Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Ametowa Heshima za Mwisho kwa Mwili wa Marehemu Benjaman Mkapa Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam.


VIONGOZI wa ndani na nje ya nchi wakishuhudiwa na maelfu ya  Watanzania wakiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Joseph Magufuli waliungana pamoja kuuaga kitaifa mwili wa Marehemu Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Benjamin William Mkapa.

Viongozi wa Kitaifa waliuaga mwili wa Hayati Mkapa wakiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli, wanafamilia, Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein na viongozi wa dini.

Tukio hilo limefanyika leo uwanja wa Uhuru Jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi mbali mbali wa ndani na nje ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na wananchi.

Aidha Rais John Pombe Magufuli alitumia fursa hiyo kwa niaba ya Serikali pamoja na wananchi kutoa mkono wa Pole kwa familia ya Hayati Mkapa akiwemo Mama Mkapa, Watoto pamoja na wajukuu na ndugu na jamaa wote.

Alieleza kuwa msiba huo ni wa Watanzania wote na sio wao pekee yao na kutoa pole kwa Watanzania wote kwa kuondokewa na kiongozi huyo na kuwataka wananchi kuendelea kua watulivu na huku wakiendelea kumuomba Mwenyezi kuipumzisha roho ya Marehemu Mkapa.

Akimuelezea Rais Mstaafu Hayati Mkapa kwa ufupi alieleza mchango na mafanikio ya Mzee Mkapa akiwa Rais na baada ya kutoka madarakani na kusema kua Tanzania na Bara la Afrika na dunia imepoteza mtu jasiri, mchapakazi, mcha Mungu, mfuatiliaji, mwenye msimamo, mwanadiplomasia nguli na mpenda amani na mshikamano.

Aidha, alieleza kuwa Mzee Mkapa ni Baba wa Demokrasia nchini, na kusema kuwa utoaji wa ruzuku wa vyama vya siasa ulianza katika Awamu ya Mzee Mkapa ikiwa ni pamoja na kuahidi kuwa Serikali yake inajengwa kwa misingi ya ukweli na uwazi ambapo baadae aliunda Tume ya Warioba na hatimae kuunda TAKUKURU.

Alisema kuwa Watanzania wengi wanamkumbuka Mzee Mkapa kwa mageuzi makubwa ya kiuchumi, jinsi alivyoweka mipango na mikakati ya kupunguza umasikini nchini ukiwemo mpango wa TASAF ambao mpaka awamu hii utakuwa umeshatumia TZS Trioni 4.19.

Alieleza jinsi alivyofuta kodi ikiwemo kodi ya baskeli, mifugo na hatua ambayo inaonesha jinsi alivyokuwa akiwapigania wanyonge na hatua za kuimarisha huduma za kijamii nchini na kujenga sekta binafsi zikiwemo Benki kubwa nchini.

Rais Magufuli alisema kuwa Hayati Mzee Mkapa alianzisha taasisi nyingi ili Tanzania ijitegemee ikiwemo Bodi ya Mfuko wa Barabara, TANROAD hatua ambayo ilipelekea ujenzi wa barabara za lami na madaraja kadhaa hapa nchini.

Aliongeza kuwa Mafanikio mengi ya kiuchumi misingi yake mengi iliwekwa katika uongozi wa Rais Mkapa ambapo pia, diara ya maendeleo ilianzishwa na Rais huyo ambapo chimbuko lake ni CCM ambacho Rais Mkapa alikitumikia na kukipenda sana.

Alijitahidi katika kuimarisha sekta ya elimu, maji,maslahi ya wahadhiri, kuimarisha sekta ya afya pamoja na  kusimamia amani na utulivu huku akisimamia haki na usawa duniani hatua ambayo ilipelekea kuzifumbua macho nchi zinazoendelea duniani.

Sambamba na hayo, alisema kuwa Mzee Mkapa aliimarisha sekta ya michezo pamoja na kuwaimarisha wasanii ikiwa ni pamoja na kuujenga uwanja wa Taifa wa Michezo na hapoa hapo alitamka kuwa kuanzia leo uwanja huo uitwe Mkapa Stadium.

