri katika Wizara kadhaa za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hatua ambayo imesaidia kumpa ujuzi na uwezo mkubwa wa kuongoza nchi.

Kutokana na Rais Mkapa kumtaja Rais Dk. Shein katika kitabu chake cha “My Life, My Purpose” Rais Dk. Shein alisema kuwa ameweza kumtaja katika kitabu chake hicho kwani alifanya kazi nae na kuishi nae vizuri kwani akiwa Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Rais Dk. Shein alifanya kazi na Marehemu Mkapa na kumuheshimu na kumuweka kuwa ni kiongozi wake, mkubwa wake na pia, alikuwa ni kiongozi wake wa Chama.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa yeye kwake ilikuwa ni rahisi sana kufanya kazi na Rais Mkapa kwani ni mkubwa wake na pia ni kiongozi wake wa kazi hivyo, alifanya kazi kwa kumuheshimu na kuishi nae vizuri na kumuacha afanye kazi zake bila ya kumuingilia hiyo ni kutokana na kumuamini wakati wote.

“Kwa vile alikuwa ananiamini, mtakumbuka hata mnamo mwaka 2003 alipokwenda nje ya nchi kwa muda kidogo lakini wakati huo yeye hayupo mimi niliweza kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa kutokana na mafunzo yake aliyonipa……..ni mtu ambaye ukifanya kazi nae unaona raha sana”, alisema Rais Dk. Shein.

Hivyo, Rais Dk. Shein alisema kuwa hatua yake hiyo ilimpelekea kufanya kazi kwa kujiamini na kusisitiza kuwa ni mtu ambaye ukifanya kazi nae unaona raha sana kwani anakuachia kufanya kazi zako vizuri kwani ni mtu aliyekuwa akishaurika na ni mtu aliyekuwa akielekeza namna ya kufanya kazi  kwani alikuwa mtu wa mfano wake.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.