Alieleza kua katika uongozi wa Mzee Mkapa pia, ndicho kipindi kilichoundwa Chama cha hati miliki (COSOTA) ikiwa na lengo la kuwasaidia wasaniii, uwanzishwaji wa vitengo vya habari na kutunga Sheria namba 30 ya kuanzisha Wakala ambapo kupitia sheria hiyo taasisi nyingi zimeundwa na kuleta mafanikio makubwa.

Sambamba na hayo, Rais Magufuli alieleza jinsi Mzee Mkapa alivyokuwa na uwezo wa kulea na kuibua vipaji vya viongozi wa ngazi za juu hapa nchini akiwemo yeye mwenyewe, Rais Mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein pamoja na Mgombea Urais kupitia CCM kwa upande wa Zanzibar Dk. Hussein Mwinyi.

“Kifo cha Mzee Mkapa kimeacha alama duniani...serikali ninayoiongoza itadumisha mambo yote mazuri yaliyoasisiwa na Mzee Mkapa.....Mzee Mkapa ni shujaa wangu na ni mtu muhimu sana katika maisha yangu na hata nilipopatwa na shida ama kupambana na changamoto mbali mbali mzee Mkapa hakuniacha alinilea kama mtoto wake”,alisema Magufuli.

“leo hapa Mkapa hayupo nimesikitika kuwaona wawili tu hiii inaumiza sana, mtakumbuka katika siku za hivi karibuni viongozi hawa watatu walikuwa pamoja katika uzinduzi wa kitabu cha Mkapa walikuwa pamoja....kwa hakika ilikuwa ikiependeza sana na kufurahisha sana lakini sasa hatutawaona mkiwa watatu tena” aliongeza Magufuli huku akibubujika na machozi.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kassim Majaaliwa Majaaliwa alisema kuwa ni vyema Watanzania wakamuezi kiongozi huyo pamoja na yale yote mazuri aliyoyafanya na kuwafanyia Watanzania pamoja na nchi za jirani ya Tanzania.

Nae Waziri wa  Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Amidi wa Sherehe alisoma wasifu wa Hayati Benjamin William Mkapa na kuyaeleza maisha yake yote kuanzia familia, masomo, kazi zake, uongozi wa serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Pia, alieleza mafanikio ya Rais Mkapa katika uongozi wake ikiwa ni pamoja na kusimamia ukombozi wa nchi za Bara la  Afrika na jinsi alivyoheshimika katika nchi za Kusini mwa Afrika na kupelekea kupewa nishani ya Juu kutokana na juhudi zake hizo.

Aidha, alieleza jinsi alivyochangia kwa kiasi kikubwa kukuza uchumi wa Tanzania na mikakati aliyoiweka ikiwa ni pamoja kuhakikisha uhuru wa vyombo vya habari na uhuru wa kisiasa unakuwepo.

Profesa Kabudi alieleza kuwa maradhi yaliyopelekea kifo cha Hayati Mzee Mkapa ni Moyo kusimama hafla pamoja na Malaria.

Waziri Mkuu wa Burundi Jenerali Alain Guillaume Bunyoni kwa upande wake akitoa salamu za pole kwa niaba ya Rais wa Burundi na wananchi wa nchi hiyo wanaungana mkono na wanatoa pole kwa msiba huo mkubwa uliowapata ndugu zao wa Tanzania.

Nae Balozi Ahmada Elbadui Mohammed Faki, Balozi wa Comoro nchini Tanzania kwa niaba ya Mabalozi wanaofanya kazi zao hapa nchini alitoa neno la pole kwa Rais Magufuli  pamoja na wananchi wote wa Tanzania na kueleza jinsi Hayati Mkapa alivyokuwa jasiri katika kupambana na uhuru wa nchi za Bara la Afrika.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.